Walishangilia Katika Ulaya ya Mashariki
KATIKA kiangazi cha mwaka jana, makumi ya maelfu ya watu walimiminika kuelekea majiji makubwa ya Ulaya ya Mashariki. Barabara za majiji yenye uzuri ya Budapest, Prague, Zagreb, na miji mingine zaidi ya 20 zilifurikwa na watu waliovaa beji za buluu na nyeupe. Beji hizo ziliwatambulisha kuwa wapendao uhuru wa kimungu wanaohudhuria mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova.
Kwa mara ya kwanza kabisa, mikusanyiko ilifanywa kwa uhuru katika jamhuri za Urusi katika Ulaya, na vilevile Siberia ya mbali na jamhuri ya Asia ya Kazakhstan katika Urusi. Kwa jumla, zaidi ya wakusanyikaji 370,000 walifurahia ushirika mchangamfu katika Chekoslovakia, Hangari, Yugoslavia, Polandi, Romania, na Urusi.
Kwa wale ambao hawakuwapo, inaweza kuwa vigumu kuwazia mshangilio uliokuwapo wakati watu 74,252 walipokutana Urusi kumwabudu Yehova Mungu kwa wazi na bila hofu. Na bado, shangwe yao kubwa haingeweza kupita ile ya watu 74,587 katika Prague na 40,601 katika Budapest waliokusanyika katika stediamu kubwa zaidi katika Chekoslovakia na Hangari, au ile ya watu 14,684 waliokutana Zagreb, katika Yugoslavia.
Jambo hilo linatokeza sana kwa sababu miaka michache tu iliyopita, Mashahidi wa Yehova walikuwa chini ya marufuku katika nchi nyingi za Ulaya ya Mashariki. Uwasiliano wao na nchi za Magharibi ulikatishwa wakati wa Vita Baridi. Hata kukutana katika vikundi vidogo kumwabudu Mungu hakukuwa halali. Basi haishangazi kwamba kulikuwa na mshangilio huo kwa kuweza kukutana kwa uhuru katika mikusanyiko mikubwa!
Shahidi mmoja Mcheko mwenye umri wa miaka 59, aliyekuwa amefungwa kwa miezi minane katika kifungo cha upweke kwa sababu ya imani yake kwa Mungu, alisema: “Wengi wetu tulioishi Prague tuliota juu ya mkusanyiko mkubwa ambao ungeweza kupangwa katika stediamu hii, lakini hatukuamini kamwe kwamba ndoto hiyo ingegeuka kuwa kweli kihalisi kwa njia hii ya kustaajabisha.”
Majuma mawili kabla ya mkusanyiko wa Prague, Agosti 9 hadi 11, gazeti moja la jiji hilo, Večerník Praha, lilisema: “Wakishtakiwa kutaka kupindua serikali na kwa kugawanya usosholisti, Mashahidi wa Yehova waliwekwa katika magereza ya Ukomunisti kwa miaka mingi.” Baada ya kueleza kwamba karibuni jiji hilo lingekuwa ndilo lenye kupokea makumi ya maelfu ya Mashahidi, makala hiyo ilimalizia hivi: “Inaelekea kwamba wewe hutaweza kukutana na watu wengi sana wenye fadhili na tabasamu katika Prague wakati mwingine wowote kuliko wakati wa mwisho-juma wa pili wa Agosti.”
Hata hivyo, huenda ukauliza: ‘Je! Mashahidi wa Yehova walinyanyaswa hapo mbeleni kwa sababu inayostahili? Je! wao walikuwa tisho kamwe kwa wenye mamlaka wa serikali za nchi walimoishi? Wajumbe wa mkusanyiko wapatao mamia ya maelfu walitoka wapi katika Ulaya ya Mashariki? Wakiwa wamekandamizwa na kutengwa kwa miaka 40 au zaidi bila uwasiliano huru na nchi za Magharibi, wao waliwezaje kukua kufikia idadi hizo kubwa?’