Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • be funzo 33 uku. 197-uku. 200 fu. 4
  • Uwe Mwenye Busara Lakini Thabiti

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Uwe Mwenye Busara Lakini Thabiti
  • Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
  • Habari Zinazolingana
  • Kutangaza Habari Njema—Kwa Ujasiri, Lakini kwa Busara
    Huduma Yetu ya Ufalme—1988
  • Kujifunza Ustadi wa Kuwa na Busara
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Kutoa Habari Njema—Kwa Utambuzi
    Huduma Yetu ya Ufalme—1991
  • Jinsi ya Kuboresha Stadi za Mazungumzo
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
Pata Habari Zaidi
Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
be funzo 33 uku. 197-uku. 200 fu. 4

SOMO LA 33

Uwe Mwenye Busara Lakini Thabiti

Unahitaji kufanya nini?

Unahitaji kutumia busara unapoongea, jinsi unavyoongea, na wakati wa kuongea ili usiwaudhi wengine.

Kwa Nini Ni Muhimu?

Ukiwa mwenye busara, watu wanaweza kusikiliza habari njema bila shida yoyote. Busara itakusaidia pia kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Wakristo wenzako.

BUSARA ni uwezo wa kushughulika na watu bila kuwaudhi. Inahusu kujua jinsi ya kuzungumza na wakati wa kuzungumza. Haimaanishi kuridhiana mambo ya kweli wala kukubali mambo yasiyo ya kweli. Kuwa na busara si kuhofu wanadamu.—Mit. 29:25.

Tunda la roho ni msingi bora wa kukuza busara. Kwa hiyo, mtu anayechochewa na upendo hapendi kuwaudhi wengine; yeye hupenda kuwasaidia. Mtu mpole na mwenye fadhili hufanya mambo kiungwana. Mtu mwenye kufanya amani hutafuta njia za kuendeleza uhusiano mzuri pamoja na wengine. Mtu mwenye ustahimilivu hudumisha utulivu hata kama wengine ni wakali.—Gal. 5:22, 23.

Hata ujumbe wa Biblia utangazwe kwa njia gani, bado kuna watu ambao wataudhika. Yesu Kristo alikuwa “jiwe la kukwaza na tungamo-mwamba la udhia” kwa Wayahudi wengi wa karne ya kwanza kwa sababu walikuwa na mioyo miovu. (1 Pet. 2:7, 8) Yesu alisema hivi kuhusu kazi yake ya kutangaza Ufalme: “Nilikuja kuanza moto juu ya dunia.” (Luka 12:49) Na ujumbe wa Ufalme wa Yehova, unaotia ndani uhitaji wa wanadamu kutambua enzi kuu ya Muumba wao, ungali jambo muhimu sana kwa wanadamu. Watu wengi huudhiwa na ujumbe wa kwamba hivi karibuni Ufalme wa Mungu utaondoa mfumo huu mwovu wa mambo. Lakini kwa kumtii Mungu, tunaendelea kuhubiri. Na tunakumbuka shauri hili la Biblia tunapohubiri: “Ikiwezekana, kwa kadiri itegemeavyo nyinyi, iweni wenye kufanya amani na watu wote.”—Rom. 12:18.

Kutumia Busara Unapohubiri. Sisi huzungumza na wengine kuhusu imani yetu katika hali nyingi. Tunafanya hivyo hasa tunapokuwa katika huduma ya shambani, ingawa sisi hutafuta pia nafasi za kuwahubiria watu wa ukoo, wafanyakazi wenzetu, na wanafunzi wenzetu. Tunahitaji kutumia busara katika hali hizi zote.

Ikiwa tunahubiri ujumbe wa Ufalme kwa njia inayofanya wengine wafikiri tunawakemea, wanaweza kuudhika. Ikiwa hawajatuomba msaada na labda hawaoni uhitaji wa kusaidiwa, wanaweza kuudhika wakiona kwamba tunajaribu kuwarekebisha. Tunawezaje kuepuka kueleweka vibaya? Kujifunza kuzungumza kwa njia ya kirafiki kunaweza kusaidia.

Jaribu kuanzisha mazungumzo kwa kutokeza jambo linalompendeza mtu huyo. Ikiwa yeye ni mtu wa ukoo, mfanyakazi mwenzako, au mwanafunzi mwenzako, labda unajua mambo yanayompendeza. Hata kama hujawahi kukutana na mtu huyo, unaweza kutaja jambo ulilosikia kwenye habari au ulilosoma magazetini. Habari kama hizo mara nyingi huonyesha mambo ambayo watu hufikiria. Uwe makini unapohubiri nyumba kwa nyumba. Mapambo ya nyumba, vitu vya kuchezea vilivyoko nje ya nyumba, ishara za kidini, na vibandiko kwenye gari ambalo limeegeshwa hapo vinaweza kukudokezea mambo yanayompendeza mwenye nyumba. Mwenye nyumba akija mlangoni, msikilize anapozungumza. Maneno yake yanaweza ama kuthibitisha maoni yako ama yatakusahihisha na kukudokezea mambo unayohitaji kuzungumzia.

Mazungumzo yanapoendelea, mweleze maoni ya Biblia na vichapo vya Biblia kuhusu habari mnayozungumzia. Usitawale mazungumzo. (Mhu. 3:7) Husisha mwenye nyumba katika mazungumzo ikiwa anapenda kushiriki. Sikiliza maoni yake. Yanaweza kukusaidia kumfikia kwa busara.

Kabla ya kuzungumza, fikiria jinsi atakavyoyaona maneno yako. Andiko la Mithali 12:8, NW, linaupongeza “mdomo wenye busara.” Usemi wa Kiebrania ambao umetumiwa hapa unahusiana na mambo kama ufahamu na utambuzi. Kwa hiyo, kuwa na busara kunahusisha kuzungumza kwa tahadhari baada ya kutafakari ili utende kwa hekima. Mstari wa 18 wa Mithali sura ya 12 unatuonya ‘tusinene bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga.’ Inawezekana kushikilia kweli ya Biblia bila kuudhi wengine.

Kuchagua maneno kwa utambuzi kunaweza kukuepusha na vizuia-mazungumzo. Ikiwa neno “Biblia” linafanya wengine wasisikilize, unaweza kutumia semi kama “maandiko matakatifu” au “kitabu ambacho sasa kinachapishwa katika zaidi ya lugha 2,000.” Ikiwa unarejelea Biblia, unaweza kumuuliza mtu huyo maoni yake kuihusu na kukumbuka maoni hayo muda wote mnapozungumza.

Mara nyingi kutumia busara hutia ndani kujua wakati mzuri wa kutaja mambo fulani. (Mit. 25:11) Labda hukubaliani na mambo yote ambayo mtu huyo anasema, lakini hakuna haja ya kupinga kila jambo analotaja ambalo halipatani na maandiko. Usijaribu kummwagia mwenye nyumba mambo yote kwa wakati mmoja. Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Nina mambo mengi ya kuwaambia nyinyi, lakini hamwezi kuyahimili wakati wa sasa.”—Yn. 16:12.

Inapowezekana, wapongeze kwa moyo mnyofu wale unaozungumza nao. Hata kama mwenye nyumba ni mbishi, bado unaweza kumpongeza kwa maoni yake. Mtume Paulo alifanya hivyo alipozungumza na wanafalsafa kule Areopago, Athene. Wanafalsafa walikuwa ‘wakiongea naye kwa mabishano.’ Angesemaje jambo ambalo alitaka kusema bila kuwaudhi? Awali, aliona madhabahu nyingi za miungu yao. Badala ya Paulo kuwashutumu Waathene kwa sababu wanaabudu sanamu, aliwapongeza kwa busara kwa sababu walikuwa watu wa kidini sana. Alisema: “Naona kwamba katika mambo yote mwaonekana kuwa wenye mwelekeo zaidi wa kuhofu miungu kuliko wengine walivyo.” Njia hiyo ilimsaidia kutangaza ujumbe wake kuhusu Mungu wa kweli. Matokeo yakawa kwamba wengine wakawa waamini.—Mdo. 17:18, 22, 34.

Usikasirike ukipingwa. Uwe mtulivu. Tumia pindi hizo kuelewa jinsi mtu huyo anavyofikiri. Unaweza kumshukuru kwa maoni yake. Lakini, vipi akisema kwa ghafula: “Nina dini yangu”? Unaweza kumuuliza hivi kwa busara: “Je, umekuwa mtu wa kidini maisha yako yote?” Kisha, baada ya jibu lake, sema: “Je, unafikiri wanadamu watawahi kuungana katika dini moja?” Hiyo inaweza kutokeza mazungumzo zaidi.

Jinsi tunavyojiona sisi wenyewe inaweza kutusaidia kutumia busara. Tunasadiki kabisa kwamba njia za Yehova ni zenye haki na Neno lake ni kweli. Sisi huzungumza kwa usadikisho kuhusu mambo hayo. Lakini hatupaswi kujiona kuwa waadilifu. (Mhu. 7:15, 16) Tunashukuru kwamba tunajua kweli na kwamba tumebarikiwa na Yehova, lakini tunajua vizuri kwamba anatukubali kwa sababu ya fadhili zake zisizostahiliwa na imani yetu katika Kristo, wala si kwa sababu sisi ni waadilifu. (Efe. 2:8, 9) Tunatambua kwamba tunahitaji ‘kufuliza kujijaribu kama tumo katika imani, tukifuliza kujithibitisha wenyewe sisi ni nini.’ (2 Kor. 13:5) Basi, tunapowaambia watu kwamba wanahitaji kufuata matakwa ya Mungu, kwa unyenyekevu sisi pia tunafuata kanuni za Biblia maishani. Hatuna haki ya kumhukumu mwingine. Yehova “amekabidhi kuhukumu kote kwa Mwana,” na ni mbele ya kiti chake cha hukumu tunapaswa kutoa hesabu ya matendo yetu.—Yn. 5:22; 2 Kor. 5:10.

Kutumia Busara Katika Familia na Ukiwa na Wakristo Wenzako. Mbali na huduma ya shambani, tunahitaji kutumia busara katika sehemu nyinginezo pia. Busara inaonyesha mtu ana matunda ya roho ya Mungu, basi tunahitaji kutumia busara nyumbani tunaposhughulika na jamaa zetu. Upendo hutuchochea kujali hisia za wengine. Mume wa Malkia Esta hakuwa mwabudu wa Yehova, lakini Esta alimheshimu na alitumia busara sana alipozungumza naye mambo yanayohusu watumishi wa Yehova. (Esta, sura ya 3-8) Nyakati nyingine, tunaposhughulika kwa busara na jamaa zetu ambao si Mashahidi, tunaweza kuwaonyesha kweli kwa mwenendo wetu badala ya mafundisho yetu.—1 Pet. 3:1, 2.

Vivyo hivyo, hata kama tunawajua vizuri washiriki wa kutaniko hatupaswi kuwazungumzia bila kujali au kwa njia isiyo ya fadhili. Hatupaswi kufikiri kwamba eti kwa sababu wao ni wakomavu, watavumilia bila kulalamika. Wala hatupaswi kutoa udhuru tukisema: “Lakini, nimezaliwa hivyo.” Ikiwa njia yetu ya kuzungumza inawaudhi wengine, tujitahidi kubadilika. ‘Upendo wetu wenye juhudi nyingi sisi kwa sisi’ na utuchochee ‘kufanya lililo jema kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.’—1 Pet. 4:8, 15; Gal. 6:10.

Kutumia Busara Unapohutubia Watu. Wale wanaohutubu jukwaani pia wanahitaji kutumia busara. Wasikilizaji wana malezi tofauti-tofauti na hali mbalimbali. Ukuzi wao wa kiroho unatofautiana. Labda wengine wamekuja kwenye Jumba la Ufalme kwa mara ya kwanza. Na labda wengine wana magumu fulani ambayo msemaji hajui. Ni nini kinachoweza kumsaidia msemaji asiwaudhi wasikilizaji?

Jaribu kufuata shauri ambalo mtume Paulo alimpa Tito kwamba ‘asiseme kwa ubaya juu ya yeyote, akubali sababu, aonyeshe wazi upole wote kuelekea watu wote.’ (Tit. 3:2) Epuka kuiga misemo ya ulimwengu inayowashushia heshima watu wa jamii nyingine, lugha nyingine, au taifa jingine. (Ufu. 7:9, 10) Taja wazi matakwa ya Yehova, na uonyeshe hekima ya kufuata matakwa hayo; lakini usiseme vibaya juu ya wale ambao bado hawafuati vizuri njia ya Yehova. Badala yake, watie moyo wote watambue mapenzi ya Mungu na kufanya yampendezayo. Unapotoa mashauri, zungumza kwa upendo na uwapongeze kwa unyofu. Sauti yako na jinsi unavyozungumza na zionyeshe upendo wa kidugu ambao sisi sote tunapaswa kudhihirisha.—1 The. 4:1-12; 1 Pet. 3:8.

JINSI YA KUFAULU

  • Zungumza na watu badala ya kuwakemea.

  • Fikiria kwa makini jinsi mtu unayezungumza naye atakavyokuelewa.

  • Kabla ya kuzungumza, fikiria kama huo ndio wakati mzuri wa kuzungumzia jambo hilo.

  • Inapowezekana, toa pongezi kutoka moyoni.

  • Usikasirike mtu akikupinga.

  • Epuka kujiona kuwa mwadilifu; usiwahukumu wengine.

MAZOEZI: Soma kwa makini masimulizi yafuatayo ya Biblia: 2 Samweli 12:1-9; Matendo 4:18-20. Katika kila simulizi, angalia (1) jinsi busara ilivyoonyeshwa na (2) semi zinazoonyesha kwa uthabiti njia za Yehova zenye uadilifu.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki