Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • be funzo 4 uku. 93-uku. 96 fu. 3
  • Ufasaha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ufasaha
  • Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Habari Zinazolingana
  • Jinsi ya Kukabiliana na Kigugumizi
    Amkeni!—2010
  • Kuzungumza kwa njia ya kawaida
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Kuielewa Hofu ya Kugugumiza
    Amkeni!—1997
  • Sanduku La Swali
    Huduma Yetu ya Ufalme—1996
Pata Habari Zaidi
Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
be funzo 4 uku. 93-uku. 96 fu. 3

SOMO LA 4

Ufasaha

Unahitaji kufanya nini?

Unahitaji kusoma na kusema kwa njia ambayo maneno yako na mawazo yako yanatiririka bila kukwama-kwama. Mtu anapotoa hotuba kwa ufasaha, hakati-kati maneno wala hasemi kwa mwendo wa polepole mno. Hajikwai-kwai anapozungumza wala hatafuti-tafuti mawazo.

Kwa Nini Ni Muhimu?

Msemaji akikosa ufasaha, akili za wasikilizaji zinaweza kutangatanga; na maneno mengine yanaweza kueleweka vibaya. Anaweza kukosa kugusa mioyo ya wasikilizaji.

UNAPOSOMA kwa sauti, je, wewe hukwama ukifikia maneno fulani? Au unapotoa hotuba mbele ya wasikilizaji, je, wewe hutafuta-tafuta maneno ya kutumia? Ikiwa ndivyo, huenda una tatizo la kukosa ufasaha. Mtu mwenye ufasaha husoma na kusema kwa njia ambayo maneno yake na mawazo yake hutiririka tu, bila shida yoyote. Hiyo haimaanishi kwamba anaongea tu bila kukoma, haraka-haraka, ama bila kufikiri. Usemi wake unafurahisha na unapendeza. Ufasaha ni sifa muhimu katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.

Kuna mambo kadhaa ambayo yanaweza kufanya tukose ufasaha. Je, unahitaji kuzingatia mojawapo ya mambo haya yanayofuata? (1) Unaposoma mbele ya watu, maneno usiyofahamu yanaweza kufanya usite. (2) Kutua-tua kifupi kunaweza kufanya usomaji wako usitiririke. (3) Kukosa kujitayarisha kunaweza kufanya usisome vizuri. (4) Unapohutubia kikundi cha watu, jambo ambalo mara nyingi husababisha ukosefu wa ufasaha ni kutopanga maneno kwa njia inayoeleweka. (5) Kukosa msamiati kunaweza kufanya mtu asite-site anapotafuta maneno anayofaa kutumia. (6) Unaweza kukosa ufasaha ikiwa unakazia maneno mengi mno. (7) Kutofahamu sarufi ya lugha kunaweza kutokeza tatizo hilo.

Kama huna ufasaha, hata kama wasikilizaji ndani ya Jumba la Ufalme hawataondoka kihalisi, akili zao zinaweza kutangatanga. Na hawatasikiliza mengi ya yale unayosema.

Kwa upande mwingine, tujihadhari ili hotuba tuliyokusudia iwe yenye nguvu na yenye ufasaha isije ikawa ya madharau, na labda hata kufanya wasomaji waone aibu. Ikiwa umetoka katika utamaduni tofauti, na kwa sababu hiyo watu wanaona hutumii busara unapoongea au wanaona husemi kwa unyofu, basi ujue unapiga hewa tu. Ni muhimu kukumbuka kwamba japo mtume Paulo alikuwa msemaji mwenye uzoefu, aliwaendea Wakorintho “katika udhaifu na katika hofu na kwa kutetemeka sana,” ili asije akajielekezea fikira mno.—1 Kor. 2:3.

Mazoea ya Kuepuka. Watu wengi wana tabia ya kutaja maneno kama “eeh” wanapozungumza. Mara nyingi wengine huanza maneno yao kwa kusema “tunaona ya kwamba,” au wanaingiza maneno kama “si ndiyo” au “yaani,” katika kila jambo wanalosema. Labda hutambui kwamba wewe hutumia maneno kama hayo mara nyingi. Unaweza kufanya mazoezi na mtu mwingine akusikilize akiyarudia maneno hayo kila wakati unapoyasema. Unaweza kushangaa sana.

Watu wengine hujirudia-rudia sana wanapoongea na wanaposoma. Wao huanza kuzungumza kisha wanajikatiza kabla hawajamaliza sentensi ile na kurudia kusema angalau baadhi ya maneno ambayo tayari walikuwa wamesema.

Wengine nao huongea haraka vizuri, lakini wao huanza kusema jambo fulani kisha wakiwa katikati ya sentensi, wao hujikatiza na kuanza kusema jambo jingine. Ingawa wanaongea kwa mtiririko mzuri, kubadili mawazo ghafula-ghafula kunaondoa ufasaha.

Jinsi ya Kufanya Maendeleo. Kama una tatizo la kutafuta-tafuta maneno ya kutumia, basi unahitaji kufanya bidii kuongeza msamiati wako. Chunguza maneno usiyofahamu katika Mnara wa Mlinzi, Amkeni!, na vichapo vingine ambavyo huenda unasoma. Tafuta maneno hayo katika kamusi, chunguza maana yake na jinsi yanavyotamkwa, na uanze kutumia maneno hayo katika mazungumzo yako. Kama huna kamusi, uliza mtu ambaye anajua lugha vizuri.

Kuzoea kusoma kwa sauti kutakusaidia ufanye maendeleo zaidi. Fikiria maneno magumu, na uyarudie mara kadhaa.

Ili usome kwa ufasaha, ni lazima uelewe jinsi maneno yanavyoungana pamoja katika sentensi. Kwa kawaida, unahitaji kusoma mafungu-mafungu ya maneno ili kutokeza wazo la mwandishi. Zingatia mafungu hayo ya maneno. Kama inafaa, yatie alama. Kusudi si kusoma tu maneno kwa usahihi, bali pia kutoa mawazo kwa usahihi. Baada ya kuchunguza sentensi moja, chunguza sentensi ifuatayo mpaka uwe umechunguza fungu lote. Tambua jinsi mawazo yanavyofuatana. Kisha jizoeze kusoma kwa sauti. Soma fungu kwa kurudia-rudia mpaka uweze kulisoma bila kukwama au kutua pasipofaa. Kisha soma mafungu mengine.

Kisha, ongeza mwendo wako wa kusoma. Baada ya kufahamu jinsi maneno yanavyoungana katika sentensi, utaweza kuona maneno mengi kwa wakati mmoja na kujua maneno yatakayofuata. Kufanya hivyo kutafanya uwe msomaji mzuri zaidi.

Kusoma kwa ukawaida kunaweza kuandaa mazoezi mazuri sana. Kwa mfano, bila kujitayarisha soma kwa sauti andiko la siku na maelezo yake kwa sauti; fanya hivyo kwa ukawaida. Zoeza jicho lako kutambua mafungu ya maneno yenye mawazo kamili-kamili badala ya kuona neno mojamoja tu.

Ili uwe na ufasaha katika mazungumzo, unahitaji kufikiri kabla ya kusema. Kila siku, jizoeze kufikiri kabla ya kuzungumza. Amua mambo unayotaka kusema, na jinsi utakavyoyasema; kisha zungumza. Usiongee haraka. Jaribu kusema jambo lote unalotaka kusema bila kutua au bila kulikatiza na jambo jingine. Inaweza kufaa kutumia sentensi fupi-fupi zilizo rahisi.

Maneno yanapaswa kutokea yenyewe tu ikiwa unajua vizuri jambo unalotaka kusema. Kwa kawaida, si lazima uchague maneno unayotaka kutumia. Hata unaweza kufanya mazoezi kwa kuhakikisha kwamba wazo lote unalotaka kusema li wazi akilini mwako ndipo ufikirie maneno unayotumia unapoendelea kuongea. Ukifanya hivyo na ukizingatia akilini wazo badala ya maneno unayosema, maneno yatatiririka tu, na mawazo yako yatatoka moyoni. Lakini mara tu uanzapo kufikiria maneno badala ya mawazo, unaweza kukwama-kwama unapoongea. Unaweza kufaulu kuongea kwa ufasaha ukifanya mazoezi, na hiyo ni sifa muhimu katika usomaji na usemaji mzuri.

Musa alipoagizwa amwakilishe Yehova mbele ya taifa la Israeli na mbele ya Farao wa Misri, aliona hawezi kutimiza mgawo huo. Kwa nini? Yeye hakuwa na ufasaha; huenda alikuwa na tatizo fulani la usemi. (Kut. 4:10; 6:12) Musa alitoa udhuru mwingi, lakini Mungu hakukubali hata udhuru mmoja. Yehova alimtuma Aroni kuwa msemaji, lakini pia Yehova alimsaidia Musa kusema. Mara nyingi na kwa matokeo mazuri, Musa alisema na watu mmoja-mmoja na pia vikundi vidogo na hata alihutubia taifa lote. (Kum. 1:1-3; 5:1; 29:2; 31:1, 2, 30; 33:1) Ukijitahidi kwa bidii na kumtumaini Yehova, wewe pia unaweza kumheshimu Mungu kwa usemi wako.

KUKABILIANA NA KIGUGUMIZI

Kuna mambo mengi yanayosababisha kigugumizi. Tiba zinazowasaidia watu fulani huenda zisiwasaidie wengine. Lakini ni muhimu kuendelea kujaribu ili ufanikiwe.

Je, kufikiria tu kutoa maelezo kwenye mikutano hukutia woga, na hata wasiwasi mwingi? Sali kwa Yehova akusaidie. (Flp. 4:6, 7) Uwe na lengo la kumheshimu Yehova na kuwasaidia wengine. Usitazamie kwamba tatizo hilo litakwisha kabisa, lakini fikiria jinsi unavyosaidiwa kukabiliana nalo. Unapopata baraka za Yehova na kitia-moyo cha akina ndugu, utafanya maendeleo zaidi.

Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inakupa nafasi ya kupata uzoefu wa kusema mbele ya watu. Unaweza kushangaa jinsi unavyofanya vizuri mbele ya kikundi kidogo kinachokutia moyo na kinachotaka ufanikiwe. Hilo linaweza kukusaidia kupata uhakika wa kusema katika hali tofauti.

Kama una mgawo wa kutoa hotuba, tayarisha vizuri. Fikiria sana jinsi utakavyoitoa. Zungumza kwa hisia inayofaa. Ukikwama unapoongea, jaribu kwa kadiri unavyoweza kudumisha utulivu wa sauti yako na hali yako. Legeza misuli ya utaya wako. Tumia sentensi fupi-fupi. Epuka kutumia maneno kama “mmh” na “eeh.”

Wengine ambao wana kigugumizi huepuka maneno ambayo yamewahi kuwatatiza na badala yake wao hutumia maneno mengine yenye maana moja na hayo. Wengine hupendelea kutambua sauti zinazowatatiza na kuzifanyia mazoezi tena na tena.

Ukishikwa na kigugumizi unapozungumza, usife moyo kuwasiliana. Unaweza kumtia moyo mtu unayezungumza naye aendelee kuongea mpaka uweze kuzungumza tena. Ikihitajika, mwandikie jambo unalotaka au mwonyeshe kichapo fulani.

JINSI YA KUFAULU

  • Unaposoma magazeti na vitabu, tia alama maneno mapya, chunguza maana ya maneno hayo na uyatumie katika mazungumzo.

  • Fanya mazoezi ya kusoma kwa sauti kwa angalau dakika tano hadi kumi kila siku.

  • Tayarisha vizuri migawo ya usomaji. Zingatia mafungu ya maneno yenye kutoa maana. Fahamu jinsi mawazo yanavyofuatana.

  • Katika mazungumzo ya kila siku, jifunze kufikiri kwanza kisha useme sentensi nzima-nzima bila kukatisha.

MAZOEZI: Pitia kwa uangalifu Waamuzi 7:1-25, ukichunguza fungu moja kwa wakati mmoja. Hakikisha unaelewa wazo la fungu hilo. Tumia kamusi kuchunguza maneno usiyofahamu. Taja kila jina kwa sauti. Kisha soma fungu hilo kwa sauti; na uwe mwangalifu ili usome kwa usahihi. Ukiridhika na fungu hilo, fanya vivyo hivyo na fungu linalofuata, na mafungu mengine pia. Kisha usome sura nzima. Uisome tena, na pindi hii uisome haraka. Uisome tena, ukisoma kwa haraka zaidi sehemu ambazo zinafaa kusomwa haraka—lakini si haraka sana hivi kwamba unajikwaa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki