Zaidi ya Miaka 40 Chini ya Marufuku ya Ukomunisti
KAMA ILIVYOSIMULIWA NA JARMILA HÁLOVÁ
Wakati: baada ya usiku wa manane, Februari 4, 1952. Mahali: nyumba yetu katika Prague, Chekoslovakia. Tuliamshwa na msisitizo wa milio ya kengele ya mlangoni. Kisha polisi wakaingia ndani.
POLISI walimweka mama, baba, na ndugu yangu Pavel, nami katika vyumba tofauti, wakamweka mlinzi kwa kila mmoja wetu, nao wakaanza kusaka kila kitu. Walikuwa wakisaka katika nyumba yetu karibu saa 12 baadaye. Baada ya wao kufanya orodha ya fasihi zote walizopata, walizipanga katika masanduku.
Baadaye, niliagizwa kuingia katika gari, na nilivalishwa miwani nyeusi. Ilionekana ajabu, lakini niliweza kuisongeza miwani kidogo ili nione walikokuwa wakinipeleka. Mitaa niliifahamu. Kikomo chetu cha safari kilikuwa makao makuu ya Ulinzi wa Serikali.
Waliniburuta kutoka kwa gari. Baadaye walipoondoa miwani, nilijikuta katika chumba kidogo, kichafu. Mwanamke katika sare aliniamrisha kutoa nguo zangu na kuvaa jozi la suruali ndefu nzito ya kazi na shati la mwanamume. Kitambaa kilifungwa kuzunguka kichwa changu ili kufunika macho yangu, nami niliongozwa, nikiwa nimefungwa macho, nje ya chumba hicho na kutembea katika ukumbi uliohisika kutokuwa na mwisho.
Hatimaye, mlinzi alisimama na kufungua mlango wa chuma, na nilisukumwa kuupitia. Kitambaa kiliondolewa kutoka kichwani mwangu, nao mlango ukafungwa nyuma yangu. Nilikuwa katika seli ya gereza. Mwanamke katika miaka yake ya 40 alikuwa pale akinikodolea macho, amevaa mavazi yafananayo na yangu. Nilijihisi kama kucheka na—ingawa huenda ionekane ajabu—singejizuia kucheka. Nikiwa msichana mchanga wa miaka 19, bila uzoefu katika mambo kama vile kifungo, nilibaki nikiwa na shauku. Mara, kuongezea furaha, niling’amua kwamba hakuna mwingine yeyote wa familia yetu aliyekuwa ameshikwa.
Ilikuwa hatari katika siku hizo kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova katika nchi iliyoitwa wakati huo Chekoslovakia. Nchi hiyo ilikuwa chini ya utawala wa Ukomunisti, na Mashahidi walipigwa marufuku. Familia yetu ilihusikaje sana na tengenezo lililopigwa marufuku?
Jinsi Tulikuja Kuwa Mashahidi
Baba, mwenyeji wa Prague, alikuwa na msingi wa Uprotestanti na mnyoofu kabisa katika usadikisho wake wa kidini. Alikutana na mama katika miaka ya 1920 alipokuja Prague kwa ajili ya masomo ya kitiba. Mama alikuwa ametoka katika eneo liitwalo Bessarabia, ambalo wakati wa utoto wake lilikuwa sehemu ya Urusi. Baada ya wao kuoana, alijiunga na kanisa la mumeye hata ingawa alikuwa Myahudi. Hata hivyo, hakuridhika nalo.
Wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, baba aliwekwa katika kambi ya kazi, na mama nusura aliepuka teketezo hilo. Hiyo ilikuwa miaka migumu kwetu, lakini sisi sote tuliokoka. Katikati mwa 1947, miaka miwili baada ya kumalizika kwa vita, mmoja wa dada za baba, aliyekuwa amekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova, aliandikisha Mnara wa Mlinzi kwa ajili ya familia yetu. Mama ndiye aliyeanza kulisoma, na mara moja alitambua ujumbe huo kuwa kweli ambayo alikuwa ametafuta.
Mwanzoni, alisema machache kwa sisi sote, lakini alijua mahali mikutano ilikuwa katika Prague na akaanza kuihudhuria. Mnamo miezi michache, katika masika ya 1948, alibatizwa katika kusanyiko la mzunguko la Mashahidi. Kisha akatualika kujiunga naye katika kuhudhuria mikutano. Shingo upande, Baba alikubali.
Mikutano iliendelezwa katika jumba dogo katikati ya Prague, mahali tulipoanza kuhudhuria tukiwa familia. Baba nami tulikuwa na hisia-moyo zilizochangamana, za kutaka kujua pamoja na kutoamini. Tulishangaa kuona kwamba mama tayari alikuwa na marafiki wapya aliotujulisha kwao. Nilipendezwa na idili yao na kiasi chao, jinsi walivyoonekana wakithamini udugu wao.
Kwa kuona itikio letu chanya, mama alidokeza kwamba Mashahidi waalikwe nyumbani kwetu kwa ajili ya mazungumzo ya kina zaidi. Jinsi baba na mimi tulivyoshangaa walipotuonyesha kutoka kwa Biblia yetu wenyewe kwamba hakuna nafsi isiyokufa na hakuna Utatu! Ndiyo, ilikuwa yenye kufungua-jicho kujifunza kinachomaanishwa na kusali kwa ajili ya kutakaswa kwa jina la Mungu na kwa ajili ya kuja kwa Ufalme wake.
Majuma machache baadaye, baba aliwaalika makasisi kadhaa wa kanisa lake nyumbani kwetu. Akasema: “Akina ndugu, nataka kuzungumza hoja fulani za Kimaandiko pamoja nanyi.” Baada ya kusema hayo alitoa, hatua kwa hatua, mafundisho ya msingi ya kanisa na akaonyesha jinsi hayo yanavyopingana na Biblia. Makasisi walikubali aliyoyasema kuwa kweli. Kisha Baba akakata kauli hivi: “Nimeamua, na nasema kwa niaba ya familia yangu, kuacha kanisa.”
Kazi ya Kuhubiri Yapigwa Marufuku
Katika Februari 1948, muda mfupi kabla ya baba na nami kuhudhuria mikutano, chama cha Ukomunisti kilidhibiti nchi. Niliwatazama wanafunzi wenzangu wakiwakana walimu wao, na kuona walimu wakiwa na hofu kwa wazazi wa wanafunzi. Watu walianza kujitenga mmoja na mwenzake. Hata hivyo, mwanzoni kazi ya Mashahidi wa Yehova kwa uhalisi ilibaki bila kuvurugwa.
Kwetu sisi jambo kubwa la 1948 lilikuwa mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova katika Prague. Zaidi ya watu 2,800 walikuwako Septemba 10 hadi 12. Majuma machache baadaye, kwenye Novemba 29, 1948, polisi wa siri walivamia ofisi ya tawi, nayo ilifungwa. Aprili uliofuata marufuku rasmi iliwekwa kwa kazi yetu.
Hakuna moja la matendo haya lililohofisha familia yetu, na katika Septemba 1949 tulihudhuria programu ya pekee kwenye vichaka nje ya Prague. Juma moja baadaye, baba nami tulibatizwa. Nijapojaribu kuwa macho katika kazi ya kuhubiri, nilitiwa mbaroni katika Februari 1952, kama ilivyoelezwa mwanzoni.
Kuhojiwa kwa Kurudia-Rudia
Baada ya kuhojiwa kwa mara kadhaa, nilikata kauli kwamba ningekuwa gerezani kwa muda mrefu. Wahoji walionekana kufikiri kwamba kadiri mtu alivyowekwa kizuizini kwa muda mrefu bila lolote la kufanya, ndivyo angekuwa na uelekeo wa kushirikiana. Lakini maagizo ya wazazi wangu yaliendelea kunijia akilini, na yalisaidia kunitegemeza. Mara nyingi walinukuu Zaburi 90:12, wakinitia moyo ‘kuhesabu siku zangu’ yaani, nizikadirie, ama kuzichanganua, ‘ili kwamba nijiletee moyo wa hekima.’
Hivyo basi, akilini mwangu nilipitia zaburi nzima na vifungu vingine vya Biblia ambavyo mapema nilikuwa nimeviweka akilini. Pia nilitafakari makala za Mnara wa Mlinzi nilizokuwa nimesoma kabla ya kufungwa, na nilijiimbia nyimbo za Ufalme. Fauka ya hayo, katika mwezi wangu wa kwanza kifungoni, kulikuwa na wafungwa-wenzi wachache wa kuzungumza nao. Kwa kuongezea, kulikuwa na kazi za kupitia nilizokuwa nimejifunza darasani kwenye shule, kwani nilikuwa tu nimefuzu mitihani yangu ya mwisho miezi michache kabla.
Mahoji yalifanya iwe wazi kwangu kwamba aliyekuwa ameripoti alikuwa amehudhuria mojapo ya mafunzo yangu ya Biblia na akaripoti utendaji wangu wa kuhubiri. Mamlaka zilikata kauli kwamba nilikuwa na daraka la nakala zilizochapwa za vichapo vya Biblia vilivyopatikana nyumbani mwetu. Kwa hakika, ndugu yangu, aliyekuwa na miaka 15 tu, alikuwa amefanya uchapaji huo.
Baada ya muda wahoji wangeweza kuona kwamba singeweza kuhusisha mwingine yeyote, hivyo basi walijitahidi kunishawishi kutoka kwa itikadi zangu. Hata walimleta mtu ambaye nilikuwa nimemjua kuwa mwangalizi asafiriye wa Mashahidi wa Yehova. Hata ingawa alikuwa mfungwa mwenyewe, alikuwa akishirikiana na Wakomunisti katika kampeni ili kuwafanya Mashahidi wengine waliofungwa wakane imani yao. Jinsi alivyokuwa wa kusikitikiwa! Miaka mingi baadaye, baada ya kufunguliwa, alichakarika kwa alkoholi mpaka akafa.
Kifungo cha Upekee
Baada ya miezi saba nilihamishwa kwa jela nyingine na nikawekwa katika kifungo cha upekee. Sasa, nikiwa peke yangu kabisa, mimi pekee nilikuwa na daraka la jinsi nilivyotumia wakati wangu. Vitabu viliandaliwa mmoja alipoagiza, lakini, bila shaka, hakuna vyovyote vya aina ya kiroho. Hivyo basi niliweka ratiba ya utendaji uliotia ndani vipindi vya kusoma pamoja na wakati kwa ajili ya kutafakari juu ya mambo ya kiroho.
Ni lazima niseme, kamwe hakuna wakati wowote uliopita nilijihisi karibu na Yehova katika sala zangu kama wakati huo. Wazo la udugu wa ulimwenguni pote lilikuwa halijapata kuwa na thamani hivyo kamwe. Kila siku nilijaribu kuwazia jinsi habari njema huenda zinaenea kwa wakati huo hususa katika maeneo mbalimbali ya dunia. Nilijifikiria mwenyewe nikishiriki katika kazi hii, nikitoa utoaji wa Biblia kwa watu.
Hata hivyo, katika hali hii tulivu, hatimaye niliingia mtegoni. Sikuzote kwa kupenda kusoma na kwa kuwa na kiu ya habari kutoka nje, wakati fulani nilinywea katika kitabu hususa kufikia kiwango cha kupuuza ratiba ya kutafakari mambo ya kiroho. Baada ya hili kutukia, sikuzote nilihisi hatia.
Hivyo, asubuhi moja nilipelekwa kwa ofisi ya kiongozi wa mashtaka. Hakuna jambo lolote hususa lililosemwa—isipokuwa matokeo ya mahoji yaliyotangulia. Nilihisi kuudhika, kwani hakuna siku iliyowekwa kwa ajili ya usikizi wa kesi yangu. Baada ya nusu saa hivi, nilikuwa katika seli tena. Nilikosa utulivu na nikaanza kulia. Kwa nini? Je, juma zima nikiwa pekee yaelekea hatimaye lilikuwa na matokeo?
Nilianza kuchanganua tatizo langu na mara nilitambua kisababishi. Siku iliyotangulia, nilikuwa nimenaswa na usomaji, na kwa mara nyingine tena sikuwa nimefuatilia utendaji wangu wa kiroho. Hivyo nilipochukuliwa bila kutazamia kwa kuhojiwa, sikuwa katika mtazamo wa akili unaofaa wa sala. Mara hiyo nilimwaga moyo wangu kwa Yehova na nikaazimia kutopuuza tena kamwe mambo ya kiroho.
Baada ya ono hilo niliamua kuacha kusoma kabisa. Wakati huo wazo zuri zaidi lilinijia, kujilazimisha kusoma Kijerumani. Wakati wa uvamizi wa Ujerumani katika Vita ya Ulimwengu 2, ilitubidi kujifunza Kijerumani shuleni. Lakini kwa sababu ya mambo yenye kutisha waliyofanya Wajerumani wakati wa uvamizi wa Prague, baada ya vita nilitaka kusahau chochote cha Kijerumani, kutia ndani lugha. Hivyo basi sasa ilinibidi kujitia nidhamu kwa kujifunza upya Kijerumani. Hata hivyo, kile kilichokuwa adhabu kilitokea kuwa baraka. Acha nisimulie.
Niliweza kupata chapa za Kijerumani na Kicheki za baadhi ya vitabu na nikaanza kujizoeza kutafsiri kutoka Kijerumani hadi Kicheki na Kicheki hadi Kijerumani. Utendaji huu haukuthibitika tu kuwa kitulizo kwa athari yenye kudhuru ya kufungwa pekee bali pia ulitumika kwa makusudi mazuri wakati wa baadaye.
Kuachiliwa na Kuendelea Kuhubiri
Mwishowe, baada ya miezi minane ya upekee, kesi yangu ilitokezwa mahakamani kwa ajili ya majaribio. Nilishtakiwa kwa utendaji wa kupotosha na nikahukumiwa kifungo cha miaka miwili. Kwa sababu tayari nilikuwa nimetumikia miezi 15 na msamaha wa serikali ulikuwa umetangazwa kwa sababu ya uchaguzi wa rais mpya, niliachiliwa.
Gerezani nilikuwa nimesali kwamba familia yangu wasiwe na wasiwasi kunihusu, na niliporudi nyumbani, nilipata kwamba sala yangu ilikuwa imejibiwa. Baba alikuwa daktari wa kitiba, naye aliwatia moyo wengi wa wagonjwa wake wajifunze Biblia. Likiwa tokeo, mama alikuwa akiongoza mafunzo karibu 15 kila juma! Kwa kuongezea, baba alikuwa akiongoza funzo la kikundi la gazeti la Mnara wa Mlinzi. Alifanya pia utafsiri wa baadhi ya fasihi za Watch Tower Society kutoka Kijerumani hadi Kicheki, na ndugu yangu alifanya uchapaji wa uandishi huo. Hivyo mara moja nilijiingiza ndani ya utendaji wa kiroho na muda si muda niliongoza mafunzo ya Biblia.
Mgawo Mpya
Alasiri moja yenye mvua katika Novemba 1954, mtu fulani alikuwa akipiga kengele ya mlangoni. Akiwa amesimama pale, maji yakitiririka kwenye jaketi-mvua yake ya kijivu, alikuwa Konstantin Paukert, mmoja wa wale wenye kuongoza katika kazi ya kuhubiri. Kwa kawaida, alitaka kuongea na baba ama ndugu yangu Pavel, lakini wakati huu aliniuliza: “Je, ungeweza kutoka kwa ajili ya matembezi mafupi?”
Tulitembea kwa ukimya kwa muda, wapita-njia wachache wakipita. Mwangaza uliofifia wa taa za barabarani uliangaza kwa kufifia kwenye uso wa sakafu ya mawe meusi. Konstantin alitazama nyuma; kulikuwa hakuna mtu yeyote nyuma yetu. “Je, ungeweza kusaidia kwa kazi fulani?” aliuliza ghafula. Kwa mshangao, nilitikisa kichwa kwa kukubali. “Tunataka utafsiri fulani ufanywe,” aliendelea. “Ni lazima utafute mahali fulani pa kufanyia kazi bali si nyumbani na si ukiwa pamoja na yeyote anayejulikana kwa polisi.”
Siku chache baadaye, niliketi kwenye dawati katika nyumba ndogo ya mume na mke wazee-wazee ambao sikuwajua kamwe. Walikuwa wagonjwa wa baba, na funzo la Biblia lilikuwa limeanzishwa pamoja nao si muda mrefu uliopita. Hivyo, kujifunza kwangu Kijerumani katika gereza kukathibitika kuwa kwenye thamani, wakati huo tulipokuwa tukitafsiri fasihi zetu kutoka Kijerumani hadi Kicheki.
Majuma machache baadaye, ndugu Wakristo wenye kuongoza katika kazi walifungwa, kutia ndani Ndugu Paukert. Hata hivyo, kuhubiri kwetu hakukusimamishwa. Wanawake, kutia ndani mama pamoja nami, tulisaidia katika kutunza vikundi vya kujifunza Biblia na huduma yetu ya Kikristo. Ndugu yangu Pavel, ingawa bado tineja, alitumika akiwa mjumbe wa kugawanya fasihi na maagizo ya kitengenezo kotekote katika eneo la nchi lililosema Kicheki.
Mwandamani Mpendwa
Baadaye katika 1957, Jaroslav Hála, Shahidi aliyekuwa amefungwa katika 1952 na kupewa kifungo cha miaka 15, aliachiliwa kwa muda kutoka gerezani kwa ajili ya matibabu ya kitiba. Mara hiyo Pavel alimtembelea, na muda si muda Jaroslav alijihusisha tena katika kusaidia akina ndugu. Akiwa anajua lugha vizuri, alianza kufanya kazi nyingi ya utafsiri.
Jioni moja katikati ya mwaka 1958, Jaroslav alialika Pavel pamoja nami kwa ajili ya matembezi. Hili lilikuwa kawaida kwa ajili ya kuzungumza mambo ya kitengenezo, kwani nyumba yetu ilikuwa imewekwa vinasa mazungumzo. Baada ya kuzungumza kwa faragha na Pavel, alimwomba akae kwenye benchi katika bustani fulani ya starehe ilhali sisi wawili tuliendelea kutembea. Baada ya mazungumzo machache kuhusu kazi yangu, aliniuliza ikiwa, ajapokuwa na afya iliyolemaa na wakati ujao usio hakika, ningeolewa naye.
Nilishtushwa na dokezo hilo la moyo mweupe, la moja kwa moja kutoka kwa mmoja niliyemstahi sana, na nikakubali bila kusitasita. Uchumba wetu ulinileta katika uhusiano wa karibu na mama ya Jaroslav, Mkristo mtiwa-mafuta. Yeye pamoja na mume wake walikuwa miongoni mwa Mashahidi wa kwanza katika Prague mwishoni mwa miaka ya 1920. Wote wawili walifungwa na Wanazi wakati wa vita ya ulimwengu ya pili, na mume wake alifia katika kambi ya Wakomunisti katika 1954.
Kabla hatujaoana, Jára, kama tulivyomwita, alishauriwa na serikali. Walimwambia kwamba ama alikuwa afanyiwe oparesheni fulani kwa sababu ya vichomi vilivyoendelea kuwa vibaya—ambayo kwa wakati ule ingemaanisha kukubali kutiwa damu mishipani—ama angelazimika kutumika kifungo kilichobaki. Kwa sababu alikataa, ilimaanisha kwamba alikuwa na karibu miaka kumi ya kifungo. Niliamua kumngojea.
Wakati wa Kutahiniwa na Ujasiri
Mapema katika 1959, Jára alipelekwa gerezani, muda si muda baadaye, tulipata barua iliyoonyesha kwamba alikuwa katika hali njema. Kisha kukawa na kipindi kirefu kilichopita kabla ya barua kufika iliyokuja kama pigo kwetu. Ilionyesha masikitiko, huzuni, na hofu, kana kwamba Jára alikuwa akiugua mfadhaiko. “Ni lazima hii iwe iliandikwa na mtu mwingine,” mama yake akasema. Lakini mwandiko ulikuwa wake!
Mimi pamoja na mama yake tuliandika na tukaonyesha tumaini letu kwa Mungu na tukamtia moyo. Baada ya majuma mengi, barua nyingine ilikuja, bado ikitatanisha zaidi. “Hangeweza kuwa aliandika hii,” mama yake akasema tena. Hata hivyo, mwandiko kwa udhahiri ulionyesha ulikuwa mtindo wake wa kuandika, na kulikuwa na aina ya mitajo yake. Hakuna barua zaidi zilizopokewa, na hakuna ziara zilizoruhusiwa.
Vivyo hivyo, Jára alikuwa amepokea barua zenye kuvuruga za kulaumu kulikokusudiwa kutoka kwetu. Barua ya mama yake ilimlaumu kwa kumwacha peke yake katika umri wake wa uzeeni, na yangu ilionyesha kukasirika kwa kumngojea kwa wakati mrefu hivyo. Hizi pia zilionyesha mfanano kamili wa miandiko yetu na namna ya kujieleza. Mwanzoni hata yeye alivurugika, lakini akasadiki kwamba hatungeweza kuwa tuliandika hizo barua.
Siku moja mtu fulani alitokea kwenye mlango, akanipatia kifurushi kidogo, na akaondoka mara. Katika hicho kulikuwa na makumi ya majani ya makaratasi ya sigareti ambayo katika hayo kulikuwa na mwandiko ulio mdogo kadiri iwezekanayo. Jára alikuwa amenakili barua ambazo zilinuiwa kuwa tuliziandika, pamoja na zile zake zisizochujwa. Baada ya kupata habari zilizokuwa zimetoroshwa na mfungwa asiye Shahidi aliyekuwa ameachiliwa huru, tulikuwa wenye utulivu na shukrani zilizoje kwa Yehova! Mpaka siku ya leo hatujapata kujua jinsi au ni kupitia kwa nani jitihada hii ya kiibilisi ya kuvunja uaminifu-maadili wetu ilibuniwa.
Baadaye, mama yake Jára aliruhusiwa kumtembelea mwanaye. Katika pindi hizi, niliandamana naye hadi kwenye kiingilio na kumtazama mwanamke huyu mdogo, dhaifu akifanya matendo ya ujasiri mkubwa. Walinzi wakiwa wanatazama, angechukua mkono wa mwanaye na kumpa fasihi iliyopigwa picha ndogo iwezekanayo. Ingawa ugunduzi ungemaanisha adhabu kali, hasa kwa mwanaye, alimtegemea Yehova aking’amua kwamba kudumisha afya ya kiroho sikuzote ni kwa umuhimu wa kwanza.
Baadaye, katika 1960 msamaha wa serikali wa ujumla ulitangazwa, na Mashahidi walio wengi waliachiliwa kutoka gerezani. Jára alikuja nyumbani, na katika majuma machache, tulikuwa mume na mke wapya waliooana wenye furaha.
Kubadili Mtindo-Maisha Wangu
Jára aligawiwa kazi ya kusafiri, kutumikia masilahi ya udugu kotekote nchini. Katika 1961 aligawiwa kupanga darasa la kwanza la Shule ya Huduma ya Ufalme katika eneo la nchi lililosema Kicheki, pamoja na kushughulikia mengi ya madarasa ya shule hiyo yaliyofuata.
Kwa sababu ya mabadiliko ya kisiasa katika Chekoslovakia katika 1968, mwaka uliofuata baadhi yetu tuliweza kuhudhuria “Amani Duniani” Mkusanyiko wa Kimataifa wa Mashahidi wa Yehova katika Nuremberg, Ujerumani. Hata hivyo, mamlaka hazingeweza kumruhusu Jára kuondoka nchini. Baadhi yetu tulichukua picha za slaidi za mkusanyiko huo mkuu, na kotekote nchini, Jára alikuwa na pendeleo la kushiriki katika kutoa programu yenye kuimarisha imani iliyoonyesha picha hizi. Wengi walitamani kuiona programu tena na tena.
Hatukujua kwamba huo ungekuwa wakati wa mwisho wa Jára kutembelea akina ndugu. Mapema katika 1970, afya yake ilidhoofika kwa njia ya kustaajabisha. Mchochota uliosedeka, aliokuwa amezoea kuishi nao, uliathiri figo zake, na kutotenda kwa figo kulithibitika kuwa msiba. Alikufa akiwa na umri wa 48.
Kutegemezwa na Msaada wa Yehova
Nilikuwa nimefiwa na mmoja ambaye nilimpenda sana. Lakini msaada wa haraka uliandaliwa katika tengenezo la Mungu, kwani niliruhusiwa kushiriki katika kutafsiri fasihi za Biblia. Kama vile katika mbio za kupokezana vijiti, nilihisi kwamba mume wangu alinipokeza kijiti ili kuendelea na sehemu ya kazi ambayo yeye mwenyewe alikuwa akifanya.
Wengi wetu katika Ulaya Mashariki tulitumikia Yehova kwa zaidi ya miaka 40 tukiwa chini ya marufuku ya Ukomunisti. Kisha, katika 1989, kwa kuondolewa ule Ukuta wa Chuma, maisha yalianza kubadilika ghafula. Ingawa niliwazia Mashahidi wa Yehova wakiwa na mkusanyiko katika Stediamu kubwa Strahov ya Prague, kamwe sikuamini kwamba ndoto hii ingekuwa kweli. Hata hivyo, katika Agosti 1991, ilitimia katika njia ya ajabu wakati zaidi ya 74,000 walipokusanyika katika ibada yenye shangwe!
Chekoslovakia ikakoma kuwapo katika Januari 1993 wakati nchi ilipogawanywa katika nchi mbili—Jamhuri ya Cheki na Slovakia. Jinsi tulivyokuwa wenye furaha, Septemba 1, 1993, Jamhuri ya Cheki ilipowatambua Mashahidi wa Yehova kirasmi.
Kutoka kwa maono yangu ya maisha, najua kwamba Yehova sikuzote anakuwa na baraka akibani kwa ajili yetu, mradi tutamruhusu atufunze jinsi ya kuhesabu siku zetu. (Zaburi 90:12) Mimi husali daima kwa Mungu ili anifunze jinsi ya kuhesabu siku zangu zilizobaki katika mfumo huu wa mambo ili kwamba kwenye siku zisizo na hesabu mbeleni katika ulimwengu mpya wake, huenda niwe miongoni mwa watumishi wake wenye furaha.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Mama na baba yangu
[Picha katika ukurasa wa 21]
Mkutano kwenye kichaka katika 1949 wakati wa marufuku 1. Ndugu yangu Pavel 2. Mama 3. Baba 4. mimi 5. Ndugu Hála
[Picha katika ukurasa wa 22]
Pamoja na mume wangu, Jára
[Picha katika ukurasa wa 23]
Mama ya Jára na fasihi iliyopigwa picha aliyomtoroshea
[Picha katika ukurasa wa 24]
Kufanya kazi leo kwenye tawi katika Prague