Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • be funzo 21 uku. 150-uku. 152 fu. 5
  • Kusoma Maandiko kwa Mkazo Unaofaa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kusoma Maandiko kwa Mkazo Unaofaa
  • Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Habari Zinazolingana
  • Kukazia Maana kwa Njia Inayofaa
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Kutumia Maandiko Vizuri
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Kukazia Mawazo Makuu
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Kuwasaidia Wasikilizaji Kutumia Biblia
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
Pata Habari Zaidi
Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
be funzo 21 uku. 150-uku. 152 fu. 5

SOMO LA 21

Kusoma Maandiko kwa Mkazo Unaofaa

Unahitaji kufanya nini?

Kazia maneno makuu ya habari unayozungumzia. Soma kwa hisia inayofaa.

Kwa Nini Ni Muhimu?

Uzito wa maandiko yanayosomwa hudhihirishwa kwa mkazo unaofaa.

UNAPOZUNGUMZA na wengine kuhusu mambo ambayo Mungu amekusudia, iwe unamhubiria mtu au unahutubu jukwaani, unapaswa kutegemea Neno la Mungu. Mara nyingi mazungumzo hayo hutia ndani kusoma Biblia, na tunapaswa kuisoma vizuri.

Mkazo Unaofaa Unatia Ndani Hisia. Tusome maandiko kwa hisia. Ebu ona mifano michache. Unaposoma kwa sauti Zaburi 37:11, sauti yako inapasa kuonyesha furaha ya kutazamia amani ambayo imeahidiwa katika andiko hilo. Unaposoma Ufunuo 21:4 kuhusu mwisho wa kuteseka na kifo, sauti yako ionyeshe shukrani za moyoni kwa sababu ya faraja hiyo nzuri ajabu ambayo imetabiriwa hapo. Soma Ufunuo 18:2, 4, 5 kwa sauti ya dharura kwa sababu linatuhimiza tutoke kwenye “Babiloni Mkubwa” mwenye dhambi tele. Hisia tunayoonyesha itoke moyoni lakini isipite kiasi. Kadiri nzuri ya hisia inategemea andiko unalosoma na jinsi unavyolitumia.

Kazia Maneno Yanayofaa. Kama unazungumzia sehemu fulani tu ya andiko, kazia sehemu hiyo unaposoma. Kwa mfano, ikiwa unataka kuelezea maana ya “kutafuta kwanza ufalme” unaposoma Mathayo 6:33, usikazie “uadilifu wake” wala “vitu vingine vyote.”

Tuseme umepanga kusoma Mathayo 28:19 katika hotuba utakayotoa katika Mkutano wa Utumishi. Utakazia maneno gani? Ikiwa unataka kutia watu moyo wawe na bidii kuanzisha mafunzo ya Biblia ya nyumbani, kazia ‘kufanya wanafunzi.’ Na kama unataka kuzungumzia daraka la Mkristo la kuwajulisha kweli za Biblia watu wa nchi za kigeni au kama unataka kuwatia moyo wahubiri wengine watumikie katika sehemu zenye uhitaji zaidi, unaweza kukazia “watu wa mataifa yote.”

Mara nyingi tunasoma andiko kujibu swali au kuunga mkono jambo fulani ambalo wengine hubisha. Ikiwa unakazia kila wazo katika andiko hilo kwa kadiri ileile, wasikilizaji wanaweza kukosa kuelewa kusudi lako la kusoma andiko hilo. Wewe unaweza kufahamu wazi kusudi lako la kulisoma lakini huenda wao wasilifahamu.

Kwa mfano, unaposoma Zaburi 83:18 katika Biblia ambayo ina jina la Mungu, mwenye nyumba anaweza kukosa kufahamu jambo linaloonekana kuwa wazi la kwamba Mungu ana jina ikiwa unakazia sana ile sehemu inayosema “Uliye juu.” Kazia jina “Yehova.” Lakini, unapotumia andiko hilo kuonyesha kwamba Yehova ni mwenye enzi kuu, kazia maneno “Uliye juu.” Vilevile unapotumia Yakobo 2:24 kuonyesha kwamba imani inapaswa kuonyeshwa kwa matendo, kukazia ‘kutangazwa kuwa mwadilifu’ badala ya kukazia “kazi” kunaweza kufanya wengine wasipate maana.

Tunaweza kupata mfano mwingine mzuri katika Waroma 15:7-13. Hii ni sehemu ya barua ambayo mtume Paulo aliandikia kutaniko lenye mchanganyiko wa watu wa Mataifa na Wayahudi wa asili. Anasema hapo kwamba huduma ya Kristo haiwafaidi tu Wayahudi waliotahiriwa bali inawafaidi pia watu wa mataifa ili “mataifa yapate kumtukuza Mungu kwa ajili ya rehema yake.” Kisha ananukuu maandiko manne kuthibitisha jambo hilo. Unapaswa kusoma manukuu hayo kwa njia gani ili kukazia jambo ambalo Paulo alimaanisha? Ikiwa unatia alama maneno ya kukazia, unaweza kutia alama “mataifa” katika mstari wa 9, “nyinyi mataifa” katika mstari wa 10, “mataifa yote” na “vikundi vyote vya watu” katika mstari wa 11, na “mataifa” katika mstari wa 12. Ebu jaribu kusoma Waroma 15:7-13 kwa mkazo huo. Unapofanya hivyo, hoja ya Paulo itakuwa wazi na kueleweka kwa urahisi.

Njia za Kutia Mkazo. Unaweza kutumia njia kadhaa kukazia maneno muhimu ambayo unataka yawe wazi. Njia unayotumia kutia mkazo ilingane na andiko unalosoma na muktadha wa hotuba yako. Hapa pana madokezo machache.

Kutia mkazo kupitia sauti. Njia hii inahusisha kubadili sauti kwa njia yoyote inayofanya maneno yenye maana yawe wazi kuliko maneno mengine katika sentensi. Unaweza kutia mkazo kwa kuinua sauti au kuipunguza. Katika lugha nyingi, kuinua sauti kunaweza kuongeza mkazo. Lakini katika lugha nyinginezo, kuinua sauti kunaweza kubadili maana ya jambo unalosema. Ukipunguza mwendo wako na kuongea polepole unapofikia maneno makuu, maneno hayo hutokea kwa uzito zaidi. Katika lugha ambazo huwezi kukazia maneno fulani kwa kubadili sauti, unaweza kufuata desturi za kukazia maneno katika lugha hizo.

Kutua kifupi. Unaweza kutua kifupi kabla ya kusoma sehemu kuu ya andiko au baada ya kuisoma, au kabla na baada ya kuisoma. Kutua kifupi kabla tu ya kusoma wazo kuu hufanya watu wawe na hamu ya kujua jambo linalofuata na kutua baada tu ya kulisoma hufanya jambo hilo lieleweke zaidi. Lakini ukitua-tua sana, hakuna jambo litakalokuwa wazi.

Kurudia jambo kuu. Unaweza kukazia jambo fulani kwa kutua na kulisoma tena. Njia nzuri ya kutua inayotumiwa mara nyingi ni kumaliza kusoma andiko lote kisha urudie kusoma wazo kuu unalotaka kukazia.

Ishara. Mara nyingi ishara za mwili na za uso zinaweza kuongezea hisia jambo unalosema.

Hali ya sauti. Katika lugha fulani, nyakati nyingine maneno yanaweza kusomwa kwa sauti inayotokeza maana fulani na kuyatia mkazo. Pia unahitaji kutumia busara kuhusu jambo hili hasa unapotumia maneno ya dhihaka.

Wengine Wanaposoma Maandiko. Mwenye nyumba anaposoma andiko, anaweza kukazia maneno yasiyostahili kukaziwa au labda asikazie neno lolote. Ufanye nini basi? Kwa ujumla ni vizuri ufafanue maana unapomwonyesha jinsi maandiko hayo yanavyotumika. Baada ya kufanya hivyo, unaweza kukazia hasa maneno yanayotokeza maana katika Biblia.

KUJUA JINSI YA KUTUMIA MKAZO

  • Jiulize hivi kuhusu andiko lolote ambalo utasoma: ‘Maneno haya yanaonyesha hisia gani? Nionyeshe hisia hizo kwa njia gani?’

  • Chunguza maandiko unayopanga kutumia. Jiulize hivi kuhusu kila mojawapo ya maandiko hayo: ‘Andiko hili litatimiza kusudi gani? Nahitaji kukazia maneno gani kutimiza kusudi hilo?’

MAZOEZI: (1) Chunguza andiko ambalo unataka kutumia katika utumishi wa shambani. Fanya mazoezi ya kulisoma kwa hisia inayofaa. Ukikumbuka jinsi unavyotaka kulitumia, lisome kwa sauti ukikazia neno au maneno yanayofaa. (2) Katika kichapo kinachotumiwa wakati huu kwenye funzo, chagua fungu moja ambalo lina manukuu ya maandiko. Chunguza jinsi ambavyo maandiko yametumiwa hapo. Tia alama maneno yanayotokeza maana. Soma fungu lote kwa sauti kwa njia inayokazia vizuri maandiko.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki