Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g98 1/22 kur. 13-15
  • Jinsi Ninavyokabiliana na Kugugumiza

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Jinsi Ninavyokabiliana na Kugugumiza
  • Amkeni!—1998
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Thawabu za Kuwa na Mwelekeo Unaofaa
  • Jinsi Wengine Wanavyoweza Kusaidia
  • Mapendeleo Makubwa Zaidi ya Utumishi
  • Jinsi ya Kukabiliana na Kigugumizi
    Amkeni!—2010
  • Kuielewa Hofu ya Kugugumiza
    Amkeni!—1997
  • ‘Na Ndimi za Wenye Kigugumizi Zitanena’
    Amkeni!—1996
  • Nimeacha Kugugumiza!
    Amkeni!—1998
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1998
g98 1/22 kur. 13-15

Jinsi Ninavyokabiliana na Kugugumiza

Kama ilivyosimuliwa na Sven Sievers

NIMEKUWA nikigugumiza tangu nilipokuwa mtoto. Ninapotazama yaliyopita, ninathamini mfikio wa wazazi wangu kwa hilo tatizo. Nilipogugumiza, sikuzote walijaribu kusikiliza kwa makini nililotaka kusema badala ya kusahihisha namna yangu ya kusema. Kulingana na wanatiba wa usemi, wazazi ambao hukazia uangalifu kugugumiza kwa watoto wao huenda wakaongezea hilo tatizo.a

Mama yangu alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova nilipokuwa na umri wa miaka mitatu. Katika miaka yangu ya utineja niliamua kufuata kielelezo chake na nilisaidiwa kujifunza Biblia kikamili. Katika Julai 24, 1982, nilibatizwa nikiwa mtumishi aliyejiweka wakfu wa Mungu kwenye mkusanyiko katika Neumünster, Ujerumani. Baadaye, nilihamia Afrika Kusini, ambapo niliendelea kushiriki katika kazi ya kuhubiri waziwazi, ambayo Wakristo wa kweli wote wanaamriwa kuishiriki. (Mathayo 28:19, 20) Waweza kushangaa, nawezaje kufaulu nikiwa mwenye kugugumiza?

Thawabu za Kuwa na Mwelekeo Unaofaa

Lazima nikiri kwamba nyakati nyingine ni vigumu kudumisha mwelekeo unaofaa, lakini nimepata ya kwamba kuwa na mwelekeo unaofaa husaidia. Uhakika ni kwamba kwa njia fulani ninaweza kuwasiliana sikuzote. Ikiwa si kwa kuzungumza, nawasiliana kwa kuandika ujumbe au kwa kuonyesha tu wengine fasihi za Biblia. Mfikio unaofaa hunisaidia kushinda tatizo la kuanzisha mazungumzo. Mimi hujaribu kurahisisha utangulizi wangu. Mwanzoni mwa mazungumzo, mimi humwacha mwenye nyumba azungumze kadiri awezavyo. Watu hupenda kuzungumza, na hili hunipa fursa ya kujua namna yao ya kufikiri. Kisha, naendeleza mazungumzo na mambo ambayo huwapendeza, nikikazia ujumbe wa Biblia. Kukazia fikira yale wanayosema hunisaidia kusahau tatizo langu la usemi, na kugugumiza mara chache.

Mfikio unaofaa hunisaidia pia kutoa maelezo katika mikutano ya Kikristo. Nimepata ya kwamba kadiri nishirikivyo zaidi katika mazungumzo ya Biblia, ndivyo wasikilizaji na kiongozi hunizoea na kusikiliza yale nisemayo badala ya jinsi ninavyoyasema.

Ili kuonea shangwe mafanikio, nalazimika kuendelea kujaribu. Hii hunizuia nisishindwe na kujihurumia na kuwa mndani. Kupigana na hali ya kujihurumia ni pigano linaloendelea. Imesemekana kwamba mtu akianguka kutoka kwa farasi, ni jambo linalofaa kwake kurudi kwenye farasi ili asipoteze uhakika. Kwa hiyo ikiwa nalazimika kuacha kusema wakati wa elezo kwa sababu nimekwama kabisa, mimi hujaribu kupanda tena juu ya farasi, kusema kitamathali, kwa kutoa elezo tena kwenye fursa inayofuata.

Jinsi Wengine Wanavyoweza Kusaidia

Wakati nilazimikapo kupiga simu au kuuliza wageni habari, mimi huthamini msaada unaotolewa kwa busara. Lakini watu fulani hupita kiasi katika tamaa yao ya kusaidia, na hunitendea kama mtoto ambaye hawezi kufanya maamuzi.

Mimi pia hufurahia msaada wa mke wangu mpendwa, Tracy. Kabla hajatumika kama “kinywa” changu, tunazungumzia hali hiyo kwa urefu na yeye hujua ninalotaka litimizwe. (Linganisha Kutoka 4:10, 14, 15.) Katika njia hiyo, ananionyesha staha nikiwa mumewe, na kunifanya nihisi kuwa bado ninadhibiti maisha yangu mwenyewe.

Msaada mwingine mkubwa umekuwa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Kwenye mkutano huu wa kila juma, wanafunzi hushiriki katika usomaji wa Biblia hadharani na kutoa hotuba fupi juu ya vichwa vya Biblia. Nilishangaa kuona kwamba mara nyingi naweza kusoma na kuzungumza vizuri kabisa mbele ya wasikilizaji. Ikiwa sikuwa nimejiandikisha katika shule, labda singalitambua kamwe uwezo huu.

Wakati ninapokuwa na migawo katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, limekuwa jambo lenye kutia moyo hasa wakati mfunzi anapokaza fikira juu ya yale ninayosema na si jinsi nilivyoyasema. Nimenufaika sana kutokana na Kiongozi cha Shule ya Huduma ya Kitheokrasi,b hata ingawa sehemu nyingine za kitabu hiki hutokeza sai kubwa zaidi kwa wenye kigugumizi kuliko wale wenye usemi wa kawaida. Kwa kielelezo, nyakati nyingine, kwa sababu ya kiasi cha kugugumiza, ninashindwa kumaliza hotuba yangu kwa wakati uliogawiwa. Ingawa hivyo, inanitia moyo sana, wakati mfunzi anapokazia hoja ambazo naweza kufanyia kazi.

Mapendeleo Makubwa Zaidi ya Utumishi

Katika wakati uliopita, nilikuwa na pendeleo la kusoma hadharani kutoka katika kichapo cha Kikristo ambacho sisi hujifunza kwenye mikutano yetu. Pia nilikuwa na pendeleo la kuongoza hilo funzo wakati ambapo hakukuwa na mhudumu mwingine yeyote anayestahili, na leo mimi hufanya hivyo kwa ukawaida. Ijapokuwa mwanzoni nilikuwa na wasiwasi, nimejionea msaada wa Mungu katika kutekeleza migawo ya namna hiyo.

Hata hivyo, kwa miaka mingi, fursa zangu za kusoma au kufundisha kutoka kwenye jukwaa la kutaniko zilikuwa chache. Hili lilieleweka, kwa kuwa kulikuwa na nyakati ambazo ilinichukua muda mrefu sana kujieleza. Kwa hiyo nilitumia nishati zangu kwa ukamili katika kutekeleza migawo mingine. Hapo kwanza, nilitumikia kama msaidizi katika kutunza ugavi wa kutaniko wa magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Ndipo baada ya kuwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma nilitunza ugavi wa Biblia, vitabu, na fasihi nyingine. Baadaye, niligawiwa kutunza kadi za maeneo ambazo hutumika katika kazi yetu ya kutolea watu wote ushahidi. Kukazia fikira migawo hii, kujaribu kufanya kazi kwa bidii, kuliniletea shangwe nyingi.

Kwa miaka minane iliyopita, nimetumikia pia nikiwa mweneza-evanjeli wa wakati wote pamoja na Tracy. Bila shaka, Yehova amenibariki katika upande huu pia. Kwa kweli, nyakati nyingine mimi hustaajabu kama Yehova hutumia udhaifu wangu wa kigugumizi. Kati ya watu watano ambao nimekuwa na pendeleo la kuwasaidia wafikie kuwa Wakristo waliojiweka wakfu, wawili ni wenye kugugumiza.

Bado mimi hukumbuka kwa shangwe siku niliyowekwa rasmi kutumikia nikiwa mzee wa kutaniko. Ingawa uwezo wangu wa kufundisha kutoka jukwaani ni wenye mipaka, mimi hujaribu kukaza fikira juu ya kuwasaidia wengine kibinafsi. Kigugumizi hakiwekei mpaka uwezo wangu wa kufanya utafiti wa Maandiko ili kusaidia washiriki wa kutaniko wanaokabili matatizo mazito.

Kwa miaka mitano iliyopita, nimepewa pendeleo la kushughulikia hotuba zaidi na zaidi. Mbali na kutoa hotuba kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, nimeweza kushughulikia matangazo mafupi katika mikutano mingine. Pole kwa pole ufasaha wangu uliboreshwa. Lakini ndipo nikarudiwa na hali hii mbaya tena. Nikiwa nimehangaika, nilifikiri, ‘Sitapewa migawo mingine tena,’ lakini kwa mshangao, jina langu lilikuwa kwenye ratiba iliyofuata! Mwangalizi-msimamizi wa kutaniko letu alisema kwamba ikiwa ningelemewa kabisa na kushindwa kuendelea, naweza tu kumtazama na atapanda jukwaani na kuendelea. Nilitumia uandalizi huu wenye upendo mara moja au mbili, lakini sijahitaji kufanya hivyo katika miezi ya juzijuzi. Kadiri usemi wangu ulivyoboreka, niligawiwa sehemu ndefu zaidi, kutia ndani hotuba za watu wote. Niling’amua tu kikamili maendeleo niliyokuwa nimefanya wakati ambapo karibuni niliombwa kushiriki katika maonyesho mawili kwenye kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova.

Kwa kweli, sielewi kikamili kwa nini usemi wangu umekuwa bora. Pia, waweza kuzorota tena katika siku za baadaye. Kwa kweli, ingawa yaonekana kuwa nimefanya maendeleo hususa katika kusema kutoka kwenye jukwaa, nimekuwa na tatizo hilo tena wakati ninaposema na watu kibinafsi. Kwa hiyo haimaanishi kwamba nimefanikiwa kabisa kushinda kigugumizi. Wakati nipatwapo na hali hii tena, mimi hujaribu kujikumbusha kwamba nahitaji kukubali kupungukiwa kwangu na ‘kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wangu.’—Mika 6:8.

Lolote lile litakalokuja wakati ujao, nitafuliza kujaribu, nikijua kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu unaokaribia, kugugumiza kutaondolewa kabisa. “Ndimi zao wenye kigugumizi,” husema Biblia, “zitakuwa tayari kunena sawasawa.” Nina hakika kwamba hili litakuwa kweli kihalisi na kiroho na kwamba hata “ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isaya 32:4; 35:6.

[Maelezo ya Chini]

a Ona makala “Kuielewa Hofu ya Kugugumiza,” katika toleo la Novemba 22, 1997.

b Kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiwa na mke wangu, Tracy

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki