SOMO LA 24
Kutumia Maneno Yanayofaa
MANENO ni njia muhimu ya mawasiliano. Lakini ili maneno yetu yatimize kusudi fulani hususa, tunahitaji kuyachagua kwa makini. Neno ambalo linafaa wakati fulani huenda lisifae katika hali nyingine. Neno lenye kuchekesha likitumiwa vibaya linaweza kuwa ‘neno liumizalo.’ Mtu anaweza kutumia maneno kama hayo ikiwa anazungumza bila kufikiri, jambo linaloonyesha kwamba hajali. Kuna maneno ambayo yana maana mbili, mojawapo ikiwa maana mbaya au yenye kushusha heshima. (Mit. 12:18; 15:1) Kwa upande mwingine, “neno jema,” yaani neno la kutia moyo, humfurahisha yule anayelipokea. (Mit. 12:25) Si rahisi hata kwa mtu mwenye hekima kupata maneno yanayofaa. Biblia inatuambia kwamba Solomoni aliona anahitaji kutafuta “maneno yapendezayo” na “maneno ya kweli.”—Mhu. 12:10.
Baadhi ya lugha zina desturi ya kutumia maneno fulani unapozungumza na mtu mwenye umri mkubwa au unapozungumza na mtu fulani mwenye mamlaka, na kutumia maneno tofauti unapoongea na marika wako au wale unaowazidi umri. Kupuuza desturi hizo huonwa kuwa kukosa adabu. Pia haifai kujibandikia heshima ambayo haikustahili kulingana na desturi. Biblia ina kanuni bora ya heshima kuliko hata kiwango cha heshima ambacho huenda kinaonyeshwa na sheria yenu au desturi zenu. Inawahimiza Wakristo ‘waheshimu watu wa namna zote.’ (1 Pet. 2:17) Wale ambao wanaheshimu wengine kutoka moyoni huzungumza na watu wa umri wote kwa njia ya heshima.
Watu wengi ambao si Wakristo wa kweli husema maneno machafu yasiyo na adabu. Labda wanadhani kwamba wanakazia mambo wanapotumia maneno kama hayo. Au labda wanatumia maneno hayo kwa sababu wamepungukiwa sana na misamiati. Ikiwa mtu alizoea kutumia maneno kama hayo kabla ya kujifunza njia za Yehova, inaweza kuwa vigumu kuacha mazoea hayo. Lakini anaweza kufaulu. Roho ya Mungu inaweza kumsaidia mtu abadili usemi wake. Lakini mtu mwenyewe pia anapaswa kuwa tayari kujifunza maneno yanayofaa, yaani maneno yanayopendeza na kujenga, na kuyatumia kwa ukawaida.—Rom. 12:2; Efe. 4:29; Kol. 3:8.
Lugha Inayoeleweka kwa Urahisi. Jambo kuu ni hili, usemi mzuri ni ule unaoeleweka kwa urahisi. (1 Kor. 14:9) Ikiwa wasikilizaji hawakuelewi kwa urahisi, ni kama unasema lugha ya kigeni.
Kuna maneno ambayo huwa na maana ya kipekee miongoni mwa watu wa taaluma fulani-fulani. Labda wanatumia maneno hayo kila wakati. Lakini ukitumia maneno kama hayo katika hali tofauti, huenda watu wasikuelewe. Na hata unapotumia maneno ya kawaida, ukianza kufafanua mambo mengi yasiyo ya lazima, akili za wasikilizaji zitaanza kutangatanga.
Msemaji mwenye kujali hutumia maneno ambayo hata wale wasio na elimu wanaelewa. Anamwiga Yehova kwa kuwajali “watu wa hali ya chini.” (Yobu 34:19, NW) Ikiwa ni lazima msemaji atumie neno ambalo wengi hawalifahamu, anapaswa kulitumia pamoja na maneno rahisi ili maana yake iwe wazi.
Maneno rahisi ambayo yamefikiriwa vizuri huwasilisha mawazo vizuri sana. Ni rahisi kuelewa sentensi fupi-fupi na maneno rahisi. Unaweza kuchanganya sentensi kama hizo na sentensi ndefu-ndefu ili hotuba yako isisikike ni kama inakatika-katika. Lakini unapozungumzia mambo ambayo hasa unataka wasikilizaji wakumbuke, tumia maneno rahisi na sentensi fupi.
Kutumia Semi Tofauti-Tofauti na Sahihi. Kuna maneno mazuri tele ya kutumia. Tumia semi tofauti-tofauti badala ya kutumia semi zilezile katika kila hali. Ukifanya hivyo, maneno yako yatapendeza na kujaa maana. Unawezaje kuongeza misamiati?
Unaposoma, tia alama maneno ambayo huelewi vizuri kisha uyachunguze katika kamusi. Chagua maneno machache kati ya yale ambayo huelewi vizuri na ujitahidi kuyatumia unapopata nafasi. Yatamke vizuri na uyatumie kwa njia ambayo yanaeleweka kwa urahisi na wala si kwa kujielekezea tu fikira. Kuongeza misamiati kutakuwezesha kutumia semi tofauti-tofauti. Lakini jihadhari kwa sababu mtu anapotamka maneno vibaya au anapoyatumia vibaya, wengine watadhani kwamba hajui analosema.
Kusudi la kuongeza misamiati ni kuweza kuwasiliana, wala si kujitukuza. Maneno yanayotatanisha na maneno marefu huelekeza fikira kwa msemaji. Tunapaswa kuwa na hamu ya kuwaeleza wengine habari muhimu na kufanya ipendeze wasikilizaji. Kumbuka ile mithali ya Biblia isemayo hivi: “Ulimi wa mwenye hekima hutamka maarifa vizuri.” (Mit. 15:2) Kutumia maneno mazuri, yanayofaa na kueleweka kwa urahisi, hufanya maneno yetu yafurahishe na kuchochea badala ya kuwa yenye kuchosha na yasiyopendeza.
Unapoongeza misamiati, fikiria sana kutumia maneno yanayofaa. Maneno mawili yanaweza kuwa na maana moja lakini yatofautiane kidogo yakitumiwa katika hali tofauti. Ukitambua jambo hilo, unaweza kufanya usemi wako uwe wazi zaidi na kuepuka kuudhi wasikilizaji. Wasikilize kwa makini watu wanaoongea vizuri. Kuna kamusi ambazo huorodhesha kila neno na visawe vyake (maneno tofauti yanayokaribiana sana katika maana) na pia vitabu ambavyo vinaonyesha maneno ya kinyume. Kwa njia hiyo, mbali na kupata maneno tofauti-tofauti yanayofafanua wazo lilelile, pia unapata maana tofauti ndogo-ndogo ya wazo hilo. Jambo hilo linasaidia sana unapotafuta neno linalofaa hali fulani. Lakini, kabla ya kuanza kutumia neno jipya, hakikisha unafahamu maana yake, matamshi yake, na jinsi linavyotumiwa.
Maneno yenye maana hususa hueleweka wazi kuliko maneno yanayotaja mambo kwa ujumla. Msemaji anaweza kusema: “Wakati huo, watu wengi wakawa wagonjwa.” Au anaweza kusema: “Miezi michache tu baada ya Vita ya Kwanza ya Ulimwengu, watu wapatao 21,000,000 walikufa kwa ugonjwa wa homa ya Hispania.” Ona tofauti kubwa inayotokea msemaji akionyesha wazi jambo ambalo anamaanisha kwa kutumia maneno kama “wakati huo,” “watu wengi” na “wakawa wagonjwa”! Ili uwe hususa unahitaji kujua mambo yanayohusiana na habari unayozungumzia na vilevile unahitaji kuchagua kwa makini maneno yanayofaa.
Pia maneno yanayofaa yanaweza kukusaidia kutaja jambo kuu bila kutumia maneno mengi. Ukitumia maneno mengi, jambo kuu haliwi wazi. Maneno rahisi huwasaidia wasikilizaji kushika mambo muhimu na kuyakumbuka. Husaidia watu kuelewa ujuzi sahihi. Mafundisho ya Yesu Kristo yalikuwa ya pekee sana kwa sababu alitumia lugha rahisi. Mwige Yesu. (Ona mifano iliyoko katika Mathayo 5:3-12 na Marko 10:17-21.) Fanya mazoezi ya kuzungumza kwa maneno machache ambayo umechagua kwa makini.
Maneno Yanayoonyesha Mkazo, Hisia, na Yanayovutia. Unapoongeza misamiati, mbali na kufikiria maneno mapya fikiria pia maneno yenye miundo fulani hususa. Kwa mfano, fikiria vitenzi vinavyotia mkazo; vivumishi vinavyopendeza; na maneno yanayoonyesha uchangamfu, fadhili, au bidii.
Biblia imejaa mifano ya lugha iliyojaa maana. Kupitia nabii Amosi, Yehova alihimiza hivi: “Tafuteni mema, na wala si mabaya . . . Yachukieni mabaya; yapendeni mema.” (Amo. 5:14, 15, italiki ni zetu.) Nabii Samweli alimtangazia Mfalme Sauli hivi: “Leo, BWANA amekurarulia ufalme wa Israeli.” (1 Sam. 15:28, italiki ni zetu.) Yehova alitumia maneno yasiyoweza kusahaulika kwa urahisi alipokuwa akizungumza na Ezekieli: “Nyumba yote ya Israeli wana vipaji vigumu, na mioyo yenye ukaidi.” (Eze. 3:7, italiki ni zetu.) Yehova alikazia uzito wa makosa ya Israeli kwa kuuliza hivi: “Je! mwanadamu atamwibia Mungu? Lakini ninyi mnaniibia mimi.” (Mal. 3:8, italiki ni zetu.) Danieli alipokuwa akieleza juu ya jaribu la imani kule Babiloni, alikoleza usemi wake aliposema kwamba ‘Nebukadreza alijaa ghadhabu’ kwa sababu Shadraka, Meshaki, na Abednego walikataa kuabudu sanamu yake, akaamuru wafungwe na kutupwa ndani ya “tanuru iliyokuwa ikiwaka moto.” Danieli anatusaidia kufahamu ukali wa moto ule anaposema kwamba mfalme aliamuru watu wake “watie moto ile tanuru mara saba kuliko desturi yake ya kutiwa moto,” ikawa moto hivi kwamba watu wa mfalme wakafa walipoikaribia tanuru hiyo. (Dan. 3:19-22, italiki ni zetu.) Yesu alipozungumza na watu wa Yerusalemu siku chache kabla ya kifo chake, alisema hivi kwa hisia nyingi: “Ni mara nyingi kadiri gani nilitaka kuwakusanya watoto wako pamoja, kama vile kuku hukusanya vifaranga vyake pamoja chini ya mabawa yake! Lakini nyinyi watu hamkutaka hilo. Tazameni! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.”—Mt. 23:37, 38.
Maneno ambayo yamechaguliwa vizuri yanaweza kutokeza picha dhahiri akilini mwa wasikilizaji. Ukitumia maneno yanayogusa hisia, ni kana kwamba wasikilizaji wanaona na kugusa mambo unayosema, wanaonja na kunusa vyakula unavyotaja, na kusikia sauti unazofafanua na watu unaonukuu. Wasikilizaji watakusikiliza kwa makini kwa sababu unafanya mambo yawe halisi.
Maneno yanayotokeza mambo kwa njia dhahiri yanaweza kufanya watu wacheke au walie. Yanaweza kumpa mtu tumaini, na kumfanya aliyeshuka moyo awe na hamu ya kuishi na kumchochea ampende Muumba. Watu ulimwenguni kote wamevutiwa sana na tumaini linalotokezwa na maandiko ya Biblia kama Zaburi 37:10, 11, 34; Yohana 3:16; na Ufunuo 21:4, 5.
Unaposoma Biblia pamoja na vichapo vya “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” utaona unamna-namna wa maneno. (Mt. 24:45) Usiyasome tu na kuyasahau. Chagua yale yanayokufurahisha, uyaongeze kwenye msamiati wako.
Usemi Unaopatana na Kanuni za Sarufi. Watu wengine wanatambua kwamba nyakati nyingine usemi wao haufuati kanuni za sarufi. Wanaweza kufanya nini?
Kama ungali mwanafunzi shuleni, tumia nafasi hiyo kujifunza sarufi na kuchagua maneno yanayofaa. Kama huna hakika na kanuni fulani ya sarufi, mwulize mwalimu. Usijifunze sarufi ili ujue tu kutumia lugha. Una kichocheo ambacho huenda wanafunzi wengine hawana. Unataka kuwa mhudumu bora wa habari njema.
Vipi ikiwa wewe ni mtu mzima na unazungumza lugha ya kigeni ambayo umejifunza baadaye maishani? Au labda hukuweza kujifunza vizuri lugha yako shuleni. Usivunjike moyo. Badala yake, tia bidii ili ufanye maendeleo kwa ajili ya habari njema. Sisi hujifunza mambo mengi kuhusu sarufi tunapowasikiliza wengine wakiongea. Basi sikiliza kwa makini wasemaji wenye uzoefu wanapotoa hotuba. Unaposoma Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia, tazama muundo wa sentensi, maneno yanayotumiwa katika fungu moja, na mazingira ambamo maneno hayo yametumiwa. Fuata mifano hiyo katika usemi wako.
Watumbuizaji na waimbaji mashuhuri wanaweza kutumia maneno na usemi unaovunja kanuni za sarufi. Na watu huwaiga. Mara nyingi walanguzi wa dawa za kulevya na wengine wenye maisha ya uhalifu au yasiyo ya maadili hutumia lugha yao wenyewe, wakibadili kabisa maana ya maneno fulani katika usemi wao. Haifai Mkristo kuwaiga watu hao. Kuwaiga kunafanya tuwe kama wao na kuishi maisha kama yao.—Yn. 17:16.
Uwe na zoea la kutumia usemi mzuri kila siku. Ukiacha usemi wako wa kawaida uwe wa kizembe, usitarajie kuzungumza vizuri katika pindi za pekee. Lakini kama kwa kawaida unatumia usemi mzuri, utazungumza kwa urahisi na kwa njia ya kawaida unapotoa hotuba jukwaani au unapohubiri kuhusu kweli.