SOMO LA 7
Kukazia Mawazo Makuu
MSOMAJI mzuri hazingatii sentensi moja tu, wala hazingatii tu fungu ambalo lina sentensi hiyo. Anaposoma, anazingatia mawazo makuu ya habari nzima anayosoma. Hiyo humsaidia kujua mahali pa kutia mkazo.
Mtu asipofanya hivyo, usomaji wake utakosa vilele. Hakuna jambo litakalokuwa wazi. Na anapomaliza kusoma, inaweza kuwa vigumu kukumbuka jambo lolote kuu.
Kukazia mawazo makuu kwa njia inayofaa mara nyingi kunaweza kuboresha sana usomaji wa simulizi lolote la Biblia. Mkazo kama huo unaweza kufanya usomaji wa mafungu uwe na maana sana kwenye funzo la Biblia la nyumbani au kwenye mkutano wa kutaniko. Na mkazo huo ni muhimu sana unapotoa hotuba ya kusomwa, kama ambavyo nyakati nyingine inafanywa katika makusanyiko yetu.
Jinsi ya Kufaulu. Unaweza kupokea mgawo wa kusoma Biblia katika shule. Ukazie nini? Ikiwa kuna wazo kuu au tukio muhimu linalozungumziwa katika habari unayosoma, ingefaa kulikazia.
Iwe sehemu unayosoma ni shairi au si shairi, mithali au masimulizi, wasikilizaji watafaidika ukiisoma vizuri. (2 Tim. 3:16, 17) Ili uweze kusoma vizuri, ni lazima uzingatie mafungu ambayo utasoma na vilevile uwafikirie wasikilizaji.
Ikiwa utasoma kwa sauti kichapo fulani katika funzo la Biblia au kwenye mkutano wa kutaniko, unahitaji kukazia mawazo gani makuu? Chukua majibu ya maswali yaliyochapishwa kuwa mawazo makuu. Pia kazia mambo yanayopatikana chini ya vichwa vidogo vyenye herufi nzito yanayohusiana na vichwa hivyo.
Haipendekezwi kusoma hotuba za kutaniko. Hata hivyo, mara kwa mara hotuba za kusomwa huandaliwa katika kusanyiko ili mawazo yaleyale yatolewe kwa njia ileile katika makusanyiko yote. Ili kukazia mawazo makuu katika hotuba kama hizo za kusomwa, kwanza ni lazima msemaji achunguze hotuba hiyo kwa makini. Mambo makuu ni yapi? Anapaswa kuyatambua. Mambo makuu si mawazo ambayo yeye anafikiri yanapendeza. Ni yale mambo muhimu ambayo yanategemeza hotuba hiyo. Mara nyingi taarifa fupi ya wazo kuu katika hotuba ya kusomwa hutanguliza masimulizi fulani au kusababu fulani. Kwa kawaida, taarifa yenye nguvu hutolewa baada ya kutajwa kwa mambo yanayothibitisha jambo fulani. Baada ya kutambua mambo makuu, msemaji anapaswa kuyatia alama katika hotuba yake ya kusomwa. Mawazo hayo makuu huwa machache, labda hayazidi manne au matano. Kisha anahitaji kujizoeza kusoma ili wasikilizaji waweze kutambua kwa urahisi hayo mambo makuu. Mambo hayo makuu ndiyo vilele vya hotuba. Hotuba hiyo ikitolewa kwa mkazo unaofaa, inaelekea mawazo hayo makuu yatakumbukwa. Msemaji anapaswa kuwa na lengo la kufanya mawazo makuu yakumbukwe.
Kuna njia kadhaa ambazo msemaji anaweza kutumia kutia mkazo unaofaa ili wasikilizaji watambue mambo makuu. Anaweza kuongeza shauku, anaweza kubadili mwendo wake wa kusoma, anaweza kuongeza hisia, au anaweza kutumia ishara zinazofaa na kadhalika.