Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g96 8/22 kur. 21-23
  • ‘Na Ndimi za Wenye Kigugumizi Zitanena’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Na Ndimi za Wenye Kigugumizi Zitanena’
  • Amkeni!—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tatizo Langu la Usemi
  • Natafuta Msaada
  • Nakutana na Mashahidi wa Yehova
  • Naelekea Kupata Uhakika Zaidi
  • Nakabili Magumu ya Kipekee
  • Jinsi Ninavyokabiliana na Kugugumiza
    Amkeni!—1998
  • Nilitawalwa na Imani Katika Mungu Nchini Ukomunisti
    Amkeni!—1996
  • Jinsi Matumaini Yangu Yalivyotimizwa
    Amkeni!—2002
  • Niliacha Kupiga Watu Barabarani Nikawa Mhudumu Mkristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1996
g96 8/22 kur. 21-23

‘Na Ndimi za Wenye Kigugumizi Zitanena’

ILIKUWA ni kipindi cha alasiri cha siku ya kusanyiko la pekee la Mashahidi wa Yehova katika Chekoslovakia (sasa inaitwa Jamhuri ya Cheki), na mamia ya watu yalikuwa yamekutanika ili kupokea mafundisho ya Biblia. Nilikuwa nimesimama nyuma ya jukwaa nikipitia sehemu yangu katika programu. Haikuwa sehemu kubwa. Mashahidi wawili wachanga walipaswa kusimulia mambo yaliyoonwa, nami ningekuwa tu mwenyekiti wa sehemu hiyo. Asubuhi hiyo nilihisi mkazo wa ndani, lakini sasa ulikuwa unaongezeka. Nikahisi nimepooza kihalisi, nikawa na wasiwasi mwingi, hata nisiweze kusema.

Huenda unafikiri kwamba karibu kila mtu angekuwa na wasiwasi katika hali hiyo. Lakini hali yangu haikuwa wasiwasi tu. Ebu niwaeleze sababu.

Tatizo Langu la Usemi

Nikiwa na umri wa miaka 12, nilianguka na kujeruhiwa kichwa, shingo, na uti wa mgongo. Baada ya kisa hicho, nilikuwa na kigugumizi kidogo au kupata ugumu wa kufanyiza maneno fulani, hasa maneno yanayoanza na herufi p, k, t, d, na m. Nyakati nyingine hata nilikuwa nikishindwa kusema.

Tatizo hilo halikunisumbua sana wakati huo; lilionekana kuwa kisumbufu tu. Lakini miaka ilipopita, nikawa na hofu kubwa ya usemaji wowote mbele ya watu. Pindi moja nilizimia shuleni nikitoa ripoti. Na nyakati nyingine nilipokuwa nikinunua vitu, wauzaji wangeniuliza kile nilichotaka, na ningeshindwa kuwajibu. Nikiwa nimesimama hapo niking’ang’ana kusema, wao wangekasirika zaidi: “Fanya haraka. Siwezi kukungoja mchana kutwa. Wanunuzi wengine wanangoja.” Basi, ningeshindwa kununua vitu nilivyohitaji.

Miaka niliyokuwa shuleni ilikuwa migumu sana. Nilipokuwa natoa ripoti za hotuba, wanashule wenzangu wangecheka kigugumizi changu. Lakini, nilihitimu shule ya sekondari na katika 1979 nikaendelea na masomo katika chuo fulani kikuu katika Prague, Chekoslovakia. Kwa kuwa nilipenda riadha, nilichukua mtaala wa kuwa mwalimu wa mazoezi ya mwili. Lakini ningetimizaje mradi wangu? Nijapokuwa na tashwishi, niliazimia kuendelea mbele.

Natafuta Msaada

Lazima kulikuwa na njia ya kuondoa tatizo langu la usemi. Hivyo baada ya kuhitimu chuo kikuu, nikaamua kutafuta msaada wa wataalamu. Nikapata kliniki moja katika Prague inayoshughulikia hasa matibabu ya matatizo ya usemi. Nilipoenda mara ya kwanza, muuguzi mmoja alisema: “Tatizo lako la akili ni baya sana!” Niliumia sana moyoni kufikiria kwamba wao waliniona kuwa mwenye tatizo la akili, hata ingawa wataalamu wanakubali kwamba kigugumizi si tatizo la akili. Haikuchukua muda mrefu kutambua kwamba nilikabili ugumu wa kipekee sana: Nilikuwa kijana mwenye umri wa miaka 24, na wagonjwa wengine wote walikuwa watoto.

Upesi, wafanyakazi wote, kutia ndani mwanasaikolojia, wakaanza kunisaidia. Walijaribu kila kitu. Pindi moja walinikataza nisiongee na mtu yeyote kwa majuma matano. Wakati mwingine, waliniruhusu niongee kwa sauti ya chini tu na polepole s-a-n-a. Ingawa njia hiyo ilisaidia, pia ilifanya nibandikwe jina Mzuzua Nyoka kwa sababu wengi walilala usingizi nilipokuwa nikitoa ripoti zangu.

Nakutana na Mashahidi wa Yehova

Siku moja ya kiangazi katika 1984, nilipokuwa nikitembea mjini, wanaume wawili wachanga walinijia. Si jinsi walivyovalia tu iliyonishtua bali kile walichosema. Walisema kwamba Mungu ana serikali, Ufalme, ambayo itamaliza matatizo yote ya wanadamu. Wakanipa nambari zao za simu, nami baadaye nikawapigia simu.

Wakati huo Mashahidi wa Yehova hawakutambuliwa kuwa shirika halali la kidini katika Chekoslovakia. Lakini, baada ya muda mfupi upendezi wangu ukakua hivi kwamba nikaanza kuhudhuria mikutano yao. Ningeweza kuhisi upendo na hangaiko ambalo Mashahidi walikuwa nalo kwa mmoja na mwenzake.

Naelekea Kupata Uhakika Zaidi

Msaada kwa tatizo langu la usemi ukaja katika kile kinachoitwa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, shule ambayo hufanywa kila juma katika kila kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Nilihimizwa nijiunge na shule hiyo, nikafanya hivyo. Kwa kutegemea madokezo yaliyo katika mojayapo vitabu vya mafundisho vya shule hiyo, Kiongozi cha Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, nilifanyia kazi sifa za usemi kama vile ufasaha wa kusema, matamshi, kukazia maana, na ubadilifu wa sauti.a

Hotuba yangu ya kwanza nikiwa mwanafunzi, ambayo ilikuwa usomaji wa Biblia, haikufaulu. Nilikuwa na wasiwasi sana na karibu nishindwe kurudi nyumbani. Nilishukuru kama nini kwa kitulizo cha maji moto niliyoyaogea!

Baada ya hotuba hiyo ya kwanza, mwangalizi wa shule kwa fadhili alianza kunishughulikia kibinafsi. Hakunipa tu mashauri yenye kujenga bali alinipongeza vilevile. Hilo lilinitia moyo niendelee kujaribu. Muda mfupi baadaye, katika 1987, nikawa Shahidi aliyebatizwa. Miezi michache baadaye, nilihama Prague na kwenda mji mmoja mdogo unaoitwa Žďár nad Sázavou. Kikundi kidogo cha Mashahidi waliokuwa huko kikanikaribisha kwa uchangamfu. Wao pia walikubali usemi wangu ambao bado ulikuwa ukisita-sita, na hilo likainua kujistahi kwangu.

Baada ya muda mfupi, nilianza kuongoza kikundi kidogo cha funzo la Biblia, kisha nikatoa hotuba yangu ya kwanza ya watu wote iliyotegemea Biblia. Hatimaye, baada ya badiliko la serikali katika Chekoslovakia, nikaanza kutoa hotuba hizo katika makutaniko jirani. Nikiwa katika mazingira nisiyoyajua tatizo langu la usemi likarudi. Lakini sikufa moyo.

Nakabili Magumu ya Kipekee

Siku moja mzee mmoja Mkristo alinialika mahali pake pa kazi. Akasema: “Petr, nina habari njema kwako! Tungependa ushiriki katika kusanyiko la mzunguko linalokuja.” Nikahisi kuzimia hata ikanibidi niketi. Rafiki yangu alivunjika moyo nilipokataa.

Nilisumbuka sana kwa kukataa. Nikashindwa kuondosha jambo hilo akilini. Wakati wowote kumtumaini Mungu kulipotajwa kwenye mikutano ya Kikristo, kule kukataa kungerudi kunifadhaisha. Gideoni, ambaye kwa mwelekezo wa Mungu alikabili jeshi lote la Wamidiani akiwa na wanaume 300 pekee, nyakati nyingine alirejezewa kwenye mikutano. (Waamuzi 7:1-25) Huyu alikuwa mtu aliyemtumaini Mungu wake, Yehova kikweli! Je, nilikuwa nimeiga kielelezo cha Gideoni nilipokataa mgawo huo? Kwa kweli, sikufanya hivyo. Niliona aibu sana.

Lakini, ndugu zangu wa Kikristo hawakuchoka na mimi. Wakanipa fursa nyingine. Nilialikwa kushiriki katika programu nyingine ya siku ya kusanyiko la pekee. Nilikubali wakati huu. Ingawa nilishukuru sana kwa kupata pendeleo hili, lakini kwa kusema kweli, wazo la kusema mbele ya jumba lililojaa watu lilinitia hofu. Ilikuwa lazima nifanye bidii ya kumtumaini Yehova zaidi. Lakini kwa njia gani?

Kwa kufikiria sana imani na tumaini ambalo Mashahidi wengine walikuwa nalo kwake. Kufanya hivi kuliniimarisha. Hata barua iliyoandikwa na Verunka mwenye umri wa miaka sita, binti ya rafiki mmoja, ilikuwa kielelezo chema kwangu. Yeye aliandika: “Septemba, nitaenda shuleni. Sijui itakuwaje kwa habari ya wimbo wa taifa. Naamini kwamba Yehova atanipigania, kama alivyopigania Israeli.”

Hayo ni baadhi tu ya matukio yaliyoongoza kwenye kipindi cha alasiri cha siku ya kusanyiko la pekee nilichotangulia kutaja. Nilikuwa nimesali kwa bidii. Sasa sikuhangaikia sana ufasaha wangu wa usemi kama nilivyohangaikia kusifu jina kuu la Mungu mbele ya umati mkubwa.

Basi nikasimama mbele ya kikuza-sauti, nikikabili mamia ya watu. Kisha, nikitambua kwamba ujumbe ni muhimu kuliko mjumbe, nikapumua kwa undani nikaanza. Baadaye, nikachukua wakati nichanganue hali. Je, nilikuwa na wasiwasi? Ndiyo, hata nilikuwa na kigugumizi mara chache. Lakini, bila utegemezo wa Mungu nilijua kwamba singeweza kusema kamwe.

Baadaye nilianza kufikiria jambo fulani ambalo ndugu mmoja Mkristo aliniambia pindi moja: “Furahi kwamba una tatizo la kigugumizi.” Nilishangaa sana wakati aliposema maneno hayo. Angewezaje kusema jambo kama hilo? Nikifikiria, sasa naelewa alichomaanisha. Tatizo langu la usemi lilinifanya nimtegemee Mungu kuliko kujitegemea.

Miaka michache imepita tangu alasiri ya siku hiyo ya kusanyiko la pekee. Katika miaka hiyo michache nimepata mapendeleo mengine ya kusema mbele ya umati mkubwa. Niliwekwa rasmi kuwa mzee Mkristo katika Žďár nad Sázavou na pia painia, kama wahudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova wanavyoitwa. Ebu wazia! Kisha nikatumia muda wa saa mia moja kila mwezi nikisema na wengine kuhusu Ufalme wa Mungu, bila kutaja wakati niliotumia kila juma nikifundisha kwenye mikutano ya Kikristo. Na sasa natumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko, nikitoa hotuba kwa kutaniko tofauti kila juma.

Moyo wangu hujaa sana uthamini wakati wowote nisomapo unabii huu hasa katika kitabu cha Biblia cha Isaya: “Na ndimi zao wenye kigugumizi zitakuwa tayari kunena sawasawa.” (Isaya 32:4; Kutoka 4:12) Kwa kweli Yehova amethibitika kuwa nami, akinisaidia “kunena sawasawa” kwa heshima, sifa, na utukufu wake. Nimeridhika nami ni mwenye furaha kuweza kumsifu Mungu wetu mwenye rehema sana.—Kama ilivyosimuliwa na Petr Kunc.

[Maelezo ya Chini]

a Kilichotangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki