Tunaweza Kumpa Yehova
1 Je, unajua kwamba wanadamu wanaweza kumpa Mungu kitu fulani? Abeli alimtolea Yehova baadhi ya mifugo yake yenye thamani kama dhabihu, na Noa na Ayubu walitoa matoleo kama hayo. (Mwa. 4:4; 8:20; Ayu. 1:5) Bila shaka, matoleo hayo hayakumtajirisha Muumba kwa njia yoyote, kwa kuwa vitu vyote ni vyake. Lakini dhabihu hizo zilionyesha kina cha upendo ambao wanaume hao waaminifu walikuwa nao kumwelekea Mungu. Leo, tunaweza kutumia wakati, nguvu, na mali zetu kumtolea Yehova “dhabihu ya sifa.”—Ebr. 13:15.
2 Wakati: Ni jambo linalofaa kama nini ‘kununua wakati’ kutokana na mambo yasiyo ya maana sana ili tushiriki zaidi katika huduma! (Efe. 5:15, 16) Labda tunaweza kurekebisha ratiba zetu ili tuwe mapainia wasaidizi mwezi mmoja au zaidi katika mwaka. Huenda tukaweza kuongeza wakati ambao kwa kawaida tunatumia katika huduma. Kuhubiri kwa dakika 30 zaidi kila juma kunaweza kuongeza angalau saa mbili katika wakati tunaotumia katika huduma kila mwezi!
3 Nguvu: Ili tuwe na nguvu za kutumia katika huduma tunahitaji kuepuka burudani na kazi zinazotuchosha sana tusiweze kumpa Yehova kilicho bora. Pia tunapaswa kuepuka kuhangaika kupita kiasi kuhusu mambo yanayoweza kufanya ‘moyo wetu uiname,’ na kumaliza nguvu ambazo tungetumia kumtumikia Mungu. (Met. 12:25) Hata ikiwa tunahangaikia jambo zuri, ingefaa sana ‘tumtupie Yehova mizigo yetu.’—Zab. 55:22; Flp. 4:6, 7.
4 Mali: Pia tunaweza kutoa mali zetu ili kutegemeza kazi ya kuhubiri. Paulo aliwatia moyo Wakristo wenzake ‘waweke kando kitu fulani katika akiba’ kwa ukawaida ili wawe na kitu cha kuwapa wale walio na uhitaji. (1 Kor. 16:1, 2) Hali kadhalika, tunaweza kuweka kando kiasi fulani cha pesa ili tutoe michango kwa ajili ya mahitaji ya kutaniko na pia kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Yehova anathamini kile tunachotoa kwa moyo, hata kikiwa kidogo kadiri gani.—Luka 21:1-4.
5 Yehova ametupa vitu vingi. (Yak. 1:17) Tunaonyesha uthamini wetu kwa kutoa wakati, nguvu, na mali zetu kwa ukarimu ili kumtumikia. Tunapofanya hivyo tunampendeza Yehova, “kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.”—2 Kor. 9:7.