Wasaidie Wengine Wafaidike na Fidia
Ukumbusho wa Kifo cha Kristo Utaadhimishwa Aprili 12
1 “Mungu apewe shukrani kwa ajili ya zawadi yake ya bure isiyoelezeka.” (2 Kor. 9:15) Maneno hayo yanaonyesha wazi jinsi tunavyohisi kuhusu wema na fadhili zenye upendo ambazo Mungu amewaonyesha watu wake kupitia Mwana wake, Yesu Kristo. Shukrani zetu zitaonekana wazi tutakapokutanika pamoja siku ya Aprili 12 ili kuadhimisha kifo cha Kristo.
2 Watu wengine milioni kumi hivi hujiunga pamoja na watumishi wa Yehova kuadhimisha Ukumbusho kila mwaka. Kwa kufanya hivyo, wao huonyesha kwa kiasi fulani shukrani zao kwa dhabihu ya Kristo. Hata hivyo, ili wafaidike, wanahitaji kuwa na imani katika fidia. (Yoh. 3:16, 36) Tunaweza kuwasaidiaje wasitawishe imani hiyo? Wakati wa majira haya ya Ukumbusho, tunaweza kuwatia moyo wajifunze Biblia na kuhudhuria mikutano ya kila juma ya kutaniko. Fikiria mapendekezo yafuatayo.
3 Mafunzo ya Biblia: Unapowaalika watu wanaopendezwa kwenye Ukumbusho, mbona usijaribu kuanza kujifunza Biblia pamoja nao ukitumia kitabu Biblia Inafundisha. Mweleze kuhusu maadhimisho ya Ukumbusho kwa kufungua ukurasa wa 206-208 na kuzungumzia habari yenye kichwa “Mlo wa Jioni wa Bwana—Maadhimisho Yanayomletea Mungu Heshima.” Unaweza kuzungumzia habari hiyo katika ziara moja au mbili, pengine ukijifunza Biblia na mtu mlangoni. Ukimaliza kuzungumzia habari hiyo, huenda mwenye nyumba akakubali mjifunze sura ya 5, “Fidia—Zawadi Bora Zaidi Kutoka kwa Mungu.” Mara mnapoanza kujifunza Biblia kwa ukawaida, rudini nyuma na kujifunza sura nne za kwanza za kitabu hicho.
4 Tunaweza kuanzisha funzo la Biblia na nani kwa kutumia njia hiyo? Huenda baadhi ya wafanyakazi, wanashule wenzako, au majirani wakapendezwa na mazungumzo hayo. Akina ndugu wanaweza kufanya hivyo na waume wasioamini wa akina dada katika kutaniko. Na usiwasahau watu wako wa ukoo ambao si Mashahidi. Kwa kuongezea, tungependa kujitahidi kwa njia ya pekee kuwaalika kwenye Ukumbusho wale ambao zamani walikuwa wakishirikiana kwa ukawaida na kutaniko. (Luka 15:3-7) Na tujitahidi kuwasaidia wote hao wafaidike na fidia.
5 Mikutano ya Kutaniko: Ukumbusho ndio mkutano wa kwanza ambao wanafunzi wengi wa Biblia na watu wengine wanaopendezwa huhudhuria. Basi, tutawatiaje moyo wahudhurie na kufaidika na mikutano yetu mingine ya kutaniko? Huduma Yetu ya Ufalme ya Aprili 2005 ilikuwa na mapendekezo haya kwenye ukurasa wa 8: “Watajie kichwa cha hotuba ya watu wote itakayotolewa. Waonyeshe habari itakayozungumziwa katika Funzo la Mnara wa Mlinzi na katika Funzo la Kitabu la Kutaniko. Waeleze kuhusu Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi. Ikiwa una hotuba katika shule unaweza kufanya mazoezi ya hotuba hiyo pamoja nao. Waambie mambo makuu yaliyozungumziwa katika mikutano. Waonyeshe picha zilizo katika vichapo vyetu ili kuwasaidia kuelewa jinsi mikutano yetu inavyofanywa. Mwanzoni kabisa, wakati unapoanzisha funzo, waalike kwenye mikutano.”
6 Watu wenye mioyo minyoofu wanapojifunza Biblia kwa ukawaida na kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida, wao hufanya maendeleo ya kiroho haraka. Basi, na tuwatie moyo wengine wafaidike na maandalizi hayo ya kiroho na zawadi kuu ya Mungu, yaani, fidia.
[Maswali ya Funzo]
1. Taja njia moja ambayo tunaweza kuonyesha shukrani zetu kwa ajili ya fidia?
2. Ni nani wengine hujiunga na watumishi wa Yehova kuadhimisha Ukumbusho, nao wanahitaji kufanya nini ili wafaidike na fidia?
3. Tunawezaje kuanzisha funzo la Biblia na wale tunaowaalika kwenye Ukumbusho?
4. Tunaweza kuanzisha funzo la Biblia na nani wakati wa majira haya ya Ukumbusho?
5. Tunaweza kuwatiaje moyo wale tunaojifunza nao Biblia na watu wengine wanaopendezwa wahudhurie mikutano ya kila juma ya kutaniko?
6. Tunaweza kuwasaidiaje watu wenye mioyo minyoofu wafaidike na fidia?