Kuishi kwa Furaha Katika Nyumba Isiyo na Watoto
“KWA wengi wetu,” akakiri mzazi mmoja, “kutengana kwa mwisho huleta mshtuko hata tuwe tumejitayarisha vema kadiri gani.” Ndiyo, kadiri kuondoka kwa mtoto kusivyoweza kuepukika, kunapotukia kwa hakika, kushughulika nako kwaweza kuwa vigumu. Baba mmoja aeleza kuhusu itikio lake mwenyewe baada ya kumwambia mwana wake kwaheri: “Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu . . . , nililia tu, na kulia na kulia.”
Kwa wazazi wengi kuondoka kwa watoto wao huacha utupu katika maisha yao—kidonda kilicho wazi. Kwa kunyimwa uhusiano wa kila siku na watoto wao, wengine hupatwa na hisia nyingi za upweke, maumivu, na hasara. Na huenda ikawa si wazazi peke yao wanaopata wakati mgumu wa kujirekebisha. Wenzi waitwao Edward na Avril watukumbusha: “Ikiwa bado kuna watoto wengine nyumbani, wao pia watahisi hasara.” Shauri la wenzi hawa ni nini? “Wapeni watoto walio nyumbani upendo na uelewevu wenu. Hili litawasaidia kujirekebisha.”
Ndiyo, maisha yaendelea. Ikiwa utawatunza watoto waliobaki—vilevile kazi yako ya kimwili au wajibu wa nyumbani—huwezi kujiruhusu ukwame kwa huzuni. Kwa hiyo, acheni tuangalie njia fulani uwezazo kupata furaha watoto wako waondokapo nyumbani.
Tazama Yaliyo Chanya
Bila shaka, ikiwa wahisi huzuni au mpweke na wataka kulia au kuzungumza kuhusu hisia zako na rafiki mwenye kukusikitikia, kwa vyovyote fanya hivyo. Biblia husema: “Uzito katika moyo wa mtu huuinamisha; bali neno jema huufurahisha.” (Mithali 12:25) Nyakati nyingine wengine waweza kukupatia mtazamo mpya wa akilini. Kwa kielelezo, wenzi waitwao Waldemar na Marianne washauri hivi: “Ona jambo hilo, si kama kupoteza, bali kama mafanikio ya mradi.” Njia chanya kama nini ya kuona mambo! “Tunafurahi kwamba tuliweza kuwalea wavulana wetu kuwa watu wazima wenye madaraka,” wasema wenzi waitwao Rudolf na Hilde.
Je, umejitahidi sana kumlea mtoto wako “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova”? (Waefeso 6:4) Hata kama umefanya hivyo, waweza bado kuwa na hangaiko kuhusu kuondoka kwake. Lakini kwa wale wanaomzoeza mtoto wao hivyo, hakikishio la Biblia ni kwamba “hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mithali 22:6) Je, hairidhishi kuona kwamba mtoto wako ameitikia mazoezi yako? Mtume Yohana alisema hivi kuhusu familia yake ya kiroho: “Sina kisababishi cha shukrani kilicho kikubwa zaidi kuliko mambo haya, kwamba niwe nikisikia kwamba watoto wangu waendelea kutembea katika kweli.” (3 Yohana 4) Labda waweza kusema maneno kama hayo kuhusiana na mtoto wako.
Ni kweli kwamba si watoto wote wanaoitikia mazoezi ya Kikristo. Ikiwa yatokea hivi kwa mtoto wako aliye mtu mzima, haimaanishi kuwa umeshindwa ukiwa mzazi. Usijishushe isivyofaa ikiwa umefanya yote uwezayo ili kumlea katika njia ya kimungu. Tambua kwamba akiwa mtu mzima mtoto wako anachukua mzigo wake mwenyewe wa daraka mbele ya Mungu. (Wagalatia 6:5) Dumisha tumaini kwamba huenda baada ya wakati aweza kufikiria tena machaguo yake na kwamba hatimaye “mshale” utaenda ulipolengwa.—Zaburi 127:4.
Ungali Mzazi!
Huku kuondoka kwa mtoto wako kukitangaza badiliko, hakumaanishi kuwa kazi yako kama mzazi imekwisha. Mwanasaikolojia Howard Halpern asema: “Wewe ndiye mzazi hadi siku utakayokufa, lakini kutoa na kutunza lazima kufanyizwe upya.”
Zamani Biblia ilikiri kwamba uzazi haukwishi kwa sababu mtoto amekuwa mtu mzima. Mithali 23:22 husema: “Msikilize baba yako aliyekuzaa, wala usimdharau mama yako akiwa mzee.” Ndiyo, hata wakati wazazi ‘wamekuwa wazee’ na watoto wao ni watu wazima, wazazi wanaweza bado kuwa na uvutano fulani katika maisha ya watoto wao. Bila shaka, marekebisho fulani yahitaji kufanywa. Lakini mahusiano yote yahitaji kurekebishwa mara kwa mara ili yabaki yakiwa mapya na yenye kuridhisha. Sasa kwa vile watoto wako wamekua, fanyia kazi kuufanya uhusiano wenu kuwa na msingi wa utu mzima zaidi. Kwa kupendeza, uchunguzi waonyesha kwamba uhusiano kati ya mzazi na mtoto mara nyingi huboreka mara watoto waondokapo nyumbani! Watoto waonapo misongo inayohusiana na mahangaiko ya kila siku, mara nyingi wao huanza kuwaona wazazi wao kwa njia tofauti. Mwanamume Mjerumani aitwaye Hartmut asema: “Sasa nawaelewa wazazi wangu vizuri zaidi na natambua kwa nini walifanya mambo jinsi walivyofanya.”
Epuka Kujiingiza
Ikiwa wajiingiza katika maisha ya kibinafsi ya mtoto wako aliye mtu mzima, madhara mengi yaweza kutokea. (Linganisha 1 Timotheo 5:13.) Mwanamke mmoja aliyeolewa ambaye anapatwa na mkazo kutoka kwa wakwe zake aomboleza hivi: “Twawapenda, lakini twataka tu kuishi maisha yetu wenyewe na kufanya maamuzi yetu wenyewe.” Bila shaka, hakuna mzazi yeyote mwenye kujali ambaye atakaa kitako tu wakati mtoto wake aliye mtu mzima aingiapo katika msiba. Lakini kwa kawaida ni vizuri zaidi kutotoa shauri la kimzazi bila kuombwa, hata liwe ni lenye hekima jinsi gani au liwe la nia njema jinsi gani. Hili ni kweli hasa baada ya mtoto kuoa au kuolewa.
Amkeni! lilitoa shauri hili katika mwaka wa 1983: “Kubali daraka lako lililobadilika. Unaacha kumtendea mtoto wako kama mtoto mchanga sana anayenyonya wakati aanzapo kutembea. Vivyo hivyo, lazima ubadilishane daraka la kuwa mtunzaji na daraka la kuwa mshauri. Kufanya maamuzi kwa ajili ya mtoto wako katika wakati huu wa maisha kungekuwa kusikofaa kama tu vile kumtoa hewa au kumnyonyesha akiwa mtu mzima. Ukiwa mshauri, una mipaka dhahiri. Huwezi tena kufanya amri yako ukiwa mzazi itumike kwa matokeo. (‘Fanya hivyo kwa sababu nimesema.’) Lazima kuwe na staha kwa hadhi ya mtoto wako ya utu mzima.”a
Huenda usikubaliane na maamuzi yote ambayo mtoto wako na mwenzi wake wafanya. Lakini staha kwa utakatifu wa ndoa itakusaidia kupima mahangaiko yako na kuepuka kuingilia isivyo lazima. Ukweli ni kwamba, kwa kawaida ni vizuri zaidi kwa wazazi kuwaacha wenzi wachanga kutatua matatizo yao wenyewe. Kama sivyo, wajihatarisha kupatwa na kabiliano lisilo la lazima unapotoa shauri lisilohitajika kwa mwana au binti-mkwe ambaye, katika hali ya ndoa iliyo rahisi kuvunjika, aweza kuwa mwenye hisia nyepesi kuelekea uchambuzi. Amkeni! lililotajwa hapo juu lilitoa shauri hili la ziada: “Vunja tamaa ya kutoa mashauri yasiyo na mwisho, yasiyoombwa, ambayo yaweza kumfanya mwana-mkwe au binti-mkwe awe adui.” Uwe mwenye tegemezo—usiwe mwenye kuongoza kwa hila. Kwa kudumisha uhusiano mzuri, unafanya iwe rahisi kwa mtoto wako kukujia ikiwa shauri lahitajiwa kikweli.
Fanyeni Upya Vifungo Vyenu vya Ndoa
Kwa wenzi wengi, kuondoka kwa watoto nyumbani kwaweza pia kufungulia uwezekano wa kuongezeka kwa furaha katika ndoa. Wakati na jitihada inayotumika katika uzazi wenye matokeo zaweza kuwa nyingi mno hivi kwamba wenzi wanapuuza uhusiano wao wenyewe. Mke mmoja asema: “Sasa kwa vile watoto wameenda, Konrad nami twajaribu kujuana upya tena.”
Kwa kuwekwa huru kutokana na madaraka ya kila siku ya uzazi, sasa mwaweza kuwa na wakati mwingi zaidi wa kuwa pamoja. Mzazi mmoja alionelea: “Wakati huu mpya usiopangiwa mambo . . . waturuhusu kuelekeza uangalifu zaidi juu ya sisi ni nani, kukazia fikira kujifunza mengi kuhusu mahusiano yetu, na kuanza kujihusisha katika utendaji unaojazia mahitaji yetu.” Yeye aongezea: “Ni wakati wa kujifunza kupya na ukuzi wa ajabu, na ingawa nyakati kama hizo zaweza kuwa zisizo na utulivu, ni zenye kuchangamsha pia.”
Wenzi fulani pia wana uhuru zaidi wa kifedha. Hobi na kazi-maisha ambazo zilikuwa zimewekwa kando sasa zaweza kufuatiwa. Miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, wenzi wengi hutumia uhuru wao walioupata upya kufuatia mapendezi ya kiroho. Baba aitwaye Hermann aeleza kwamba baada ya watoto wake kuondoka nyumbani, yeye na mke wake mara moja waligeuzia uangalifu wao kurudia utumishi wa wakati wote.
Wazazi Walio Pekee Wakiwaacha Waende
Kujipatanisha na hali baada ya watoto kuondoka nyumbani kwaweza kuwa vigumu hata zaidi kwa wazazi walio pekee. Rebecca, mama aliye mzazi pekee wa watoto wawili aeleza: “Watoto wetu waondokapo, hatuna mume wa kutupatia ushirika na upendo.” Mama aliye mzazi pekee huenda akawaona watoto wake kuwa chanzo cha tegemezo la kihisia-moyo. Na ikiwa walikuwa wanachangia fedha za nyumbani, kuondoka kwao kwaweza pia kuleta ugumu wa kiuchumi.
Wengine huweza kuboresha hali yao ya kiuchumi kwa kujiunga na programu za kuzoeza kikazi au kuchukua mitaala ya muda mfupi katika shule. Lakini mmoja hujaziaje utupu wa upweke? Mzazi aliye pekee asema: “Kile ambacho hufanya kazi kwangu ni kuwa na jambo la kufanya kila wakati. Yaweza kuwa ni kusoma Biblia, kusafisha nyumba yangu, au kwenda tu matembezi au kukimbia. Lakini njia yenye kuridhisha zaidi kwangu ni kuzungumza na rafiki wa kiroho.” Ndiyo, ‘panuka,’ na utafute marafiki wapya wenye kuridhisha. (2 Wakorintho 6:13) ‘Dumu katika dua na sala’ unapohisi mpweke kabisa. (1 Timotheo 5:5) Uwe na uhakika kuwa Yehova atakupa nguvu na kukutegemeza katika kipindi hiki kigumu cha kujirekebisha.
Kuwaacha Waende kwa Furaha
Hata hali yako iweje, tambua kwamba maisha hayaishi wakati watoto wako waondokapo nyumbani. Wala vifungo vya familia havivunjiki. Upendo halisi unaoelezwa katika Biblia ni wenye nguvu za kutosha kuwaunganisha watu pamoja, hata wakiwa wako mbali. Mtume Paulo atukumbusha kwamba upendo “huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.” (1 Wakorintho 13:7, 8) Upendo usio na ubinafsi ambao umekuza katika familia yako hautashindwa kwa sababu tu watoto wako wameondoka nyumbani.
Kwa kupendeza, wakati watoto waondokapo nyumbani na kuanza kukabiliana na maumivu ya kutengana na kukosa nyumbani au wakati waanzapo kuhisi msongo wa kiuchumi, mara nyingi wao ndio huwa wa kwanza kurudisha upya uhusiano. Hans na Ingrid washauri hivi: “Waache watoto wajue kwamba wanakaribishwa nyumbani wakati wowote.” Ziara za kawaida, barua, au simu za mara fulani-fulani zitasaidia kudumisha uhusiano. “Pendezwa na wanayofanya bila kuingilia mambo yao,” hivyo ndivyo Jack na Nora walivyoeleza.
Watoto waondokapo nyumbani, maisha hubadilika. Lakini maisha katika nyumba isiyo na watoto yaweza kuwa yenye shughuli nyingi, yenye utendaji, na yenye kuridhisha. Pia, uhusiano wako na watoto wako hubadilika. Lakini, uhusiano wenu waweza kuwa wenye furaha na wenye kupendeza. “Kusitawisha uhuru kutoka kwa wazazi,” wasema Maprofesa Geoffrey Leigh na Gary Peterson, “hakudokezi kukosa upendo, uaminifu-mshikamanifu, au staha kwa wazazi. . . . Kwa kweli, vifungo vyenye nguvu vya familia huendelea muda wote wa duru ya maisha.” Ndiyo, hutaacha kamwe kuwapenda watoto wako, na hutaacha kamwe kuwa mzazi wao. Na kwa sababu umewapenda watoto wako kiasi cha kwamba umewaruhusu waende, kwa kweli hujawapoteza.
[Maelezo ya Chini]
a Ona ile makala “Huachi Kuwa Mzazi Wakati Wowote,” katika toleo la Amkeni! la Februari 8, 1983, la Kiingereza.
[Blabu katika ukurasa wa 12]
“Kwa mara ya kwanza katika maisha yangu . . . , nililia tu, na kulia na kulia”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]
Neno kwa Watoto Walio Watu Wazima—Wasaidieni Wazazi Wenu Kuwaacha Mwende
Kuondoka kwa kawaida ni rahisi kushughulika nako kuliko kuachwa. Kwa hiyo huku ukifurahia uhuru wako na utu mzima, waonyeshe wazazi wako fadhili na uelewevu ikiwa wanakuwa na tatizo katika kujirekebisha. Wahakikishie upendo wako na shauku kwa kuendelea. Barua fupi, zawadi isiyotazamiwa, au simu ya kirafiki yaweza kufanya mengi katika kuwachangamsha wazazi waliohuzunika! Wajulishe kuhusu matukio hususa katika maisha yako. Hili huwajulisha kuwa vifungo vya familia vingali vyenye nguvu.
Ukabilipo misongo ya maisha ya utu mzima, huenda ukathamini zaidi yale ambayo yaliwapata wazazi wako walipokuwa wakikutunza. Huenda hili litakusukuma uwaambie wazazi wako: “Asanteni kwa ya le yote mliyonifanyia!”