Wasaidie Wanafunzi wa Biblia Wawe Wahubiri wa Habari Njema ya Ufalme
1 Kazi ambayo Yesu aliwapa wanafunzi wake inayotajwa kwenye Mathayo 28:19, 20 ilikuwa kubwa sana. Wanafunzi wa Kristo waliagizwa wafanye wanafunzi, na wanafunzi hao wangeendeleza kazi hiyo ya kufanya wanafunzi. Msingi ungewekwa kwa ajili ya kutangazwa kwa habari njema ya Ufalme wa Mungu ulimwenguni pote wakati wa kipindi hiki muhimu cha mwisho tunamoishi.—Mt. 24:14.
2 Wanafunzi wetu wa Biblia wanaweza kutia ndani watoto wetu au watu wengine ambao wako tayari kujifunza Biblia pamoja nasi. Kwa kweli tunataka kuwasaidia watambue na kutimiza daraka lao la kuwasaidia wengine kuwa wanafunzi wa Yesu Kristo.—Luka 6:40.
3 Watayarishe Watoe Ushahidi: Watie moyo wale unaojifunza nao wawaambie wengine mambo wanayojifunza. Wasimulie mambo uliyoona shambani. Tangu utotoni, wazoeze watoto wako kushiriki katika huduma kadiri wawezavyo. (Zab. 148:12, 13) Onyesha kwa maneno na matendo kwamba unaiona huduma kuwa jambo muhimu maishani mwako.—1 Tim. 1:12.
4 Yehova huwatumia wale tu wanaotii na kuishi kupatana na viwango vyake vya uadilifu. Bila shaka, wahubiri wapya hawana ujuzi mwingi kama wahudumu wa Ufalme wenye uzoefu waliojiweka wakfu na kubatizwa. Lakini wapya wanapaswa kuamini mafundisho ya msingi ya Biblia na waweze kuwaeleza wengine mafundisho hayo. (Ona Tengenezo, uku. 79-82.) Wanapaswa pia kuwa wamejitenga kabisa na “Babiloni Mkubwa,” hawajihusishi katika siasa zozote, na wanahudhuria mikutano ya kutaniko kwa kawaida.—Ufu. 18:2, 4; Yoh. 17:16; Ebr. 10:24, 25.
5 Mara tu unapoona kwamba mwanafunzi wako wa Biblia anastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa, unapaswa kumweleza mwangalizi-msimamizi. Yeye atapanga wazee wawili waketi pamoja nawe na mwanafunzi wako wa Biblia ili kuamua ikiwa anastahili kuwa mhubiri ambaye hajabatizwa wa habari njema ya Ufalme kutanikoni. Akistahili, utakuwa na pendeleo la kumzoeza zaidi mwanafunzi wako wa Biblia wakati ambapo mnaambatana katika utumishi wa shambani.