Kutayarisha Migawo ya Shule
KILA hotuba katika shule inakupa nafasi ya kufanya maendeleo. Tia bidii sana, na polepole maendeleo yako yatakuwa dhahiri kwako na kwa wengine. (1 Tim. 4:15) Shule itakusaidia kukuza uwezo wako zaidi.
Je, unakuwa na wasiwasi unapofikiria kuhutubu mbele ya kutaniko? Hiyo ni kawaida, hata kama umeshiriki katika shule hii kwa muda mrefu. Lakini kuna mambo fulani ambayo yanaweza kukusaidia kupunguza wasiwasi. Uwe na zoea la kusoma kwa sauti unapokuwa nyumbani. Toa maelezo mara nyingi kwenye mikutano ya kutaniko na ikiwa wewe ni mhubiri, uwe wa kawaida katika huduma ya shambani. Ukifanya hivyo utazoea kusema mbele ya watu. Pia, tayarisha migawo yako mapema, na ufanye mazoezi ya kuzitoa hotuba hizo kwa sauti. Kumbuka kwamba utatoa hotuba mbele ya wasikilizaji wenye urafiki. Kabla ya kutoa hotuba yoyote, sali kwa Yehova. Kwa furaha yeye huwapa roho takatifu watumishi wake wanaomwomba.—Luka 11:13; Flp. 4:6, 7.
Usitarajie kwamba hotuba yako itakuwa bora kabisa. Inachukua muda kuwa msemaji mwenye uzoefu na mwalimu bora. (Mika 6:8) Ikiwa umejiunga na shule hivi karibuni, usitarajie kutoa hotuba kamilifu mara hiyo. Badala yake, fanyia kazi shauri moja la usemi kwa wakati mmoja. Soma sehemu ya kitabu hiki inayozungumzia shauri hilo. Ikiwezekana, fanya mazoezi ambayo yamedokezwa katika sehemu hiyo. Hiyo itafanya ujue mambo yanayohusu shauri hilo kabla ya kutoa hotuba yako kutanikoni. Na utafanya maendeleo.
Jinsi ya Kutayarisha Mgawo wa Usomaji
Kujitayarisha kusoma mbele ya watu kunahusu mambo mengi kuliko tu kuweza kutaja maneno unayosoma. Jitahidi kuelewa kabisa habari hiyo. Mara tu unapopokea mgawo wa usomaji, soma habari hiyo ili uielewe vizuri. Ili uweze kuwasilisha mawazo kwa usahihi na kwa hisia inayofaa, jaribu kuelewa jambo kuu la kila sentensi na wazo kuu la kila fungu. Ikiwezekana, chunguza kamusi ili ujue matamshi sahihi ya maneno usiyoyafahamu. Fahamu kabisa habari hiyo. Wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao wadogo kufanya hivyo.
Je, umepata mgawo wa kusoma Biblia au labda mafungu ya Mnara wa Mlinzi? Kama kuna kaseti za kusikiliza katika lugha unazoelewa ambazo zina habari utakayosoma, unaweza kufaidika sana kusikiliza usomaji huo na kufikiria mambo kama matamshi, namna ya kusoma maneno, kutia mkazo, na kubadilisha sauti. Kisha jaribu kutumia sifa hizo unaposoma.
Unapoanza kutayarisha mgawo wako, hakikisha kwamba umesoma kwa makini somo linalozungumzia shauri la usemi ambalo utafanyia kazi. Ikiwezekana, lipitie tena somo hilo baada ya kusoma kwa sauti mgawo wako mara kadhaa. Jaribu kufuata shauri lililoandikwa kwa kadiri iwezekanavyo.
Mazoezi haya yatakusaidia sana katika huduma. Unapokuwa katika utumishi wa shambani, unapata nafasi nyingi za kusomea wengine. Kwa kuwa Neno la Mungu lina uwezo wa kubadili maisha ya watu, ni muhimu kulisoma vizuri. (Ebr. 4:12) Usifikiri kwamba utaweza kufikiria kanuni zote za usomaji mzuri utimizapo migawo michache ya usomaji. Mtume Paulo alimwandikia hivi mzee mmoja Mkristo aliyekuwa na uzoefu wa miaka mingi: “Endelea kujitahidi mwenyewe kusoma mbele ya watu wote.”—1 Tim. 4:13.
Kutayarisha Ukifikiria Kichwa Kikuu na Kikao
Ukipokea mgawo katika shule ambao unahusu kikao, ufanyeje?
Kuna mambo matatu ya kufikiria: (1) habari utakayozungumzia, (2) kikao chako na yule ambaye utazungumza naye, na (3) shauri ambalo unapaswa kufanyia kazi.
Unahitaji kufanya utafiti. Lakini kabla ya kufanya utafiti huo, fikiria sana kikao chako na vilevile yule ambaye utazungumza naye, kwa sababu mambo haya yanahusu sana habari ambayo utatoa na jinsi utakavyoitoa. Utatumia kikao gani? Je, utaonyesha jinsi ya kumhubiria mtu unayemjua? Au utaonyesha jambo unaloweza kusema unapokutana na mtu kwa mara ya kwanza? Je, mtu huyo anakuzidi umri ama wewe unamzidi umri? Anaweza kuwa na maoni gani kuhusu habari unayotaka kuzungumza? Huenda ikawa tayari anajua nini kuhusu habari hiyo? Unatumaini kutimiza kusudi gani katika mazungumzo yenu? Majibu ya maswali hayo yataandaa miongozo muhimu ya kukusaidia kutayarisha.
Utapata wapi habari zinazohusu hotuba yako? Kuna habari inayohusu “Jinsi ya Kufanya Utafiti” kwenye ukurasa wa 33 hadi 38 katika kitabu hiki. Soma sehemu hiyo, kisha utumie vifaa vya kufanyia utafiti vinavyopatikana. Mara nyingi utagundua haraka kwamba kuna habari nyingi kuliko unavyoweza kutumia. Soma kiasi cha habari kinachokuwezesha kutambua mambo uwezayo kupata. Lakini unaposoma, kumbuka kikao utakachotumia katika hotuba yako na vilevile yule ambaye utazungumza naye. Tia alama mambo yanayofaa kutumiwa.
Kabla ya kupanga hotuba yako na hatimaye kuchagua habari ambayo utazungumzia, usome shauri ambalo unafanyia kazi. Mojawapo ya sababu kubwa zinazofanya upewe mgawo wa kutoa hotuba ni kujifunza kufuata shauri hilo.
Ukitoa hotuba kwa wakati uliowekwa, utakuwa na nafasi ya kutoa umalizio wake, kwa kuwa ishara itatolewa wakati muda uliowekwa unapoisha. Lakini tunapokuwa katika huduma ya shambani kwa kawaida hatuwekewi wakati wa kufuata. Basi unapotayarisha, fikiria wakati uliowekewa, lakini hakikisha utafundisha vizuri.
Kuhusu Vikao. Chunguza madokezo yaliyo kwenye ukurasa wa 82, na uchague dokezo moja ambalo unaweza kutumia katika huduma yako na ambalo litakuwezesha kutumia habari ya hotuba yako. Ikiwa umekuwa katika shule kwa muda fulani, chukua nafasi hii kufanya maendeleo na kukuza uwezo zaidi wa kutimiza huduma.
Ikiwa mwangalizi wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi amekupa kikao, ukitumie. Vikao vingi huhusu kutoa ushahidi. Ikiwa hujapata kutoa ushahidi katika hali kama hizo zinazoonyeshwa, omba maoni ya wahubiri wengine ambao wamepata kutoa ushahidi katika hali kama hizo. Ikiwezekana, jaribu kufanya mazoezi ya kutoa hotuba yako ukitumia kikao ambacho utatumia katika shule. Hiyo itakusaidia kutimiza kusudi muhimu la mazoezi yako.
Kama Una Mgawo wa Kutoa Hotuba
Ikiwa wewe ni mwanamume, unaweza kupewa mgawo wa kutoa hotuba fupi mbele ya kutaniko. Unapotayarisha hotuba hizo, mambo ya msingi ambayo unahitaji kufikiria yanafanana na yale ambayo tayari yameorodheshwa kuhusu hotuba ya mwanafunzi inayotolewa kwa njia ya maonyesho. Tofauti kubwa iliyopo ni wale unaozungumza nao na jinsi ya kuitoa hotuba hiyo.
Kwa kawaida inafaa kutayarisha habari yako ili ifaidi kila mmoja wa wasikilizaji. Tayari wengi kati ya wahudhuriaji wanajua kweli za msingi za Biblia. Inawezekana kwamba wanafahamu vizuri hotuba yako. Fikiria mambo ambayo tayari wanajua kuhusu habari hiyo. Jaribu kufanya utoaji wako uwafaidi kwa njia fulani. Jiulize: ‘Nawezaje kutumia habari hii kwa njia ambayo itanifanya mimi na wasikilizaji tumthamini Yehova hata zaidi? Habari hii itatusaidiaje kufahamu mapenzi ya Mungu? Habari hii inaweza kutusaidiaje kufanya maamuzi mazuri katika ulimwengu uliojaa tamaa za kimwili?’ (Efe. 2:3) Utafiti unahitajiwa ili kupata majibu yenye kuridhisha ya maswali haya. Unapotumia Biblia, usisome tu maandiko. Fafanua maandiko unayotumia, na uonyeshe jinsi yanavyoandaa msingi wa kufikia maamuzi. (Mdo. 17:2, 3) Usijaribu kuzungumzia mambo mengi mno. Toa hotuba yako kwa njia itakayofanya wasikilizaji waikumbuke kwa urahisi.
Matayarisho yanatia ndani kufikiria jinsi utakavyotoa hotuba hiyo. Usipuuze jambo hilo. Ufanye mazoezi ya kutoa hotuba yako kwa sauti. Jitihada zako za kujifunza na kufuata mashauri ya usemi zitakusaidia sana kufanya maendeleo. Uwe msemaji mpya au msemaji mwenye uzoefu, tayarisha vizuri ili uweze kutoa hotuba kwa usadikisho na hisia zinazofaa habari yako. Unapotimiza kila mgawo katika shule, kumbuka kwamba kusudi lako ni kutumia zawadi ya usemi uliyopewa na Mungu kumheshimu Yehova.—Zab. 150:6.