SOMO LA 6
Kukazia Maana kwa Njia Inayofaa
UNAPOZUNGUMZA au unaposoma kwa sauti, ni muhimu kusema neno mojamoja vizuri na kukazia kwa njia inayotokeza wazi maneno muhimu na yale yanayowasilisha mawazo yako.
Kukazia maana kwa njia inayofaa si kukazia tu maneno machache au hata kukazia maneno mengi. Ni lazima maneno yanayofaa yakaziwe. Ukikazia maneno ambayo hayastahili kukaziwa, huenda wasikilizaji wasielewe jambo unalomaanisha, na akili zao zinaweza kuanza kutangatanga. Hata kama habari yenyewe inapendeza, haitachochea wasikilizaji sana ikiwa maana haikaziwi vizuri.
Unaweza kutia mkazo zaidi kwa njia kadhaa, na mara nyingi njia hizo hutumika pamoja: kuinua sauti, kuongeza hisia, kupunguza mwendo na kutamka kila neno kwa utaratibu, kutua kabla au baada ya kusema jambo (au kutua kabla na baada ya kusema jambo), na kwa ishara za mwili na za uso. Katika lugha nyinginezo, mtu anaweza kutia mkazo kwa kupunguza sauti au kuiinua. Fikiria habari hiyo na hali zake ili uone jambo linalofaa kukaziwa.
Unapofikiria jambo la kukazia, zingatia yafuatayo. (1) Maneno yanayopaswa kukaziwa zaidi katika sentensi yoyote hutegemea sehemu inayobaki ya sentensi hiyo na pia muktadha. (2) Unaweza kukazia maana unapoanza wazo jipya, iwe ni jambo kuu au iwe unabadili tu mawazo yako na kuanza kuzungumzia jambo jingine. Pia unaweza kukazia maana ili kuonyesha kwamba unamaliza kusema jambo fulani. (3) Msemaji anaweza kukazia maana anapotaka kuonyesha jinsi anavyohisi kuhusu jambo fulani. (4) Unaweza kukazia maana kwa njia inayofaa ili kudhihirisha mambo makuu ya hotuba.
Ili kukazia maana katika njia hizo ambazo zimeonyeshwa, ni lazima mtu anayehutubia watu au anayesoma mbele ya watu aelewe vizuri habari hiyo na awe anataka wasikilizaji waielewe. Andiko la Nehemia 8:8 linasema hivi kuhusu maagizo yaliyotolewa wakati wa Ezra: “Nao wakasoma katika kitabu, katika torati ya Mungu, kwa sauti ya kusikilika; wakaeleza maana yake, hata wakayafahamu yaliyosomwa.” Ni wazi kwamba wale waliosoma Neno la Mungu na kulifafanua katika pindi hiyo walitambua umuhimu wa kuwasaidia wasikilizaji waelewe yaliyosomwa, wayashike, na kuyafuata maishani.
Tatizo Linaweza Kutokezwa na Nini? Watu wengi wanaweza kuongea kwa njia inayoeleweka vizuri katika mazungumzo ya kila siku. Lakini, wanaposoma habari iliyoandikwa na mtu mwingine, wanaweza kushindwa mambo ya kukazia. Basi siri ni kuelewa vizuri habari hiyo. Hiyo inamaanisha kuchunguza kwa makini habari hiyo. Kwa hiyo, ukipewa mgawo wa kusoma katika mkutano wa kutaniko, tayarisha kwa bidii.
Watu wengine hukazia maneno baada ya kila pindi fulani badala ya kukazia maana, iwe mkazo huo unafaa au haufai. Wengine hukazia maneno ambayo hayapaswi kukaziwa, labda wakikazia mno vihusishi na viunganishi. Ikiwa mkazo haufanyi jambo liwe wazi, ni rahisi sana uwe zoea linalokengeusha watu.
Ili kukazia maana, wasemaji wengine huinua sauti zao hivi kwamba wasikilizaji wanaona ni kana kwamba wanazomewa. Kwa wazi si rahisi njia hiyo iwe na matokeo mazuri. Kama hukazii maneno kwa njia ya kawaida, wasikilizaji wanaweza kufikiri kwamba msemaji anawashusha chini. Ni afadhali kama nini kuwachochea kwa upendo na kuwasaidia waone kwamba mambo wanayosikia yanatokana na Maandiko na yanafaa!
Jinsi ya Kufanya Maendeleo. Mara nyingi mtu ambaye hukazia maana kwa njia isiyofaa hajui ana tatizo hilo. Ni mtu mwingine anayeweza kumtajia. Ikiwa unahitaji kufanya maendeleo kuhusu jambo hili, mwangalizi wa shule atakusaidia. Pia, unaweza kumwomba mtu mwingine ambaye ni msemaji mzuri akusaidie. Mwambie akusikilize kwa makini unaposoma na unaposema na akushauri mahali unapohitaji kufanyia maendeleo.
Kwanza, mwenye kukushauri anaweza kupendekeza ufanye mazoezi kwa kusoma sehemu fulani ya Mnara wa Mlinzi. Yamkini, atakuambia uchunguze kila sentensi ili ujue ni maneno yapi au mafungu yapi ya maneno yanayopaswa kukaziwa ili maana ieleweke kwa urahisi. Anaweza kukukumbusha utilie maanani maneno fulani ambayo yameandikwa kwa italiki. Kumbuka kwamba maneno yanayofanyiza sentensi yameungana ili kutokeza maana. Mara nyingi ni fungu la maneno linalopaswa kukaziwa, bali si neno moja tu. Katika lugha nyinginezo, wanafunzi wanaweza kuambiwa wazingatie kwa makini jinsi alama za matamshi zinavyoonyesha mkazo unaofaa.
Hatua inayofuata sasa ni kujifunza jambo la kukazia, na mwenye kukushauri anaweza kukuhimiza ufikirie muktadha na si sentensi tu. Fungu lote linazungumzia jambo gani kuu? Jambo hilo linahusikaje na kile unachokazia katika sentensi? Tazama kichwa kikuu cha habari unayosoma na kichwa chake kidogo chenye maandishi mazito. Vichwa hivyo vina uhusiano gani na habari unayochagua kukazia? Unapaswa kuzingatia mambo hayo yote. Lakini jihadhari usikazie maneno mengi mno.
Iwe utatoa hotuba au utasoma, mwenye kukushauri anaweza pia kukuambia ukazie maana kulingana na hoja zako. Unahitaji kujua mahali ambapo hoja zako zinaishia au mahali ambapo unaanza kuzungumzia jambo jingine muhimu. Wasikilizaji watathamini ikiwa jinsi unavyotoa hotuba inawasaidia kutambua mambo hayo kimbele. Unaweza kufaulu kwa kukazia maneno kama kwanza kabisa, halafu, hatimaye, basi, na kwa kufaa.
Mwenye kukushauri pia atakuambia uzingatie maneno ambayo unataka kusema kwa hisia. Ili ufanye hivyo huenda ukahitaji kukazia maneno kama sana, bila shaka, kwa vyovyote vile, haiwezekani, muhimu, na siku zote. Ukifanya hivyo, wasikilizaji wako wanaweza kuona jinsi unavyohisi kuhusu jambo unalosema. Tutazungumzia zaidi jambo hili katika Somo la 11, “Zungumza kwa Hisia.”
Ili uboreshe njia yako ya kukazia maana, pia utatiwa moyo uyaweke wazi akilini mambo makuu ambayo unataka wasikilizaji wakumbuke. Jambo hili litafafanuliwa zaidi tutakapozungumzia kusoma mbele ya watu katika Somo la 7, “Kukazia Mawazo Makuu,” na pia katika hali ya usemaji katika Somo la 37, “Kukazia Mambo Makuu.”
Ikiwa unajaribu kuboresha huduma yako ya shambani, fikiria sana jinsi unavyosoma maandiko. Jiulize hivi kila mara, ‘Kwa nini ninasoma andiko hili?’ Ukiwa mwalimu, haitoshi kusema tu maneno ifaavyo. Huenda hata kusoma andiko hilo kwa hisia tu hakutoshi. Kama unajibu swali la mtu au unafundisha kweli ya msingi, unaposoma maandiko ni vizuri kukazia maneno yanayotegemeza jambo unalozungumzia. Usipofanya hivyo mtu unayemsomea anaweza kukosa kukuelewa.
Kwa kuwa kukazia maana kunaongezea mkazo maneno mengine, msemaji ambaye hana uzoefu anaweza kuwa na mwelekeo wa kukazia maneno hayo kupita kiasi. Anafanana na mtu ambaye anaanza kujifunza ala fulani ya muziki. Lakini akiendelea kufanya mazoezi, hatimaye atafaulu kucheza muziki mtamu unaofurahisha.
Baada ya kujifunza mambo ya msingi, utafaidika ukiwasikiliza wasemaji wenye uzoefu. Upesi utatambua jinsi mkazo wa kadiri tofauti-tofauti unavyoweza kutimiza mengi. Na utaona faida ya kukazia maana kwa njia mbalimbali ili mambo unayosema yawe wazi. Utaboresha sana usomaji wako na usemaji wako ukijua jinsi ya kukazia maana kwa njia inayofaa.
Usijifunze kukazia maana ili tu utimize wajibu. Ili uwe msemaji mzuri, endelea kujizoeza mpaka uwe umejua sana kukazia maana na kuweza kufanya hivyo kwa njia inayoonekana kuwa ya kawaida kwa wasikilizaji.