Nimeacha Kugugumiza!
KWA miongo minane hivi, Amkeni! limewasaidia wasomaji wake wakabiliane na matatizo ya kila siku. Nyakati nyingine, Amkeni! huwatahadharisha juu ya matukio mapya na mitazamo katika mambo ya kitiba, ambayo yaweza kubadili maisha zao sana, kama masimulizi yafuatayo yafunuavyo.
Matthew alizaliwa mnamo 1989 kaskazini mwa Uingereza. Kufikia umri wa miaka miwili, alikuwa mtoto asiye na kasoro. Kisha, kwa ghafula sana akiwa likizoni, akaanza kugugumiza vibaya sana.
“Mimi na mume wangu tulienda kwenye kituo cha tiba ya usemi kilichopo eneo letu,” aeleza Margaret, mamake, “tukaambiwa kwamba hakuna jambo wanaloweza kumfanyia mpaka afikie umri wa miaka saba kwa sababu kufikia umri huo, watoto hawawezi kudhibiti nyuzi zinazotokeza sauti. Lakini Matthew alipoenda shuleni, alipata ugumu wa kukabiliana na mizaha ya watoto wengine, na kigugumizi chake kikawa kibaya zaidi. Alichukia kuwa miongoni mwa watu akawa mwenye kujitenga. Hata kuhudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme likawa jambo gumu.
“Kisha tukaona ‘Tumaini kwa Wenye Kigugumizi,’ katika ‘Kuutazama Ulimwengu,’ katika toleo la Amkeni! la Aprili 8, 1995. Ilieleza kifupi kazi ya kikundi fulani cha matabibu wa usemi kule Sydney, Australia, ambacho kilifanikiwa kutibu kigugumizi katika watoto wadogo.
“Tuliandikia Chuo Kikuu cha Sydney na kupokea jibu kutoka kwa Dakt. Mark Onslow, akipendekeza kwamba tuwasiliane naye kupitia simu. Kwa kuwa tunaishi mbali sana nao, kikundi chake cha matabibu wa usemi kiliamua kujaribu ‘kumtibu kwa umbali.’ Sisi, tukiwa wazazi wa Matthew tulifunzwa mbinu za kikundi hicho kupitia simu, faksi, na kaseti ya kusikiliza. Tiba hiyo ilitayarishwa ifae mahitaji hususa ya Matthew. Nilikuwa nikiketi naye na katika hali yenye starehe isiyo rasmi ningemsaidia kusahihisha maneno yaliyokuwa yakimsumbua. Nilimpongeza sana na kumthawabisha akisema bila kigugumizi.
“Miezi sita baadaye Matthew hakuwa na kigugumizi tena wala mwenye kujitenga tena, lakini akawa kijana wa kawaida, mwenye furaha na mwenye urafiki. Sasa anajibu katika mikutano ya kutaniko naye anafurahia sana kutoa usomaji wa Biblia kwenye Jumba la Ufalme. Yeye pia anashiriki vizuri katika huduma ya nyumba hadi nyumba. Usemi wake ni wa kawaida!
“Tunashukuru kama nini kwa habari za Amkeni!, ambazo zimebadilisha maisha ya mwana wetu!”—Imechangwa.