Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Angalia Sana Jinsi Unavyotumia Wakati
    Huduma ya Ufalme—2004 | Januari
    • Angalia Sana Jinsi Unavyotumia Wakati

      1 Siku hizi ambapo kuna vyombo vinavyookoa wakati na kurahisisha kazi, watu wengi hujikuta wakiwa na mambo mengi ya kufanya na wakati mchache wa kuyafanya. Je, wewe huona ni vigumu kudumisha kawaida nzuri ya kiroho? Je, unatamani kuwa na wakati zaidi kwa ajili ya huduma? Tunaweza kutumiaje wakati wetu kwa njia nzuri zaidi?—Zab. 90:12; Flp. 1:9-11.

      2 Tambua Mambo Yanayopoteza Wakati: Sisi sote tunapaswa kujichunguza mara kwa mara kuhusu jinsi tunavyotumia wakati wetu. Biblia inatuhimiza hivi: “Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa, kwa sababu siku hizi ni zenye uovu.” (Efe. 5:15, 16) Fikiria magumu yanayotokezwa na maendeleo katika teknolojia ya habari. Ingawa kompyuta na vyombo vingine vya elektroni vina matumizi mazuri, vinaweza kuwa mtego tukishindwa kuangalia sana jinsi tunavyotumia wakati wetu.—1 Kor. 7:29, 31.

      3 Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza: ‘Je, mimi hutumia wakati kila siku nikisoma au nikijibu ujumbe wa barua-pepe ambao ni usumbufu mtupu tu? Je, mara nyingi mimi hujishughulisha kupiga simu au kutuma ujumbe wa elektroni kuhusu mambo madogo-madogo? (1 Tim. 5:13) Je, mimi husoma-soma Intaneti bila kusudi lolote au kubadili-badili kituo cha televisheni bila lengo? Je, kujishughulisha mno na michezo ya kompyuta kumeanza kuingilia funzo langu la Neno la Mungu?’ Kufuatilia mambo hayo kunaweza kutufanya tupoteze polepole hali yetu ya kiroho.—Met. 12:11.

      4 Kutumia Wakati kwa Hekima: Vyombo vya elektroni huchukua wakati na uangalifu wetu. Kijana mmoja aliyekuwa amejiingiza sana katika michezo ya kompyuta alikiri hivi: “Wakati mwingine nilipocheza kabla ya kwenda katika huduma au katika mkutano wa Kikristo, ilikuwa vigumu kukaza fikira. Nyakati zote nilikuwa nikifikiri jinsi ya kucheza mchezo kwa njia bora zaidi baada ya kufika nyumbani. Funzo langu na usomaji wangu wa Biblia viliathirika. Shangwe yangu ya kumtumikia Mungu ilianza kupungua.” Akitambua kwamba alihitaji kufanya mabadiliko, alifuta michezo yake yote ya kompyuta. Anasema, “Hilo lilikuwa jambo gumu kwelikweli. Nilikuwa nimejiingiza sana katika michezo kuliko nilivyofikiri. Lakini pia nilihisi ushindi mkubwa kwa sababu nilijua kwamba nimefanya jambo hilo kwa faida yangu mwenyewe.”—Mt. 5:29, 30.

      5 Huenda ikawa lazima kuchukua hatua hizo ikiwa kuna mambo unayopaswa kufanyia marekebisho. Je, unaweza kununua nusu saa kila siku kutokana na shughuli zisizo za lazima? Huo ndio wakati unaohitaji kila siku ili kuisoma Biblia nzima katika mwaka mmoja. Hilo lingekuwa jambo lenye faida kama nini! (Zab. 19:7-11; 119:97-100) Tenga wakati hususa wa kusoma Biblia, kutayarisha mikutano, na kushiriki katika huduma ya shambani. (1 Kor. 15:58) Kufanya hivyo kutakusaidia kuzuia mambo yanayopoteza wakati na kukuwezesha ‘kuendelea kufahamu yale yaliyo mapenzi ya Yehova.’—Efe. 5:17.

  • Habari za Kitheokrasi
    Huduma ya Ufalme—2004 | Januari
    • Habari za Kitheokrasi

      ◼ Majumba ya Ufalme yafuatayo yaliwekwa wakfu hivi karibuni:

      Kenya:Bumala, Kibui, Mbuyu, Nunguni, Ugunja, na Ukwala.

      Tanzania:Chanji, Madaba, Namanyere, na Tindingoma.

      Uganda:Bushenyi.

  • Mambo ya Kusema Kuhusu Magazeti
    Huduma ya Ufalme—2004 | Januari
    • Mambo ya Kusema Kuhusu Magazeti

      Mnara wa Mlinzi Des. 15

      “Wakati huu wa mwaka, watu wengi hufikiria kuhusu kuzaliwa kwa Yesu. Je, umewahi kujiuliza alikulia katika familia ya aina gani? [Mruhusu ajibu. Kisha soma Luka 2:51, 52.] Gazeti hili la Mnara wa Mlinzi linazungumzia mambo tunayoweza kujifunza kutokana na masimulizi ya Biblia kuhusu malezi ya Yesu.”

      Amkeni! Des. 22

      “Sote tunatamani kuona watoto wetu wakiishi maisha yenye furaha na mafanikio. Unafikiri watoto wanahitaji nini ili kukabiliana na ulimwengu huu wa leo wenye mikazo? [Mruhusu ajibu. Kisha soma Methali 22:6.] Gazeti hili la Amkeni! linazungumzia kile ambacho watoto wanahitaji na jinsi wazazi wanavyoweza kutimiza mahitaji hayo.”

      Mnara wa Mlinzi Jan. 1

      “Watu wengi hutamani amani duniani. Je, unafikiri kwamba tutapata kuona mambo hayo yakitimizwa? [Soma Zaburi 46:9. Kisha mruhusu ajibu.] Gazeti hili la Mnara wa Mlinzi linazungumzia jinsi jambo hilo litakavyotimizwa na kwa nini tunaweza kuwa na uhakika katika ahadi ya Mungu kuhusu ulimwengu usio na vita.”

      Amkeni! Jan. 8

      “Ulimwenguni pote, mamilioni ya watu wanaugua ugonjwa wa kihisia, kama vile kushuka moyo na hisia zinazobadilika-badilika. Muumba wetu anawajali sana watu hao. [Soma Zaburi 34:18.] Gazeti hili linazungumzia jinsi watu wanaougua wanavyoweza kusaidiwa. Pia linataja ahadi ya Biblia kwamba hivi karibuni ugonjwa utaondolewa.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki