Ukuzi Wenye Kutazamisha
MASHAHIDI WA YEHOVA hawajapata kamwe kuwa tisho kwa serikali za nchi wanamoishi, na hilo linatambuliwa sasa. Gazeti moja liitwalo Krasnoyarskiy Komsomolets likizungumzia kuhusu mmoja wa mikusanyiko hiyo ya kiangazi katika Urusi lilisema: “Wenye kushikilia mawazo wa nchi yetu wameng’amua hatimaye kwamba watu wa Yehova si tisho kwa sheria na utengamano wa umma kwa njia yoyote.”
Vivyo hivyo, gazeti la Urusi Vostochno-Sibirskaya Pravda liliripoti hivi: “Kwa kuwa shirika la Mashahidi wa Yehova hujihusisha na mambo ya kidini tu, wao hawashiriki mahitilafiano ya kisiasa na hawatii moyo washiriki wao kuunga mkono siasa za upande wowote, lakini wao huunga mkono mamlaka ya Biblia na Mtungaji wayo, Yehova Mungu.”
Ukuzi Katika Miaka ya Mapema
Kwa miongo mingi Mashahidi wa Yehova wamekuwa wenye kutenda katika Ulaya ya Mashariki. Tayari kufikia mwishoni mwa miaka ya 1930, Romania ilikuwa na zaidi ya elfu mbili yao, Polandi ilikuwa na elfu moja, na Chekoslovakia na Hangari mamia, na kulikuwa na makumi kadhaa katika Yugoslavia. Ingawa Urusi yenye eneo kubwa ilikuwa na idadi ndogo tu, hilo lilibadilika upesi.
Mtaalamu wa mambo ya Urusi, Walter Kolarz, alisema katika kitabu chake Religion in the Soviet Union kwamba Mashahidi wengine waliingia Urusi “kupitia maeneo yaliyotiishwa na Urusi katika 1939-40, ambapo kulikuwa vikundi vya Mashahidi wa Yehova vilivyo vidogo lakini vyenye kutenda sana.” Hivyo, Mashahidi walioishi sehemu za mashariki mwa Polandi, Chekoslovakia, na Romania walijipata ghafula wamehamishwa, kana kwamba kwa usiku mmoja, hadi Urusi!
Njia nyingine ya kutokeza ambayo Mashahidi wa Yehova waliingia Urusi ilikuwa ni kwa kambi za mateso za Ujerumani. Jinsi gani hivyo? Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya 2, wafungwa Warusi walijipata humo kambini pamoja na maelfu ya Mashahidi Wajerumani. Wajerumani hao walitupwa kwenye kambi hizo kwa sababu walidumisha msimamo thabiti wa kutokuwamo kwa Kikristo. (Yohana 17:16; 18:36) Wao walichagua kuteseka na kufa badala ya kuvunja sheria za Mungu kwa kujiunga na majeshi ya Hitla na hivyo kuwa wenye hatia ya kuua Wakristo wenzi katika nchi nyinginezo au hata kuua mtu yeyote kwa ujumla.—1 Yohana 3:10-12.
Hivyo, kama vile Kolarz alivyoandika, “hata isikike kuwa vigumu kuaminika jinsi gani, kambi za mateso za Ujerumani, ni mojawapo njia ambazo ujumbe wa Mashahidi wa Yehova ulifika Urusi. Ulipelekwa huko na wafungwa Warusi katika Ujerumani walioshangazwa na ujasiri na imara ya ‘Mashahidi’ na labda kwa sababu hiyo wakaona itikadi yao kuwa yenye kuvutia.” Katika kambi ya wanawake ya Ravensbrück pekee, Warusi makumi kadhaa wachanga waliripotiwa kuwa walikubali ujumbe wa Biblia uliotangazwa na Mashahidi wa Yehova.
Baada ya vita, wafungwa kutoka nchi za Ulaya ya Mashariki waliopata kuwa Mashahidi wa Yehova walirudi makwao. Huko, walifundisha kwa bidii kwamba utawala wa Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee la amani ya kudumu. Hivyo, idadi ya Mashahidi katika Ulaya ya Mashariki ikaongezeka kwa kutazamisha. Kufikia Aprili 1946, kulikuwa na zaidi ya watu elfu nne wenye kuhubiri katika Urusi, na idadi hii ilirudufika upesi. Katika Septemba 1946, Mashahidi katika Romania walikuwa na mkusanyiko Bucharest uliohudhuriwa na watu 15,000 hivi.
Punde baada ya hapo, Vita Baridi ikaanza, na hiyo ilikatiza usafiri na uwasiliano kati ya Ulaya ya Mashariki na nchi za Magharibi. Zaidi ya hiyo, serikali mpya zenye kutawala za Ulaya ya Mashariki zilianza kuwapinga Mashahidi wa Yehova. Kwa kusikitisha, waliwaona Mashahidi kuwa tisho, na wengi walifungwa. Ijapokuwa hivyo, kufikia 1951, Chekoslovakia ilikuwa na Mashahidi 3,705 watendaji; Hangari, 2,583; Yugoslavia, 617; na Polandi zaidi ya 15,000.
Walipingwa, na Bado Ukuzi Ukaendelea
Katika 1967, Maurice Hindus aliandika kuhusu Mashahidi wa Yehova katika kitabu chake The Kremlin’s Human Dilemma. Yale aliyosema yalitumika kwa Mashahidi katika Urusi pamoja na sehemu nyinginezo za Ulaya ya Mashariki. “Ingawa wanaendelea na shughuli zao kichinichini, wanawindwa na kukamatwa na kupewa hukumu kali. Lakini hawakomeshwi. Wakikandamizwa sehemu moja, wanajitokeza sehemu nyingine . . . Wanaonekana kuwa wasioweza kuharibiwa kama polisi wa Urusi.”
Wakati wa masika ya 1951, Mashahidi wa Yehova katika Urusi walipatwa na pigo kubwa. Zaidi ya elfu saba kati yao katika jamhuri za Ulaya za Urusi walikamatwa na kupelekwa kwenye kambi za wafungwa sehemu za mbali za nchi hiyo, kutia na Siberia na Vorkuta, katika kaskazini ya mbali. Tokeo likawa nini?
“Huo haukuwa ndio mwisho wa ‘Mashahidi’ katika Urusi,” akasema Kolarz, “bali ulikuwa mwanzo tu wa sehemu mpya ya kazi yao ya kutoa ushahidi. Hata walipotua katika stesheni wakielekea uhamishoni, walijaribu kueneza imani yao. Kwa kuwahamisha Serikali ya Urusi ilisaidia sana kusambazwa kwa imani yao. Wakiwa wametolewa kwenye upweke wa vijijini vyao, ‘Mashahidi’ hao waliletwa kwenye ulimwengu wenye eneo kubwa zaidi, hata kama huo ulimaanisha ulimwengu mbaya sana wa kambi za mateso na utumwa.”
Ndani na Nje ya Magereza
Kama vile Wakristo wa karne ya kwanza walivyoendelea kuhubiri bila kuacha waliponyanyaswa, ndivyo Mashahidi wa Yehova walivyofanya katika Urusi. (Matendo 5:42) Mlatvia aliyefungwa kwa madai ya uhalifu, aitwaye Helene Celmina, asema kwamba katika sehemu ya kambi ya Potma ambamo alifungiwa kuanzia 1962 hadi 1966, mlikuwamo wafungwa 350. “Karibu nusu yao,” yeye alisema, “walikuwa Mashahidi wa Yehova.” Katika kitabu chake Women in Soviet Prisons, Celmina aliandika kuhusu yale aliyoona humo kambini:
“Fasihi kutoka Brooklyn hufika kwa ukawaida, katika hali nzuri na kwa viasi vikubwa kupitia njia za kichinichini zilizopangwa vizuri . . . Hakuna yeyote angeweza kuelewa ni jinsi gani fasihi zilizopigwa marufuku zingeweza kuingizwa bara hili la waya za seng’enge na uwasiliano haba—na hasa zikitoka United States! Mashahidi wa Yehova wengi walihukumiwa miaka kumi ya kazi ngumu kwa kuwa tu na nakala chache za gazeti Mnara wa Mlinzi nyumbani mwao. Kwa kuwa watu wakipatikana na magazeti hayo hukamatwa, wasiwasi na ghadhabu ya wasimamizi wa kambi kuhusu kuwapo kwa fasihi hiyo kambini inaeleweka.”
Kwa msaada wa Yehova, hakuna kitu kingeweza kusimamisha usambazaji wa chakula hicho cha kiroho! Celmina aliandika: “Hakuna yeyote amegundua jinsi [Mnara wa Mlinzi] huingizwa kambini. Kwa vyovyote, baada ya kuhukumiwa, kila mfungwa hutolewa mavazi yote na kupekuliwa kabisa. Anapofika kambini kila mfungwa hupekuliwa kabisa kabisa kwa mara nyingine, hadi walinzi wanaporidhika. Mifuko ya kubebea vitu huchunguzwa kuhakikisha haina mifuko iliyositirika ndani yake. Hakuna mtu yeyote anayeruhusiwa kuingia kambini bila sababu nzuri. Wafungwa wanapopelekwa nje ya kambi kwenye maeneo ya kazi, wao huzungukwa na walinzi wenye silaha na hakuna mtu anayeruhusiwa kuwakaribia. Upekuzi wa makini hufanywa kwa kila mfungwa anaporudi kambini jioni. Lakini kujapokuwa uchunguzi huo wote, fasihi ya Brooklyn hufikia wasomaji wayo.”
Wakati uo huo, Wakristo dhabiti waliokuwa nje ya kambi za wafungwa za Urusi waliendelea na utendaji wao wa kuhubiri na kufundisha. Hiyo ilithibitishwa na vichapo na filamu zilizotolewa katika jitihada za kukinza huduma yao. Kwa mfano, katika 1978 kitabu The Truths About Jehovah’s Witnesses (Mambo ya Kweli Kuhusu Mashahidi wa Yehova) kilichapishwa, kwa kusudi la “kuelimisha wafuasi wa shirika hili la kidini kuhusu kutokuwako kwa mungu,” kama ilivyoelezwa kwenye utangulizi wacho.
Miongoni mwa mambo mengine, mwandikaji wacho, V. V. Konik, aliandika kwamba Mashahidi wa Yehova huwa na hotuba za watu wote sana sana kwenye maziko na arusi zao. “Kwa mfano,” yeye aandika, “mnamo Agosti 1973, katika kijiji cha Krasnaya Polyana, eneo la Krasnodarskiy, kulikuwa arusi ya washiriki wawili wa shirika hilo, iliyohudhuriwa na watu 500 hivi. Wahubiri sita waliwatolea hotuba, na hotuba zao zilienezwa kwa vikuza sauti viwili. Halafu drama ilifanywa kuonyesha jinsi Mashahidi wa Yehova huongoza mazungumzo na watu wa dini nyinginezo na wale wasioamini kuwako kwa Mungu.”
Ndiyo, kujapokuwa marufuku juu ya kazi yao, Mashahidi wa Yehova kote kote Ulaya ya Mashariki waliendelea kwa bidii kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu kwa kutii amri ya Kristo ya kiunabii. (Mathayo 24:14) Hatimaye, katika Mei na Juni 1989, Mashahidi wa Yehova walitambuliwa kisheria katika Polandi na Hangari, Aprili 1990 katika Romania, Machi 1991 katika Urusi, na Julai 1991 katika Bulgaria. Na kazi yao inaendelea katika Chekoslovakia pia bila kupingwa.
Wanamkusanyiko Wenye Furaha
Kwa kufikiria historia hiyo yao, labda waweza kuelewa vema zaidi kwa nini makumi ya maelfu ya wajumbe kwenye mikusanyiko ya Ulaya ya Mashariki walishangilia—wakilia, wakikumbatiana, wakipiga makofi, na kupungiana mikono kutoka upande huu hadi ule mwingine wa stediamu.
Budapest, Prague, na Zagreb ilipangwa iwe “mikusanyiko ya kimataifa,” na mipango ya pekee ilifanywa ili kuweza kupokea makumi ya maelfu ya wajumbe kutoka nchi nyinginezo. Katika Urusi, mikusanyiko ilifanywa katika majiji saba kukiwa na watu 74,252 waliohudhuria; Polandi ilikuwa na 131,554 kwenye mikusanyiko yayo 12; na 34,808 walihudhuria mikusanyiko 8 katika Romania. Ingawa Mashahidi hawakuweza kufanya mkusanyiko katika Bulgaria, karibu watu mia tatu kutoka huko walivuka mpaka kuingia Thesalonike, Ugiriki, ambapo walionea shangwe programu katika lugha yao wenyewe.
Halikuwa jambo rahisi kwa Mashahidi wa Ulaya ya Mashariki kuweza kutayarisha na kupokea maelfu ya wajumbe. Ebu wazia: Katika Urusi, hakujapata kamwe kufanywa mikusanyiko kama hiyo! Na ni kazi kubwa sana kuweza kushughulikia makumi ya maelfu ya wageni, jinsi Mashahidi wa Budapest na Prague walivyofanya. Isitoshe, wazia kufanya mkusanyiko katika Zagreb wakati kulipokuwa na tisho la vita vya wenyewe kwa wenyewe na milipuko ingeweza kusikika mbali!
Bila shaka, utasisimuliwa kusoma ripoti inayofuata kuhusu mikusanyiko hiyo.
[Ramani katika ukurasa wa 7]
SEHEMU TATU ZA MIKUSANYIKO YA KIMATAIFA NA MAHALI SABA PA MIKUSANYIKO KATIKA URUSI
URUSI
TALLINN
KIEV
LVOV
CHERNOVTSY
ODESSA
POLANDI
UJERUMANI
CHEKOSLOVAKIA
PRAGUE
AUSTRIA
HANGARI
BUDAPEST
ALBANIA
ITALIA
UGIRIKI
UTURUKI
[Ramani]
URUSI
ALMA-ATA
USOLYE-SIBIRSKOYE