Maandalizi ya Kutusaidia Tujiepushe na Damu
Baraza Linaloongoza liliidhinisha matumizi ya kadi ya Mwelekezo wa Mapema Kuhusu Tiba/Ondoleo la Hatia. Kila mhubiri aliyebatizwa anapaswa kuwa na kadi hiyo siku zote.
Unahitaji kuhakikisha kwamba kadi yako imejazwa vizuri. Kadi hiyo ambayo muda wake wa kutumika haumaliziki, inaweza kutumiwa mahali popote nchini, na pia inaweza kuonyesha matakwa yako kuhusu damu unaposafiri nchi za nje. Unapaswa kujaza kadi nyingine ya Mwelekezo wa Mapema Kuhusu Tiba/Ondoleo la Hatia ikiwa (1) unataka kubadili mambo fulani kwenye kadi yako kama vile anwani, namba zako za simu, au (2) kadi yako imepotea au imeharibika.
Kadi ya Mwelekezo wa Mapema Kuhusu Tiba/Ondoleo la Hatia, inapaswa kujazwa nyumbani na kwa makini baada ya kutoa sala. Hata hivyo, kabla ya kuitia sahihi, ni muhimu kufuata kwa makini matakwa ya kisheria. Kwa mfano, kadi yako inasema kwamba unahitaji kuwa na mashahidi wawili unapoitia sahihi, hivyo wanapaswa kuwepo unapofanya hivyo. Mara kwa mara, waangalizi wa funzo la kitabu, wanaweza kuzungumza na wale ambao hawajajaza kadi mpya kuona kama wanahitaji msaada. Unapaswa kuwa na kadi yenyewe bali si fotokopi.
Ile Kadi ya Utambulisho iliyochapishwa 3/99 ya watoto ambao hawajabatizwa na ambao wazazi wao ni Mashahidi, inapaswa kutumiwa. Wazazi wanapaswa kuhakikisha kwamba kadi ya kila mtoto imejazwa vizuri na kutiwa sahihi, na kwamba anakuwa nayo nyakati zifaazo.
Wahubiri ambao hawajabatizwa wanaweza kuandika mwelekezo wao wenyewe na wa watoto wao wakitumia maneno yaliyo katika kadi ya Mwelekezo wa Mapema Kuhusu Tiba/Ondoleo la Hatia na Kadi ya Utambulisho. Wahubiri wote ambao huenda wakabatizwa mwaka huu wanapaswa kupewa kadi ya Mwelekezo wa Mapema Kuhusu Tiba/Ondoleo la Hatia punde baada ya kubatizwa.