SOMO LA 28
Kutoa Hotuba kwa Njia ya Maongezi
KWA kawaida watu hustarehe wanapozungumza na marafiki. Maneno yao yanatiririka tu. Watu wengine ni wachangamfu sana ilhali wengine huwa kimya. Hata hivyo, maongezi ya kawaida kama hayo huvutia.
Lakini unapokutana na mtu ambaye humjui si vizuri kuzungumza naye kana kwamba unamjua sana wala kuzungumza naye kwa njia inayokosa adabu. Katika jamii nyingi mazungumzo yote kati ya watu ambao hawajuani huanza kwa njia rasmi sana. Lakini baada ya salamu za heshima, kwa busara unaweza kuanza kuzungumza kwa njia ya kawaida ya maongezi.
Tahadhari pia unapotoa hotuba jukwaani. Kutoa hotuba kwa njia ya kizembe kutafanya mkutano wa Kikristo ukose heshima na watu wakose kuthamini mambo unayosema. Katika jamii fulani unapaswa kusema maneno fulani unapozungumza na mtu anayekuzidi umri, mwalimu, ofisa fulani, au mzazi. (Ebu ona maneno yanayotumiwa katika Matendo 7:2 na 13:16.) Maneno tofauti-tofauti hutumiwa kumwita mume au mke au rafiki unayempenda. Ingawa hatupaswi kuongea kwa njia rasmi sana jukwaani, tunapaswa kuongea kwa heshima.
Hata hivyo, kuna mambo ambayo yanaweza kumfanya mtu atoe hotuba bila kubadilikana. Mojawapo ya sababu hizo ni muundo wa sentensi. Tatizo huzuka msemaji anapojaribu kurudia maneno yaleyale kama yalivyoandikwa katika vichapo. Kwa kawaida watu huzungumza kwa njia tofauti na jinsi maneno yanavyoandikwa. Ni kweli kwamba kwa kawaida tunatayarisha hotuba kupitia habari iliyochapwa. Labda muhtasari uliochapwa ndio msingi wa hotuba. Lakini ikiwa unazungumza kana kwamba unasoma kichapo au ikiwa unasoma moja kwa moja muhtasari wa hotuba, inaelekea hutatoa hotuba kwa njia ya maongezi. Ili utoe hotuba kwa njia ya maongezi, tumia maneno yako mwenyewe na kuepuka sentensi ngumu-ngumu.
Jambo jingine ni kubadili-kubadili mwendo wako wa kuzungumza. Usemi baridi-baridi na ulio rasmi kupita kiasi husababishwa na maneno yanayofuatana kwa mwendo uleule mmoja usiobadilika. Katika mazungumzo ya kawaida, watu hubadili-badili mwendo na kutua-tua kwa njia tofauti-tofauti.
Bila shaka, unapohutubia watu wengi unapaswa kuhutubu kwa njia ya maongezi na kwa sauti ya juu, kwa mkazo, na kwa shauku ili waendelee kukusikiliza kwa makini.
Ili uzungumze kwa njia ya maongezi inayofaa utumishi, unahitaji kuwa na mazoea ya kuzungumza vizuri kila siku. Haimaanishi kwamba ni lazima uwe na elimu ya juu. Lakini ni vizuri uwe na mazoea mazuri ya usemi ambayo yatafanya wengine wakusikilize kwa heshima. Basi, ukiwa na mambo hayo akilini, ebu ona kama unahitaji kufanyia kazi sifa zifuatazo katika mazungumzo ya kawaida:
Epuka lugha chafu au matusi kwa kupatana na shauri la Wakolosai 3:8. Kwa upande mwingine, si vibaya kutumia lugha inayotumiwa kwa kawaida inayopatana na lugha sanifu ingawa si rasmi.
Jifunze kutumia maneno yanayoonyesha wazi jambo unalomaanisha.
Uwe na mazoea ya kusema jambo unalotaka watu wakumbuke kwa njia inayoeleweka wazi na kwa maneno rahisi.