SOMO LA 14
Kuzungumza kwa njia ya kawaida
KUONGEA kwa njia ya kawaida hufanya wengine wakuamini. Je, unaweza kuamini maneno ya mtu ambaye amefunika uso wake kwa kitu fulani? Na je, ungeamini maneno yake kama kitu hicho kinavutia kuliko sura yake halisi? Hapana. Basi uwe jinsi ulivyo kwa kawaida badala ya kuiga usemi mwingine.
Kuzungumza kwa njia ya kawaida si uzembe. Kutotumia lugha sanifu, kutamka maneno vibaya, na kutosema maneno yanayosikika wazi hakufai. Tuepuke lugha ya mtaani. Nyakati zote maneno yetu na tabia zetu ziwe na adabu. Mtu ambaye anaongea kwa njia ya kawaida haongei kwa njia rasmi kupita kiasi wala hafikirii tu kuvutia watu.
Katika Huduma ya Shambani. Unapokaribia nyumba au unapoelekea kukutana na mtu hadharani ili umhubirie, je, unakuwa na wasiwasi? Wengi wetu huwa na wasiwasi, lakini wengine huwa na wasiwasi zaidi. Wasiwasi unaweza kufanya sauti ibadilike au itetemeke, au unaweza kufanya utoe ishara isiyofaa kwa mikono na kichwa.
Kuna sababu kadhaa zinazoweza kumfanya mhubiri apate tatizo hilo. Labda anafikiria watu watamwonaje au anafikiria iwapo atafanikiwa kutoa ushahidi. Hiyo ni kawaida, lakini matatizo hutokea tunapofikiria mambo hayo kupita kiasi. Ukishikwa na wasiwasi kabla ya kuanza huduma, ni nini kinachoweza kukusaidia? Jitayarishe vizuri na usali sana kwa Yehova. (Mdo. 4:29) Fikiria rehema kubwa ambayo Yehova anaonyesha kwa kuwaalika watu wafurahie afya kamilifu na uhai wa milele katika Paradiso. Wafikirie wale unaojaribu kuwasaidia na uhitaji wao wa kusikia habari njema.
Ukumbuke pia kwamba watu wana hiari, kwa hiyo ama wanaweza kukubali ujumbe wako ama waukatae. Ndivyo ilivyokuwa Yesu alipohubiri katika Israeli la kale. Mgawo wako ni kuhubiri tu. (Mt. 24:14) Hata kama watu hawakupi nafasi ya kuzungumza, unatoa ushahidi unapowatembelea. Utakuwa umefaulu kwa sababu umemruhusu Yehova akutumie kutimiza mapenzi yake. Na ukipata fursa za kuongea, utazungumzaje? Ukijifunza kufikiria mahitaji ya wengine, utaongea kwa njia ya kuvutia na ya kawaida.
Ukitenda na kuzungumza kama kawaida unapohubiri, wale wanaokusikiliza watastarehe. Hata wanaweza kukubali kwa urahisi zaidi Maandiko ambayo unataka kuwaeleza. Badala ya kuwahutubia, zungumza nao. Uwe mwenye urafiki. Pendezwa nao, na uwaruhusu wajieleze. Kama kuna desturi fulani katika lugha ama jamii ya kuonyesha adabu unapoongea na watu usiowajua, ni vizuri kuzifuata. Lakini, uwe tayari nyakati zote kutabasamu kirafiki.
Jukwaani. Unapohutubia watu, njia bora ni kuzungumza kwa njia ya kawaida na ya maongezi. Bila shaka unahitaji kuinua sauti ikiwa wasikilizaji ni wengi. Ukiona unajaribu kukariri hotuba yako au kama una maandishi mengi mno, labda sababu ni kwamba unaogopa kukosea. Ni muhimu kutumia maneno yanayofaa, lakini maneno hayo yakizingatiwa kupita kiasi, hotuba haitapendeza wala kuvutia. Haitatokea kwa njia ya kawaida. Unapaswa kufikiria mapema kwa makini mambo ambayo utasema, lakini zingatia zaidi mawazo yako badala ya kufikiria maneno hususa utakayotumia.
Na ndivyo ilivyo unapohojiwa mkutanoni. Jitayarishe vizuri, lakini usisome wala kukariri majibu yako. Zungumza kwa njia ya kawaida ili maelezo yako yatoke moyoni na kuvutia.
Hata sifa nzuri zinaweza kuonwa na wasikilizaji kuwa si za kawaida zikitumiwa kupita kiasi. Kwa mfano, unapaswa kuzungumza kwa njia inayoeleweka wazi na kutamka maneno vizuri, au kwa njia ya kawaida. Hotuba yako inaweza kuchangamsha ukitumia vizuri ishara za kutia mkazo au za ufafanuzi, lakini ishara zinazolazimishwa au zenye kupita kiasi hukengeusha wasikilizaji. Zungumza kwa kiasi kinachofaa cha sauti lakini si kwa sauti kubwa kupita kiasi. Inafaa kuwa na shauku mara kwa mara katika hotuba, lakini epuka kuongea kwa majivuno. Ubadilifu wa sauti, shauku, na hisia zinapasa kuonyeshwa kwa njia ambayo haifanyi mtu ajielekezee fikira au kufanya wasikilizaji wawe na wasiwasi.
Watu wengine wana njia zao za kawaida za kuongea, hata wakati hawatoi hotuba. Wengine hutoa hotuba kwa njia ya maongezi zaidi. Jambo muhimu ni kuzungumza kwa njia nzuri kila siku na kujiendesha kwa njia ya Kikristo. Kisha unapotoa hotuba jukwaani, itakuwa rahisi kuongea na kutenda kwa njia ya kawaida inayopendeza.
Unaposoma Mbele ya Watu. Unahitaji kutia bidii ili usome kwa njia ya kawaida. Ili ufaulu, tambua mawazo makuu katika habari utakayosoma, na utazame jinsi mawazo hayo yanavyokuzwa. Uyaweke wazi akilini; ama sivyo, utakuwa ukisoma tu maneno. Chunguza jinsi maneno usiyofahamu yanavyotamkwa. Fanya mazoezi ya kusoma kwa sauti ili ujue jinsi ya kubadili sauti na kusoma maneno fulani pamoja kwa njia inayofanya maana iwe wazi. Fanya mazoezi hayo kwa kurudia-rudia mpaka uweze kusoma vizuri. Fahamu habari hiyo kabisa ili unaposoma kwa sauti, usomaji wako usikike kana kwamba ni mazungumzo yenye shauku. Huko ndiko kuzungumza kwa njia ya kawaida.
Bila shaka, mara nyingi sisi husoma vichapo vyetu vinavyotegemea Biblia. Mbali na migawo ya usomaji tunayopata katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, sisi husoma maandiko katika utumishi wa shambani na tunapotoa hotuba jukwaani. Akina ndugu hupewa migawo ya kusoma katika Funzo la Mnara wa Mlinzi na Funzo la Kitabu la Kutaniko. Ndugu wengine wanaostahili hupewa migawo ya kutoa hotuba za kusoma katika kusanyiko. Iwe unasoma Biblia au vichapo vingine, soma sehemu zenye alama za mnukuo kwa njia inayofanya habari iwe halisi. Kama watu kadhaa wananukuliwa katika habari unayosoma, badili sauti yako kwa njia fulani ili kuiga sauti zao. Lakini tahadhari: Usiige sauti hizo kupita kiasi, lakini usome kwa uchangamfu na kwa njia ya kawaida.
Kusoma kwa njia ya kawaida ni kama mazungumzo. Ni halisi na inasadikisha.