Kuwezana na Mchafuko wa Bahari ya Ainabinadamu Wasiotulia
Nabii Isaya alilinganisha waovu na bahari ambayo inachafuka, akatabiri kwamba “hapana amani kwa wabaya.” (Isa. 57:20, 21) Jinsi hilo linavyoelezea vema hali ya machafuko tunayoona kutuzunguka! Kadiri wakati ukaribiavyo ili “dhiki kubwa” ifyatuke, “bahari” ya ainabinadamu yazidi kusukasuka mawimbi ya matukio yenye kutikisa ulimwengu. (Mt. 24:21) Hata hivyo, tumeona kwamba Yehova hugeuzia mbali mishtuo kama hiyo kwa kuimarisha udugu wetu wa ulimwenguni pote kwa kutupa sisi roho takatifu yake na kwa kutuweka tukiwa tumelishwa kiroho kwa mfululizo wa vichapo pamoja na mikusanyiko yenye kutokeza. Hivyo, yeye hutuongoza kwa usalama kupitia siku hizi za mwisho zenye machafuko.—Isa. 30:20, 21.
Kwa mfano, katika mwaka wa utumishi wa 1990, katika Novemba 9, 1989, Ukuta wa Berlin ulibomolewa. Hilo lilitokeza furiko la watu waliofunguliwa upya pamoja na hali mpya ambazo zingeathiri kazi yetu ya kuhubiri katika tufe lote. Ndugu zetu katika mabara mengi ya Ulaya ya Mashariki wangeimarishwaje na kuwa na mambo ya kiroho ya kisasa? Baraza Linaloongoza lilianzisha programu ya ulishaji wa kiroho mara moja. Kupatana na Mathayo 24:45-47, utafsiri katika mabara haya upesi ulirekebishwa hivi kwamba, kwa wakati mfupi, Mnara wa Mlinzi likawa likitokea mara mbili kwa mwezi kwa rangi kamili katika lugha tisa kati ya zile zao. Viwanda vya Sosaiti katika nchi zilizoko karibu vimefanya kazi ya ajabu ya kuchapisha na kusafirisha magazeti na chakula kingine cha kiroho kwa wale waliokihitaji sana.
Iliamuliwa pia kufanya mpango wa kuwa na mikusanyiko ya pekee ya kimataifa ambayo ingeendelea hadi mwaka wa utumishi wa 1991. Mkusanyiko wa kimataifa wa Berlin Julai 24-27, 1990, miezi tisa baada ya kufunguliwa kwa ule ukuta, ulikuwa sehemu ya programu hiyo. Mwaka huu umekuwa wakati wenye matukio ya kusisimua kama nini, kama inavyoonyeshwa katika ripoti ya tufe lote iliyochapishwa katika Kitabu-Mwaka hiki!
Kwa kupitia yale yaliyofanywa katika mwaka wa utumishi wa 1991 katika Ulaya ya Mashariki na eneo kubwa la Urusi, tisa kati yetu washiriki wa Baraza Linaloongoza tulizungumza na familia nzima ya Betheli iliyokusanyika katika sehemu zao mbalimbali Jumatatu, Septemba 9, 1991, kufuatia Funzo la Mnara wa Mlinzi. Ulikuwa mkutano wa pekee sana kwa familia ya Betheli ambao ulikuwa wa zaidi ya saa mbili. Milango zaidi ya fursa za kitheokrasi ilielezwa kuwa inafunguliwa, kukiwa na makundi mapya yenye kuchipuka kila mahali! Mapainia katika mabara haya yaliyokuwa ya Kikomunisti waliongeza kwa shauku hesabu za wahubiri wenzao wa wakati wote kuzunguka ulimwengu. Kwa mara nyingine tena Mashahidi wa Yehova walionekana wakihubiri peupe katika majiji ambako kazi ilikuwa imepigwa marufuku hapo mbeleni! The New York Times la Septemba 1, 1991, liliripoti kwamba “Mashahidi wa Yehova wakitafuta waongofu” wangeweza kuonekana peupe kwenye barabara za mji wa St. Petersburg, iliyokuwa Leningrad hapo kwanza.
Kufuatia mabadiliko makubwa hayo, mikusanyiko ya pekee ya kimataifa mitatu ilifanywa katika 1991: Budapest, Hungari, Julai 26-28; Prague, Chekoslovakia, Agosti 9-11; na Zagreb, Yugoslavia, Agosti 16-18. Wajumbe wengi kutoka nchi zaidi ya 30 walipokutana na ndugu zao wa Ulaya ya Mashariki kwa mara ya kwanza, tabasamu zao za uchangamfu ziligeuka kuwa machozi ya shangwe.
Wakati ule ule, katika Julai na Agosti, mikusanyiko kadhaa ya wilaya ilifanywa katika Urusi. Kwenye saba ya mikusanyiko hiyo, yaani, Tallinn katika Estonia (sasa taifa huru), Usolye-Sibirskoye katika Siberia, Alma-Ata katika Kazakhstan, na Kiev na Lvov katika Ukrainia, pamoja na Odessa na Chernovtsy, jumla ya wahudhuriaji ilikuwa kilele cha 74,252, watu 7,820 wakibatizwa—asilimia 10.5 ya kutazamisha! Ilikuwa baraka iliyoje kwamba mikusanyiko hiyo ingeendelea hadi mwisho wayo hata kupita kipindi cha matukio yenye mchafuko ya Agosti.
Barua za furaha kuhusu mikusanyiko hiyo zilitufikia kutoka kwa ndugu zetu wa Urusi. Hapa pana mfano wa barua moja, yenye tarehe ya Julai 10, 1991: “Ndugu Wapendwa: Tunashukuru sana kwa fasihi nzuri tunazopokea. Kila mara ninapoenda kwenye ziara za kurudia na kuweka fasihi kwenye mkoba wangu wa kuhubiri, mimi humshukuru Yehova sana na kutoa shukrani kwa wale waliofanya kazi kwa bidii katika kupeleka fasihi hizi kwetu sisi katika Urusi. Mmetayarisha chakula cha kiroho chenye kuvutia sana kwa ajili yetu. Pia, watu tunaoangushia fasihi shambani wanatueleza tuwashukuru kwa ajili yazo. Nyongeza: Nimetayarisha watu watano kwa ubatizo kwenye mkusanyiko unaokuja katika Tallinn, Julai 13, 14.”
Kiu cha maarifa sahihi kinaonyeshwa na tamaa ya kupata tafsiri ya New World Translation of the Holy Scriptures katika lugha za watu wanaoishi katika nchi zilizokuwa zimezuiwa na Pazia la Chuma la zamani. Shangwe nyingi ilijaa stediamu kwenye mkusanyiko wa kimataifa wa Prague, wakati New World Translation of the Holy Scriptures ilipotolewa katika Kichekoslovakia na Kislovakia. Wahudhuriaji walisimama na kupiga makofi kwa dakika kumi. Hizo ndizo New World Translation za kwanza zinazopatikana katika lugha zozote za nchi zilizokuwa za Kikomunisti.
Imepangwa kuwe na New World Translation iliyo kamili, ambayo sasa yapatikana katika lugha 11, iweze kupatikana katika lugha nyingi zaidi zinazosemwa na umati mkubwa wa Yehova unaozidi kuongezeka ili kuendeleza uelimishaji wetu sahihi wa Biblia kwa kiwango cha juu, cha tufe lote. Ili kuangalia kazi hii, tumeanzisha Idara ya Huduma za Kutafsiri katika Brooklyn. Pia, kwa sababu ya milango mingi ya kuhubiri inayofunguka, idadi ya wanafunzi wamisionari itakayosajiliwa mwaka wa utumishi wa 1992 katika darasa linalofuata la 93 la Gileadi, itarudufishwa. Na Darasa Lililoendelezwa la Shule ya Gileadi katika Ujerumani na India litafunguliwa tena ili kuwazoeza watumishi wa wakati wote kwa ajili ya shamba la Ulaya ya Mashariki na Esia. Matukio hayo yote yenye kutokeza yanaonyesha umaana wa kuendelea kuitibari katika Yehova.
Tunaendelea kushikamana kiimara na yale aliyosema Paulo katika 2 Timotheo 3:16, 17: “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.” Tuna furaha kwa kuwa tunamfuata Mfalme na Kuhani Mkuu wetu, Yesu Kristo, tunapokaribia wakati wa kutakaswa kwa jina la Yehova lililotukuka! Tunashangilia matazamio ya mwaka mpya wa utumishi, na pamoja nanyi tunafikiria kwa uzito andiko letu la mwaka wa 1992: “Kwa tumaini, mkifurahi . . . Katika kusali, mkidumu.”—Rum. 12:12.
Ndugu zenu katika utumishi wenye utendaji wa Yehova,
BARAZA LINALOONGOZA LA MASHAHIDI WA YEHOVA