Upendo—Siri ya Kupata Mafanikio Shambani
1 “Njooni kwangu, . . . nami nitawaburudisha ninyi.” (Mt. 11:28) Maneno hayo yenye kuvutia yalionyesha jinsi Yesu alivyowapenda sana watu. Tukiwa wahudumu Wakristo, tunataka kumwiga Yesu kwa kuwaonyesha upendo watu ambao wamechoshwa na ulimwengu huu usio na upendo. Tunaweza kufanyaje hivyo tunapohubiri habari njema?
2 kwa Maneno: Kuwapenda watu kulimchochea Yesu kutumia kila fursa kuwahubiria habari njema. (Yoh. 4:7-14) Upendo utatusaidia tusisite kuwahubiria watu isivyo rasmi. Msichana mmoja mwenye umri wa miaka sita alimhubiria mwanamke mmoja aliyekuwa ameketi kando yake kwenye chumba cha kungojea kumwona daktari. Ni nini kilichomchochea kufanya hivyo? Alieleza hivi: “Mwanamke huyo alionekana kama anahitaji kumjua Yehova.”
3 Tunaweza kuonyesha kwamba tunapendezwa na watu kwa kutabasamu kwa uchangamfu na kuzungumza kwa urafiki. Pia kusikiliza kwa makini maoni yao, kutambua mahangaiko yao, na kuwajali kikweli, kutaonyesha tunawapenda. (Met. 15:23) Kama Yesu, tutakazia ujumbe wa Ufalme wenye kutia moyo na kuwaonyesha kwamba Yehova ana huruma yenye upendo kuwaelekea watu.—Mt. 24:14; Luka 4:18.
4 kwa Matendo: Yesu alishughulikia kwa haraka mahitaji ya wengine. (Mt. 15:32) Huenda sisi pia tukapata fursa ya kuwatendea wengine kwa fadhili zenye upendo tukiwa utumishini. Dada mmoja aliona kwamba mwanamke fulani hakuwa anamwelewa mtu fulani aliyekuwa akizungumza naye kwenye simu. Dada yetu alijitolea kumtafsiria simu hiyo muhimu. Tendo hilo la upendo lilitokeza fursa ya mazungumzo zaidi ya Biblia ambayo yalimfanya mwanamke huyo kukubali funzo la Biblia. Katika kisa kingine, ndugu aliyekuwa akifanya ziara ya kurudia alimkuta mwenye nyumba akiwa ameudhika kwa sababu sofa aliyokuwa akijaribu kuingiza ndani ya nyumba ilikuwa imekwama mlangoni. Baada ya kumsaidia mwenye nyumba kuiingiza, ndugu huyo aliketi kwenye sofa hiyo na kuanzisha funzo la Biblia na mwenye nyumba huyo mwenye shukrani.
5 Tunapohubiri, tunaonyesha kwamba tunampenda Mungu na jirani zetu. (Mt. 22:36-40) Upendo huo tunaoonyesha kwa maneno na matendo unawasaidia wenye mioyo minyofu kutambua kwamba tuna kweli.