Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuwasaidia Wengine Wamtukuze Yehova
    Huduma ya Ufalme—2002 | Septemba
    • Kuwasaidia Wengine Wamtukuze Yehova

      1 Watu wanatangaziwa ujumbe muhimu kotekote duniani leo: “Hofuni Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imewasili, na kwa hiyo mwabuduni Yeye aliyezifanya mbingu na dunia na bahari na mabubujiko ya maji.” (Ufu. 14:6, 7) Ni pendeleo letu kushiriki kutangaza ujumbe huo. Watu wanahitaji kujua nini kumhusu Yehova ili wamhofu na kumwabudu?

      2 Jina Lake: Watu wanahitaji kumjua Mungu wa kweli kwa jina ili wamtofautishe na miungu mingi ya uwongo inayoabudiwa leo. (Kum. 4:35; 1 Kor. 8:5, 6) Waandishi wa Biblia walilitumia jina tukufu la Yehova zaidi ya mara 7,000. Ijapokuwa sisi hutumia busara tunapowajulisha watu jina la Mungu, hatupaswi kamwe kulificha wala kuacha kulitumia. Mungu anataka wanadamu wote walijue jina lake.—Zab. 83:18.

      3 Sifa Zake: Ili wamtukuze Yehova, watu wanahitaji kujua sifa zake. Inatubidi kuwafundisha kuhusu upendo wake mkuu, hekima yake isiyo na kifani, haki kamili, na kwamba yeye ndiye mwenye nguvu zote. Wanahitaji pia kujua kuhusu rehema yake, fadhili yake yenye upendo, na sifa nyingine nzuri ajabu. (Kut. 34:6, 7) Ni lazima pia wafundishwe kumhofu Mungu kwa njia inayofaa na kumheshimu, wakitambua kwamba wataweza kuishi milele tu iwapo watapata kibali chake.—Zab. 89:7.

      4 Kumkaribia Mungu: Ili waokoke hukumu ya Mungu inayokuja, ni lazima watu wamwitie Yehova kwa imani. (Rom. 10:13, 14; 2 The. 1:8) Jambo hilo linatia ndani mengi zaidi kuliko kujua tu jina la Mungu na sifa zake. Tunahitaji kuwasaidia watu kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, ili wamtumaini kwa moyo wao wote. (Mit. 3:5, 6) Wanapofuata yale wanayojifunza maishani mwao, wanaposali kwa Mungu kwa moyo wao wote, na kuona jinsi anavyowasaidia maishani, imani yao itaimarishwa, nao watasaidiwa kumkaribia Yehova.—Zab. 34:8.

      5 Na tutangaze jina la Mungu kwa bidii na tuwasaidie wengine kumtumaini kabisa na kumhofu. Huenda tukaweza kuwasaidia wengi zaidi kumjua Yehova na kumtukuza kwa sababu yeye ni ‘Mungu wao wa wokovu.’—Zab. 25:5.

  • Onyesha Kwamba Unathamini Vichapo vya Biblia
    Huduma ya Ufalme—2002 | Septemba
    • Onyesha Kwamba Unathamini Vichapo vya Biblia

      1 Mfalme Yosia alipofanya mipango ya kurekebisha hekalu aliwasifu wale waliopewa kazi hiyo kwa kusema hivi: ‘Wasiulizwe habari za ile fedha waliyokabidhiwa; maana wanatenda kazi kwa uaminifu.’ (2 Fal. 22:3-7) Wanaume hao walionyesha kwamba walitambua thamani ya vitu vitakatifu kwa kushughulikia mali walizokabidhiwa kwa njia inayofaa. Hali kadhalika, sisi tunapofanya kazi takatifu ya habari njema ya Mungu leo, twahitaji kutumia mali ambazo tumekabidhiwa kwa uaminifu.

      2 Katika Utumishi wa Shambani: Tutavithamini sana vichapo vyetu iwapo tutaelewa ujumbe muhimu uliomo na kutambua gharama za kuvitengeneza. Vichapo vyetu havipaswi kutolewa kwa watu ambao hawathamini ujumbe wa Biblia kwa dhati. Iwapo mtu hapendezwi sana na habari njema, tunaweza kumpatia trakti badala ya kichapo kingine.

      3 Vigawe vichapo kwa njia inayoonyesha kwamba ni vyenye thamani. Epuka kuviacha mahali pa umma ambapo vitatapanyika ovyoovyo tu. Ili kuepuka kupoteza vichapo bure, hesabu vichapo ulivyo navyo nyumbani kabla ya kuchukua vingine. Unaweza kupunguza agizo lako la magazeti ikiwa wewe hubaki na magazeti kadhaa ya kila toleo.

      4 Vichapo Vyako Mwenyewe: Tunapaswa kuagiza vichapo ambavyo tunavihitaji tu. Tunapaswa kufikiria gharama hasa tunapoagiza Biblia aina ya deluxe, Reference Bible, na vichapo vikubwa kama vile Concordance, Index, Insight, na kitabu cha Wapiga-Mbiu. Fedha nyingi hutumiwa kuvitengeneza vichapo hivyo.

      5 Je, wewe huandika jina lako na anwani yako katika vichapo vyako mwenyewe? Jambo hilo hupunguza uhitaji wa kuchukua vichapo vipya kichapo fulani kikipotea. Ukipoteza kitabu chako cha nyimbo, Biblia yako, au kitabu cha funzo, huenda ukakipata katika idara ya vitu vilivyopotea na kupatikana kwenye kusanyiko au katika Jumba la Ufalme.—Luka 15:8, 9.

      6 Na tujitahidi kutumia vichapo vyetu kwa njia ya hekima. Tukifanya hivyo tutaonyesha kwamba sisi tu waaminifu tunaposhughulikia mali za Ufalme ambazo Yehova ametukabidhi.—Luka 16:10.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki