-
Thamini Ifaavyo Zawadi Yako ya UhaiMnara wa Mlinzi—2004 | Juni 15
-
-
Thamini Ifaavyo Zawadi Yako ya Uhai
“Damu ya Kristo . . . itazisafisha dhamiri zetu kutoka katika matendo yaliyokufa ili tutoe utumishi mtakatifu kwa Mungu aliye hai.”—WAEBRANIA 9:14.
1. Kuna uthibitisho gani kwamba tunathamini sana uhai?
KAMA ungeombwa ukadirie thamani ya uhai wako, ungejibuje? Tunathamini sana uhai—wetu wenyewe na ule wa wengine. Na hiyo ni kweli, kwa kuwa huenda tukaenda kumwona daktari tunapokuwa wagonjwa au tunapotaka kufanyiwa uchunguzi wa kawaida wa kitiba. Tunataka kuendelea kuwa hai na wenye afya. Hata wengi walio wazee au walemavu, hawataki kufa; wanataka kuendelea kuwa hai.
2, 3. (a) Andiko la Methali 23:22 linakazia wajibu gani? (b) Mungu anahusikaje katika wajibu unaotajwa kwenye Methali 23:22?
2 Uhusiano wako pamoja na wengine huathiriwa na jinsi unavyothamini uhai. Kwa mfano, Neno la Mungu hutuagiza hivi: “Msikilize baba yako aliyekuzaa, wala usimdharau mama yako kwa sababu tu amezeeka.” (Methali 23:22) “Kusikiliza” humaanisha mengi zaidi ya kusikia maneno tu; methali hiyo inamaanisha kusikia kisha kutii. (Kutoka 15:26; Kumbukumbu la Torati 7:12; 13:18; 15:5; Yoshua 22:2; Zaburi 81:13) Kwa nini Neno la Mungu linasema usikilize baba na mama yako? Si kwa sababu tu baba na mama yako wana umri mkubwa kuliko wewe au wana ujuzi zaidi. Sababu ni kwamba ‘walikuzaa.’ Biblia fulani hutafsiri hivi mstari huo: “Msikilize baba yako aliyekupa uhai.” Inaeleweka kwamba, kama unathamini uhai wako, unahisi ukiwa na wajibu kwa chanzo cha uhai huo.
3 Bila shaka, ikiwa wewe ni Mkristo wa kweli unamtambua Yehova kuwa Chanzo hasa cha uhai wako. Kwake yeye ‘una uhai;’ unaweza ‘kwenda,’ kuhisi; na sasa ‘uko,’ na unaweza kufikiri au kupangia wakati ujao, kutia ndani uzima wa milele. (Matendo 17:28; Zaburi 36:9; Mhubiri 3:11) Kupatana na andiko la Methali 23:22, inafaa ‘kumsikiliza’ Mungu kwa utii, ukiwa na tamaa ya kuelewa na kutenda kupatana na maoni yake kuhusu uhai badala ya kuwa na maoni tofauti na yake.
Heshimu Uhai
4. Mapema katika historia ya mwanadamu, heshima kwa uhai ilipataje kuwa suala muhimu?
4 Mapema katika historia ya mwanadamu, Yehova alionyesha wazi kwamba hakuwaruhusu wanadamu watumie (au watumie vibaya) uhai kwa njia yoyote ile. Akiwa mwenye hasira nyingi yenye wivu, Kaini alimuua ndugu yake Abeli asiyekuwa na hatia. Je, unafikiri kwamba Kaini alikuwa na haki ya kufanya uamuzi kama huo kuhusu uhai? Mungu hakufikiri hivyo. Alimtaka Kaini atoe hesabu: “Umefanya nini? Sikiliza! Damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika udongo.” (Mwanzo 4:10) Ona kwamba damu ya Abeli kwenye udongo iliwakilisha uhai wake, uliokuwa umekatishwa kikatili, nayo ilimlilia Mungu alipize kisasi.—Waebrania 12:24.
5. (a) Mungu aliweka kizuizi gani katika siku za Noa, nacho kiliwahusu nani? (b) Kizuizi hicho kilikuwa hatua muhimu katika maana gani?
5 Baada ya Gharika, jamii ya kibinadamu ilianza upya ikiwa na watu wanane tu. Katika tangazo kwa wanadamu wote, Mungu alitoa habari zaidi kuhusu jinsi anavyothamini uhai na damu. Alisema kwamba wanadamu wanaweza kula nyama, lakini akaweka kizuizi hiki: “Kila mnyama anayetembea ambaye yuko hai anaweza kuwa chakula chenu. Kama nilivyowapa mimea ya majani, nawapeni hao wote. Isipokuwa tu nyama pamoja na nafsi yake—damu yake—msile.” (Mwanzo 9:3, 4) Wayahudi fulani hufasiri mstari wa 4 kuwa unamaanisha kwamba wanadamu hawakupaswa kula nyama au damu ya mnyama aliye hai. Lakini baadaye ilionyeshwa wazi kwamba hapa Mungu alikataza kula damu ili kutegemeza uhai. Isitoshe, amri ya Mungu kupitia Noa ilikuwa hatua muhimu katika kutimizwa kwa kusudi Lake kuu kuhusu damu—kusudi ambalo lingewawezesha wanadamu kupata uzima wa milele.
6. Kupitia Noa, Mungu alikaziaje maoni Yake kuhusu thamani ya uhai?
6 Mungu aliendelea kusema: “Damu ya nafsi zenu nitaitaka. Kwa mkono wa kila kiumbe kilicho hai nitaitaka; na kwa mkono wa mwanadamu, kwa mkono wa kila mmoja ambaye ni ndugu yake, nitaitaka nafsi ya mwanadamu. Yeyote anayemwaga damu ya mwanadamu, damu yake nayo itamwagwa na mwanadamu, kwa maana kwa mfano wa Mungu alimfanya mwanadamu.” (Mwanzo 9:5, 6) Unaweza kuona kutokana na tangazo hilo lililotolewa kwa wanadamu wote kwamba Mungu huiona damu ya mwanadamu kuwa inawakilisha uhai. Muumba humpa mtu uhai, na hakuna mtu anayepaswa kukomesha uhai huo unaowakilishwa na damu. Ikiwa kama Kaini, mtu anamuua mwenzake, Muumba ana haki ya ‘kutaka’ uhai wa muuaji huyo.
7. Kwa nini tupendezwe na tangazo ambalo Mungu alimtolea Noa kuhusu damu?
7 Kupitia tangazo lake, Mungu alikuwa akiwaamuru wanadamu wasiitumie damu vibaya. Je, umewahi kujiuliza ni kwa nini? Naam, kwa nini Mungu alikuwa na maoni hayo kuhusu damu? Kwa kweli, jibu linahusu mojawapo ya mafundisho muhimu zaidi ya Biblia. Hilo ni fundisho la msingi katika ujumbe wa Kikristo, ingawa dini nyingi hulipuuza. Fundisho hilo ni gani, nalo linahusuje maisha, maamuzi, na matendo yako?
Damu Ingeweza Kutumiwaje?
8. Yehova aliweka kizuizi gani kuhusu matumizi ya damu katika Sheria?
8 Yehova alitoa habari zaidi kuhusu uhai na damu alipowapa Waisraeli Sheria. Alipowapa Sheria, Mungu alichukua hatua nyingine katika kutimiza kusudi lake. Labda unajua kwamba kulingana na Sheria, Waisraeli walitakiwa kumtolea Mungu matoleo kama vile nafaka, mafuta, na divai. (Mambo ya Walawi 2:1-4; 23:13; Hesabu 15:1-5) Pia walitakiwa kutoa dhabibu za wanyama. Mungu alisema hivi kuhusu dhabihu hizo: “Nafsi ya mwili iko katika damu, nami mwenyewe nimeiweka juu ya madhabahu ili ninyi mfanye upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu, kwa sababu damu ndiyo hufanya upatanisho kupitia nafsi iliyo ndani yake. Ndiyo sababu nimewaambia wana wa Israeli: ‘Nafsi yoyote kati yenu isile damu.’” Yehova aliongeza kusema kwamba ikiwa mtu kama vile mwindaji au mkulima aliua mnyama kwa ajili ya chakula, alipaswa kutoa damu na kuifunika kwa mavumbi. Kwa kuimwaga damu hiyo kwenye dunia ambayo ni kiti cha miguu cha Mungu, mtu huyo alitambua kwamba uhai huo ulikuwa ukirudishwa kwa Mpaji-Uhai.—Mambo ya Walawi 17:11-13; Isaya 66:1.
9. Kulingana na Sheria damu ingetumiwa kwa jambo gani pekee, na kusudi lilikuwa nini?
9 Sheria hiyo haikuwa desturi tu ya kidini isiyo na maana kwetu. Je, uliona ni kwa nini Waisraeli hawakupaswa kula damu? Mungu alisema: “Ndiyo sababu nimewaambia wana wa Israeli: ‘Nafsi yoyote kati yenu isile damu.’” Kwa nini alisema hivyo? “Nami mwenyewe nimeiweka juu ya madhabahu ili ninyi mfanye upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu.” Je, unaona kwamba andiko hilo linafafanua ni kwa nini Mungu alimwambia Noa kwamba wanadamu hawapaswi kula damu? Muumba aliamua kuiona damu kuwa na umuhimu mkubwa sana, na kukubali itumiwe tu kwa njia moja ya pekee ambayo ingeweza kuokoa uhai wa watu wengi. Damu ingetimiza fungu kubwa katika kufunika dhambi (upatanisho). Kwa hiyo, chini ya Sheria, Yehova alikubali damu itumiwe tu kwenye madhabahu ili kufanya upatanisho kwa ajili ya uhai wa Waisraeli, waliotaka kupata msamaha wake.
10. Kwa nini damu ya mnyama haingeweza kutokeza msamaha kamili, lakini dhabihu zilizotolewa chini ya Sheria ziliwakumbusha Waisraeli nini?
10 Wazo hilo linajulikana katika Ukristo. Akirejelea sehemu hiyo ya Sheria iliyopangwa na Mungu, mtume Mkristo Paulo aliandika hivi: “Karibu vitu vyote husafishwa kwa damu kulingana na Sheria, na damu isipomwagwa hakuna msamaha unaotokea.” (Waebrania 9:22) Paulo alionyesha wazi kwamba dhabihu zilizotolewa hazikuwafanya Waisraeli wawe wanadamu wakamilifu, wasio na dhambi. Aliandika hivi: “Kwa dhabihu hizo kuna kukumbusha juu ya dhambi mwaka baada ya mwaka, kwa maana haiwezekani damu ya ng’ombe na ya mbuzi kuondolea mbali dhambi.” (Waebrania 10:1-4) Hata hivyo, dhabihu hizo zilitimiza kusudi fulani. Ziliwakumbusha Waisraeli kwamba walikuwa wenye dhambi na walihitaji kitu fulani zaidi ili kupata msamaha kamili. Lakini ikiwa damu ambayo iliwakilisha uhai wa wanyama haingeweza kufunika kabisa dhambi za wanadamu, je, kuna damu nyingine ambayo ingeweza kufanya hivyo?
Suluhisho la Mpaji-Uhai
11. Tunajuaje kwamba dhabihu za damu ya wanyama zilielekeza kwenye kitu fulani?
11 Kwa kweli, Sheria ilikuwa ikielekeza kwenye kitu fulani chenye matokeo zaidi katika kutimiza mapenzi ya Mungu. Paulo aliuliza: “Basi, kwa nini Sheria?” Akajibu: “Iliongezwa ili kufanya makosa yawe wazi, mpaka ufike uzao ambao ulikuwa umepewa ahadi; na ilipitishwa kupitia malaika kwa mkono wa mpatanishi [Musa].” (Wagalatia 3:19) Vivyo hivyo, Paulo aliandika hivi: “Sheria ina kivuli cha mambo mema yatakayokuja, lakini si umbo halisi la mambo hayo.”—Waebrania 10:1.
12. Tunaweza kuelewaje ufunuo wa kusudi la Mungu kuhusu damu?
12 Kwa ufupi, kumbuka kwamba katika siku za Noa, Mungu aliagiza kwamba wanadamu wangeweza kula nyama ili wategemeze uhai, lakini hawakupaswa kula damu. Baadaye, Mungu alisema kwamba “nafsi ya mwili iko katika damu.” Kwa kweli, aliamua kuiona damu kuwa inawakilisha uhai na kusema: “Nami mwenyewe nimeiweka [damu] juu ya madhabahu ili ninyi mfanye upatanisho kwa ajili ya nafsi zenu.” Hata hivyo, kungekuwa na ufunuo mkuu zaidi wa kusudi la Mungu. Sheria ilikuwa kivuli cha mambo mema ambayo yangekuja. Ni mambo gani hayo?
13. Kwa nini kifo cha Yesu kilikuwa muhimu?
13 Umbo hilo halisi lilihusu hasa kifo cha Yesu Kristo. Unajua kwamba Yesu aliteswa na kutundikwa mtini. Alikufa kama mhalifu. Paulo aliandika hivi: “Tulipokuwa tungali bado dhaifu, Kristo alikufa wakati uliowekwa. . . . Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Waroma 5:6, 8) Kwa kufa kwa ajili yetu, Kristo aliandaa fidia ili kufunika dhambi zetu. Fidia hiyo ni fundisho la msingi katika ujumbe wa Kikristo. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16; 1 Wakorintho 15:3; 1 Timotheo 2:6) Fidia inahusianaje na damu na uhai, nao uhai wako unahusikaje?
14, 15. (a) Tafsiri fulani hukaziaje kifo cha Yesu kwenye Waefeso 1:7? (b) Ni jambo gani ambalo huenda ukakosa kuona kwenye Waefeso 1:7?
14 Makanisa fulani hukazia kifo cha Yesu, huku wafuasi wake wakisema mambo kama vile “Yesu alikufa kwa ajili yangu.” Ona jinsi Biblia fulani zinavyotafsiri andiko la Waefeso 1:7: “Ni katika yeye na kupitia kifo chake tunakombolewa, yaani, kuondolewa kwa makosa yetu.” (The American Bible, ya Frank Scheil Ballentine, 1902) “Kupitia kifo cha Kristo tunawekwa huru, na kusamehewa dhambi.” (Today’s English Version, 1966) “Ni katika Kristo na kupitia dhabihu ya uhai wake tumekombolewa, ukombozi unaomaanisha kusamehewa dhambi.” (The New Testament, ya William Barclay, 1969) “Tunasamehewa dhambi na kuwekwa huru kupitia kifo cha Kristo.” (The Translator’s New Testament, 1973) Unaweza kuona kwamba tafsiri hizo zinakazia kifo cha Yesu. Huenda wengine wakasema, ‘Lakini kifo cha Yesu ni muhimu kwelikweli. Hivyo, tafsiri hizo zinakosa kutaja nini?’
15 Kwa kweli, kama ungetegemea tafsiri hizo, ungekosa kuona jambo fulani muhimu sana, na hilo lingekuzuia usielewe vizuri ujumbe wa Biblia. Tafsiri hizo hazionyeshi ukweli wa kwamba katika maandishi ya awali andiko la Waefeso 1:7 lina neno la Kigiriki linalomaanisha “damu.” Hivyo, Biblia nyingi kama vile Tafsiri ya Ulimwengu Mpya hutafsiri maandishi ya awali kwa usahihi zaidi: “Kwa njia yake tuna kuachiliwa huru kwa njia ya fidia kupitia damu ya huyo, ndiyo, msamaha wa makosa yetu, kulingana na utajiri wa fadhili zake zisizostahiliwa.”
16. Tafsiri “damu ya huyo” inapaswa kutukumbusha nini?
16 Tafsiri “damu ya huyo” ina maana muhimu sana na inapaswa kutufanya tufikirie mambo mengi kuhusu damu. Mengi yalihitajiwa kuliko tu kifo cha mtu fulani, hata kifo cha mwanadamu mkamilifu Yesu. Alitimiza mambo yaliyoonyeshwa kimbele katika Sheria, hasa kuhusu Siku ya Upatanisho. Katika siku hiyo ya pekee, wanyama ambao walitajwa na Sheria walitolewa wakiwa dhabihu. Kisha kuhani mkuu alipeleka kiasi fulani cha damu yao katika chumba cha Patakatifu Zaidi cha maskani au hekalu, na huko akaitoa, kana kwamba alikuwa mbele za Mungu.—Kutoka 25:22; Mambo ya Walawi 16:2-19.
17. Yesu alitimizaje mambo yaliyoonyeshwa kimbele na Siku ya Upatanisho?
17 Yesu alitimiza mambo yaliyoonyeshwa kimbele na Siku ya Upatanisho, kama alivyoeleza Paulo. Kwanza, Paulo alitaja kwamba kuhani mkuu katika Israeli aliingia Patakatifu Zaidi mara moja kwa mwaka akiwa na damu iliyotolewa “kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya dhambi za hali ya watu ya kutojua.” (Waebrania 9:6, 7) Kupatana na yaliyotokea siku hiyo, Yesu alienda mbinguni kwenyewe baada ya kufufuliwa akiwa kiumbe wa roho. Kwa kuwa alikuwa kiumbe wa roho, asiye na mwili wa nyama na damu, Yesu angeweza kuonekana “mbele za uso wa Mungu kwa ajili yetu.” Alimtolea Mungu nini? Hakutoa kitu halisi bali kitu muhimu sana. Paulo aliendelea kusema: “Kristo alipokuja akiwa kuhani mkuu . . . aliingia, si kwa damu ya mbuzi na ya ng’ombe-dume wachanga, bali kwa damu yake mwenyewe, mara moja kwa wakati wote ndani ya mahali patakatifu na kupata ukombozi wa milele kwa ajili yetu. Kwa maana ikiwa damu ya mbuzi na ya ng’ombe-dume . . . hutakasa kufikia usafi wa mwili, je, si zaidi damu ya Kristo, ambaye kupitia roho inayodumu milele alijitoa mwenyewe bila dosari kwa Mungu, itazisafisha dhamiri zetu kutoka katika matendo yaliyokufa ili tutoe utumishi mtakatifu kwa Mungu aliye hai?” Naam, Yesu alimtolea Mungu thamani ya damu yake.—Waebrania 9:11-14, 24, 28; 10:11-14; 1 Petro 3:18.
18. Kwa nini maandiko ya Biblia kuhusu damu ni muhimu kwa Wakristo leo?
18 Ukweli huo kutoka kwa Mungu hutuwezesha kuelewa mambo yenye kustaajabisha ambayo Biblia husema kuhusu damu—kwa nini Mungu ana maoni hayo kuihusu, jinsi tunavyopaswa kuiona, na kwa nini tunapaswa kuheshimu vizuizi ambavyo Mungu ameweka kuhusu matumizi ya damu. Unaposoma vitabu vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, utaona kwamba vinataja damu ya Kristo mara nyingi. (Ona sanduku.) Hivyo vinaonyesha wazi kwamba kila Mkristo anapaswa kuwa na imani ‘katika damu ya Yesu.’ (Waroma 3:25) Tunaweza tu kupata msamaha na kuwa na amani pamoja na Mungu ‘kupitia damu ambayo Yesu alimwaga.’ (Wakolosai 1:20) Bila shaka, hiyo ni kweli kuhusu wale ambao Yesu alifanya nao agano la pekee la kutawala pamoja naye mbinguni. (Luka 22:20, 28-30; 1 Wakorintho 11:25; Waebrania 13:20) Pia, hilo ni kweli kuhusu “umati mkubwa” leo, ambao utaokoka “dhiki kuu” inayokuja na kuishi milele katika paradiso duniani. Kwa njia ya mfano, ‘wanafua kanzu zao katika damu ya Mwana-Kondoo.’—Ufunuo 7:9, 14.
19, 20. (a) Kwa nini Mungu aliamua kuweka vizuizi kuhusu matumizi ya damu, na tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu jambo hilo? (b) Tunapaswa kupendezwa kujua nini?
19 Ni wazi kwamba damu ina maana ya kipekee machoni pa Mungu. Sisi pia tunapaswa kuiona hivyo. Muumba, ambaye anajali uhai, ana haki ya kuweka vizuizi kuhusu jinsi wanadamu wanavyotumia damu. Kwa kuwa anajali sana uhai wetu, aliazimia damu itumiwe tu kwa njia moja muhimu sana, ambayo hutuwezesha kupata uzima wa milele. Njia hiyo inahusisha damu ya Yesu yenye thamani. Tunashukuru kama nini kwamba Yehova Mungu alitunufaisha kwa kutumia damu—damu ya Yesu—katika njia hii yenye kuokoa uhai! Na tunamshukuru Yesu kama nini kwa kumwaga damu yake kuwa dhabihu kwa ajili yetu! Kwa kweli, tunaweza kuelewa maneno haya ya mtume Yohana: “Kwake yeye anayetupenda na aliyetufungua kutoka katika dhambi zetu kupitia damu yake mwenyewe—naye alitufanya tuwe ufalme, makuhani kwa Mungu na Baba yake—ndiyo, kwake yeye na kuwe utukufu na nguvu milele. Amina.”—Ufunuo 1:5, 6.
20 Mungu wetu mwenye hekima yote na Mpaji-Uhai alifikiria kwa muda mrefu fungu hilo ambalo damu ingetimiza katika kuokoa uhai. Basi, huenda tukajiuliza, ‘Hilo linapaswa kuathirije maamuzi na matendo yetu?’ Swali hilo litajibiwa katika makala inayofuata.
Ungejibuje?
• Tunaweza kujifunza nini kuhusu maoni ya Mungu kuelekea damu kutokana na masimulizi juu ya Abeli na Noa?
• Katika Sheria, Mungu aliweka vizuizi gani kuhusu matumizi ya damu, na kwa nini?
• Yesu alitimizaje mambo yaliyoonyeshwa kimbele na Siku ya Upatanisho?
• Damu ya Yesu inawezaje kuokoa uhai wetu?
-
-
Kubali Mwongozo wa Mungu Aliye HaiMnara wa Mlinzi—2004 | Juni 15
-
-
Kubali Mwongozo wa Mungu Aliye Hai
“Mgeuke . . . mpate kumjia Mungu aliye hai, aliyefanya mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo.”—MATENDO 14:15.
1, 2. Kwa nini inafaa kumtambua Yehova kuwa “Mungu aliye hai”?
BAADA ya mitume Paulo na Barnaba kumponya mtu fulani, Paulo aliwahakikishia hivi watazamaji huko Listra: “Sisi pia ni wanadamu tulio na udhaifu uleule kama ninyi, nasi tunawatangazia ninyi habari njema, ili mgeuke kutoka kwa mambo haya ya bure mpate kumjia Mungu aliye hai, aliyefanya mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo.”—Matendo 14:15.
2 Kwa kweli, Yehova ni “Mungu aliye hai” wala si sanamu isiyo hai! (Yeremia 10:10; 1 Wathesalonike 1:9, 10) Zaidi ya kuwa hai, Yehova ndiye Chanzo cha uhai wetu. “Yeye mwenyewe huwapa watu wote uhai na pumzi na vitu vyote.” (Matendo 17:25) Anataka tufurahie uhai sasa na wakati ujao. Paulo aliongeza kusema kwamba Mungu “hakujiacha mwenyewe bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa ninyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo yenu kikamili kwa chakula na uchangamfu.”—Matendo 14:17.
3. Kwa nini tunaweza kutumaini mwongozo wa Mungu?
3 Kwa kuwa Mungu anapendezwa na uhai wetu hiyo hutupa sababu ya kutumaini mwongozo wake. (Zaburi 147:8; Mathayo 5:45) Huenda wengine wasikubali mwongozo wake wakipata amri ya Biblia wasiyoielewa au inayoonekana kuwa inawazuia kufanya jambo fulani. Lakini limekuwa jambo la hekima kutumaini mwongozo wa Yehova. Kwa mfano: Hata kama Mwisraeli hakuelewa sheria kuhusu kutogusa maiti, alinufaika kwa kuitii. Kwanza, utii wake ungemfanya amkaribie Mungu aliye hai; pili, ungemsaidia kuepuka magonjwa.—Mambo ya Walawi 5:2; 11:24.
4, 5. (a) Kabla ya enzi ya Ukristo, Yehova alitoa mwongozo gani kuhusu damu? (b) Tunajuaje kwamba mwongozo wa Mungu kuhusu damu unawahusu Wakristo?
4 Ndivyo ilivyo na mwongozo wa Mungu kuhusu damu. Alimwambia Noa kwamba wanadamu hawapaswi kula damu. Kisha katika Sheria, Mungu akafunua kwamba damu ilipaswa kutumiwa tu kwenye madhabahu—kwa ajili ya msamaha wa dhambi. Kupitia miongozo hiyo Mungu alikuwa akiweka msingi kwa ajili ya matumizi yaliyo bora zaidi ya damu, yaani, kuokoa uhai kupitia fidia ya Yesu. (Waebrania 9:14) Naam, Mungu alitoa mwongozo huo kwa kufikiria uhai na hali yetu njema. Akizungumzia andiko la Mwanzo 9:4, msomi wa Biblia wa karne ya 19, Adam Clarke, aliandika hivi: “Amri hii [kwa Noa] ingali inafuatwa kwa makini na Wakristo wa Kanisa la Othodoksi . . . Chini ya sheria, damu haikuliwa, kwa sababu iliwakilisha ile damu ambayo ingemwagwa kwa ajili ya dhambi za ulimwengu; na chini ya mpango wa Kikristo damu hiyo haipaswi kuliwa, kwa sababu sikuzote inapaswa kuonwa kuwa inawakilisha damu ambayo imemwagwa kwa ajili ya msamaha wa dhambi.”
5 Huenda msomi huyo alikuwa akirejelea habari njema za msingi kumhusu Yesu. Habari hizo zinatia ndani Mungu kumtuma Mwanaye kufa kwa ajili yetu, amwage damu yake ili tuweze kupata uzima wa milele. (Mathayo 20:28; Yohana 3:16; Waroma 5:8, 9) Maelezo ya msomi huyo yalitia ndani pia amri ya baadaye kwamba wafuasi wa Kristo wajiepushe na damu.
6. Wakristo walipewa mwongozo gani kuhusu damu, na kwa nini?
6 Unajua kwamba Mungu aliwapa Waisraeli masharti mengi sana. Yesu alipokufa, haikuwa lazima kwa wanafunzi wake kufuata sheria hizo zote. (Waroma 7:4, 6; Wakolosai 2:13, 14, 17; Waebrania 8:6, 13) Hata hivyo, baada ya muda kulitokea swali kuhusu sharti moja la msingi—kutahiriwa kwa wanaume. Je, ingekuwa lazima kwa watu wasio Wayahudi waliotaka kunufaika na damu ya Kristo watahiriwe ili kuonyesha kwamba bado walikuwa chini ya Sheria? Mnamo mwaka wa 49 W.K., baraza linaloongoza la Kikristo lilishughulikia suala hilo. (Matendo, sura ya 15) Wakisaidiwa na roho ya Mungu, mitume na wanaume wazee walifikia mkataa kwamba lile takwa la kutahiriwa lilikoma pamoja na Sheria. Lakini, kuna baadhi ya matakwa ya Mungu ambayo Wakristo walihitaji kuendelea kuyafuata. Baraza linaloongoza liliandikia makutaniko barua hii: “Roho takatifu na sisi wenyewe tumependelea tusiwaongezee ninyi mzigo zaidi, ila mambo haya ya lazima, kuendelea kujiepusha na vitu vilivyotolewa dhabihu kwa sanamu na damu na vitu vilivyonyongwa na uasherati. Mkijiepusha kwa uangalifu na mambo haya, mtafanikiwa.”—Matendo 15:28, 29.
7. Ni jambo muhimu kadiri gani kwa Wakristo ‘kujiepusha na damu’?
7 Ni wazi kwamba baraza linaloongoza liliona kwamba ‘kujiepusha na damu’ ni muhimu kiadili kama vile kujiepusha na uasherati au ibada ya sanamu. Hiyo inathibitisha kwamba katazo la damu ni jambo zito. Wakristo wanaofanya uasherati au kuabudu sanamu bila kutubu hawawezi ‘kuurithi ufalme wa Mungu’; “fungu lao litakuwa . . . kifo cha pili.” (1 Wakorintho 6:9, 10; Ufunuo 21:8; 22:15) Ona tofauti: Kupuuza mwongozo wa Mungu kuhusu utakatifu wa damu kunaweza kutokeza kifo cha milele. Kuheshimu dhabihu ya Yesu kunaweza kuongoza kwenye uzima wa milele.
8. Ni nini kinachoonyesha kwamba Wakristo wa mapema walichukua kwa uzito mwongozo wa Mungu kuhusu damu?
8 Wakristo wa mapema walielewa na kufuataje mwongozo wa Mungu kuhusu damu? Kumbuka maelezo ya Clarke: “Chini ya mpango wa Kikristo haipaswi kuliwa, kwa sababu sikuzote inapaswa kuonwa kuwa inawakilisha damu ambayo imemwagwa kwa ajili ya msamaha wa dhambi.” Historia inathibitisha kwamba Wakristo wa mapema waliona jambo hilo kuwa zito sana. Tertullian aliandika: “Fikiria jinsi ambavyo wale wenye kiu yenye pupa kwenye maonyesho katika uwanja, hunywa damu mbichi ya wahalifu waovu . . . na kuichukua ili wakaponye ugonjwa wao wa kifafa.” Ingawa wapagani walikula damu, Tertullian alisema kwamba Wakristo “hata hawana damu ya wanyama kwenye chakula [chao] . . . Kwenye kesi za Wakristo, nyinyi huwapa soseji zilizojazwa damu. Bila shaka, tayari mnajua kwamba [hiyo] ni kinyume cha sheria yao.” Naam, licha ya kutishwa kuuawa, Wakristo walikataa kabisa kula damu. Mwongozo wa Mungu ulikuwa muhimu sana kwao.
9. Kujiepusha na damu kulitia ndani nini mbali na kuila moja kwa moja?
9 Huenda wengine wakafikiri kwamba baraza linaloongoza lilimaanisha tu kwamba Wakristo hawakupaswa kula au kunywa damu moja kwa moja, kula nyama iliyo na damu, au kuchanganya damu na chakula. Ni kweli kwamba Mungu alimaanisha hivyo mwanzoni alipompa Noa amri hiyo. Nalo agizo la mitume liliwaeleza Wakristo ‘wajiepushe na vitu vilivyonyongwa,’ yaani, nyama iliyo na damu. (Mwanzo 9:3, 4; Matendo 21:25) Hata hivyo, Wakristo wa mapema walijua kwamba kuna mengi yaliyohusika. Wakati mwingine, damu ililiwa kwa sababu za kitiba. Tertullian alisema kwamba wapagani fulani walikunywa damu mbichi ili kuponya ugonjwa wao wa kifafa. Na huenda kulikuwa na matumizi mengine ya damu ya kutibu magonjwa au kuboresha afya. Hivyo, msimamo wa Wakristo wa kuepuka damu ulitia ndani kutoitumia kwa sababu za “kitiba.” Walidumisha msimamo huo hata kama kufanya hivyo kungehatarisha uhai wao.
Kutumia Damu Kama Dawa
10. Damu inatumiwa katika njia zipi kitiba, na hiyo inatokeza swali gani?
10 Leo ni jambo la kawaida kutumia damu kama dawa. Mwanzoni, watu walitiwa damu mishipani ikiwa na sehemu zake zote. Damu hiyo ilitolewa kwa mtu, ikahifadhiwa, na kutiwa mgonjwa, labda majeruhi wa vita. Baadaye, wachunguzi walijua jinsi ya kutenganisha damu katika sehemu kuu mbalimbali. Kwa kutumia sehemu kuu za damu, madaktari wangeweza kugawanya damu iliyotolewa kuwatibu wagonjwa wengi zaidi, labda mtu aliyejeruhiwa angetiwa plazima (umajimaji wa damu) naye mwingine atiwe chembe nyekundu. Baada ya uchunguzi zaidi ilionekana kwamba sehemu fulani ya damu, kama vile plazima, inaweza kugawanywa kuwa visehemu mbalimbali, na hivyo kutumiwa kuwatibu wagonjwa wengi zaidi. Jitihada za kugawanya damu katika visehemu zaidi bado zinaendelea, na matumizi mapya ya visehemu hivyo yanaendelea kuripotiwa. Mkristo afanyeje kuhusiana na matumizi ya visehemu hivyo? Tuseme Mkristo ameamua kabisa kutotiwa damu mishipani, lakini daktari wake anamhimiza akubali kutiwa mojawapo ya zile sehemu kuu za damu, labda chembe nyekundu zilizotengenishwa. Au huenda matibabu hayo yakahusisha matumizi ya kisehemu kimoja tu kilichotokana na sehemu moja kuu. Mtumishi wa Mungu anawezaje kuamua kuhusu maswali hayo, kwa kukumbuka kwamba damu ni takatifu na kwamba damu ya Kristo inaokoa uhai katika maana iliyo kubwa zaidi?
11. Kwa miaka mingi, Mashahidi wamechukua msimamo gani sahihi wa kitiba kuhusu damu?
11 Mashahidi wa Yehova walijulisha waziwazi msimamo wao miaka mingi iliyopita. Kwa mfano, waliandika makala iliyochapishwa katika The Journal of the American Medical Association (Novemba 27, 1981; ilichapishwa tena katika broshua Damu Yaweza Kuokoaje Uhai Wako? ukurasa wa 27-29).a Makala hiyo ilinukuu kitabu cha Mwanzo, Mambo ya Walawi, na Matendo. Ilisema: ‘Ingawa mistari hii haikusemwa kwa semi za kitiba, Mashahidi huiona kuwa hairuhusu kutiwa mishipani damu nzima, RBCs, na plazima, pamoja na WBC na vigandisha-damu.’ Kitabu Emergency Care, cha mwaka wa 2001, chini ya kichwa, “Composition of the Blood” (Sehemu za Damu), kilisema: “Damu imefanyizwa kwa sehemu mbalimbali: plazima, chembe nyekundu na nyeupe, na vigandisha-damu.” Hivyo, kupatana na habari za kitiba, Mashahidi hukataa kutiwa damu ikiwa na sehemu zake zote au yoyote kati ya sehemu zake kuu nne.
12. (a) Ni msimamo gani ambao umetolewa kuhusu visehemu vya damu vilivyotolewa katika zile sehemu kuu za damu? (b) Unaweza kupata wapi habari za ziada kuhusu matumizi ya damu?
12 Makala hiyo ya kitiba iliendelea kusema: “Uelewevu wa kidini wa Mashahidi haukatazi kabisa kabisa utumizi wa sehemu kama vile albyumini, globyulini za kinga, na matayarisho ya hemofiliaki; kila Shahidi lazima aamue kama aweza kupokea hivi.” Tangu 1981, visehemu vingi (ambavyo hutolewa katika mojawapo ya sehemu kuu nne za damu) vimetenganishwa kwa ajili ya matumizi ya kitiba. Hivyo, gazeti Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 2000, lilitoa habari zenye manufaa kuhusu matumizi ya damu katika makala, “Maswali Kutoka kwa Wasomaji.” Ili kunufaisha wasomaji wengi leo, jibu hilo limechapishwa tena katika ukurasa wa 29-31 wa gazeti hili. Inaeleza mambo kindani na kutoa hoja kwa njia ya akili, lakini utaona kwamba yale ambayo makala hiyo inasema yanakubaliana na mambo ya msingi yaliyochapishwa mnamo 1981.
Daraka la Dhamiri Yako
13, 14. (a) Dhamiri ni nini, nayo inahusikaje katika mambo yanayohusu damu? (b) Mungu aliwapa Waisraeli mwongozo gani kuhusu kula nyama, lakini ni maswali gani ambayo huenda yalitokea?
13 Habari hizo humtaka mtu atumie dhamiri yake. Kwa nini? Wakristo wanakubali kwamba wanahitaji kufuata mwongozo wa Mungu, lakini katika hali fulani lazima wafanye maamuzi ya kibinafsi nayo huhusisha dhamiri. Dhamiri ni uwezo wa asili wa kuchanganua na kuamua mambo, mara nyingi mambo yanayohusiana na maadili. (Waroma 2:14, 15) Hata hivyo, unajua kwamba dhamiri hutofautiana.b Biblia hutaja kwamba watu wengine wana ‘dhamiri zilizo dhaifu,’ ikimaanisha kwamba kuna wengine walio na dhamiri zenye nguvu. (1 Wakorintho 8:12) Wakristo hutofautiana katika kiwango cha kufanya maendeleo kuhusiana na kujifunza mapenzi ya Mungu, kujua maoni yake, na kutumia maoni hayo wanapofanya maamuzi. Tunaweza kuonyesha jambo hilo kwa kufikiria Wayahudi na ulaji wa nyama.
14 Biblia inaonyesha wazi kwamba mtu anayemtii Mungu hapaswi kula nyama isiyotolewa damu. Hiyo ilikuwa muhimu sana hivi kwamba hata wakati wa dharura ambapo askari wa Israeli walikula nyama isiyotolewa damu, walikuwa na hatia ya kosa au dhambi nzito. (Kumbukumbu la Torati 12:15, 16; 1 Samweli 14:31-35) Hata hivyo, huenda kulitokea maswali. Mwisraeli alipomuua kondoo, alipaswa kutoa damu yake haraka kadiri gani? Je, alipaswa kukata koo la mnyama ili aitoe? Je, ilikuwa lazima kumning’iniza kondoo huyo kwa miguu yake ya nyuma? Kwa muda gani? Angeitoaje damu ya ng’ombe mkubwa? Hata baada ya kuitoa, kiasi fulani cha damu kingeweza kubaki katika nyama. Je, angekula nyama hiyo? Ni nani angeamua?
15. Wayahudi fulani walitendaje kuhusiana na kula nyama, lakini Mungu alitoa agizo gani?
15 Wazia Myahudi mwenye bidii aliyekabili masuala hayo. Huenda angefikiri kwamba ni salama zaidi kuepuka nyama zilizouzwa sokoni, huku Myahudi mwingine akikataa kula nyama ambayo huenda kwanza ilikuwa imetolewa kwa sanamu. Huenda Wayahudi wengine walikula nyama tu baada ya kufuata desturi fulani za kutoa damu.c (Mathayo 23:23, 24) Unaonaje kuhusu hatua hizo tofauti? Isitoshe, kwa kuwa Mungu hakuwataka watende hivyo, je, ingefaa Wayahudi walipelekee baraza la marabi maswali mengi ili watoe uamuzi kuhusu kila mojawapo ya maswali hayo? Ingawa Dini ya Kiyahudi ilikuwa na desturi hiyo, tunaweza kufurahi kwamba Yehova hakuwaagiza waabudu wa kweli waamue mambo yanayohusiana na damu kwa njia hiyo. Mungu alitoa mwongozo wa msingi juu ya kuchinja wanyama safi na kutoa damu yao, lakini hakusema zaidi ya hayo.—Yohana 8:32.
16. Kwa nini huenda Wakristo wakawa na maoni yaliyotofautiana kuhusu kukubali kudungwa sindano yenye kisehemu fulani kidogo kilichotokana na sehemu fulani ya damu?
16 Kama ilivyotajwa katika mafungu ya 11 na 12, Mashahidi wa Yehova hawakubali kutiwa damu ikiwa na sehemu zake zote au zile sehemu zake kuu nne, yaani, plazima, chembe nyekundu, chembe nyeupe, na vigandisha-damu. Namna gani visehemu vidogo vinavyotolewa katika mojawapo ya zile sehemu kubwa, kama vile umajimaji wenye kinga za mwili za kupambana na ugonjwa au sumu ya nyoka? (Ona ukurasa wa 30, fungu la 4.) Wengine wamefikia mkataa kwamba visehemu vidogo fulani si damu na hivyo havihusishwi katika amri ya ‘kujiepusha na damu.’ (Matendo 15:29; 21:25; ukurasa wa 31, fungu la 1) Watatoa hesabu kwa maamuzi yao. Dhamiri za wengine huwachochea wakatae chochote kinachotokana na damu (ya wanyama au ya binadamu), hata kama ni kisehemu kidogo tu cha mojawapo ya zile sehemu kuu.d Huenda wengine wakakubali kudungwa sindano za plazima yenye protini ili kupambana na ugonjwa au sumu ya nyoka, lakini huenda wakatae visehemu vingine vidogo. Isitoshe, huenda kazi inayotimizwa na visehemu fulani vinavyotolewa katika mojawapo ya zile sehemu kuu nne ikafanana sana na kazi ya sehemu hiyo kuu ya damu ya kutegemeza uhai mwilini hivi kwamba Wakristo wengi wangeviona kuwa visivyokubalika.
17. (a) Dhamiri yetu inaweza kutusaidiaje tunapokabili masuala yanayohusu visehemu vya damu? (b) Kwa nini ni jambo zito sana kufanya maamuzi kuhusu suala hilo?
17 Yale ambayo Biblia husema kuhusu dhamiri hutusaidia tunapofanya maamuzi kama hayo. Hatua ya kwanza ni kujifunza yale yanayosemwa na Neno la Mungu na kujitahidi kuzoeza dhamiri yako kuyafuata. Hilo litakusaidia kuamua mambo kupatana na mwongozo wa Mungu, badala ya kumwomba mtu mwingine akuamulie. (Zaburi 25:4, 5) Kuhusu kukubali visehemu fulani vya damu, wengine wamewaza, ‘Hili ni jambo linalotegemea dhamiri, hivyo si la maana.’ Huko si kufikiri kuzuri. Kwa kuwa tu jambo fulani linategemea dhamiri, hiyo haimaanishi kwamba halina maana. Linaweza kuwa jambo zito sana. Sababu moja ni kwamba linaweza kuathiri watu ambao dhamiri zao si sawa na zetu. Tunaona jambo hilo kutokana na shauri la Paulo kuhusu nyama ambazo huenda zilikuwa kwanza zimetolewa kwa sanamu na baadaye kuuzwa sokoni. Mkristo anapaswa kuhangaika kuhusu ‘kuumiza dhamiri zilizo dhaifu.’ Akiwakwaza wengine, anaweza ‘kumharibu ndugu yake ambaye Kristo alikufa kwa ajili yake’ na hivyo kutenda dhambi dhidi ya Kristo. Kwa hiyo, ingawa mtu binafsi ndiye anayepaswa kuamua kuhusu matumizi ya visehemu vidogo vya damu, maamuzi hayo yanapaswa kuchukuliwa kwa uzito sana.—1 Wakorintho 8:8, 11-13; 10:25-31.
18. Mkristo anawezaje kuepuka kuruhusu dhamiri yake ife ganzi anapofanya maamuzi kuhusu damu?
18 Jambo lingine la kufikiria linakazia uzito wa maamuzi unayofanya kuhusu damu. Jambo hilo linahusu jinsi unavyoweza kuathiriwa na maamuzi yako. Ikiwa kukubali kisehemu kidogo cha damu kungesumbua dhamiri yako iliyozoezwa na Biblia, basi hupaswi kuipuuza. Wala hupaswi kupuuza mwelekezo wa dhamiri yako kwa kuwa tu mtu fulani anakuambia, “Ni sawa tu kukubali kisehemu hiki; wengi wamekikubali.” Kumbuka, leo watu wengi sana hupuuza dhamiri yao, nayo hufa ganzi, na kuwaruhusu wadanganye au kufanya makosa mengine bila kuhisi majuto. Bila shaka, Wakristo wanataka kuepuka mtazamo huo.—2 Samweli 24:10; 1 Timotheo 4:1, 2.
19. Tunapoamua masuala ya kitiba yanayohusu damu, tunapaswa kukumbuka hasa jambo gani?
19 Sehemu ya mwisho ya makala iliyochapwa tena ya jibu hilo kwenye ukurasa wa 29-31 inasema: “Je, jambo la kwamba maoni na maamuzi yanayotegemea dhamiri yaweza kutofautiana laonyesha kwamba hilo ni jambo dogo tu? La. Jambo hilo ni zito.” Ni zito sana kwa sababu uhusiano wako na “Mungu aliye hai” unahusika. Uhusiano huo ndio tu unaoweza kukuongoza kwenye uzima wa milele, unaotegemea nguvu za kuokoa za damu ya Yesu iliyomwagwa. Sitawisha heshima kubwa kuelekea damu kwa sababu ya yale Mungu anayotimiza kupitia damu, yaani, kuokoa uhai. Kwa kufaa, Paulo aliandika hivi: “Hamkuwa na tumaini na mlikuwa bila Mungu katika ulimwengu. Lakini sasa katika muungano na Kristo Yesu ninyi ambao wakati mmoja mlikuwa mbali sana mmekuja kuwa karibu kupitia damu ya Kristo.”—Waefeso 2:12, 13.
-