SOMO LA 53
Kuwatia Moyo na Kuwatia Nguvu Wasikilizaji
HATA iwe watumishi wa Mungu wanakabili matatizo ya aina gani, wanapaswa kutiwa moyo katika kutaniko la Kikristo. Basi, hasa wazee wahakikishe kwamba wanatoa hotuba na mashauri yenye kutia moyo. Wazee wanapaswa kuwa “kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.”—Isa. 32:2.
Ikiwa wewe ni mzee, je, hotuba zako zinafariji? Je, zinawatia nguvu wale wanaojaribu kumtumikia Yehova kwa uaminifu? Je, zinawachochea waendelee kuvumilia wanapofanya mapenzi ya Mungu japo upinzani au kutojali kwa watu? Namna gani kama baadhi ya wahudhuriaji wamevunjika moyo, wana mikazo ya kiuchumi, au wanaugua magonjwa ambayo hayawezi kutibiwa wakati huu? Unaweza ‘kuwatia nguvu ndugu zako kwa kinywa chako.’—Ayu. 16:5.
Tumia nafasi ambayo umepata ukiwa msemaji kuwasaidia ndugu zako kupata tumaini na nguvu kutoka kwa Yehova na maandalizi yake.—Rom. 15:13; Efe. 6:10.
Wakumbushe Matendo ya Yehova. Njia muhimu ya kuwatia moyo ni kuwaonyesha jinsi Yehova alivyowasaidia watu wake walipokabili magumu wakati uliopita.—Rom. 15:4.
Yehova alimwambia Musa ‘amtie Yoshua moyo’ na ‘kumtia nguvu’ kabla ya Israeli kuingia katika Nchi ya Ahadi, ambayo wakati huo ilikaliwa na mataifa adui. Musa alifanyaje? Yoshua akiwapo, Musa alikumbusha taifa lote mambo ambayo Yehova aliwafanyia walipokuwa wakitoka Misri. (Kum. 3:28; 7:18) Pia Musa aliwakumbusha jinsi ambavyo Yehova aliwasaidia kuwashinda Waamori. Musa akamhimiza Yoshua: ‘Uwe hodari na moyo wa ushujaa.’ (Kum. 31:1-8) Unapotaka kuwatia moyo ndugu zako, je, unawasaidia kupata nguvu kwa kuwakumbusha mambo ambayo tayari Yehova amewafanyia?
Nyakati nyingine watu hulemewa sana na matatizo hivi kwamba wanaona ni kama hawatapata baraka za Ufalme. Wakumbushe kwamba ahadi za Yehova ni za kutegemeka.—Yos. 23:14.
Kuna nchi ambazo ndugu zetu wamepigwa marufuku kuhubiri habari njema. Katika hali kama hizo, wazee wenye upendo wanaweza kuwasaidia waamini wenzao kupata nguvu kutokana na mambo yaliyowapata mitume wa Yesu Kristo. (Mdo. 4:1–5:42) Na kuonyesha jinsi Mungu alivyoongoza mambo kulingana na masimulizi ya kitabu cha Esta kutawachochea akina ndugu kuwa na ujasiri.
Nyakati nyingine watu fulani huhudhuria mikutano ya kutaniko lakini hawafanyi maendeleo zaidi. Labda wanahisi kwamba Mungu hawezi kamwe kuwasamehe kwa sababu waliishi maisha maovu zamani. Unaweza kuwasimulia jinsi Yehova alivyomsamehe Mfalme Manase. (2 Nya. 33:1-16) Au unaweza kuwasimulia kuhusu wakazi wa Korintho la kale ambao walibadili maisha yao, wakawa Wakristo, na Mungu akawatangaza kuwa waadilifu.—1 Kor. 6:9-11.
Je, kuna wengine wanaofikiri wanapata matatizo kwa sababu Mungu amewaacha? Unaweza kuwakumbusha matatizo ya Yobu na baraka alizopata kwa sababu ya kudumisha sana uaminifu wake kwa Yehova. (Ayu. 1:1-22; 10:1; 42:12, 13; Zab. 34:19) Wafariji bandia wa Yobu walidai isivyo kweli kwamba ni lazima Yobu awe alitenda dhambi fulani. (Ayu. 4:7, 8; 8:5, 6) Tofauti na hao, Paulo na Barnaba walipokuwa wakiwatia nguvu wanafunzi na ‘kuwatia moyo kubaki katika imani,’ walisema: “Lazima tuingie katika ufalme wa Mungu kupitia dhiki nyingi.” (Mdo. 14:21, 22) Leo vilevile, unaweza kuwatia nguvu wale wanaopata majaribu kwa kuwaonyesha kwamba Wakristo wote wanapaswa kuvumilia majaribu na kwamba Mungu anathamini sana uvumilivu wao.—Mit. 27:11; Mt. 24:13; Rom. 5:3, 4; 2 Tim. 3:12.
Watie moyo wasikilizaji wafikirie jinsi ambavyo Yehova ametimiza ahadi zake katika maisha yao. Wakikumbushwa kidogo tu, wanaweza kuona mambo ambayo Yehova tayari amewatendea kama alivyoahidi. Zaburi 32:8 inasema: “Nitakufundisha na kukuonyesha njia utakayoiendea; nitakushauri, jicho langu likikutazama.” Kuwakumbusha wasikilizaji jinsi ambavyo Yehova amewaongoza au kuwatia nguvu kutawasaidia kutambua wazi kwamba Yehova anawajali na kwamba kwa kweli atawasaidia wanapokabili majaribu yoyote wakati huu.—Isa. 41:10, 13; 1 Pet. 5:7.
Furahia Matendo ya Mungu Sasa. Unapotaka kuwatia moyo ndugu zako, waonyeshe mambo ambayo Yehova anafanya sasa. Ukizungumzia mambo hayo kwa furaha, utawachochea wasikilizaji pia wayafurahie katika mioyo yao.
Zungumzia jinsi Yehova anavyotusaidia kushinda mikazo ya maisha. Anatuonyesha njia bora zaidi ya kuishi. (Isa. 30:21) Anatueleza chanzo cha uhalifu, ukosefu wa haki, umaskini, ugonjwa, na kifo na kutuambia jinsi atakavyokomesha mambo hayo yote. Ametuzingira kwa udugu wenye upendo. Ametupatia pendeleo kubwa la sala. Ametukabidhi pendeleo la kuwa Mashahidi wake. Ametufunulia kwamba tayari Kristo ametawazwa mbinguni na kwamba siku za mwisho za mfumo huu wa kale zinamalizika upesi.—Ufu. 12:1-12.
Mbali na baraka hizo, kuna mikutano ya kutaniko na makusanyiko. Unapozungumzia maandalizi hayo kwa njia inayoonyesha unayathamini sana, utatia nguvu azimio la wengine la kukusanyika pamoja na akina ndugu bila kukosa.—Ebr. 10:23-25.
Tunatiwa nguvu pia na ripoti zinazothibitisha kwamba kwa kweli Yehova anabariki jitihada zetu katika huduma ya shambani. Katika karne ya kwanza wakati Paulo na Barnaba walipokuwa njiani kuelekea Yerusalemu, ‘walisababisha shangwe kubwa kwa akina ndugu wote’ kwa kuwasimulia kwa undani jinsi watu wa mataifa walivyogeuka. (Mdo. 15:3) Wewe pia unaweza kuwapa akina ndugu shangwe kwa kuwasimulia mambo yaliyoonwa yanayopendeza.
Watu hutiwa moyo zaidi wanaposaidiwa kuona umuhimu wa utendaji wao. Wapongeze kwa kazi wanayofanya katika huduma ya Kikristo. Wapongeze wale ambao utendaji wao umepungua kwa sababu ya uzee au ugonjwa lakini bado wanaendelea kuvumilia kwa uaminifu. Wakumbushe kwamba Yehova hasahau upendo ambao wameonyesha kwa ajili ya jina lake. (Ebr. 6:10) Imani inayothibitishwa na jaribu ni bora sana. (1 Pet. 1:6, 7) Akina ndugu wanahitaji kukumbushwa jambo hilo.
Zungumza kwa Hisia Kuhusu Tumaini la Wakati Ujao. Ahadi za Mungu za mambo yajayo huwatia moyo sana wote wanaompenda. Labda wengi miongoni mwa wasikilizaji wamesikia ahadi hizo. Lakini unaweza kufanya baraka hizo ziwe halisi kwa kuzizungumzia kwa uthamini sana, na kuwahakikishia wasikilizaji kwamba zitatimizwa, na kufanya mioyo yao ijae shukrani. Kutumia mambo ambayo umejifunza katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi kunaweza kukusaidia kutimiza jambo hilo.
Yehova mwenyewe ndiye Chanzo kikuu cha kitia-moyo na nguvu. Lakini unaweza kushirikiana naye kuwatia moyo wengine na kuwapa nguvu. Unapohutubia kutaniko, tumia vizuri pindi hiyo kuwatia moyo na kuwapa nguvu akina ndugu.