Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g97 3/8 kur. 22-25
  • Wajumbe wa Amani Katika Ulaya Mashariki

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wajumbe wa Amani Katika Ulaya Mashariki
  • Amkeni!—1997
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Viziwi “Wasikia” Katika Budapest
  • Kushiriki Kweli na Wengine
  • Kutoka Kuwa Mkatoliki Hadi Mkomunisti Hadi Kuwa Shahidi
  • Ripoti Nzuri za Vyombo vya Habari Katika Poland
  • Nchi Ndogo ya Estonia Yapata Ushahidi Mkubwa
  • Viziwi Pia “Wasikia” Katika Estonia
  • “Jambo Jipya Katika Drama ya Agano Jipya”
  • Walishangaa kwa Yale Waliyoona
    Amkeni!—1992
  • “Tumegawanywa na Lugha Lakini Tumeunganishwa na Upendo”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Mikusanyiko Uthibitisho wa Udugu Wetu
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
  • Polandi Yakaribisha Mashahidi wa Yehova
    Amkeni!—1990
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1997
g97 3/8 kur. 22-25

Wajumbe wa Amani Katika Ulaya Mashariki

VIZIWI walikuwa wakisikia! Wafungwa walikuwa wakipata uhuru! Polisi hata hawakuwa na kitu cha kufanya! Tunazungumzia nini? Tunarejezea kile kilichotukia katika mikusanyiko ya kimataifa ya Mashahidi wa Yehova iliyofanywa majuzi katika Ulaya Mashariki katika miezi ya Julai na Agosti ya mwaka uliopita.

“Wajumbe wa Amani ya Kimungu” kilikuwa ndicho kichwa cha programu hiyo, na watu wengi waliona kwamba japo matatizo yaliyochochewa na makasisi katika Rumania,a Mashahidi wa Yehova wana amani itokanayo na kumjua Mungu na Kristo Yesu.—Isaya 26:2, 3; Wafilipi 4:7.

Mikusanyiko ilifanywa katika Prague, Jamhuri ya Cheki; Budapest, Hungaria; Warsaw na Lodz, Poland; Tallinn, Estonia; na Brasov na Cluj-Napoca, Rumania.

Wajumbe kutoka nchi nyingi za kigeni walihudhuria mikusanyiko hii na kutokeza mandhari ya kimataifa kwenye matukio hayo. Katika Prague kulikuwa na vikundi vikubwa kutoka Ujerumani, Japani, Poland, na Marekani. Ripoti moja kutoka ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika Cheki ilisema hivi: “Tulitiwa moyo sana na waabudu wengi wa Yehova Mungu wenye kushika ukamilifu wa maadili kutoka nchi nyinginezo. Kwa mfano, wengi wa wajumbe Wajapani walikuwa mapainia, na mavazi yao nadhifu na utaratibu wao ulipamba waziwazi sehemu ya stediamu waliokuwa wameketi. Tuliona pia ukunjufu wa wajumbe wa Poland, shukrani za ndugu Waslovakia, ukarimu wa Wajerumani, uchangamfu wa Wamarekani. Wote walitupa somo fulani.”

Washiriki wapya waliathiriwaje na mikusanyiko hiyo? Mtu mmoja mwenye umri wa miaka 85 ambaye ni msomi, mwandikaji, na mtaalamu wa lugha alihudhuria, ijapokuwa anaugua ugonjwa wa kisukari na maradhi fulani ya mguu. Amekuwa akijifunza Biblia kwa msaada wa kitabu Ujuzi kwa miezi sita hivi. Wakati wa programu, yeye alikuwa akikazia, si utaalamu na sarufi ya lugha, bali jambo jingine. “Ilikuwa nzuri ajabu!” akapaaza sauti. “Upendo na ufikirio ambao mnao miongoni mwenu ni zaidi ya maneno tu.”—Yohana 13:34, 35; 1 Wakorintho 13:1-8.

Wageni kutoka nchi za nje katika Prague walifurahia kuzuru sehemu za kihistoria na kutoa ushahidi wa vivi hivi kila pindi. Katika ngome moja kusini ya Prague, Shahidi mmoja wa Marekani, ambaye ni mke wa wakili, alikuwa akingoja juu ya mnara wa ngome hiyo ili atoe trakti katika lugha ya Cheki kwa wale wote waliopanda ngazi hizo. Wengine walitoa trakti walipokutana na kikundi cha wanafunzi wasichana kilichozuru kaburi la zamani la Wayahudi. Na, bila shaka wote watembezi wa wageni na madereva wa basi walipokea fasihi.—1 Petro 3:15.

Mtembezi mmoja aliyeshukuru Mashahidi kwa mwenendo wao aliandika: “Sijapata kamwe kukutana na watu wengi wenye urafiki na uchangamfu kama nyinyi, maishani mwangu mwote. Ingawa mimi ni Mkatoliki, nilivutiwa na mtazamo wenu wa kiroho. Nyinyi nyote mlinipa tumaini fulani kwamba kuna wakati ujao kwa wanadamu. Acheni niwashukuru kwa fadhili yenu. Mungu awabariki!”

Ingawa mvua kubwa ilinyesha Ijumaa katika Prague, familia ziliketi nje katika stediamu, zikitwaa chakula cha kiroho kilichotolewa na wasemaji wa huko na wa kigeni. Kulikuwa na vitoto vingi huko kiasi cha kwamba ili kuepuka aksidenti katika vijia, eneo fulani la kuegesha vigari vya pekee vya kubebea watoto lilitengwa nje ya stediamu.

Mkusanyiko wa Prague ulihudhuriwa na zaidi ya watu 22,000, na Mashahidi wapya waliojiweka wakfu 432 walibatizwa, kutia ndani watu wawili wenye kutumia viti vya magurudumu na wengine watano ambao hawajiwezi kimwili.

Viziwi “Wasikia” Katika Budapest

Jiji maridadi la Budapest, ambalo limevuka Mto Danube lilikuwa mahali pa mkusanyiko wa kimataifa katika Julai. Kilele cha watu 23,893 walihudhuria, kutia ndani wajumbe 3,341 kutoka nchi 11 bila kuhesabu Hungaria.

Katika hema iliyokuwa karibu na jukwaa, programu nzima ilitafsiriwa kwa viziwi, na wapatao 100 walihudhuria. Katika maneno ya ukaribishaji kwa wajumbe wote wasiofahamu Kihungaria, viziwi walikaribishwa kipekee, kwa maneno: “Lugha moja ambayo hatutaki kusahau kutaja na ambayo programu nzima itatafsiriwa ni lugha ya ishara. Tunafurahi kuwa na viziwi miongoni mwetu.”

Kushiriki Kweli na Wengine

Kwenye mikusanyiko hii fasihi mpya za Biblia zilitolewa, kutia ndani kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia. Baada ya kupokea kichapo hiki, wajumbe wa Ufaransa walipanda basi kurudi hoteli yao. Njiani waliona bwana na bibi arusi pamoja na wageni wao wa arusi. Ndugu hao walimwomba dereva asimamishe basi hilo. Mmoja wa Mashahidi hao akatoka nje na kuwapa wenzi hao kitabu hicho kipya katika Kihungaria. Walikichukua mara moja na kuanza kukipitia mara hiyo. Labda hicho kilikuwa mojawapo ya nakala za kwanza kabisa kuangushwa baada ya kutolewa!

Kutoka Kuwa Mkatoliki Hadi Mkomunisti Hadi Kuwa Shahidi

Wale watu 510 waliobatizwa katika mkusanyiko huu walikuwa asilimia 2 ya wahudhuriaji. Watatu kati ya Mashahidi hao wapya wangali wamo gerezani, wakiwa wamefungwa kwa sababu ya uhalifu waliokuwa wamefanya kabla ya wao kujifunza kweli ya Biblia. Ndugu wa huko huwazuru kwa ukawaida na kuongoza mafunzo ya Biblia na wengine. Katika gereza moja la Budapest, karibu wafungwa 50 wanafundishwa Biblia.

Mtu mmoja aliyelelewa katika shule ya Katoliki ya Benedict aliacha kuamini Kanisa Katoliki na, akiwa na umri wa miaka 20, akawa mshiriki wa Chama cha Ukomunisti. Baadaye alijiunga na jeshi na kupanda cheo hadi kuwa luteni. Akiwa mshiriki wa Wanamgambo wa Wafanyakazi, yeye alifundisha nadharia ya Marx na Lenin kwenye chuo kikuu. Yeye alivutiwa na shime ya Kikomunisti ya “uhuru, udugu, usawa.” Lakini, kwa sababu watu wenye mamlaka walitumia vibaya shime “serikali ya watu,” yeye alifikiria tena Ukomunisti. Akahisi kwamba kuna kasoro. Hatimaye, alistaafu. Mashahidi walipobisha mlango wake, alikuwa tayari kusikiliza. Yeye aripoti: “Katika ziara yangu ya kwanza katika Jumba la Ufalme, nilisadiki kwamba hatimaye huu ulikuwa udugu wa kweli. Nilizingirwa na upendo wa wafuasi halisi wa Kristo. Mgeuko wangu kutoka kuwa Mkomunisti hadi kuwa Shahidi ulichukua miaka minne. Lakini nimechagua kweli.” Alibatizwa kwenye mkusanyiko huo.

Kwa polisi, hali huwa tofauti kufanya kazi kwenye mkusanyiko. Polisi mmoja aliyepewa mgawo wa kufanya kazi kwenye malango ya stediamu alisema kwamba kazi katika mikusanyiko ya Mashahidi ni ngumu sana. Kwa nini? Kwa sababu kila kitu ni shwari hivi kwamba ni lazima polisi wajitahidi wasilale usingizi!

Ripoti Nzuri za Vyombo vya Habari Katika Poland

Mikusanyiko miwili ya kimataifa ilifanywa Poland, kukiwa na wahudhuriaji 20,000 katika Warsaw, ambalo ndilo jiji kuu, na karibu 12,000 katika Lodz, ambalo ni jiji la pili kwa ukubwa katika Poland.

Gazeti mashuhuri la Warsaw, Życie Warszawy, lilikuwa na habari hii: “‘Kuna habari njema za kutangazwa! Ni habari ya amani, amani halisi. Upendo wetu kwa Yehova na kwa majirani wetu hutuchochea kuendelea kuhubiri bila kuacha mpaka Mungu aseme kwamba kazi hiyo imefanywa,’ akasema Carey Barber, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova.”

Mwandikaji wa gazeti Sztandar Młodych alisema: “Kwa siku mbili Mashahidi wa Yehova 12,000 hivi walikusanyika kwenye kusanyiko la kidini katika Stediamu ya Legia, katika Warsaw. Kulikuwa na utangamano sana, na hata ingawa niliangalia kwa uangalifu, sikuona magari ya polisi au vikundi vya polisi vya kuchunguza hali.

“Kwa ujumla karibu Poland yote ni nchi ya Kikatoliki. Lakini vijana wetu wa Katoliki wanapokusanyika kwenye stediamu hiyohiyo, kundi kubwa la polisi huwapo nyakati zote, tayari kuzima fujo.

“Kwa hakika inashtusha kwamba hao watoro wa Ukatoliki, mafarakano, au vyovyote uwaitavyo [Mashahidi wa Yehova] wanaweza kukusanyika kwa wingi sana bila kuhatarisha utangamano na usalama wa umma, huku vijana wetu wenyewe wa Katoliki wanapokuwa katika umati huwa hatari, na hulazimu polisi kutoa ulinzi dhidi ya ghasia zao za ujana. Kuna mengi ya kufikiria juu ya jambo hili.”

Ubatizo wa waamini wapya pia ulifanywa hapa, 462 wakibatizwa Warsaw na 278 Lodz. Mmoja wa hao alikuwa Sylwia mwenye umri wa miaka 19, ambaye hakuwapenda Mashahidi. Shahidi mmoja alimfikia barabarani katika siku moja yenye mvua. “Nilifaulu kumfanya aende zake, nami nikaenda zangu. Lakini nikamfunika msichana mmoja aliyekuwa akilowa maji kwa mwavuli wangu. Ikatukia kwamba yeye pia ni Shahidi! Aliniambia ataniletea kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi. Kwa sababu ya adabu, nilimpa anwani ya mahali ninapoishi, na . . . nilibatizwa leo!”

Nchi Ndogo ya Estonia Yapata Ushahidi Mkubwa

Estonia, Latvia, na Lithuania hufanyiza Mataifa ya Baltiki. Estonia ina watu wapatao milioni 1.5 pekee, na jiji layo kuu lina wakazi wapatao 450,000. Mikusanyiko miwili ilifanywa huko katika Agosti 1996.

Mvutano wa mikutano hiyo miwili mikubwa ulikuwa mkubwa sana hivi kwamba gazeti moja la habari lilisema: “Tallinn limejaa kihalisi ibada ya Mashahidi wa Yehova. Mkusanyiko wao uliofanywa Linnahall inasemekana kuwa ulikuwa na hudhurio kubwa zaidi lililopata kuonekana kati ya dini zote katika Estonia.” Hoteli zote zilikuwa zimejaa Mashahidi.

Baadaye Ndugu Carey Barber alitoa ripoti ambamo alisema: “Si ajabu kwamba ndugu wa Finland na wengine waliopewa migawo kwenda Estonia wapenda sana kuwa huko. Nchi hii ndogo lakini maridadi imekandamizwa na mataifa makubwa nayo imevumilia kuteseka kwingi. Sasa Waestonia . . . watazamia sana kuwa na wakati ujao wa amani na usalama wa kudumu kutoka kwa Yehova.” Kuna zaidi ya Mashahidi 3,100 walio watendaji katika Estonia, nusu yao wakizungumza Kirusi.

Mikusanyiko hiyo ilitumikia Waestonia, Waestonia na Walatvia wanaozungumza Kirusi, Walithuania, na wajumbe wenye kuzuru kutoka nchi 15, kutia ndani 155 kutoka Uingereza na 300 kutoka Finland.

Viziwi Pia “Wasikia” Katika Estonia

Miaka mitatu iliyopita mzee mmoja kiziwi kutoka Finland alienda Tallin, Estonia, ili aone kile awezacho kuwafanyia viziwi katika nchi hiyo. Yeye hakujua hata mtu mmoja kiziwi huko, kwa hiyo alienda kwenye jumba ambalo viziwi hukutania katika Tallinn, akiwa na marundo ya magazeti ya Mnara wa Mlinzi na fasihi nyingine. Viziwi wa Estonia walimkaribisha nao walitaka kujua amebeba nini. Aliangusha fasihi zote alizokuwa nazo katika ziara ya kwanza na kuandika majina na anwani za wenye kupendezwa, majina 70 kwa ujumla.

Karibu wote walitaka kuwa na funzo la Biblia, na ndugu huyo akatambua kwamba hawezi kusoma na hao wote. Kwa hiyo ilikuwa lazima achague watu waliopendezwa zaidi. Upesi baada ya ziara yake ya kwanza Estonia, alikuwa na mafunzo 30 ya Biblia na orodha ya watu 40 waliokuwa wakingoja kuwa mafunzo ya Biblia! Sasa kuna watafsiri wanne wa lugha ya ishara kwa ajili ya viziwi katika Tallinn.

“Jambo Jipya Katika Drama ya Agano Jipya”

Shahidi mmoja alikuwa akifanya kazi katika kituo cha feri akisalimu wajumbe wa mkusanyiko. Akamwendea mtembezi mmoja Mwestonia na kumwuliza kile alichofikiri juu ya tukio hilo kubwa la mkusanyiko. Mtembezi huyo alimwambia kwamba alikuwa ametembeza vikundi kadhaa vya Mashahidi kutoka nchi kadhaa za Ulaya na kuona kwamba sikuzote Mashahidi walikuwa watu wazuri wenye adabu. Alikuwa amealikwa kuona ofisi ya Watch Tower Society kwenye Barabara ya Puhangu, naye alishangaa kuona utaratibu mzuri na vijana wenye fadhili wenye furaha. Hakuelewa ni kwa nini Mashahidi hukabili upinzani mkali na kuwekewa mashtaka bandia wakati ambapo mambo ya hakika yathibitisha mashtaka hayo kuwa ya uwongo. Yeye alisema: “Akilini mwangu, utumishi wenu, ni kama jambo jipya katika drama ya Agano Jipya.”

Kwa hakika wakiwa wajumbe wa amani ya kimungu, Mashahidi wa Yehova watazamia kuweka sifa nzuri ulimwenguni pote kwa sababu ya mwenendo wao wenye staha na fadhili yao kwa wageni. (1 Petro 3:16) Mikusanyiko hiyo katika Ulaya Mashariki yaonyesha kwamba japo uchongezi na masingizio ya maadui na waasi-imani wa kidini, Mashahidi wa Yehova wana baraka za Mungu watangazapo ujumbe wa amani ambao ulimwengu wetu uliovurugwa kwa vita na kujaa chuki unahitaji sana.—Isaya 2:2-4; Marko 13:10.

[Maelezo ya Chini]

a Kwa maelezo zaidi juu ya mikusanyiko ya Rumania, ona makala “Mikusanyiko ya Rumania Yafanywa Japo Upinzani,” katika Amkeni! la Februari 22, 1997. Kwa habari juu ya programu hiyo, ona makala “Wajumbe wa Amani ya Kimungu Wakusanyika,” katika Mnara wa Mlinzi la Januari 15, 1997.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Japo mvua, familia zilitoa uangalifu kwa programu

[Picha katika ukurasa wa 24]

Mashahidi Wapoland wenye furaha wakiwa na vitolewaji vyao vipya

[Picha katika ukurasa wa 25]

Mashahidi Waestonia wenye shangwe wakiwa wamevaa mavazi ya kidesturi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki