Kumpa Yehova Kilicho Bora
1 Sheria ya Yehova kwa Waisraeli iliagiza kwamba wanyama waliotolewa kuwa dhabihu ‘hawakupaswa kuwa na kasoro.’ Mnyama mwenye kasoro hakukubaliwa. (Law. 22:18-20; Mal. 1:6-9) Isitoshe, dhabihu ilipotolewa, Yehova alipewa mafuta yote, yaani, sehemu iliyo bora. (Law. 3:14-16) Akiwa Baba na Bwana-Mkuu wa Israeli, Yehova alistahili kupewa kilicho bora zaidi.
2 Kama ilivyokuwa nyakati za kale, Mungu anapendezwa sana na ubora wa dhabihu zetu leo. Utumishi wetu unapaswa kuonyesha heshima inayofaa kwa Yehova. Ni kweli kwamba hali za watu hutofautiana. Hata hivyo, tuna sababu nzuri za kujichunguza ili kuhakikisha kwamba tunampa Yehova kilicho bora.—Efe. 5:10.
3 Utumishi wa Moyo Wote: Ili huduma yetu imheshimu Yehova na kuchochea mioyo ya wasikilizaji wetu, haipaswi kuwa ya kidesturi. Yale tunayosema kumhusu Mungu wetu na makusudi yake matukufu yanapaswa kutoka katika mioyo iliyojaa shukrani. (Zab. 145:7) Hilo linakazia umuhimu wa kuwa na programu nzuri ya kusoma na kujifunza Biblia kibinafsi.—Met. 15:28.
4 Kumpa Yehova kilicho bora kunatia ndani kuiga upendo wake kwa watu. (Efe. 5:1, 2) Upendo wetu kwa watu utatuchochea kujaribu kuwajulisha wengi iwezekanavyo ujumbe wa kweli wenye kuokoa uhai. (Marko 6:34) Unatusukuma tupendezwe kibinafsi na wale tunaozungumza nao. Unatufanya tuendelee kuwafikiria baada ya kukutana nao mara ya kwanza na kutuchochea turudi tena. Unatuchochea kufanya yote tuwezayo kuwasaidia wafanye maendeleo ya kiroho.—Mdo. 20:24; 26:28, 29.
5 “Dhabihu ya Sifa”: Kuwa na bidii katika huduma ni njia nyingine ya kumpa Yehova kilicho bora. Tunaweza kutimiza mengi katika muda mfupi ikiwa tuna ratiba nzuri na tunakazia fikira kazi iliyo mbele yetu. (1 Tim. 4:10) Yaelekea watu wengi watatusikiliza ikiwa tutajitayarisha vizuri na kuzungumza kwa njia inayoeleweka na kwa usadikisho. (Met. 16:21) Tunapowahubiria wengine habari njema, yale tunayosema kutoka moyoni yanaweza kwa kufaa kuitwa “dhabihu ya sifa.”—Ebr. 13:15.