SOMO LA 4
Ufasaha
UNAPOSOMA kwa sauti, je, wewe hukwama ukifikia maneno fulani? Au unapotoa hotuba mbele ya wasikilizaji, je, wewe hutafuta-tafuta maneno ya kutumia? Ikiwa ndivyo, huenda una tatizo la kukosa ufasaha. Mtu mwenye ufasaha husoma na kusema kwa njia ambayo maneno yake na mawazo yake hutiririka tu, bila shida yoyote. Hiyo haimaanishi kwamba anaongea tu bila kukoma, haraka-haraka, ama bila kufikiri. Usemi wake unafurahisha na unapendeza. Ufasaha ni sifa muhimu katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi.
Kuna mambo kadhaa ambayo yanaweza kufanya tukose ufasaha. Je, unahitaji kuzingatia mojawapo ya mambo haya yanayofuata? (1) Unaposoma mbele ya watu, maneno usiyofahamu yanaweza kufanya usite. (2) Kutua-tua kifupi kunaweza kufanya usomaji wako usitiririke. (3) Kukosa kujitayarisha kunaweza kufanya usisome vizuri. (4) Unapohutubia kikundi cha watu, jambo ambalo mara nyingi husababisha ukosefu wa ufasaha ni kutopanga maneno kwa njia inayoeleweka. (5) Kukosa msamiati kunaweza kufanya mtu asite-site anapotafuta maneno anayofaa kutumia. (6) Unaweza kukosa ufasaha ikiwa unakazia maneno mengi mno. (7) Kutofahamu sarufi ya lugha kunaweza kutokeza tatizo hilo.
Kama huna ufasaha, hata kama wasikilizaji ndani ya Jumba la Ufalme hawataondoka kihalisi, akili zao zinaweza kutangatanga. Na hawatasikiliza mengi ya yale unayosema.
Kwa upande mwingine, tujihadhari ili hotuba tuliyokusudia iwe yenye nguvu na yenye ufasaha isije ikawa ya madharau, na labda hata kufanya wasomaji waone aibu. Ikiwa umetoka katika utamaduni tofauti, na kwa sababu hiyo watu wanaona hutumii busara unapoongea au wanaona husemi kwa unyofu, basi ujue unapiga hewa tu. Ni muhimu kukumbuka kwamba japo mtume Paulo alikuwa msemaji mwenye uzoefu, aliwaendea Wakorintho “katika udhaifu na katika hofu na kwa kutetemeka sana,” ili asije akajielekezea fikira mno.—1 Kor. 2:3.
Mazoea ya Kuepuka. Watu wengi wana tabia ya kutaja maneno kama “eeh” wanapozungumza. Mara nyingi wengine huanza maneno yao kwa kusema “tunaona ya kwamba,” au wanaingiza maneno kama “si ndiyo” au “yaani,” katika kila jambo wanalosema. Labda hutambui kwamba wewe hutumia maneno kama hayo mara nyingi. Unaweza kufanya mazoezi na mtu mwingine akusikilize akiyarudia maneno hayo kila wakati unapoyasema. Unaweza kushangaa sana.
Watu wengine hujirudia-rudia sana wanapoongea na wanaposoma. Wao huanza kuzungumza kisha wanajikatiza kabla hawajamaliza sentensi ile na kurudia kusema angalau baadhi ya maneno ambayo tayari walikuwa wamesema.
Wengine nao huongea haraka vizuri, lakini wao huanza kusema jambo fulani kisha wakiwa katikati ya sentensi, wao hujikatiza na kuanza kusema jambo jingine. Ingawa wanaongea kwa mtiririko mzuri, kubadili mawazo ghafula-ghafula kunaondoa ufasaha.
Jinsi ya Kufanya Maendeleo. Kama una tatizo la kutafuta-tafuta maneno ya kutumia, basi unahitaji kufanya bidii kuongeza msamiati wako. Chunguza maneno usiyofahamu katika Mnara wa Mlinzi, Amkeni!, na vichapo vingine ambavyo huenda unasoma. Tafuta maneno hayo katika kamusi, chunguza maana yake na jinsi yanavyotamkwa, na uanze kutumia maneno hayo katika mazungumzo yako. Kama huna kamusi, uliza mtu ambaye anajua lugha vizuri.
Kuzoea kusoma kwa sauti kutakusaidia ufanye maendeleo zaidi. Fikiria maneno magumu, na uyarudie mara kadhaa.
Ili usome kwa ufasaha, ni lazima uelewe jinsi maneno yanavyoungana pamoja katika sentensi. Kwa kawaida, unahitaji kusoma mafungu-mafungu ya maneno ili kutokeza wazo la mwandishi. Zingatia mafungu hayo ya maneno. Kama inafaa, yatie alama. Kusudi si kusoma tu maneno kwa usahihi, bali pia kutoa mawazo kwa usahihi. Baada ya kuchunguza sentensi moja, chunguza sentensi ifuatayo mpaka uwe umechunguza fungu lote. Tambua jinsi mawazo yanavyofuatana. Kisha jizoeze kusoma kwa sauti. Soma fungu kwa kurudia-rudia mpaka uweze kulisoma bila kukwama au kutua pasipofaa. Kisha soma mafungu mengine.
Kisha, ongeza mwendo wako wa kusoma. Baada ya kufahamu jinsi maneno yanavyoungana katika sentensi, utaweza kuona maneno mengi kwa wakati mmoja na kujua maneno yatakayofuata. Kufanya hivyo kutafanya uwe msomaji mzuri zaidi.
Kusoma kwa ukawaida kunaweza kuandaa mazoezi mazuri sana. Kwa mfano, bila kujitayarisha soma kwa sauti andiko la siku na maelezo yake kwa sauti; fanya hivyo kwa ukawaida. Zoeza jicho lako kutambua mafungu ya maneno yenye mawazo kamili-kamili badala ya kuona neno mojamoja tu.
Ili uwe na ufasaha katika mazungumzo, unahitaji kufikiri kabla ya kusema. Kila siku, jizoeze kufikiri kabla ya kuzungumza. Amua mambo unayotaka kusema, na jinsi utakavyoyasema; kisha zungumza. Usiongee haraka. Jaribu kusema jambo lote unalotaka kusema bila kutua au bila kulikatiza na jambo jingine. Inaweza kufaa kutumia sentensi fupi-fupi zilizo rahisi.
Maneno yanapaswa kutokea yenyewe tu ikiwa unajua vizuri jambo unalotaka kusema. Kwa kawaida, si lazima uchague maneno unayotaka kutumia. Hata unaweza kufanya mazoezi kwa kuhakikisha kwamba wazo lote unalotaka kusema li wazi akilini mwako ndipo ufikirie maneno unayotumia unapoendelea kuongea. Ukifanya hivyo na ukizingatia akilini wazo badala ya maneno unayosema, maneno yatatiririka tu, na mawazo yako yatatoka moyoni. Lakini mara tu uanzapo kufikiria maneno badala ya mawazo, unaweza kukwama-kwama unapoongea. Unaweza kufaulu kuongea kwa ufasaha ukifanya mazoezi, na hiyo ni sifa muhimu katika usomaji na usemaji mzuri.
Musa alipoagizwa amwakilishe Yehova mbele ya taifa la Israeli na mbele ya Farao wa Misri, aliona hawezi kutimiza mgawo huo. Kwa nini? Yeye hakuwa na ufasaha; huenda alikuwa na tatizo fulani la usemi. (Kut. 4:10; 6:12) Musa alitoa udhuru mwingi, lakini Mungu hakukubali hata udhuru mmoja. Yehova alimtuma Aroni kuwa msemaji, lakini pia Yehova alimsaidia Musa kusema. Mara nyingi na kwa matokeo mazuri, Musa alisema na watu mmoja-mmoja na pia vikundi vidogo na hata alihutubia taifa lote. (Kum. 1:1-3; 5:1; 29:2; 31:1, 2, 30; 33:1) Ukijitahidi kwa bidii na kumtumaini Yehova, wewe pia unaweza kumheshimu Mungu kwa usemi wako.