Onyesha Kwamba Unathamini Vichapo vya Biblia
1 Mfalme Yosia alipofanya mipango ya kurekebisha hekalu aliwasifu wale waliopewa kazi hiyo kwa kusema hivi: ‘Wasiulizwe habari za ile fedha waliyokabidhiwa; maana wanatenda kazi kwa uaminifu.’ (2 Fal. 22:3-7) Wanaume hao walionyesha kwamba walitambua thamani ya vitu vitakatifu kwa kushughulikia mali walizokabidhiwa kwa njia inayofaa. Hali kadhalika, sisi tunapofanya kazi takatifu ya habari njema ya Mungu leo, twahitaji kutumia mali ambazo tumekabidhiwa kwa uaminifu.
2 Katika Utumishi wa Shambani: Tutavithamini sana vichapo vyetu iwapo tutaelewa ujumbe muhimu uliomo na kutambua gharama za kuvitengeneza. Vichapo vyetu havipaswi kutolewa kwa watu ambao hawathamini ujumbe wa Biblia kwa dhati. Iwapo mtu hapendezwi sana na habari njema, tunaweza kumpatia trakti badala ya kichapo kingine.
3 Vigawe vichapo kwa njia inayoonyesha kwamba ni vyenye thamani. Epuka kuviacha mahali pa umma ambapo vitatapanyika ovyoovyo tu. Ili kuepuka kupoteza vichapo bure, hesabu vichapo ulivyo navyo nyumbani kabla ya kuchukua vingine. Unaweza kupunguza agizo lako la magazeti ikiwa wewe hubaki na magazeti kadhaa ya kila toleo.
4 Vichapo Vyako Mwenyewe: Tunapaswa kuagiza vichapo ambavyo tunavihitaji tu. Tunapaswa kufikiria gharama hasa tunapoagiza Biblia aina ya deluxe, Reference Bible, na vichapo vikubwa kama vile Concordance, Index, Insight, na kitabu cha Wapiga-Mbiu. Fedha nyingi hutumiwa kuvitengeneza vichapo hivyo.
5 Je, wewe huandika jina lako na anwani yako katika vichapo vyako mwenyewe? Jambo hilo hupunguza uhitaji wa kuchukua vichapo vipya kichapo fulani kikipotea. Ukipoteza kitabu chako cha nyimbo, Biblia yako, au kitabu cha funzo, huenda ukakipata katika idara ya vitu vilivyopotea na kupatikana kwenye kusanyiko au katika Jumba la Ufalme.—Luka 15:8, 9.
6 Na tujitahidi kutumia vichapo vyetu kwa njia ya hekima. Tukifanya hivyo tutaonyesha kwamba sisi tu waaminifu tunaposhughulikia mali za Ufalme ambazo Yehova ametukabidhi.—Luka 16:10.