Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Kuutazama Ulimwengu Mimi ni mwandishi wa gazeti la habari, na wengi wa wafanyakazi wenzangu hupenda kusoma makala “Kuutazama Ulimwengu” ili kupata mawazo kwa ajili ya kazi yao. Mimi mwenyewe naungama kwamba nimechochewa na makala fulani. Hasa mimi huvutiwa na watafsiri na wasahihishaji wenu. Viwango vya juu vya lugha vya namna hiyo si kawaida katika vyombo vya habari.
J. B., Czechia
Miaka kadhaa iliyopita nilipoanza kusoma Amkeni!, sikufurahia sana ile sehemu “Kuutazama Ulimwengu.” Sasa naiona kuwa yenye kuelimisha kwelikweli. Kwa kweli, matukio mengi ya ulimwengu ambayo sijayaona katika taarifa za habari za televisheni yametajwa katika sehemu hiyo ya “Kuutazama Ulimwengu.” Endeleeni kufanya kazi hiyo nzuri!
I. K. M. C., Brazili
Magonjwa ya Kuambukiza Mfululizo “Magonjwa Ya Kuambukiza—Je, Yataisha Wakati Wowote?” (Novemba 22, 1997) ulitaarifu hivi: “Maradhi ya kuambukiza yabaki yakiwa kisababishi kikuu cha vifo ulimwenguni, yakiua zaidi ya watu milioni 50 katika mwaka wa 1996 pekee.” Hata hivyo, ripoti ya Shirika la Afya Ulimwenguni yasema kwamba kuhusu vifo zaidi ya milioni 52 katika mwaka wa 1996, zaidi ya milioni 17 vilisababishwa na maradhi ya kuambukiza au maradhi yasababishwayo na vimelea.
B. B., Marekani
Maelezo yetu yalitegemea gazeti la habari la Kijerumani “Nassauische Neue Presse.” Kwa wazi Shirika la Afya Ulimwenguni lilinukuliwa kimakosa na makala hii ya gazeti la habari. Kwa hiyo twathamini ufafanuzi huu.—Mhariri.
Kugugumiza Asanteni kwa makala “Kuielewa Hofu ya Kugugumiza.” (Novemba 22, 1997) Kutanikoni mwetu tuna vijana wachache walio na tatizo hili, na sikuzote sijajihisi huru kushirikiana nao. Kwa hiyo nilifurahia kusoma madokezo yafanyayo kazi mliyotupatia ili kutusaidia kushughulika na wenye kigugumizi. Mlituchochea kuwategemeza watu wa namna hiyo, na kutuonyesha namna ya kufanya hivyo.
Y. N., Japani
Katika darasa letu shuleni, wanafunzi wawili wana kigugumizi. Hawatoi majibu kamwe darasani, na kama ilivyotaja makala yenu, wanapoombwa wasome kwa sauti, huonekana kuwa wenye wasiwasi. Asante kwa makala yenu, naweza kuelewa vema zaidi hofu wanayohitaji kushinda ili kuzungumza darasani.
S. L., Ujerumani
Nina umri wa miaka 16 na nina kigugumizi. Kwa unyoofu wa moyo nataka kuwashukuru kwa ajili ya kitia-moyo nilichopata kwa kusoma makala hiyo. Nyakati nyingine sisi huvunjika moyo kwa sababu hatuwezi kufanya yote ambayo tungependa kufanya. Kwa hiyo inapendeza kuona jinsi Yehova hufikiri juu yetu na kututia moyo. Natumaini kila mtu atakayesoma makala hiyo atasaidiwa kuthamini jitihada zinazofanywa na wenye kigugumizi.
S. D. A., Italia
Makala hiyo ilifumbua kumbukumbu nyingi sana za kuhuzunisha. Lakini pia ilinifanya kung’amua jinsi Yehova hujali na jinsi ambavyo amenibariki kwa miaka iliyopita. Nilipobatizwa nikiwa na umri wa miaka 11, tamaa yangu kubwa ilikuwa kumsifu Yehova nikiwa msemaji wa watu wote. Nilifikiri ningehitaji kungojea ulimwengu mpya wa Mungu ili kufikia mradi huo. Lakini kwa miaka zaidi ya 37 iliyopita, nimepata pendeleo la kutoa hotuba nyingi sana za watu wote vilevile kwenye makusanyiko na mikusanyiko ya wilaya.
R. F. D., Uingereza
Kwa sababu ya hofu yangu ya kugugumiza, mimi sitoi maelezo katika mikutano ya kutaniko. Pia mimi huwa na wasiwasi juu ya kugugumiza ninapokuwa katika kazi ya kuhubiri mlango hadi mlango, hasa ninapohubiri na mtu mwenye ufasaha. Makala hii ilinisaidia kuona kwamba Yehova huelewa matatizo yangu.
C. C. L., Brazili