Kuielewa Hofu ya Kugugumiza
JE, WAWEZA kutofautisha kati ya msemaji mwenye ufasaha na mmoja anayeogopa kugugumiza? ‘Bila shaka,’ huenda ukajibu. Lakini fikiria kile ambacho mwandikaji Peter Louw aandika katika kitabu chake cha Kiafrikaan Hhhakkel (Kkkugugumiza): “Kwa kila mwenye kugugumiza ‘ajulikanaye,’ kwaweza kuwa na kumi wanaotaka kubaki bila kutambulika iwezekanavyo na kuna wale ambao huficha kizuizi chao cha usemi katika njia mbalimbali.” Kuficha kizuizi cha usemi? Hilo lawezekanaje?
Watu fulani wenye kigugumizi wameweza kuficha kizuizi chao kwa kufikiria kimbele maneno ambayo yamewasababishia matatizo katika siku zilizopita. Kisha, badala ya kulisema neno hilo, wanaunda upya sentensi au wanatumia neno tofauti lililo na maana sawa. Mume mmoja alificha kigugumizi chake kwa muda wa miaka 19 ya ndoa. Wakati mke wake alipojua ukweli, alimwuliza mtaalamu wa matibabu ya usemi: “Wafikiri ndiyo sababu hunifanya nipige simu, na sababu ya kunifanya sikuzote niagize chakula katika mikahawa, na sababu inayofanya asizungumze katika . . . mikutano?”
Fikiria pia, Gerard na Maria, wenzi waliooana wenye furaha kutoka Afrika Kusini.a Katika pindi kadhaa, Maria alikuwa akijaribu kumweleza mumewe kuwa yeye hujizuia kutoa maelezo katika mikutano ya funzo la Biblia kwa sababu ya kuogopa kugugumiza. “Upuuzi,” angesema bila kuthibitisha, “wewe si mwenye kigugumizi.” Gerard alikata shauri kwa kutegemea asili ya mke wake ambaye kwa kawaida ni mwongeaji sana. Ni hali fulani tu za kusema ambazo humfanya aogope kugugumiza. Gerard alijua hili kwa mara ya kwanza baada ya miaka mitano ya ndoa, naye akakiri kwamba: “Sikujua na sikuwa mwenye ufikirio.” Sasa, badala ya kumchambua, yeye humpongeza awapo jasiri kuzungumza mbele ya wasikilizaji wengi.
Kwa kueleweka, watu wengi wenye kigugumizi hutaabishwa na “hofu . . . nyakati fulani ni yenye kusumbua, mara nyingi ni yenye kuzidi sana” aeleza mwenye kigugumizi David Compton katika kitabu chake Stammering. “Wakati ambapo ni rahisi zaidi kutatizika, wakati ulio muhimu zaidi kwake kuwasiliana na wanadamu wenzake, kwa kuwafikia katika usemi, uwe ni mambo ya kawaida au ya kindani, katika hali kama hizo mwenye kigugumizi aweza kutarajia kuumizwa, ahisi kudhihakiwa. . . . Hata wale wanaokabiliana vizuri zaidi bado wanakiri kuwa wamefinyangwa na hofu yao, na kuwa haiwaachi kabisa kamwe.”
Hali Ambazo Zaweza Kuamsha Hofu
Mtu mwenye kigugumizi anapoombwa kujibu swali mbele ya wasikilizaji, kama vile katika darasa shuleni, mkutano wa kibiashara, au kikusanyiko cha kidini, hiyo inaweza kusababisha hangaiko ambalo laweza kutokeza kigugumizi kibaya sana. “Je, kuna wakati ufikiripo kuwa ni rahisi zaidi kunyamaza tu?” akaulizwa Rosanne mwenye miaka 15 kutoka Afrika Kusini katika mahojiano ya redio. Yeye alijibu, “mara nyingi, kwa kielelezo, katika darasa ninapokuwa na jibu zuri ambalo najua litanipa maksi nyingi lakini najua kuwa linahitaji jitihada kubwa kuzungumza.”
Mfanya-biashara mmoja aitwaye Simon pia alihojiwa katika programu hiyo ya redio iliyotajwa hapo juu. Kama Rosanne, Simon amefanya maendeleo kwa msaada wa tiba ya usemi. Lakini wakati mwingine angali ana vipindi vibaya vya kigugumizi. Hii yaweza kuzidishwa na mtazamo wa wasikilizaji wake. “Ukiwa katika mkutano wa wanakamati ambapo wapaswa kuzungumza sana na unakuwa na magumu ya kuzungumza, watu walioketi kuizunguka meza hukosa subira sana,” yeye aeleza.
Hofu ambayo mwenye kigugumizi anayo haipaswi kufikiriwa kuwa ni ile hofu ambayo mtu mwenye haya aweza kuwa nayo juu ya kuzungumza na watu asiowajua. Mfikirie Lisa, ambaye amekuwa akihudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kwa miaka miwili iliyopita. Katika mazungumzo madogo pamoja na marafiki, anaweza kuzungumza kwa ufasaha sana. Yeye pia hushiriki kwa bidii katika kazi ya kueneza-evanjeli ambayo inahusisha kuchukua nafasi ya kuwafikia watu usiowajua. Lakini ana hofu iliyo ya kawaida kwa watu wengi wenye kigugumizi—kuzungumza mbele ya wasikilizaji wengi. “Katika mikutano yetu,” Lisa aeleza, “mara chache mimi hufaulu kunyoosha mkono na kujibu swali. Ikiwa nitajibu kwa vyovyote, ni neno moja au sentensi fupi. Ingawa yaweza kuwa kidogo, ndiyo bora zaidi kwangu. Mara nyingi, majibu yako akilini na midomoni kwa kuwa kila wakati mimi hutayarisha kimbele. Lakini ulimi wangu hukataa tu kushirikiana.”
Hali iliyo mbaya zaidi kwa wenye kigugumizi fulani ni kusoma kwa sauti. Hili huwalazimu kutumia maneno ambayo kwa kawaida wangeyaepuka. “Katika mmoja wa mikutano yetu,” Lisa aendelea, “wakati fulani sisi huombwa huchukua zamu kusoma Maandiko yanayozungumziwa. Katika pindi kama hizo mimi huketi kwa hofu, nikitetemeka, nikingoja zamu yangu, bila kujua ikiwa nitaweza kusoma andiko au la. Nyakati fulani nasoma lakini siwezi kutamka neno fulani. Kisha naliruka tu na kuendelea kusoma.”
Kwa wazi, ufikirio wenye uangalifu wapaswa kutolewa kabla ya kumtia moyo mwenye kigugumizi asome kwa sauti. “Kitia-moyo” kama hicho chaweza kumfanya mwenye kigugumizi ajihisi vibaya zaidi. Badala ya hivyo, mtu kama huyo apaswa kupongezwa kwa uchangamfu kwa kufanya yote awezayo.
Wakati Unapojaribu Kusaidia
Kigugumizi ni tatizo lenye kutatanisha sana. Linalofaa kwa mmoja huenda lisifae kwa mwingine. Kwa kweli, watu wengi wenye kigugumizi ambao walipata kipindi cha “kupona” hurudiwa na tatizo baadaye. Utafiti zaidi umefanywa kuhusu kugugumiza kuliko tatizo jingine lolote la usemi. Na bado, wataalamu hawajapata kisababishi hususa. Kwa kweli, wengi hukubali kwamba mambo mengi huchangia kugugumiza. Kulingana na chunguzi za karibuni, nadharia moja ni kwamba kwatokana na mpangilio usio wa kawaida wa chembe za ubongo mapema maishani mwa mwenye kigugumizi. Kulingana na Madakt. Theodore J. Peters na Barry Guitar, katika kitabu chao cha mafundisho Stuttering—An Integrated Approach to Its Nature and Treatment, maoni ya karibuni kuhusu visababishi “yatakuwa yasiyotumika tena kadiri uchunguzi mwingi uendeleavyo kuujaza ujuzi wetu haba kuhusu kugugumiza.”
Kwa vile mwanadamu anajua machache sana kuhusu kugugumiza, kuna uhitaji wa kuwa mwangalifu wakati unapopendekeza mojawapo ya tiba nyingi kwa wale wanaoteseka kwa tatizo hilo. “Wengi walio na kigugumizi kibaya,” kitabu cha mafundisho kilicho juu chaongezea, “watapata nafuu ya kiasi tu. Watajifunza kuzungumza polepole zaidi au kugugumiza kwa urahisi zaidi, na kutosumbuka sana na tatizo hilo. . . . Kwa sababu ambazo hatuwezi kuzielewa, watu wachache wenye kigugumizi hawabadiliki sana kwa matibabu.”b
Matibabu yanaposhindwa kufanya kazi, wanatiba fulani wa usemi wamewalaumu wenye kigugumizi kwa kutokufanya jitihada zaidi. Mwanatiba mmoja alisisitiza: “Uwezekano tu wa kutofaulu huwa katika mwelekeo wa moyo nusunusu kwa upande wa mwenye kigugumizi.” Kuhusu madai kama hayo, mwandikaji David Compton alisema: “Sina maneno ya kuelezea hasira ambayo wenye kigugumizi huhisi kwa sababu ya maelezo kama hayo. Kwanza, kwa sababu maneno hayo ni dhahiri kuwa si ya kweli. Hakuna tiba moja ambayo yaweza kuwafaa wenye kigugumizi wote, na hata iliyo sawa kwa mwenye kigugumizi hususa inaweza kukosea sana. Pili, kwa kuwa wenye kigugumizi huishi wakihisi wameshindwa . . . Chochote kinachoongezea [kushindwa kwao] isivyo lazima, isivyo haki, ni uhalifu.”
Kuwapunguzia Mzigo
Kwa kawaida wenye kigugumizi hawataki kuhurumiwa. Hata hivyo, kuna mengi yawezayo kufanywa ili kuwapunguzia mzigo. Wanapogugumiza, usiangalie kando kwa kuaibika. Badala ya kuangalia mdomo wao, watazame kwenye macho. Kwa kawaida wao ni wenye hisia nyepesi kuelekea ishara za mwili za wasikilizaji wao. Ukionekana kuwa mtulivu, hiyo itasaidia kupunguza hofu yao. “Mwonyeshe mtu huyo kuwa umejitayarisha kumsikiliza kama tu vile ungekuwa tayari kumsikiliza mtu yeyote unayezungumza naye,” akasema mwanatiba wa usemi.
Walimu ambao wana mwanafunzi mwenye kigugumizi kati ya wanafunzi wao wanaweza kufanya mengi ili kumpunguzia hofu. Katika jarida la elimu la Afrika Kusini Die Unie, walimu walipewa shauri lifuatalo: “Watu wengi wenye kigugumizi hugugumiza kidogo zaidi wanapojua ya kwamba anayewasikiliza hatarajii ufasaha.”
Kulingana na jarida lililotajwa hapo juu, ni jambo la maana pia kwa mwalimu kujua hisia za mwanafunzi. Badala ya kuwaepuka wanafunzi kama hao kwa sababu ya aibu, walimu wanashauriwa kuzungumza nao na kuwatia moyo waeleze jinsi wanavyohisi kuhusu tatizo hilo. Kwa njia hii mwalimu aweza kupata kujua ni hali gani za kuzungumza ambazo mwanafunzi anaogopa zaidi. “Asilimia 80 ya ufasaha wake wa kusema wakutegemea wewe,” jarida hilo laripoti. Ufasaha wake utaboreka akijua kwamba anakubalika ijapokuwa ana tatizo hilo. Jarida hilo laeleza hivi zaidi: “Mazingira yenye utulivu yenye kukazia fikira masomo darasani hayatamfaidi mwenye kigugumizi tu bali pia wengine katika darasa.”
Kwa hakika, madokezo haya yaweza kubadilikana ili yafae kwa matokeo katika hali zinazohusisha kuwafunza watu wazima.
Muumba Wetu Aelewa
Muumba wetu, Yehova Mungu, aelewa kikamili kutokamilika kwa kibinadamu. Alimwagiza Musa awe msemaji wake katika kuwaongoza Waisraeli kutoka Misri. Alifanya hivi akijua vizuri kuwa Musa alikuwa na kasoro ya usemi iliyofanya iwe vigumu kwake kuwasiliana. Mungu pia alijua kuwa, kwa upande mwingine, Aroni, ndugu ya Musa, alikuwa msemaji mwenye ufasaha. “Najua ya kuwa yeye aweza kusema vizuri,” Mungu akasema. (Kutoka 4:14) Hata hivyo, Musa alikuwa na sifa nyingine za maana zaidi, kama vile uaminifu-mshikamanifu, fadhili, imani, na upole wa tabia. (Hesabu 12:3; Waebrania 11:24, 25) Mungu alishikamana na chaguo lake la Musa kuwa kiongozi wa watu Wake hata ingawa Musa alikuwa na vipingamizi. Wakati huohuo, Mungu alifikiria hofu za Musa na akamweka rasmi Aroni awe msemaji wa Musa.—Kutoka 4:10-17.
Twaweza kumwiga Mungu kwa kuonyesha uelewevu. Watendee wenye kigugumizi kwa adhama, na usiache hitilafu ya usemi ikuzuie kuona ubora wa mtu. Kielezi cha hilo ni jambo lililoonwa la msichana mdogo na baba yake mwenye kigugumizi. Baba huyo alijifunza njia ya kusoma kwa ufasaha zaidi. Usiku mmoja, aliijaribu kwa kumsomea binti yake mwenye umri wa miaka sita hadithi na akajihisi vizuri sana kwa ajili ya ufasaha wake.
“Sema vizuri, baba,” akasema wakati baba yake alipomaliza kusoma.
“Nasema vizuri sana,” akajibu kwa ghadhabu.
“La,” akasisitiza, “sema kama kawaida.”
Ndiyo, msichana huyu mdogo alimpenda baba yake jinsi alivyokuwa, hata na kasoro yake ya usemi. Kwa hiyo wakati ujao unaposhughulika na mtu mwenye kigugumizi, kumbuka kuwa mtu huyo aweza kuwa na mawazo yenye faida na sifa zenye kutamanika. Kwa hakika ana hisia. Kuwa mwenye subira na mwenye kuelewa.
[Maelezo ya Chini]
a Majina fulani katika makala hii yamebadilishwa.
b Matazamio ya kupata nafuu ni bora kwa watoto kuliko kwa watu wazima. Mwanatiba wa usemi mwenye uzoefu Ann Irwin aeleza katika kitabu chake Stammering in Young Children: “Watatu kati ya watoto wanne hushinda kigugumizi chao wenyewe. Ikiwa mtoto wako ni mmoja wa wale asilimia ishirini na tano ambao hawashindi kigugumizi chao wenyewe, kuna uwezekano mkubwa kuwa atakishinda kwa Tiba ya Kuzuia.”
[Picha katika ukurasa wa 25]
Mwenye kigugumizi huenda akaogopa kuzungumza hadharani
[Picha katika ukurasa wa 26]
Uwe mwenye subira ikiwa mwenye kigugumizi ana tatizo anapozungumza nawe
[Picha katika ukurasa wa 27]
Kwa kawaida wenye kigugumizi huogopa simu