Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 11/8 kur. 8-17
  • Walishangaa kwa Yale Waliyoona

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Walishangaa kwa Yale Waliyoona
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Watu Walishangazwa
  • Udugu wa Kimataifa
  • Kutayarisha Stediamu
  • Kushughulikia Wajumbe
  • Jitihada za Kuhudhuria
  • Ubatizo na Vichapo Vipya
  • Kutumia Uhuru Ifaavyo
  • Walishangilia Katika Ulaya ya Mashariki
    Amkeni!—1992
  • Muungano Unaostaajabisha Ulimwengu
    Amkeni!—1993
  • Mikusanyiko Uthibitisho wa Udugu Wetu
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Wajumbe wa Amani Katika Ulaya Mashariki
    Amkeni!—1997
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 11/8 kur. 8-17

Walishangaa kwa Yale Waliyoona

KATIKA kiangazi cha mwaka jana katika sehemu nyingi za Ulaya ya Mashariki pamoja na Kazakhstan na Siberia ya mbali, Mashahidi wa Yehova walionekana kwa njia wasizopata kuonwa kamwe. Wakazi wa huko na wageni waliokuwapo kwenye mkusanyiko katika sehemu hizo walivutiwa, naam, hata kushangazwa, na yale waliyoona.

Wajumbe wa Zagreb waliambiwa tena na tena: “Hatukudhani kuwa mngekuja!” Watalii wengineo wengi walikuwa wamefutilia mbali mipango yao ya kusafiri—lakini si Mashahidi wa Yehova. The Times ya London iliripoti hivi kuhusu mkusanyiko: “Huo, kwa hakika, ndio wa kwanza kupangwa na Mashahidi wa Yehova katika taifa lenye vita baina yalo lenyewe.”

Polisi hasa walistaajabishwa. Mmoja katika Zagreb alisema: “Ingekuwa vema kuwaonyesha watangazaji wa habari kile kinachotendeka katika stediamu hii, papa hapa, tunapowaona Waserbia, Wakroatia, Waslovenia, Wamontenegro, na wengine wamekaa mmoja kando ya mwingine kwa amani.”

Katika Budapest polisi mmoja aliulizwa alinganishe Mashahidi waliokusanyika stediamu hiyo kubwa na umati wa kandanda wa kawaida. Yeye alitabasamu, akainua kichwa, na kusema: “Tofauti iliyopo ni kama ile iliyo kati ya mbingu na dunia.”

“Unamaanisha nini?”

“Ebu tazama tu,” akajibu. “Hakuna yeyote anayevuta sigareti, hakuna takataka mahali popote, na watu ni wenye adabu. Wanafanya yale unayowaambia wafanye.”

Katika Kiev, jiji kuu la Ukraine, watu 14,654 walikutana katika Stediamu ya Dynamo, wachache wao ambao waweza kuonwa kwenye jalada la mbele la gazeti hili. Shahidi mmoja huko alimwuliza mmoja wa makapteni wa polisi kama polisi wenzake walikuwa na kazi ngumu wakati wa mkusanyiko. “La, wakati ule utakaofuata tutawaletea polisi wawili tu.”

“Mbona wawili?” yeye akaulizwa.

“Iwapo mmoja analala usingizi,” akajibu kwa ucheshi, “yule mwingine anaweza kumtunza.”

Watu Walishangazwa

Gazeti la Budapest, liitwalo Pesti Hírlap, liliripoti: “Watu zaidi ya 40,000 walikuwako Népstadion mwisho-juma huu. Hakukuwa na karatasi, baki la mkate, wala baki la sigareti lililoachwa.” Gazeti jingine la jijini liitwalo Fehérvár Hírlap, lilisema: “Wale walioingia stediamu ya Népstadion bila kupangia kati ya Julai 26 na 28 bila shaka walishtuliwa. . . . Wangeweza kuona mfano wa mwenendo wa Kikristo na njia ya maisha inayoonwa mara chache sana.”

Mwisho-juma huo mvua kubwa ilinyesha Budapest; zaidi ya milimita hamsini. Lakini haikuwazuia Mashahidi. Polisi mmoja alisikika akisema “Ni ajabu kabisa! Inaduwaza akili!” “Wanaendelea kuja tu . . . Hakuna kitu kiwezacho kuwazuia.” Jumatatu gazeti moja lilikuwa na kichwa kikuu cha makala “Sala Kwenye Mvua” na likanukuu wajumbe wakisema: “Sisi tunanyeshewa tu na mvua, hatuchukuliwi mbali nayo!”

Katika Lvov, ambapo 17,531 walikutana kwenye Stediamu ya Central Ukraine, ofisa mmoja wa polisi alimwambia mmoja wa Mashahidi hivi: “Katika tukio jingine lolote la watu wengi ambapo kuna umati mkubwa unaohudhuria, tungehitaji mamia ya polisi. Kwenye mkusanyiko wenu tulikuwa na kumi, na hawakuhitajika kikweli.”

Halafu, akifunua jinsi alivyovutiwa sana na mkusanyiko huo, ofisa huyo akasema: “Mnafanya vema sana kufundisha wengine yaliyo mema, mnasema juu ya Mungu, na hamjiingizi katika jeuri. Tulikuwa tukizungumzia kwa nini tuliwanyanyasa, na tukakata kauli kwamba hatukuwa tumewasikiliza na hatukuwa tumejua lolote kuwahusu.”

Baada ya ziara yake kwenye mkusanyiko wa Usolye-Sibirskoye, Siberia, ripota wa gazeti la Urusi Leninskiy Put’ aliandika: “Ilishangaza kuona adabu, pamoja na uwezo wa kuona na kuitikia mahitaji ya wengine, ambayo watumishi wa Yehova walionyesha mmoja na mwenzake. Sitasahau kamwe maneno yaliyosemwa kwenye mkusanyiko: ‘Usiibe! Usiseme uwongo! Usinywe [kupindukia]! Uwe mwenye bidii! Saidia jirani yako!’ Kwa vyovyote, kanuni hizo ndizo watu kwa ujumla wanapaswa kujitahidi kutimiza. Lakini mara nyingi sisi huzisahau.

Wenye kuvutia pia, ni mwelekeo wa kindugu ulioonyeshwa kwa wengine, na hiari ya kusaidia. Mwanamke mmoja alitupatia gazeti ili tusiketie benchi yenye vumbi. Kulipoanza kunyesha, mwanamke mchanga aliyeketi kando yangu alinipatia mwavuli wake kwa tabasamu, na hapo karibu mwanamume alimvuta kihalisi mvulana aliyeloweshwa na mvua aingie chini ya mwavuli wake. . . .

“Hali yenyewe ya mkusanyiko ilifanya mtu awe mwema zaidi, mwenye adabu zaidi, na mstaarabu zaidi. Ilikuwa haiwezekani kukosa kuitikia kwa tabasamu yenye fadhili iliyoonyeshwa na wageni. . . . Tuliondoka stediamu tukihisi kuwa tumesafishwa, tukihisi kuwa tulipata kitu chema sana.”

Kwa habari ya mkusanyiko wa Kiev, zaidi ya 2,000 walikuja kutoka Moscow na 4,500 hivi kutoka Kaukasus. Dawati la habari liliwekwa kwenye uwanja wa ndege, na fasihi za Biblia zikaonyeshwa. Wengi waliuliza maswali yaliyojibiwa kwa fadhili. Jioni moja mwanamume mmoja alikaribia na kusema: “Nimekuwa nikiwatazama kwa muda mrefu. Nimeshangazwa na jinsi mnavyotumia fadhili kusema na watu kuhusu Ufalme. Tafadhali niruhusuni niwape maua haya yakiwa zawadi kwa ajili ya kazi yenu bora.”

Wakati wa ubatizo kwenye mkusanyiko wa Usolye-Sibirskoye, mwandishi mmoja wa habari alivutiwa alipoona idadi fulani ya Warusi wakikumbatia na kupongeza mtu aliyetoka kubatizwa aliye wa jamii ya Waburyat. Ingawa kwa ujumla Siberia haina ubaguzi wa kitaifa, urafiki halisi kati ya Warusi na watu kama hao si wa kawaida. “Mliwezaje kushinda mipaka ya kitaifa?” mwandishi habari huyo akauliza.

“Kwa kutumia kanuni ya Biblia ‘umpende jirani yako kama nafsi yako,’” yeye akaambiwa.

Udugu wa Kimataifa

Kile kilichochangamsha moyo sana hasa kwenye mikusanyiko mitatu ya kimataifa ni ule mbadilishano wa upendo kati ya wajumbe kutoka ulimwenguni pote. Budapest lilikuwa na wageni kutoka nchi 35, wengi wao kutoka Polandi na Ujerumani, lakini wawakilishi wengi kadiri fulani walitoka sehemu nyinginezo pia, kutia ndani 500 hivi kutoka Urusi. Prague lilikuwa na wajumbe kutoka nchi 39, kutia zaidi ya 26,000 kutoka Ujerumani, karibu 13,000 kutoka Polandi, zaidi ya 900 kutoka Italia, 819 kutoka Uholanzi, 746 kutoka Swedeni, na 743 kutoka Japan. Zagreb lilikuwa na wageni kutoka nchi 15, kujapokuwa na tisho la vita vya wenyewe kwa wenyewe.

Kwenye kila mkusanyiko wa kimataifa, majukwaa matatu yaliwekwa uwanjani yakikabili sehemu tofauti za stediamu. Kutoka kwa majukwaa hayo programu nzima ilitolewa wakati ule ule katika lugha tatu. Katika Budapest lugha zilikuwa Kihangari, Kipolandi, na Kijerumani; katika Prague kulikuwa lugha ya Kicheki/Kislovaki, Kipolandi, na Kijerumani; na katika Zagreb kulikuwa na lugha ya Kikroatia/Kiserbia, Kislovenia, na Kiitalia. Wakati wa drama ya Kibiblia yenye kufundisha, iliyokazia maono ya Ezra wa kale na washiriki wake, wajumbe wenye kusema lugha tofauti wangeweza kutazama wonyesho huo kutoka kwa sehemu yoyote ya lugha waliyochagua kuketi.

Hotuba nyingi za msingi za mkusanyiko zilitolewa kwa Kiingereza wakati ule ule na washiriki tofauti wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova. Kila mmoja wa hao alisema akiwa kwenye moja ya majukwaa yale matatu. Bila shaka, hotuba hizo zilitafsiriwa kwa faida ya vikundi vile vitatu vya lugha maarufu, na katika Budapest na Prague, zilitafsiriwa katika lugha nyingine nyingi pia.

Watafsiri mbalimbali wa sehemu hizo za lugha walisimama uwanjani wakiwa mbele ya kikundi chao cha lugha. Kuelekezwa kwa vikuza sauti kwenye sehemu hiyo hususa ya lugha kuliwezesha watu wasikie lugha yao bila kusumbuliwa na tafsiri inayotolewa katika lugha nyinginezo katika sehemu nyingine. Katika Budapest, kwa mfano, hotuba za washiriki wa Baraza Linaloongoza zilitafsiriwa katika Kiholanzi, Kifinlandi, Kifaransa, Kigiriki, Kiitalia, Kijapan, Kinorwei, Kihispania, na Kiswedeni, kuongezea na lugha za msingi za Kihangari, Kipolandi, na Kijerumani.

Kwenye kila mkusanyiko wa kimataifa, hotuba ya mwisho yenye kuchochea ilitolewa na washiriki watatu wa Baraza Linaloongoza. Tatizo kwao lilikuwa ni kumaliza kwa wakati ule ule kwa kadiri iwezekanavyo. Baadaye, sauti za watu wa mataifa mengi zilijiunga kuimba, na hatimaye mioyo iliunganishwa kwa sala ya kusihi ya kumshukuru Yehova kwa kubariki kwa mafanikio mikusanyiko hiyo ya ajabu.

Wakati “Amina!” ya kumalizia iliposemwa, hakuna yule aliyetaka kuondoka. Machozi yalitiririka maelfu ya nyuso. Kutoka pande mbalimbali za stediamu hizo kubwa, vitambaa, shali (kitambaa kizito cha mabegani), na miavuli ilipungwa huku na huku katika salamu za kuagana na rafiki wapendwa waliodumisha uaminifu wa kimaadili kwa Mungu walipokabiliwa na marufuku na vifungo vya miaka mingi. Katika Prague rafiki wengi walibaki kwa zaidi ya saa moja, wakiimba na kufurahia ushirika.

Haikuwa bila jitihada kwamba mikusanyiko hiyo ikaweza kufanikiwa ajabu. Mamia ya maelfu ya saa zilitumika kihalisi na Mashahidi wa Yehova si katika kufanya matayarisho ya kuhudhuria tu bali pia katika kushughulikia mamia ya mambo madogo madogo yaliyo ya lazima ili kufanikisha mikusanyiko hiyo.

Kutayarisha Stediamu

Stediamu kubwa sana ya Strahov katika Prague, ambayo haikuwa imetumiwa kwa mkusanyiko mkubwa wa watu kwa miaka mingi, ilihitaji marekebisho makubwa. Kulikuwako tu viti 55,000 hivi vinavyoweza kutumiwa, na hivyo havingewatosha waliotarajiwa kuwako kwenye mkusanyiko huo wa kiangazi ulio mkubwa zaidi katika Ulaya ya Mashariki. Kwa hiyo mashine iliyoharibika ya kupiga randa ilipatikana, ikarekebishwa, na kutumiwa kujengea benchi zenye umbali wa kilomita 19 za kukaliwa na watu karibu 30,000 zaidi.

Bila shaka, kutengeneza na kupanga benchi kulikuwa sehemu tu ya kazi yenyewe. Kupaka rangi, kusafisha, kuondoa magugu, na marekebisho ya ujumla yalihitajika. Hatimaye, stediamu hiyo ilirembeshwa kwa vyungu 8,300 vya maua vikiwa na maua 33,200 na miti ya msonobari 1,357. Nyakati nyingine wafanyakazi elfu moja walikuwako. Kwa ujumla saa 66,000 zilitumiwa na wafanyakazi wa kujitolea kutoka makundi 260 ya Mashahidi wa Yehova.

Kazi iyo hiyo ilifanywa Budapest, Zagreb, na majiji mengine ili kutayarisha stediamu. Katika Lvov wafanyakazi wa kujitolea 4,000 walitumia zaidi ya saa 40,000 wakifanya kazi kwenye stediamu. Kazi yao ilionwa kuwa malipo ya kodi ya stediamu. Benchi zote kwenye stediamu zilirekebishwa na kupakwa rangi, na vyoo vyote vikasafishwa na kurekebishwa. Pia, jengo lenye urefu wa mita 30 lilijengwa likiwa na vyoo vya ziada. Vivyo hivyo, katika Stediamu ya Khimik katika Usolye-Sibirskoye, vyoo 52 vya ziada vilijengwa vya kutumiwa wakati wa mkusanyiko.

Mhandisi mkuu kwenye stediamu ya Lvov alisema: “Katika maisha yangu yote, sijapata kuona watu wa ajabu kama hao. Mnafanya kazi mkiwa familia moja kubwa. Siwezi kuelewa hilo, lakini kufanya kazi pamoja nanyi kunapendeza sana.” Wasimamizi wa stediamu walitayarisha taarifa ambamo waliwashukuru Mashahidi “kwa kujitoa sana kwa kazi waliofanya na kwa sifa zao njema na kujali madaraka.” Taarifa hiyo ilimalizia: “Tunawatakia mkusanyiko wenye mafanikio katika Lvov.”

Katika Kiev sakafu ya chumba ambacho kingetumiwa kutayarishia chakula ilihitaji kurekebishwa. Kwa siku mbili kazi hiyo ilimalizika. Wafanyakazi wawili wa stediamu walikuja kuona “muujiza huo,” mmoja akimwambia yule mwingine: “Kwa siku mbili wamekamilisha kazi ambayo huchukua watu wetu nusu mwaka kukamilisha.” Msimamizi wa kilabu cha michezo ya kuogelea alimwambia mwangalizi wa mkusanyiko: “Mliibadili stediamu sana hivi kwamba sisi hatuwezi kuitambua tena.”

Wafanyakazi wa stediamu ya Kiev waliandika hivi kwa kushukuru: “Tunasisimuliwa mioyoni na utaratibu wa mkusanyiko wa Mashahidi wa Yehova. . . . Kama vile ambavyo vijito vya chemchemi za maji huungana na kufanyiza kijito chenye kufurika, ndivyo kijito cha Mashahidi wa Yehova wadogo kwa wakubwa kinavyotiririka pamoja kwenye karamu yao. Hilo linastahili kustaajabiwa. Tunaliona kwa mara ya kwanza. Tunawashukuru kwamba mmetufunza jambo fulani kwa mfano wenu.”

Kushughulikia Wajumbe

Miongoni mwa kazi zilizokuwa ngumu zaidi ni kupangia mahali pa kulala maelfu ya wageni. Mashahidi wa huko waliwakaribisha wajumbe nyumbani mwao. Kwenye mkusanyiko wa Prague, Mashahidi Wacheki waliwapokea wageni 6,280 kutoka Polandi nyumbani mwao wenyewe. Katika Budapest, wajumbe 2,203 walikaa katika nyumba za faragha. Na Mashahidi 278 wa Kiev waliwapokea wageni 750 hadi 800.

Kwa kuongezea, shule nyingi na majumba ya mazoezi ya mwili katika Budapest na Prague zilitumika kuwa mahali pa kulala. Shule zaidi ya 40 zilitumiwa Budapest ili kuwapokea watu 7,930. Katika Prague, 12,530 walilala katika majumba ya mazoezi ya mwili na shule. Maelfu ya magodoro ya hewa yalinunuliwa ili kutumiwa sehemu hizo. Wajumbe zaidi ya 29,000 waliohudhuria mkusanyiko wa Prague walikaa katika mabweni ya wanafunzi na majumba ya kulala ya wageni, na maelfu zaidi walipokewa katika hoteli za kawaida.

Kwenye baadhi ya mikusanyiko, mipango ilifanywa ili wajumbe walale ndani ya magari ya moshi yaliyowaleta. Mashahidi wapatao elfu mbili kutoka Zakarpatskaya Oblast walitumia makochi ya magari ya moshi kuwa mahali pa kulala katika Kiev. Wengine kutoka Kaukasus waliokuja Kiev walifanya vivyo hivyo. Vivyo hivyo, Mashahidi Walithuania waliosafiri kwenda mkusanyiko wa Tallinn, Estonia, walilala katika magari ya moshi yaliyowaleta.

Hata baada ya kuwasili, wajumbe walishughulikiwa kwa njia nyingi na wapokezi wao wenye ufikirio. Kwa mfano, mipango ilifanywa Prague ya kuendesha mabasi 40 ili kuimarisha usafiri kwenye barabara inayoshughulikiwa na basi moja tu kwa kawaida. Isitoshe, kwa sababu ya malipo ya mapema, wajumbe waliweza kusafiri bila malipo kwenye usafiri wa umma kuelekea mkusanyiko asubuhi na kuelekea nyumbani jioni kwa kuonyesha tu kadi zao za mkusanyiko. Katika Urusi, mabasi 11 yaliyoelekea mkusanyiko Usolye-Sibirskoye kutoka Angarsk isiyo mbali yalisindikizwa na magari mawili ya polisi wa barabarani, moja likiwa mbele na lingine nyuma!

Jitihada za Kuhudhuria

Wajumbe walioelekea hasa mikusanyiko fulani ya Urusi walisafiri mwendo mrefu wakijilipia nauli wenyewe. Wengine waliweka akiba ya fedha mwaka mzima ili waweze kulipia nauli. Kikundi cha wajumbe kilitoka bandari ya Vladivostok ya Bahari ya Pasifiki, kikisafiri zaidi ya kilomita 3,200 hadi Usolye-Sibirskoye. Wajumbe wengine kumi na wawili walitoka kisiwa cha Sakhalin katika Bahari ya Pasifiki kaskazini mwa Japan. Mmoja wao alikuwa kijana mwenye umri wa miaka 20 aliyeandamana na vijana wengine watatu ambao yeye huwafunza Biblia.

Dereva wa basi kutoka Sayanogorsk, aliyekusudia kubatizwa Usolye, alimwuliza-uliza mwajiri wake apate siku chache za kupumzika ili ahudhurie mkusanyiko, lakini mkubwa wake hakutaka aende. Kwa hiyo mtu huyo aliendesha basi hadi jiji la Abakan na kupata nakala ya hati ya Urusi ya March 27 ya mwaka uliopita iliyowatambua rasmi Mashahidi wa Yehova kuwa shirika la kidini. Hata ingawa alionyeshwa hati hiyo, mkubwa wake bado alikataa kumpa ruhusa ya kuondoka. Mapema kwenye siku ya kuondoka kwake, baada ya kusali kwa bidii, mtu huyo alifanya maombi tena na hatimaye akapata ruhusa ya kwenda.

Ubatizo na Vichapo Vipya

Ubatizo ulikuwa jambo lenye kusisimua kwenye mikusanyiko hiyo yote ya Ulaya ya Mashariki. Kwa tendo hilo la ufananisho la kuzamishwa majini, watu 18,293 waliohudhuria mikusanyiko hiyo waliingia kwenye rekodi mbele ya mashahidi kwamba walikuwa wameweka maisha zao wakfu kumtumikia Yehova Mungu bila masharti yoyote. Kijana mmoja aliyebatizwa katika Prague, ambaye alikuwa amepewa kazi yenye mshahara mzuri, alisema: “Nilihisi kwamba nilikuwa na uchaguzi kati ya mungu wa utatu aliyefanyizwa na dola ya U.S., marki ya Ujerumani, na shilingi ya Austria kwa upande mmoja na Yehova upande ule mwingine. Nilichagua Yehova na nikakataa kazi hiyo.”

Ubatizo katika Tallinn ulifanywa katika kidimbwi cha nje karibu na Bahari ya Baltiki mahali ambapo boma la zamani lililotumiwa kuwa gereza lingeweza kuonwa kwa mbali. Humo Mashahidi wengi Waestonia walifungiwa kabla ya kupelekwa kwenye kambi za mateso Urusi mapema katika miaka ya 1950. Ulikuwa msisimuko ulioje, hasa kwa walio wazee-wazee, kuona waamini wapya 447 wakionyesha wakfu wao kwa Yehova kwenye sherehe ya hadharani!

Jambo jingine la kupendeza kwenye mikusanyiko hiyo lilikuwa ni kutolewa kwa vichapo vipya. Ndugu Walithuania katika Tallinn waliruka kihalisi kutoka kwa viti vyao na kulia walipoambiwa kwamba broshua “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya” sasa inapatikana katika lugha yao. Vivyo hivyo, jambo kuu la mikusanyiko Romania lilikuwa ni kutolewa kwa kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! katika Kiromania, na kwa Wacheki na Waslovaki katika Prague, ilikuwa ni kupokea New World Translation of the Holy Scriptures katika lugha zao.

Na bado, kwenye mikusanyiko mingi, kitolewaji kilicholeta furaha ya kupita yote ni kitabu kipya Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi. Tayari nakala milioni kumi zimechapishwa katika lugha 59.

Kutumia Uhuru Ifaavyo

Leo, fasihi ya Biblia inakubaliwa Ulaya ya Mashariki, kutia na Urusi. Malori yaliyojazwa Mnara wa Mlinzi na Amkeni! huondoka kwenye matbaa kubwa za uchapishaji za Mashahidi wa Yehova katika Selters/Taunus, Ujerumani, na kuvuka mipaka na kuingia nchi za Ulaya ya Mashariki. Ni tofauti kama nini na nyakati ambapo, huku Mashahidi wakijasiria kufungwa, walilazimika kuingiza fasihi kisirisiri katika nchi hizo!

Ili kutoa kielezi cha badiliko hilo nzuri ajabu, mazungumzo yafuatayo yalikuwa kati ya ofisa wa forodha na mmoja wa Mashahidi wa Yehova karibu na wakati wa mkusanyiko katika Tallinn:

“Ni nini kilichomo ndani ya katoni hiyo ndogo?”

“Magazeti.”

“Magazeti gani? Je! ni magazeti ya Mungu?”

“Aah, ndiyo.”

“Magazeti ya Yehova Mungu?”

“Naam!”

“Jaa’a, ni vizuri. Unaweza kusonga mbele.”

Baada ya mkusanyiko wa Budapest, rais wa Hangari, Arpad Goncz, alimwalika Shahidi mmoja aliyeshiriki seli moja pamoja naye wakati wa uonezi wa Kikomunisti. Bw. Goncz alitumia muda wa saa moja pamoja naye na baadaye akamwomba huyo aliyekuwa hapo zamani ameshiriki seli pamoja naye awapelekee Mashahidi wa Yehova salamu zake. Wapendao uhuru wa kimungu kila mahali wana shukrani kikweli kwamba maofisa walioko sasa, kama vile Bw. Goncz, wanaruhusu uhuru wa ibada katika Ulaya ya Mashariki.

Ili kuonyesha kwamba watu wa Yehova wanatumia uhuru wao ifaavyo, The New York Times la Septemba mwaka jana likizungumzia mandhari moja katika St. Petersburg (Leningrad hapo mbeleni), lilieleza: “Maandishi ya Gershwin ya ‘Wakati wa Kiangazi’ huelea juu ya maji ya Mto Neva . . . Maandishi hayo yanaelea yakipita waotaji jua wanene, watoto wanaofukuza mbwa, wachuuzi wanaouza ramani za St. Pertersburg ya zamani na Mashahidi wa Yehova wanaotafuta waongofu.”

Naam, Mashahidi wanatumia uhuru wao kwa kuhubiri habari njema kwa bidii! Je! ungependa kujua mengi zaidi kuhusu ujumbe wao? Gazeti la Urusi Vostochno-Sibirskaya Pravda lilieleza: “Habari nyingi zenye mambo madogo-madogo kuhusu utendaji wao zaweza kupatikana kwenye mahali mbalimbali pa elimu ya Biblia pa Mashahidi wa Yehova katika jiji lolote.” Mahali popote unapoishi ulimwenguni, usisite kuulizia.

MIKUSANYIKO KATIKA ULAYA YA MASHARIKI NA URUSI

Nchi Kilele cha Hudhurio Waliobatizwa

Chekoslovakia (Prague) 74,587 2,337

Hangari (Budapest) 40,601 1,134

Polandi (majiji 12) 131,554 4,250

Romania (majiji 8) 34,808 2,260

Urusi (majiji 7) 74,252 7,820

Yugoslavia (Zagreb) 14,684 492

Jumla mikusanyiko 30: 370,486 18,293

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Kulia: Kutafsiria vikundi vya lugha tofauti katika Prague

Chini: Stediamu ya Strahov katika Prague yenye wajumbe zaidi ya 74,000

[Picha katika ukurasa wa 10]

Juu: Mkusanyiko katika Tallinn, Estonia

Mkusanyiko wa Budapest, ambapo, kuwe mvua au jua, wajumbe 40,000 walifurahia programu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Juu: Baadhi ya vyoo vilivyojengwa vitumiwe kwenye mkusanyiko wa Usolye-Sibirskoye, Siberia

Kupaka stediamu rangi na kutengeneza mabenchi ya ziada ya kukalia katika Prague

[Picha katika ukurasa wa 16]

Drama ya Biblia na ubatizo katika Zagreb

[Picha katika ukurasa wa 17]

Juu: Kuwekwa wakfu kwa Jumba la Ufalme la kwanza Juni 1991 lililojengwa na Mashahidi katika Hangari

Katikati: Watu zaidi ya 20,000 walilala kwenye majumba ya mazoezi ya mwili na shule katika Budapest na Prague

Chini: Kugawanywa kwa kitabu “Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi” katika Usolye-Sibirskoye, Siberia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki