Sura ya 16
‘Yesu Aliwapenda Mpaka Mwisho’
1, 2. Yesu anatumia jinsi gani usiku wake wa mwisho pamoja na mitume wake, na kwa nini saa hizo za mwisho ni za maana sana kwake?
YESU anapokutana na mitume wake katika chumba cha juu cha nyumba fulani huko Yerusalemu, anajua kwamba huo ndio usiku wa mwisho atakaokuwa pamoja nao. Wakati wa kurudi kwa Baba yake unakaribia. Baada ya muda mfupi, Yesu atakamatwa na imani yake itajaribiwa sana. Ingawa anajua kwamba anakaribia kufa, bado anawahangaikia mitume wake.
2 Ijapokuwa Yesu tayari amewaambia mitume wake kwamba atawaacha, bado ana mengi ya kuwaambia ili kuwatia nguvu kwa ajili ya wakati ujao. Hivyo, anatumia muda mfupi unaobaki akiwafundisha mambo ya maana yatakayowasaidia kuendelea kuwa waaminifu. Hayo ni baadhi ya mambo yenye kusisimua na yenye kugusa moyo zaidi ambayo amepata kuwaambia. Lakini, kwa nini Yesu anawahangaikia sana mitume wake kuliko anavyojihangaikia? Kwa nini saa hizo za mwisho pamoja nao ni za maana sana kwake? Kwa ufupi, ni kwa sababu ya upendo. Ndiyo, anawapenda sana.
3. Je, Yesu alingoja mpaka usiku wa mwisho ili kuwaonyesha wafuasi wake kwamba anawapenda? Eleza.
3 Makumi ya miaka baadaye, mtume Yohana akiongozwa na roho aliandika hivi katika utangulizi wa masimulizi yake kuhusu usiku huo: “Kwa sababu alijua kabla ya sherehe ya pasaka kwamba saa yake ya kutoka katika ulimwengu huu kwenda kwa Baba ilikuwa imefika, Yesu, akiwa amewapenda walio wake mwenyewe waliokuwa ulimwenguni, akawapenda mpaka mwisho.” (Yohana 13:1) Yesu hakungoja mpaka usiku huo ili kuonyesha kwamba anawapenda “walio wake mwenyewe.” Wakati wote wa huduma yake, na katika njia mbalimbali, alithibitisha kwamba anawapenda wanafunzi wake. Tutafaidika kwa kuchunguza baadhi ya njia ambazo alionyesha upendo, kwa sababu kwa kumwiga, tunathibitisha kwamba sisi ni wanafunzi wake wa kweli.
Kuonyesha Subira
4, 5. (a) Kwa nini Yesu alihitaji kuwa na subira alipokuwa akishughulika na wanafunzi wake? (b) Yesu alifanya nini mitume wake watatu waliposhindwa kukesha katika bustani ya Gethsemane?
4 Kuna uhusiano kati ya upendo na subira. “Upendo ni wenye ustahimilivu,” lasema andiko la 1 Wakorintho 13:4, nao ustahimilivu unatia ndani kuwavumilia wengine kwa subira. Je, Yesu alihitaji subira aliposhughulika na wanafunzi wake? Bila shaka! Kama tulivyoona katika Sura ya 3, iliwachukua mitume muda mrefu kusitawisha unyenyekevu. Walibishana mara kadhaa kuhusu ni nani aliye mkuu kati yao. Yesu alifanya nini? Je, aliudhika, akawajibu kwa hasira, na kuwafungia kinyongo? Hapana, alizungumza nao kwa subira, hata wakati “bishano kali” lilipotokea kuhusu suala hilo usiku wa mwisho aliokuwa pamoja nao!—Luka 22:24-30; Mathayo 20:20-28; Marko 9:33-37.
5 Baadaye, usiku huohuo, Yesu alipoenda katika bustani ya Gethsemane pamoja na wale mitume waaminifu 11, subira yake ilijaribiwa tena. Akiwaacha mitume wake wanane, Yesu aliwachukua Petro, Yakobo, na Yohana na kuingia nao ndani zaidi katika bustani hiyo. Ndipo Yesu akawaambia: “Nafsi yangu ina huzuni sana, kiasi cha kufa. Kaeni hapa na mwendelee kukesha pamoja nami.” Akasonga mbele kidogo, na kuanza kusali kwa bidii. Baada ya kusali kwa muda mrefu, akarudi mahali walipokuwa wale mitume watatu. Aliwakuta wakifanya nini? Saa hiyo, saa aliyokuwa akijaribiwa vikali zaidi, walikuwa wamelala fofofo! Je, aliwakemea kwa sababu hawakukesha? Hapana, aliwahimiza kwa subira. Maneno yake yenye fadhili yalionyesha kwamba alielewa uchovu waliokuwa nao na udhaifu wao mbalimbali.a Alisema: “Bila shaka, roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.” Yesu aliendelea kuwa mwenye subira jioni hiyo hata aliporudi na kuwakuta wakiwa wamelala, si mara ya kwanza tu bali pia mara ya pili na ya tatu!—Mathayo 26:36-46.
6. Tunaposhughulika na wengine tunaweza kuonyesha subira kama Yesu jinsi gani?
6 Inatia moyo kujua kwamba Yesu hakuchoshwa na mitume wake. Mwishowe, subira yake ilikuwa na matokeo mazuri, kwa kuwa wanaume hao waaminifu walijifunza faida ya kuwa wanyenyekevu na wenye kukesha. (1 Petro 3:8; 4:7) Tunaweza kumwiga Yesu jinsi gani tunaposhughulika na wengine? Wazee hasa wanapaswa kuwa na subira. Huenda mzee akafikiwa na waamini wenzake wakiwa na matatizo, wakati ambapo amechoka au ana mahangaiko yake mwenyewe. Wakati mwingine, wale wanaohitaji msaada huenda wasikubali shauri mara moja. Hata hivyo, wazee wenye subira watawafundisha “kwa upole” na ‘kulitendea kundi kwa wororo.’ (2 Timotheo 2:24, 25; Matendo 20:28, 29) Wazazi pia wanapaswa kumwiga Yesu kwa kuonyesha subira, kwa kuwa wakati mwingine huenda watoto wasikubali shauri au rekebisho mara moja. Ikiwa wazazi wana upendo na subira, hawatachoka kuwazoeza watoto wao. Subira hiyo inaweza kutokeza thawabu kubwa kwelikweli.—Zaburi 127:3.
Kushughulikia Mahitaji Yao
7. Yesu alishughulikia namna gani mahitaji ya kimwili ya wanafunzi wake?
7 Upendo huonyeshwa kwa matendo yasiyo ya ubinafsi. (1 Yohana 3:17, 18) “Hautafuti faida zake wenyewe.” (1 Wakorintho 13:5) Upendo ulimchochea Yesu kushughulikia mahitaji ya kimwili ya wanafunzi wake. Mara nyingi alichukua hatua hata kabla hawajamweleza mahitaji yao. Alipoona kwamba wamechoka, alipendekeza waandamane naye kwenda ‘faraghani katika mahali pasipo na watu wapumzike kidogo.’ (Marko 6:31) Alipotambua kwamba wana njaa, alichukua hatua mara moja na kuwalisha watu hao pamoja na maelfu ya watu wengine waliokuwa wamekuja kumsikiliza akifundisha.—Mathayo 14:19, 20; 15:35-37.
8, 9. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu alitambua mahitaji ya kiroho ya wanafunzi wake na kuyashughulikia? (b) Alipokuwa kwenye mti wa mateso, Yesu alionyesha jinsi gani kwamba anamhangaikia sana mama yake?
8 Yesu alitambua mahitaji ya kiroho ya wanafunzi wake na kuyashughulikia. (Mathayo 4:4; 5:3) Alipokuwa akifundisha, mara nyingi aliwafikiria wao hasa. Mahubiri ya Mlimani yalitolewa hasa kwa manufaa ya wanafunzi wake. (Mathayo 5:1, 2, 13-16) Alipofundisha kwa kutumia mifano, “kwa faragha alikuwa akiwaeleza wanafunzi wake mambo yote.” (Marko 4:34) Yesu alitabiri kwamba angemweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ili kuhakikisha kwamba wafuasi wake wanalishwa vizuri kiroho katika kipindi cha siku za mwisho. Mtumwa huyo mwaminifu, ni kikundi kidogo cha ndugu watiwa-mafuta wa Yesu walio duniani na amekuwa akiandaa chakula cha kiroho “kwa wakati unaofaa” tangu mwaka 1919 W.K.—Mathayo 24:45.
9 Siku ya kifo chake, Yesu alionyesha kwa njia yenye kugusa moyo sana jinsi anavyohangaikia hali ya kiroho ya wale anaowapenda. Hebu wazia jinsi ilivyokuwa. Yesu alikuwa kwenye mti wa mateso, akiwa na maumivu makali sana. Ili avute pumzi, alilazimika kujiinua kwa kujisukuma kwa miguu yake. Na haikosi kufanya hivyo kulisababisha maumivu makali sana kwa kuwa uzito wa mwili wake ulizidisha majeraha ya misumari katika miguu yake huku mgongo wake uliojeruhiwa kwa mijeledi ukisuguliwa na mti. Kwa kuwa mtu anahitaji kusawazisha pumzi anapozungumza, ingekuwa vigumu kwake kuzungumza na angepata maumivu makali. Hata hivyo, kabla tu hajafa, Yesu alitaja maneno yaliyoonyesha kwamba anampenda sana mama yake, Maria. Alipomwona Maria na mtume Yohana wakiwa wamesimama karibu, Yesu alizungumza kwa sauti inayoweza kusikika na mtu aliye karibu, na kumwambia mama yake: “Mwanamke, ona! Mwana wako!” Halafu akamwambia Yohana: “Ona! Mama yako!” (Yohana 19:26, 27) Yesu alijua kwamba mtume huyo mwaminifu angemtunza Maria kimwili na kiroho vilevile.b
Wazazi wanaojali ni wenye subira na wanashughulikia mahitaji ya watoto wao
10. Wazazi wanaweza kumwiga Yesu jinsi gani wanaposhughulikia mahitaji ya watoto wao?
10 Wazazi wanaojali wanaweza kufaidika kwa kumwiga Yesu. Baba anayeipenda familia yake kikweli, ataitegemeza kimwili. (1 Timotheo 5:8) Mara kwa mara, vichwa vya familia wenye usawaziko hupanga vipindi vya pumziko na tafrija. Isitoshe, wazazi Wakristo wanashughulikia mahitaji ya kiroho ya watoto wao. Jinsi gani? Wazazi hao hupanga kuwa na funzo la Biblia kwa ukawaida, nao wanajitahidi kufanya pindi hizo za funzo ziwajenge na kuwafurahisha watoto wao. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Kupitia maneno yao na mfano wao, wazazi wanawafundisha watoto wao kwamba huduma ni utendaji wa maana na kwamba kutayarisha na kuhudhuria mikutano ya Kikristo ni sehemu ya maana ya utendaji wao wa kiroho.—Waebrania 10:24, 25.
Kuwa Tayari Kusamehe
11. Yesu aliwafundisha wafuasi wake nini kuhusu kusamehe?
11 Kusamehe ni njia moja ya kuonyesha upendo. (Wakolosai 3:13, 14) Andiko la 1 Wakorintho 13:5 linasema upendo “hauweki hesabu ya ubaya.” Pindi nyingi, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake faida ya kusamehe. Aliwahimiza wawasamehe wengine “si, Mpaka mara 7, bali, Mpaka mara 77,” yaani, bila kipimo. (Mathayo 18:21, 22) Aliwafundisha kwamba mtenda-dhambi anapaswa kusamehewa iwapo baada ya kukemewa, anatubu. (Luka 17:3, 4) Hata hivyo, Yesu hakuwa kama Mafarisayo wanafiki waliofundisha kwa maneno tu; alifundisha kupitia mfano wake pia. (Mathayo 23:2-4) Hebu tuone jinsi Yesu alivyoonyesha kwamba alikuwa tayari kusamehe hata wakati rafiki aliyemtumaini sana alipotenda kinyume na matarajio yake.
12, 13. (a) Petro alifanya jambo gani lililomsikitisha Yesu usiku ambao Yesu alikamatwa? (b) Baada ya kufufuliwa, matendo ya Yesu yalionyesha jinsi gani kwamba alikuwa mwenye kusamehe kama alivyofundisha?
12 Yesu alikuwa na uhusiano wa karibu pamoja na mtume Petro, aliyekuwa mchangamfu na wakati mwingine alitenda bila kufikiri. Yesu alitambua sifa nzuri za Petro, naye akampa mapendeleo ya pekee. Petro, Yakobo, na Yohana walijionea miujiza fulani ambayo mitume wale wengine hawakuona. (Mathayo 17:1, 2; Luka 8:49-55) Kama tulivyotangulia kuona, Petro alikuwa mmoja wa mitume waliokuwa pamoja na Yesu alipoingia ndani zaidi ya bustani ya Gethsemane usiku ambao alikamatwa. Hata hivyo, usiku huohuo Yesu aliposalitiwa na kukamatwa, Petro na wale mitume wengine walimwacha na kutoroka. Baadaye, Petro alionyesha uhodari kwa kusimama nje huku Yesu akishtakiwa kwa uwongo. Lakini, baadaye Petro aliingiwa na woga, naye akafanya kosa zito—mara tatu alikana kwa uwongo kwamba hata hamjui Yesu! (Mathayo 26:69-75) Yesu alifanya nini? Ungefanya nini ikiwa rafiki yako wa karibu angefanya jambo kama hilo?
13 Yesu alikuwa tayari kumsamehe Petro. Alijua kwamba dhambi hiyo ilimsumbua sana Petro. Kwa kweli, mtume huyo aliyetubu ‘alianza kulia.’ (Marko 14:72) Yesu alipofufuliwa, alimtokea Petro, huenda ili kumfariji na kumtia moyo. (Luka 24:34; 1 Wakorintho 15:5) Baadaye, kabla ya miezi miwili kupita, Yesu alimkweza Petro kwa kumruhusu atoe ushahidi mbele ya umati huko Yerusalemu katika siku ya Pentekoste. (Matendo 2:14-40) Na tukumbuke pia kwamba Yesu hakuwawekea kinyongo mitume wake kwa sababu walimwacha. Badala yake, baada ya kufufuliwa, bado aliwaita “ndugu zangu.” (Mathayo 28:10) Je, si wazi kwamba mbali na kuwahimiza watu wawasamehe wengine, Yesu mwenyewe alikuwa mwenye kusamehe?
14. Kwa nini tunapaswa kujifunza kuwasamehe wengine, nasi tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tuko tayari kusamehe?
14 Tukiwa wanafunzi wa Kristo, tunahitaji kujifunza kuwasamehe wengine. Kwa nini? Tofauti na Yesu, sisi si wakamilifu, na ndivyo na wale ambao huenda wakatukosea. Mara kwa mara, sisi sote tunajikwaa katika neno na tendo. (Waroma 3:23; Yakobo 3:2) Kwa kuwasamehe wengine ikiwa kuna msingi wa kuwaonyesha rehema, tunafungua njia ili Mungu atusamehe. (Marko 11:25) Basi, tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tuko tayari kuwasamehe wale ambao huenda wakatukosea? Mara nyingi, upendo unatusaidia kuachilia makosa madogo-madogo tunayotendewa na wengine. (1 Petro 4:8) Wale waliotukosea wanapotubu kikweli, kama Petro alivyofanya, bila shaka, tungependa kumwiga Yesu kwa kuwa tayari kuwasamehe. Badala ya kuwawekea kinyongo, tunatenda kwa hekima tunapowasamehe. (Waefeso 4:32) Kwa kufanya hivyo, tunachangia amani kutanikoni, na pia amani yetu wenyewe ya akilini na moyoni.—1 Petro 3:11.
Kuwatumaini
15. Kwa nini Yesu aliwatumaini wanafunzi wake ingawa hawakuwa wakamilifu?
15 Upendo unahusianishwa na tumaini. Upendo “huamini mambo yote.”c (1 Wakorintho 13:7) Upendo wa Yesu ulimsukuma kuwatumaini wanafunzi wake ingawa hawakuwa wakamilifu. Aliwatumaini na kuamini kwamba kwa kweli wanampenda Yehova na wanataka kufanya mapenzi Yake. Hata walipokosea, Yesu hakutilia shaka nia zao. Kwa mfano, pindi moja inaonekana mitume Yakobo na Yohana walimtuma mama yao amwombe Yesu awape mitume hao pendeleo la kuketi kando yake katika Ufalme wake. Hata hivyo, Yesu hakutilia shaka ushikamanifu wao wala kuwanyang’anya pendeleo la kuwa mitume.—Mathayo 20:20-28.
16, 17. Yesu aliwapa wanafunzi wake kazi gani?
16 Yesu alionyesha kwamba anawatumaini wanafunzi wake kwa kuwapa kazi mbalimbali. Pindi mbili alipotokeza chakula kingi kimuujiza na kulisha umati wa watu, aliwapa wanafunzi wake kazi ya kugawa chakula hicho. (Mathayo 14:19; 15:36) Aliwapa Petro na Yohana mgawo wa kwenda Yerusalemu na kufanya matayarisho kwa ajili ya Pasaka yake ya mwisho. Walitafuta mwana-kondoo, divai, mkate usio na chachu, mboga chungu za majani, na vitu vingine vya maana vilivyohitajiwa. Huo haukuwa mgawo mdogo, kwa kuwa Sheria ya Musa iliagiza Pasaka iadhimishwe ifaavyo, naye Yesu alihitaji kutii Sheria hiyo. Isitoshe, baadaye usiku huo, Yesu alitumia divai hiyo na mkate huo usio na chachu kuwa mifano muhimu alipoanzisha Ukumbusho wa kifo chake.—Mathayo 26:17-19; Luka 22:8, 13.
17 Yesu aliwapa wanafunzi wake madaraka mazito hata zaidi. Kama tulivyoona mapema, alikikabidhi kikundi kidogo cha wafuasi wake watiwa-mafuta hapa duniani daraka zito la kutayarisha na kugawa chakula cha kiroho. (Luka 12:42-44) Pia, kumbuka kwamba aliwapa wanafunzi wake kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. (Mathayo 28:18-20) Hata sasa, ingawa anatawala mbinguni na hatuwezi kumwona, Yesu amewapa watu wenye sifa za kiroho, “zawadi katika wanadamu,” daraka la kutunza kutaniko lake lililo duniani.—Waefeso 4:8, 11, 12.
18-20. (a) Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunawatumaini waamini wenzetu? (b) Ni kwa njia gani tunaweza kuiga mfano wa Yesu wa kuwa tayari kuwapa wengine migawo? (c) Ni nini kitakachozungumziwa katika sura inayofuata?
18 Tunaweza kumwiga Yesu jinsi gani tunaposhughulika na watu wengine? Kuwatumaini waamini wenzetu kunaonyesha kwamba tunawapenda. Tusisahau kwamba upendo huangalia mambo mazuri bali si mabaya. Wakati ambapo watu wengine wanatuvunja moyo, jambo ambalo mara kwa mara linatokea, upendo utatuzuia tusikate kauli mara moja kwamba nia zao ni mbovu. (Mathayo 7:1, 2) Tukiwa na maoni yanayofaa kuhusu waamini wenzetu, tutawatendea kwa njia zenye kuwajenga badala ya kuwabomoa.—1 Wathesalonike 5:11.
19 Je, tunaweza kumwiga Yesu kwa kuwa tayari kuwapa wengine mapendeleo? Ndugu walio na madaraka kutanikoni wanapaswa kuwapa wengine migawo inayowafaa na inayotimiza kusudi fulani wakiamini kwamba ndugu hao watafanya yote wanayoweza. Kwa njia hiyo, wazee wenye uzoefu wanaweza kuwazoeza vijana wanaostahili ambao ‘wanajitahidi kufikia’ mapendeleo ya kulisaidia kutaniko. (1 Timotheo 3:1; 2 Timotheo 2:2) Mazoezi hayo ni ya maana. Yehova anapoendelea kuharakisha ukuzi wa Ufalme, wanaume wanaostahili watahitaji kuzoezwa kushughulikia ongezeko hilo.—Isaya 60:22.
20 Yesu alituwekea mfano mzuri kwa kuwapenda wengine. Kati ya mambo yote tunayoweza kuiga kutoka kwa Yesu, jambo la maana zaidi ni upendo. Katika sura inayofuata, tutazungumzia njia kuu aliyotuonyesha upendo—kuwa tayari kuutoa uhai wake.
a Mbali na uchovu wa kimwili, kuna jambo lingine lililofanya mitume hao walale. Masimulizi kama hayo kwenye Luka 22:45 yanasema kwamba Yesu ‘aliwakuta wakisinzia kwa huzuni.’
b Inaonekana kufikia wakati huo Maria alikuwa mjane, na huenda bado wale watoto wake wengine hawakuwa wanafunzi wa Yesu.—Yohana 7:5.
c Bila shaka, haimaanishi kwamba upendo ni mpumbavu au unadanganyika upesi. Badala yake, inamaanisha kwamba upendo hauchambui au kuwa na shaka juu ya mambo bila sababu. Upendo huepuka kutilia shaka nia za wengine au kukata kauli kwamba hawana nia nzuri.