Nilitawalwa na Imani Katika Mungu Nchini Ukomunisti
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA ONDREJ KADLEC
KATIKA kiangazi cha 1966, nilikuwa nikiongoza safari ya kuona mji wangu wa nyumbani—Prague, Chekoslovakia. Nikiwa mwenye bidii katika imani yangu mpya, niliongea juu ya Mungu huku nikionyesha kile kikundi makanisa na mahekalu ya mji wetu yenye kupendeza.
“Je, wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova?” profesa wa mambo ya kiuchumi Mmarekani akauliza.
“La,” nikajibu. “Sijapata kamwe kusikia juu ya Mashahidi wa Yehova. Mimi ni Mkatoliki wa Kiroma.”
Kuwa Mwamini Mungu
Nililelewa na wazazi waliojulikana sana katika nyanja za elimu, siasa, na tiba. Muda mfupi baada ya kuzaliwa kwangu katika 1944 na baada ya kumalizika kwa Vita ya Ulimwengu 2 mwaka uliofuata, baba yangu akawa Mkomunisti. Hata alikuwa mwanzilishi mwenzi wa harakati za kuanzisha upya Ukomunisti, na katika 1966 akawa mkuu wa Chuo Kikuu cha Mambo ya Uchumi kilichoko Prague. Miaka kadhaa baadaye, aliwekwa rasmi kuwa waziri wa elimu wa Chekoslovakia, ambayo kwa wakati huo ilikuwa nchi ya Kikomunisti na isiyoamini kuwepo kwa Mungu.
Mama alikuwa mwanamke mnyoofu sana na mwenye kipawa. Alikuwa mpasuaji wa macho, aliyesemekana kuwa bora zaidi katika nchi. Hata hivyo, yeye alitoa matibabu kwa wale wenye uhitaji bila malipo. Yeye alikuwa akisema: “Kipawa chochote alichokabidhiwa mtu, lazima hicho kitumiwe kwa faida ya jamii na taifa.” Yeye hata hakuchukua livu ya uja-uzito nilipozaliwa ili apatikane kwenye kliniki yake.
Nilitarajiwa kufanya vyema kimasomo. Baba angeuliza: “Je, kuna yeyote afanyaye vizuri kukushinda?” Nikaja kufurahia hayo mashindano, kwa kuwa mara nyingi nilishinda tuzo za kimasomo kwa kuwa na matokeo mazuri. Nilijifunza Kirusi, Kiingereza, na Kijerumani na kusafiri sana katika ulimwengu wa Kikomunisti na hata mbali zaidi. Nilifurahia kubisha imani za kidini kuwa ushirikina wenye upumbavu. Na ingawa nililikubali kabisa lile wazo la kutoamini kuwepo kwa Mungu, nilikuja kuchukia lilivyotumiwa kisiasa.
Safari ya kwenda Uingereza katika 1965, nilipokuwa na umri wa miaka 21 tu, ilikuwa na matokeo makubwa kwangu. Nilikutana na watu waliotetea imani yao katika Mtu Mkuu Kuliko Wote kwa uthabiti na kiakili. Baada ya kurudi Prague, Mkatoliki wa Kiroma niliyemjua akadokeza: “Usisome juu ya Ukristo. Soma Biblia.” Hilo ndilo nililofa2nya. Ilinichukua miezi mitatu kuimaliza.
Kilichonipendeza ni jinsi waandikaji wa Biblia walivyoandika jumbe zao. Walikuwa wanyoofu na waliandika juu ya makosa yao wenyewe. Nilikuja kuamini kwamba wakati ujao mtukufu waliozungumza juu yao ulikuwa jambo ambalo Mungu halisi tu ndiye angeweza kufikiria na kuandaa.
Baada ya miezi kadhaa ya kujifunza na kuitafakari Biblia kivyangu, nilihisi nikiwa tayari kukabili baba yangu na rafiki zangu. Nilijua wangeipinga imani yangu mpya. Baada ya hilo, nikawa mgeuza imani mwenye bidii. Yeyote aliyekuwa karibu na mimi—kama yule profesa Mmarekani aliyetajwa mwanzoni—alilazimika kukabiliana na hali yangu ya kugeuza imani. Hata niliangika kisalaba kwenye ukuta juu ya kitanda changu ili kumjulisha kila mtu juu ya imani yangu.
Hata hivyo, mama alipinga kwamba singeweza kamwe kuwa Mkristo, kwa kuwa nilifanana sana na baba yangu, Mkomunisti mwenye bidii. Na bado, nikaendelea. Nilisoma Biblia mara ya pili na ya tatu. Kufikia wakati huo nikatambua kuwa ili kufanya maendeleo zaidi, nilihitaji uongozi.
Kutafuta Kwangu Kwathawabishwa
Niliendea Kanisa Katoliki ya Kiroma. Upendezi mkuu wa kasisi mchanga ulikuwa kunifundisha mafundisho ya kanisa, jambo ambalo nilikubali kabisa. Kisha katika 1966—kwa aibu ya baba yangu—nilibatizwa. Baada ya kuninyunyizia maji, huyo kasisi akadokeza kwamba niisome Biblia, lakini akaongeza: “Papa tayari amekubali ile nadharia ya mageuzi, kwa hivyo usijali; tutatofautisha ngano kutoka kwa magugu.” Nilishangaa kwamba kitabu ambacho kilikuwa kimenipa imani kingeweza kutiliwa shaka.
Wakati huohuo, katika vuli ya 1966, nilizungumza na rafiki aliyetoka katika jamaa ya Kikatoliki na kushiriki itikadi zangu pamoja naye. Yeye pia aliifahamu Biblia, na akazungumza nami juu ya Har–Magedoni. (Ufunuo 16:16) Alisema alikuwa amekutana na Mashahidi wa Yehova, ambao nilisikia juu yao kwa mara ya kwanza miezi michache kabla ya wakati huo nilipokuwa nikiongoza ile safari ya kuona mji iliyotajwa mapema. Hata hivyo, nililiona kundi lake kuwa si kitu kwa kulinganishwa na Kanisa Katoliki ya Kiroma langu lenye nguvu, tajiri, na lenye watu wengi.
Kwenye majadiliano zaidi, tulichunguza masuala matatu yenye uzito. Kwanza, Je, Kanisa Katoliki ya Kiroma ndilo lililorithi Ukristo wa karne ya kwanza? Pili, Ni nini kipaswacho kuonwa kuwa mamlaka kuu—kanisa langu au Biblia? Na tatu, Ni ipi iliyo sahihi, masimulizi ya Biblia juu ya uumbaji au nadharia ya mageuzi?
Kwa kuwa Biblia ilikuwa chanzo cha imani yetu sote wawili, rafiki yangu hakuwa na shida yoyote kunithibitishia kwamba mafundisho ya Kanisa Katoliki ni tofauti sana na yale ya Ukristo wa mapema. Kwa kielelezo, nilijifunza kwamba hata vyanzo vya Kikatoliki vilikubali kwamba lile fundisho kuu la kanisa la Utatu halina msingi katika mafundisho ya Yesu Kristo na mitume wake.
Hilo lilituleta kwenye swali linalohusiana nalo, mamlaka yetu kuu yapaswa kuwa nini? Nilirejezea nukuu la St. Augustine: “Roma locuta est; causa finita est,” yaani, “Roma imenena; kesi imemalizika.” Lakini rafiki yangu alishikilia kwamba Neno la Mungu, Biblia, lapaswa liwe mamlaka yetu kuu kuliko zote. Nililazimika kukubaliana na maneno ya mtume Paulo: “Acheni Mungu apatikane kuwa wa kweli, lakini acheni kila mwanadamu apatikane kuwa mwongo.”—Warumi 3:4, NW.
Hatimaye, rafiki yangu alinitolea hati iliyochakaa iliyopigwa chapa yenye kichwa Evolution Versus the New World. Kwa kuwa Mashahidi wa Yehova walikuwa wamepigwa marufuku katika Chekoslovakia mwishoni mwa miaka ya 1940, wao walifanyiza nakala za vichapo vyao na kuwa wenye uangalifu juu ya ni nani waliozipokea. Baada ya kusoma kijitabu hiki, nilijua kilikuwa na kweli. Rafiki yangu akaanzisha funzo la Biblia pamoja nami. Kwa kila funzo, aliniazima kurasa kadhaa kutoka kwa ule msaada wa kujifunza Biblia “Let God Be True,” nasi tulizungumza kurasa hizo pamoja.
Muda mfupi baada ya kuanza mazungumzo haya—wakati wa majira ya Krismasi ya 1966—marafiki kutoka Ujerumani Magharibi walikuja Prague kuniona. Katika mojawapo mazungumzo yetu, waliwadhihaki Wakristo kuwa waanzilishi wa vita walio wanafiki. “Tukiwa wanajeshi wa nchi za Shirika la Kijeshi la Mataifa ya Ulaya (NATO), tungeweza kupigana dhidi yenu mkiwa wenye kudai kuwa Wakristo katika nchi za Muungano wa Kikomunisti wa Warsaw,” wakasema. Mkataa wao: “Ni afadhali kuwa asiyejali kuliko kuwa mnafiki.” Nilihisi kwamba huenda walisema kweli. Hivyo katika funzo la Biblia langu lililofuata, nilimuuliza rafiki yangu jinsi Wakristo wa kweli hushughulika na vita na kujifunza vita.
Maamuzi Niliyokabili
Nilishangazwa na maelezo ya rafiki yangu yaliyokuwa wazi. Lakini, kuishi kulingana na mafundisho ya Biblia kwa ‘kufua panga ziwe majembe’ kungebadili kabisa maisha yangu na kazi-maisha niliyonuia kufanya. (Isaya 2:4) Baada ya miezi mitano nilipaswa kufuzu kutoka kwenye chuo kikuu cha kitiba, kufuatia hilo ningehitajiwa kufanya utumishi wa kijeshi wa lazima kwa kipindi fulani. Nifanyeje? Nilikuwa na masumbufu ya kiakili. Hivyo nikasali kwa Mungu.
Baada ya siku kadhaa za kutafakari kwa kina, sikupata kisababu cha kutoishi kulingana na takwa la Wakristo wa kweli la kuwa watu wa amani. Baada ya kufuzu kutoka kile chuo kikuu, niliazimia kwamba hadi nitakapohukumiwa nikiwa mkataaji kidhamira, ningekubali wadhifa kwenye hospitali fulani. Lakini kisha nikajifunza yale ambayo Biblia inasema juu ya kujiepusha na damu. Nikitambua kuwa huenda kazi yangu ihusishe kutia damu, nikaamua kuacha kufanya kazi kwenye hiyo hospitali. (Matendo 15:19, 20, 28, 29) Uamuzi huo ulifanya nipate sifa mbaya kwa wengi.
Baada ya baba yangu kuhakikisha kuwa sikuwa mfanya-matata wa kukusudia aliyetafuta kuharibu kazi-maisha yake ya kisiasa, akaingilia na kufanya utumishi wangu wa kijeshi wa lazima uahirishwe kwa mwaka mmoja. Wakati wa kile kiangazi cha 1967 ulikuwa mgumu kwangu. Fikiria hali yangu: Nilikuwa mwanafunzi wa Biblia mpya ambaye mfunzi wake, Shahidi mmoja tu niliyepata kukutana naye, hakuwepo wakati wa kiangazi. Naye alikuwa ameacha sura chache tu za kile kitabu “Let God Be True” kwa ajili ya funzo langu la kibinafsi. Hizo na Biblia yangu tu ndizo zilikuwa miongozo yangu ya kiroho.
Baadaye, nikafahamiana na Mashahidi wengine, na katika Machi 8, 1968, nikaonyesha wakfu wangu kwa Yehova Mungu kwa ubatizo wa maji. Mwaka uliofuata nilipewa fursa ya mtaala wa mafunzo ya ziada ya miaka miwili kwenye Chuo Kikuu cha Oxford katika Uingereza. Wengine walidokeza kwamba nikubali hilo toleo na kwenda Uingereza ambapo ningeweza kukua kiroho katika nchi ambayo Mashahidi hawakuwa chini ya marufuku. Na wakati uleule ningeweza kujitayarisha kwa ajili ya kazi-maisha ya kitaaluma iliyo nzuri. Lakini mzee Mkristo alisema kwamba utumishi wangu haukuhitajika sana huko Uingereza kama ulivyokuwa ukihitajiwa Chekoslovakia. Hivyo nikaamua kukataa toleo hilo la kuendeleza elimu yangu ya kilimwengu, na kubaki Chekoslovakia ili kusaidia katika utendaji wetu wa kuhubiri kichini-chini.
Katika 1969, nilialikwa kuhudhuria mtaala wa Shule ya Huduma ya Ufalme ambao ulitoa mafundisho ya pekee kwa ajili ya waangalizi Wakristo. Mwaka huo huo nikapata tuzo la kuwa mtaalamu wa dawa bora zaidi katika Chekoslovakia. Likiwa tokeo, nilihudhuria mkusanyiko wa Muungano wa Kimataifa wa Utaalamu wa Dawa katika Uswisi.
Mwanasayansi Abadili Maoni Yake
Kwenye mhadhara niliohudhuria katika 1970, mwanasayansi aitwaye Frantis̆ek Vyskočil alieleza juu ya habari tata ya upitishaji wa mipwito ya neva. Alisema kwamba wakati wowote kulipokuwa na uhitaji katika kiumbe, suluhisho la ajabu lilitolewa. “Mambo ya asili hujua jinsi ya kufanya hayo,” akamalizia.
Baada ya mhadhara nilimwendea. “Je, wewe hufikiri,” nikamuuliza, “kwamba sifa kwa ajili ya ubuni bora kabisa wenye kupendeza katika vitu vyenye uhai zapaswa kumwendea Mungu?” Hakutarajia swali langu kwa kuwa alikuwa mwatheisti. Alijibu kwa maswali tofauti. Aliuliza: “Uovu ulitoka wapi?” na, “Ni nani apaswaye kulaumiwa kwa kuwa watoto wengi ni mayatima?”
Nilipompa majibu yafaayo, yenye msingi katika Biblia, upendezi wake uliamshwa. Lakini aliuliza ni kwa nini Biblia haitoi habari hususa za kisayansi, kama vile maelezo juu ya umbo la seli, ili watu wajue kwa urahisi kuwa mtungaji wayo ndiye Muumba. “Ni nini kilicho kigumu zaidi,” nikajibu, “kueleza au kuumba?” Nikamwazima kile kitabu Did Man Get Here by Evolution or by Creation?
Baada ya kukisoma juu-juu, Frantis̆ek alikiita sahili na kisicho sahihi. Pia alichambua yale ambayo Biblia ilisema juu ya kuoa wake wengi, uzinzi wa Daudi, na kuua kwake mtu asiye na hatia. (Mwanzo 29:23-29; 2 Samweli 11:1-25) Nilipinga hoja zake, nikionyesha kwamba Biblia huripoti kwa unyoofu hata makosa ya watumishi wa Mungu, na vilevile ukiukaji-sheria wa moja kwa moja.
Hatimaye, katika mojawapo mazungumzo yetu, nilimwambia Frantis̆ek kuwa ikiwa mtu hana kusudio zuri, ikiwa hapendi kweli, hakuna aina yoyote ya mabishano au kusababu ingeweza kumhakikishia kuwepo kwa Mungu. Nilipokuwa karibu kuondoka, alinisimamisha na kuomba funzo la Biblia. Akasema angesoma tena kile kitabu Did Man Get Here by Evolution or by Creation?—wakati huu akiwa na akili iliyofunguka. Baadaye, mtazamo wake ulibadilika kabisa, kama ithibitishwavyo na nukuu alilotia ndani ya mojawapo barua zake: “Na majivuno ya mwanadamu yatainamishwa, na kiburi cha watu kitashushwa; naye BWANA, yeye peke yake, atatukuzwa siku hiyo.”—Isaya 2:17.
Katika kiangazi cha 1973, Frantis̆ek na mke wake walibatizwa wakiwa Mashahidi wa Yehova. Sasa anatumikia akiwa mzee katika mojawapo makutaniko katika Prague.
Kuhubiri Chini ya Marufuku
Wakati wa marufuku tuliagizwa kufanya huduma yetu ya shambani kwa busara nyingi. Wakati mmoja, Shahidi mmoja mchanga zaidi aliniomba tena na tena nishiriki katika kazi ya kuhubiri pamoja naye. Alitilia shaka ikiwa wale waongozao katika tengenezo la Mashahidi wa Yehova kwa hakika walienda kwenye huduma, wao wenyewe. Tulifurahia mazungumzo mengi mazuri katika huduma yetu ya vivi hivi. Lakini hatimaye tukakutana na mtu ambaye, ingawa sikufahamu wakati huo, alitambua sura yangu kutoka kwenye picha katika kitabu cha picha cha polisi wa siri wa serikali. Ingawa sikukamatwa, kuanzia wakati huo na kuendelea nikawa nikichunguzwa kwa ukaribu na maofisa ambao walizuia mafanikio yangu katika kazi yetu ya kuhubiri kichini-chini.
Wakati wa kiangazi cha 1983, kama lilivyokuwa limekuwa zoea langu katika miaka iliyotangulia, nilipanga kikundi cha Mashahidi wachanga ili kutumia siku kadhaa tukitoa ushahidi wa vivi hivi katika sehemu ya mbali ya nchi. Bila kutii shauri lenye hekima, niliendesha gari langu kwa kuwa ilikuwa rahisi kuliko kutumia usafiri wa umma. Tulipopumzika kidogo ili kununua bidhaa kadhaa kwenye duka, niliegesha gari langu mbele yalo. Nilipokuwa nikilipia hizo bidhaa, niliwaashiria wasaidizi wachanga wa duka na kumtajia mwajiriwa aliyekuwa na umri zaidi: “Siku zijazo, sote twaweza kuwa wachanga.” Mwanamke huyo akatabasamu. “Hata hivyo, hilo ni jambo ambalo wanadamu hawawezi kutimiza,” nikaendelea. “Ingekuwa lazima kupata usaidizi kutoka juu.”
Kwa kuwa hakukuwa na itikio la ziada, niliondoka. Bila mimi kujua, huyo mwajiriwa, akinishuku kuwa nilikuwa nikiendeleza maoni ya kidini, aliniangalia kupitia dirisha nilipokuwa nikiweka kifurushi kwenye gari langu. Kisha akawajulisha polisi. Muda wa saa nyingi baadaye, baada ya kushiriki katika kutoa ushahidi katika sehemu nyinginezo za mji, mwenzangu nami tulirudi kwenye gari. Ghafula, polisi wawili wakatokea na kutupeleka korokoroni.
Kwenye kituo cha polisi, tulihojiwa kwa muda wa saa nyingi kabla ya kuambiwa twende. Wazo langu la kwanza lilikuwa juu ya jambo la kufanya na zile anwani za watu waliopendezwa tulizokuwa tumepata siku hiyo. Hivyo nikaenda chooni ili kuzipiga maji. Lakini kabla ya kufanya hilo, mkono wenye nguvu wa polisi ulinizuia. Akayachukua hayo makaratasi kutoka kwenye bakuli la choo na kuyasafisha. Hili lilitokeza mkazo zaidi kwangu, kwa kuwa watu waliokuwa wamenipa anwani zao sasa walikuwa hatarini.
Baadaye, sote tulipelekwa kwenye hoteli yetu, ambapo polisi walikuwa wamepekua chumba chetu. Lakini hawakuwa wamepata anwani nyinginezo zozote za watu waliopendezwa, ingawa hizo hazikuwa zimefichwa kwa uangalifu. Baada ya muda, kwenye mahali pangu pa kazi nikiwa mtaalamu wa dawa za neva, nilikemewa hadharani kwa kushiriki katika kazi isiyo halali. Pia, niliadhibiwa na mwangalizi wa kazi ya kuhubiri katika Chekoslovakia, ambaye mapema alikuwa amenionya nisitumie gari langu tusafiripo kushiriki katika huduma.
Kukubali Nidhamu
Katika 1976, nilikuwa nimepewa mgawo kutumikia kwenye halmashauri inayosimamia kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova katika Chekoslovakia. Lakini kwa kuwa maisha yangu yalikuwa yamechunguzwa kwa ukaribu na polisi wa siri kwa sababu ya yale niliyofanya bila ya kufikiri kuzuri katika mambo yaliyotangulia kutajwa mapema, niliachishwa kutumikia katika halmashauri ya nchi na kwenye mapendeleo mengine mbalimbali. Mojawapo mapendeleo hayo nililopenda sana lilikuwa lile la kufundisha waangalizi wasafirio na mapainia, kama waitwavyo wahudumu wa wakati wote.
Niliikubali nidhamu niliyopokea, lakini kipindi hiki cha kati ya miaka ya 1980 kilikuwa kigumu sana cha kujichunguza mimi mwenyewe. Je, ningejifunza kufanya kazi kwa hekima zaidi na kuepuka kukosa hekima tena. Zaburi 30, mstari wa 5, husema: “Huenda kilio huja kukaa usiku, lakini asubuhi huwa furaha.” Asubuhi hiyo ilinijia wakati ambapo utawala wa Kikomunisti ulipoanguka katika Chekoslovakia katika Novemba 1989.
Baraka za Ajabu
Lilikuwa badiliko kama nini kushiriki katika huduma kwa uhuru na kufurahia mawasiliano ya moja kwa moja na makao makuu ya Mashahidi wa Yehova katika Brooklyn, New York! Upesi nikapewa mgawo wa kuwa mwangalizi asafiriye, nami nikaanza kazi hii katika Januari 1990.
Kisha, katika 1991, nilipata pendeleo la kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma katika Manchester, Uingereza. Ilikuwa baraka iliyoje kutumia miezi miwili nikifurahia ushirika pamoja na ufundishaji kutoka kwa wanaume wakomavu wa Kikristo! Kwa kipindi fulani kila siku, sisi wanafunzi tulikuwa na migawo ya kazi, ambayo ilitutuliza kutokana na ufundishaji mwingi wa kimasomo. Nilipewa mgawo wa kusafisha madirisha.
Mara tu baada ya kurudi kutoka Uingereza, nilianza kusaidia kutayarisha kwa ajili ya mkusanyiko mkubwa wa Mashahidi wa Yehova uliofanywa Agosti 9 hadi 11 kwenye Stediamu ya Strahov iliyo kubwa katika Prague. Kwenye pindi hiyo watu 74,587 kutoka nchi nyingi walikutana kwa uhuru ili kumwabudu Mungu wetu, Yehova!
Mwaka uliofuata niliacha kufanya kazi ya kimwili nikiwa mtaalamu wa dawa za neva. Kwa karibu miaka minne, nimekuwa nikifanya kazi ofisini Prague, ambapo natumika tena kwenye halmashauri inayosimamia kazi ya Mashahidi wa Yehova katika Jamhuri ya Cheki. Majuzi jengo jipya la orofa kumi, walilopewa Mashahidi wa Yehova, lilifanyiwa marekebisho na kuanza kutumiwa likiwa ofisi ya tawi. Katika Mei 28, 1994, jengo hili liliwekwa wakfu kwa ajili ya utumishi wa Yehova.
Kati ya baraka zangu zilizo kuu ni lile pendeleo la kushiriki kweli za Biblia pamoja na wengine, kutia ndani watu wa ukoo. Kufikia sasa, baba na mama yangu hawajawa Mashahidi, lakini sasa wanapendelea utendaji wangu. Katika miaka michache iliyopita, wamehudhuria baadhi ya mikutano yetu. Tumaini langu la moyoni ni kwamba wao, pamoja na mamilioni zaidi ya watu wenye moyo wa haki, kwa unyenyekevu watajitiisha kwa utawala wa Ufalme wa Mungu na kufurahia baraka za milele ambazo Mungu ameweka akibani kwa ajili ya wale wachaguao kumtumikia.
(Vichapo virejezewavyo katika makala hii vimetangazwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.)
[Picha katika ukurasa wa 12]
Nilipokuwa mwanafunzi wa chuo kikuu
[Picha katika ukurasa wa 13]
Baba yangu, aliyekuja kuwa waziri wa elimu wa Chekoslovakia, naye mama yangu, aliyekuwa mpasuaji wa macho aliyejulikana sana
[Picha katika ukurasa wa 15]
Frantis̆ek Vyskočil, mwanasayansi na mwatheisti, aliyekuja kuwa Shahidi
[Picha katika kurasa za 16, 17]
Tangu kuanguka kwa Ukomunisti, Mashahidi wa Yehova wamekuwa na mikusanyiko mikubwa mingi katika Ulaya Mashariki. Watu zaidi ya 74,000 walihudhuria huu katika Prague katika 1991
[Picha katika ukurasa wa 18]
Katika mgawo wangu wa kazi nikihudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma katika Uingereza
[Picha katika ukurasa wa 18]
Majengo yetu ya tawi katika Prague, yaliwekwa wakfu Mei 28, 1994