SOMO LA 5
Kutua kwa Njia Inayofaa
UNAPOONGEA, ni muhimu kutua mahali panapofaa. Na ni muhimu kutua iwe unatoa hotuba au unaongea na mtu. Bila kutua, mambo yanayosemwa yanaweza kukosa kueleweka wazi. Kutua mahali panapofaa husaidia kufanya maneno yako yawe wazi. Pia unaweza kutua ili mambo makuu yakumbukwe daima.
Unaweza kujuaje wakati wa kutua? Na utue kwa muda gani?
Kutua kwa Kufuata Alama za Vituo. Alama za vituo ni sehemu muhimu ya maandishi. Zinaweza kuonyesha mwisho wa taarifa au swali. Baadhi ya lugha hutumia alama za vituo kuonyesha maneno yaliyonukuliwa. Alama nyingine za vituo huonyesha uhusiano uliopo kati ya sehemu moja ya sentensi na sehemu nyingine. Mtu anayesoma anaweza kuona alama za vituo. Lakini anaposoma mbele ya wengine kwa sauti, ni lazima sauti yake ionyeshe alama za vituo zilizoko katika habari anayosoma. (Kwa maelezo zaidi, ona Somo la 1, “Kusoma kwa Usahihi.”) Ukikosa kutua mahali penye alama ya kituo, wengine wanaweza kukosa kuelewa jambo unalosoma au hata wanaweza kulielewa vibaya.
Pia, jinsi mawazo yanavyotokezwa katika sentensi huonyesha mahali panapofaa kutua. Pindi moja mwanamuziki fulani mashuhuri aliandika hivi: “Mimi sipigi piano vizuri kuliko wengine. Lakini siri ni kutua mahali panapofaa.” Ndivyo ilivyo na kuzungumza. Kutua kwa njia inayofaa kutafanya hotuba uliyotayarisha vizuri ivutie na iwe na maana.
Unapotayarisha kusoma mbele ya watu, inafaa kutia alama habari utakayosoma. Ukifika mahali ambapo unapaswa kutua kifupi, chora mstari mfupi ambao umesimama wima. Chora mistari miwili iliyo wima na karibu-karibu ili ujue mahali ambapo utatua kwa muda mrefu zaidi. Sentensi fulani ikiwa ngumu na kila mara unatua mahali pasipotakikana, tia alama kwa penseli maneno yote yanayounganisha sentensi hiyo ngumu. Kisha soma fungu hilo lote mwanzo hadi mwisho. Wasemaji wengi wenye uzoefu hufanya hivyo.
Kwa kawaida hupati tatizo la kutua unapozungumza kwa sababu unajua mambo unayotaka kusema. Lakini usemi wako hautakuwa na nguvu wala hautakuwa wazi kama una tabia ya kutua kila wakati hata iwe unazungumzia nini. Madokezo yanayoonyesha jinsi ya kuboresha jambo hili yako katika Funzo la 4, “Ufasaha.”
Kutua ili Kubadili Mawazo. Unapomaliza kuzungumzia jambo fulani na kuanza jambo tofauti, kutua kunaweza kuwasaidia wasikilizaji wafikirie, wajitayarishe, na hata kutambua kwamba unaanza kuzungumzia mambo tofauti, na kuelewa vizuri zaidi mambo utakayosema. Ni muhimu kutua unapomaliza kusema jambo moja na kuanza kusema jingine kama tu ilivyo muhimu kupunguza mwendo unapopiga kona kutoka njia moja na kushika njia nyingine.
Wanapotoa hotuba, wasemaji wengine humaliza kuzungumzia jambo moja na kuanza jambo jingine mbio-mbio bila kutua. Hiyo ni kwa sababu wao hujaribu kuzungumzia mambo mengi mno. Wengine wana tabia hiyo katika mazungumzo yao ya kawaida. Labda watu wanaoshirikiana nao wanazungumza hivyo. Lakini huko si kufundisha kuzuri. Ikiwa unataka kusema jambo la maana ambalo litakumbukwa, basi tumia wakati kulikazia. Tambua kwamba kutua ni muhimu sana ili ueleweke vizuri.
Ikiwa hotuba yako inategemea muhtasari, ipange vizuri ili ujue mahali pa kutua kati ya mambo makuu. Ikiwa una hotuba ya kusoma, tia alama sehemu ambayo jambo fulani kuu linaishia na jingine kuanzia.
Mara nyingi kutua ili kubadili mawazo ni kurefu kuliko kule kutua kwa kufuata alama za vituo, lakini usitue kwa muda mrefu hivi kwamba hotuba ionekane inajivuta. Ikiwa unatua kwa muda mrefu sana, watu watafikiri hujatayarisha vizuri na unajaribu kufikiria jambo unalotaka kusema.
Kutua ili Kutia Mkazo. Mara nyingi kutua ili kutia mkazo ni kutua kwa njia inayotokeza sana, yaani, ni kule kutua kunakotangulia au kufuata maneno yanayosemwa kwa mkazo fulani. Kutua huko kunasaidia wasikilizaji wafikirie jambo ambalo umetoka tu kusema, au kunawapa hamu ya kujua jambo linalofuata. Kuna namna nyingi za kutua kwa njia hiyo. Basi ni juu yako kuamua njia inayofaa ya kutua. Lakini ukumbuke kwamba kutua ili kukazia jambo kunafaa kutumiwa kwa mambo muhimu pekee. Ama sivyo, kutua huko hakutatimiza jambo lolote.
Yesu aliposoma Maandiko kwa sauti katika sinagogi ya Nazareti, alitua vizuri sana. Kwanza, alisoma utume wake katika hati ya nabii Isaya. Lakini, kabla ya kufafanua maandiko hayo, alifunga hati, akampa mtumishi, akaketi. Kisha, wote katika sinagogi wakimtazama kwa makini, akasema: “Leo andiko hili ambalo mmetoka tu kusikia limetimizwa.”—Luka 4:16-21.
Tua Kulingana na Hali. Pindi kwa pindi kelele zinaweza kufanya utue kama unazungumza. Kama unaongea na mtu katika huduma ya shambani, unaweza kutua ikiwa kuna kelele za gari linalopita au mtoto anayelia. Katika kusanyiko, unaweza kuinua sauti yako na kuendelea kuzungumza ikiwa kelele haivurugi sana. Lakini ni lazima utue ikiwa kuna kelele nyingi mno yenye kuendelea. Hata wasikilizaji hawatakuwa wakikusikiliza. Basi tua kwa njia inayofaa ili wasikilizaji wafaidike kikamili na mambo mema unayowaambia.
Tua ili Uruhusu Wasikilizaji Wajibu. Ingawa huenda unatoa hotuba isiyoshirikisha wasikilizaji, ni muhimu kuruhusu wasikilizaji wajijibu kimoyomoyo. Ukitokeza maswali ambayo yanafanya wasikilizaji wafikiri lakini hutui kwa njia inayofaa, maswali hayo hayatakuwa na maana sana.
Bila shaka ni muhimu kutua unapohubiria wengine na vilevile unapotoa hotuba jukwaani. Watu wengine ni kama hawatui kamwe. Kama una tatizo hilo, jaribu sana kukuza sifa hii ya usemi. Mawasiliano yako pamoja na wengine yataboreka na pia utakuwa na matokeo mazuri katika huduma ya shambani. Kutua ni ukimya wa muda mfupi na kama inavyosemekana, kwa kweli ukimya huonyesha vituo, hutia mkazo, hushika akili za mtu, na hupendeza wasikilizaji.
Mazungumzo ya kawaida hushirikisha watu wawili au zaidi. Inaelekea wengine watakusikiliza ikiwa unawasikiliza na kuzingatia mambo wanayosema. Hiyo inamaanisha kutua kwa muda wa kutosha ili wapate nafasi ya kujieleza.
Mahubiri yetu shambani huwa na matokeo zaidi tunapoongea na wengine kwa njia ya kawaida. Baada ya kusalimiana, Mashahidi wengi hupendelea kumjua mtu wanayemkuta kisha wamwulize swali. Wao hutua ili kumpa mtu huyo fursa ya kujibu, na kusikiliza jibu lake. Wanaweza kumpa fursa za kusema wanapozungumza naye. Wanajua kwamba kwa kawaida wanaweza kumsaidia mtu sana wakijua maoni yake juu ya jambo wanalozungumzia.—Mit. 20:5.
Bila shaka si watu wote hujibu maswali vizuri. Lakini jambo hilo halikumzuia Yesu asitue vya kutosha ili awape hata wapinzani wake fursa ya kusema. (Mk. 3:1-5) Kumpa mtu fursa ya kusema humsaidia kufikiri na hiyo inaweza kumfanya afunue yaliyo moyoni mwake. Hata mojawapo ya makusudi yetu katika huduma ni kuchochea mioyo kwa kuwajulisha watu mambo muhimu yanayotokana na Neno la Mungu ambayo ni lazima wafanye maamuzi kuyahusu.—Ebr. 4:12.
Kwa kweli kutua kwa njia inayofaa tukiwa katika huduma kunahitaji ustadi. Tunapotua kwa njia inayofaa, mambo tunayosema hueleweka vizuri zaidi na kukumbukwa daima.