Tunaweza Kufanya Matakwa ya Yehova
1 Kutii sheria na kanuni za Yehova ndilo jambo bora maishani leo, na hutusaidia kuwa na msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao wa milele. (Zab. 19:7-11; 1 Tim. 6:19) Hata hivyo, ulimwengu wa Shetani hutusonga sana. Kutokamilika kwetu huzidisha ugumu huo. Huenda nyakati nyingine tukahisi tumelemewa tunapojaribu kutimiza madaraka yetu ya Kimaandiko. (Zab. 40:12; 55:1-8) Huenda tukajiuliza kama tunaweza kufanya matakwa yote ya Yehova. Nyakati kama hizo, ni nini kinachoweza kutusaidia tuwe na usawaziko wa kiroho?
2 Amri za Yehova Si Mzigo Mzito: Yehova hutupatia matakwa yenye usawaziko. Amri zake si mzigo mzito bali ni kwa faida yetu. (Kum. 10:12, 13; 1 Yoh. 5:3) Yeye hutambua udhaifu wetu, “akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” (Zab. 103:13, 14) Mungu hukubali kwa rehema jitihada zetu za kumtumikia hata kama tunadhoofishwa na hali zetu. (Law. 5:7, 11; Marko 14:8) Anatualika tumtupie mizigo yetu na kutuhakikishia kwamba atatusaidia tuendelee kuwa waaminifu.—Zab. 55:22; 1 Kor. 10:13.
3 Uvumilivu Unahitajiwa: Masimulizi ya Biblia kuwahusu watu waaminifu kama vile Eliya, Yeremia, na Paulo yanaonyesha uhitaji wa kuwa na uvumilivu. (Ebr. 10:36) Yehova aliwategemeza nyakati za magumu na kuvunjika moyo. (1 Fal. 19:14-18; Yer. 20:7-11; 2 Kor. 1:8-11) Nasi tunachochewa na ushikamanifu wa ndugu zetu katika nyakati zetu. (1 Pet. 5:9) Kutafakari mifano hiyo kwaweza kutusaidia tusivunjike moyo.
4 Tumaini katika ahadi za Mungu ni “nanga ya nafsi.” (Ebr. 6:19) Lilimchochea Abrahamu na Sara kukubali ombi la Yehova la kuondoka nyumbani kwao na ‘kukaa kama wageni katika nchi ya ahadi.’ Lilimwimarisha Musa kuchukua msimamo wa ujasiri kwa ajili ya ibada ya kweli. Lilimwimarisha Yesu kuvumilia mti wa mateso. (Ebr. 11:8-10, 13, 24-26; 12:2, 3) Vivyo hivyo, kudumisha ahadi ya Mungu ya ulimwengu mpya wenye uadilifu mioyoni mwetu kutatusaidia kuendelea kuwa imara.—2 Pet. 3:11-13.
5 Pia, kukumbuka matendo yetu ya zamani ya ushikamanifu, kujidhabihu, na ujasiri kwaweza kutuimarisha katika utumishi wetu. (Ebr. 10:32-34) Hutukumbusha shangwe tunayopata tunapofanya matakwa ya Yehova—ujitoaji wetu wa nafsi yote.—Mt. 22:37.
[Maswali ya Funzo]
1. Nyakati nyingine huenda tukapambana na hisia gani, na kwa nini?
2. Ni kwa njia gani Yehova hutupatia matakwa yenye usawaziko?
3. Yehova hutuimarishaje ili tuvumilie?
4. Kwa nini ni muhimu kukumbuka sikuzote ahadi za Mungu?
5. Kwa nini ni jambo lenye kutia moyo kukumbuka matendo yetu ya ushikamanifu ya zamani?