Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 9/15 kur. 16-21
  • Yehova na Apendezwe na Hesabu Yako

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Yehova na Apendezwe na Hesabu Yako
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ujuzi Hutufanya Tuwe na Wajibu wa Kutoa Hesabu
  • Wenye Wajibu wa Kutoa Hesabu kwa Ajili ya Huduma Yetu
  • Kutoa Hesabu Nzuri Tukiwa Familia
  • Wazee Hutoa Hesabu—Jinsi Gani?
  • Endelea Kutoa Hesabu Nzuri
  • Lazima Wote Watoe Hesabu kwa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Nehemia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • “Unikumbuke Kwa Ajili ya Wema, Ee Mungu Wangu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Kitabu Cha Biblia Namba 16—Nehemia
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 9/15 kur. 16-21

Yehova na Apendezwe na Hesabu Yako

“Hili . . . ulikumbuke kwenye hesabu yangu, Ee Mungu wangu . . . Unikumbuke, Ee Mungu wangu, kwa ajili ya mema.”—NEHEMIA 13:22, 31, NW.

1. Ni jambo gani ambalo huwasaidia wale waliojiweka wakfu kwa Mungu kutoa hesabu nzuri kwa Yehova?

WATUMISHI wa Yehova wana msaada wote unaohitajiwa ili kutoa hesabu nzuri kwake. Kwa nini? Kwa sababu wana uhusiano wa karibu pamoja na Mungu wakiwa sehemu ya tengenezo lake la kidunia. Amewafunulia makusudi yake, na amewapa msaada na ufahamu wa kiroho wenye kina kupitia roho yake takatifu. (Zaburi 51:11; 119:105; 1 Wakorintho 2:10-13) Kwa kufikiria hali hizo za pekee, Yehova, kwa upendo, huwapasisha watumishi wake wa kidunia kutoa hesabu kwake kuhusu wao wenyewe kwa jinsi walivyo na kwa mambo wanayotimiza katika nguvu zake na kwa msaada wa roho yake takatifu.

2. (a) Nehemia alitoa hesabu njema kwa Mungu kujihusu mwenyewe katika njia zipi? (b) Nehemia alimalizia kitabu cha Biblia chenye jina lake kwa ombi jipi?

2 Mtu mmoja aliyetoa hesabu njema kwa Mungu kujihusu mwenyewe, alikuwa Nehemia, mnyweshaji wa Mfalme wa Uajemi Artashasta (Longimano). (Nehemia 2:1) Nehemia alipata kuwa gavana wa Wayahudi, akajenga upya ukuta wa Yerusalemu akikabili maadui na hatari mbalimbali. Akiwa na bidii kwa ajili ya ibada ya kweli, alitekeleza Sheria ya Mungu na kuwaonyesha ufikirio wale walioonewa. (Nehemia 5:14-19) Nehemia aliwasihi sana Walawi wajisafishe kwa ukawaida, walinde malango, na kutakasa siku ya Sabato. Kwa hiyo aliweza kusali hivi: “Hili, nalo, ulikumbuke kwenye hesabu yangu, Ee Mungu wangu, na unisikitikie kulingana na wingi wa fadhili-upendo zako.” Pia, kwa kufaa, Nehemia alimalizia hivi, kitabu chake kilichopuliziwa kimungu: “Unikumbuke, Ee Mungu wangu, kwa ajili ya mema.”—Nehemia 13:22, 31, NW.

3. (a) Ungemfafanuaje mtu anayefanya mema? (b) Kufikiria mwendo wa Nehemia huenda kukatufanya tujiulize maswali yapi?

3 Mtu afanyaye mema ni mwenye wema wa adili na hufanya vitendo vya unyoofu vinavyonufaisha wengine. Nehemia alikuwa mtu wa aina hiyo. Alikuwa na hofu yenye staha kwa Mungu na bidii nyingi kwa ajili ya ibada ya kweli. Zaidi ya hayo, alikuwa mwenye shukrani kwa ajili ya mapendeleo yake katika utumishi wa Mungu na alitoa hesabu nzuri kwa Yehova kujihusu mwenyewe. Kufikiria mwendo wake huenda kutatufanya tujiulize, ‘Mimi huyaonaje mapendeleo na madaraka niliyopewa na Mungu? Ninatoa hesabu ya aina gani kwa Yehova Mungu na Yesu Kristo kujihusu mwenyewe?’

Ujuzi Hutufanya Tuwe na Wajibu wa Kutoa Hesabu

4. Yesu aliwapa wafuasi wake utume gani, na wale wenye “mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele” walipaswa kufanya nini?

4 Yesu aliwapa wafuasi wake utume huu: “Enendeni . . . mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza . . . , na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi.” (Mathayo 28:19, 20) Wanafunzi wangefanywa kwa kuwafundisha. Wale ambao wangefundishwa kwa njia hiyo na waliokuwa “na mwelekeo ufaao kwa ajili ya uhai udumuo milele” wangebatizwa, sawa na alivyobatizwa Yesu. (Matendo 13:48; Marko 1:9-11, linganisha NW.) Kutamani kwao kushika mambo yote aliyokuwa ameamuru kungetoka moyoni. Wangefikia hatua ya wakfu kwa kuendelea kutwaa na kutumia ujuzi sahihi juu ya Neno la Mungu.—Yohana 17:3.

5, 6. Tueleweje Yakobo 4:17? Toa kielezi cha matumizi yalo.

5 Kadiri ujuzi wetu wa Kimaandiko ulivyo wenye kina zaidi, ndivyo msingi wa imani yetu unavyokuwa bora zaidi. Wakati uo huo, wajibu wetu wa kutoa hesabu kwa Mungu unakuwa mkubwa zaidi. Yakobo 4:17 husema hivi: “Ajuaye kutenda mema, wala hayatendi, kwake huyo ni dhambi.” Taarifa hiyo yaonekana kuwa mkataa wa yale mwanafunzi Yakobo aliyokuwa ametoka tu kusema juu ya kujivuna badala ya kumtegemea Mungu kikamili. Mtu akijua kwamba hawezi kutimiza jambo lolote lile lenye kudumu bila msaada wa Yehova lakini hatendi kulingana na ujuzi huo, hiyo ni dhambi. Lakini maneno ya Yakobo yaweza pia kutumiwa kuhusu dhambi ya kutokufanya yanayopasa kufanywa. Mathalani, katika mfano wa Yesu wa kondoo na mbuzi, mbuzi wanalaumiwa, si kwa sababu ya matendo mabaya, bali ni kwa sababu ya kutowasaidia ndugu za Kristo.—Mathayo 25:41-46.

6 Mwanamume mmoja ambaye Mashahidi wa Yehova walikuwa wakiongoza funzo la Biblia pamoja naye alikuwa akifanya maendeleo machache ya kiroho, yaonekana ni kwa sababu hakuacha kuvuta sigareti, ingawa alijua kwamba alipaswa kufanya hivyo. Mzee mmoja akamwomba asome Yakobo 4:17. Baada ya kueleza juu ya umaana wa andiko hilo, huyo mzee akasema hivi: “Ingawa hujabatizwa, una wajibu wa kutoa hesabu na ni lazima uchukue daraka kamili kwa ajili ya uamuzi wako.” Kwa furaha, mtu huyo aliitikia, akaacha kuvuta sigareti, na upesi akastahili kubatizwa kwa ufananisho wa kujiweka kwake wakfu kwa Yehova Mungu.

Wenye Wajibu wa Kutoa Hesabu kwa Ajili ya Huduma Yetu

7. Ni ipi njia moja ya kuonyesha shukrani yetu kwa ajili ya “ujuzi wenyewe juu ya Mungu”?

7 Tamaa yetu ya kuhisiwa moyoni yapaswa kuwa kumpendeza Muumba wetu. Njia moja ya kuonyesha shukrani yetu kwa ajili ya “ujuzi wenyewe juu ya Mungu” ni kutimiza utume wa kufanya wanafunzi wa Mwana wake, Yesu Kristo. Hiyo ni njia pia ya kuonyesha kumpenda kwetu Mungu na jirani. (Mithali 2:1-5; Mathayo 22:35-40) Ndiyo, ujuzi wetu juu ya Mungu hutufanya tuwe na wajibu wa kutoa hesabu kwake, na twahitaji kuwaona wanadamu wenzetu kuwa watu wawezao kuwa wanafunzi.

8. Kwa nini twaweza kusema kwamba Paulo alihisi ana wajibu wa kutoa hesabu kwa Mungu kwa ajili ya huduma yake?

8 Mtume Paulo alijua kwamba kuikubali kwa moyo wote habari njema na kuitii hutokeza wokovu, hali kuikataa kwaweza kuleta uharibifu. (2 Wathesalonike 1:6-8) Kwa hiyo alihisi ana wajibu wa kutoa hesabu kwa Yehova kwa ajili ya huduma yake. Kwa kweli, Paulo na washiriki wake waliithamini huduma yao sana hivi kwamba waliepuka kwa uangalifu hata kuonyesha watu wazo la kwamba walikuwa wakipata faida ya kifedha kutokana nayo. Zaidi ya hayo, moyo wa Paulo ulimsukuma aseme hivi: “Ijapokuwa naihubiri Injili [“habari njema,” NW], sina la kujisifia; maana nimewekewa sharti; tena ole wangu nisipoihubiri Injili!”—1 Wakorintho 9:11-16.

9. Wakristo wote wana deni gani la maana la kulipa?

9 Kwa kuwa sisi ni watumishi wa Yehova tuliojiweka wakfu, ‘tumewekewa sharti kuihubiri injili.’ Utume wetu ni kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Tulikubali daraka hilo tulipojiweka wakfu kwa Mungu. (Linganisha Luka 9:23, 24.) Zaidi ya hayo, tuna deni la kulipa. Paulo alisema hivi: “Nawiwa na Wayunani na wasio Wayunani, nawiwa na wenye hekima na wasio na hekima. Kwa hiyo, kwa upande wangu, mimi ni tayari kuihubiri Injili hata na kwenu ninyi mnaokaa Rumi.” (Warumi 1:14, 15) Paulo alikuwa mdeni kwa sababu alijua kwamba alikuwa na wajibu wa kuhubiri ili watu waweze kusikia habari njema na kuokolewa. (1 Timotheo 1:12-16; 2:3, 4) Kwa hiyo alijitahidi sana kutimiza utume wake na kulipa deni lake kwa wanadamu wenzake. Tukiwa Wakristo, sisi pia tuna deni la jinsi hiyo la kulipa. Kuhubiri Ufalme ni njia kuu pia ya kuonyesha upendo kwa Mungu, kwa Mwana wake, na kwa majirani wetu.—Luka 10:25-28.

10. Watu fulani wamepanua huduma yao kwa kufanya nini?

10 Njia moja ya kutoa hesabu yenye kukubalika kwa Mungu ni kutumia uwezo wetu mbalimbali kupanua huduma yetu. Ili kutoa kielezi: Miaka ya juzijuzi kumekuwa na ongezeko katika Uingereza la watu wa kutoka vikundi vingi vya kitaifa. Ili kuwafikia watu hao na habari njema, mapainia (wahubiri wa Ufalme wa wakati wote) zaidi ya 800 na mamia ya Mashahidi wengine wanajifunza lugha tofauti-tofauti. Hilo limetokeza kichocheo kizuri kwa huduma. Painia mmoja anayefundisha Kichina alisema hivi: “Sikufikiri kamwe kwamba ningepata wakati wowote kuwafundisha Mashahidi wengine lugha yangu, ili waweze kushiriki kweli pamoja na wengine katika njia hii. Inaridhisha sana!” Je, ungeweza kuupanua utumishi wako katika njia kama hiyo?

11. Tokeo lilikuwa nini Mkristo mmoja alipotoa ushahidi kivivihivi?

11 Yamkini, kila mmoja wetu angefanya lolote lile awezalo kufanya ili kumwokoa mtu anayekufa maji. Vivyo hivyo, watumishi wa Yehova wana hamu ya kutumia uwezo wao mbalimbali ili kutoa ushahidi kwenye kila fursa. Majuzi Shahidi mmoja aliketi karibu na mwanamke fulani katika basi na akaongea naye kuhusu Maandiko. Kwa sababu ya kusisimuliwa na yale aliyoyasikia, huyo mwanamke aliuliza maswali mengi. Shahidi alipokuwa karibu kushuka katika basi, yule mwanamke alimsihi aje nyumbani kwake badala ya kushuka, kwa kuwa alikuwa na maswali mengi bado. Shahidi akakubali. Tokeo likawa nini? Funzo la Biblia lilianzishwa, na miezi sita baadaye huyo mwanamke akawa mtangazaji wa Ufalme asiyebatizwa. Upesi alikuwa akiongoza mafunzo yake mwenyewe sita, ya Biblia nyumbani. Ilikuwa thawabu iliyoje kwa sababu ya kutumia uwezo mbalimbali katika utumishi wa Ufalme!

12. Uwezo wetu mbalimbali tukiwa wahudumu waweza kutumiwaje kwa matokeo katika utumishi wa shambani?

12 Uwezo wetu mbalimbali tukiwa wahudumu waweza kutumiwa kwa matokeo shambani kwa kutumia vichapo kama kile kitabu chenye kurasa 192 kiitwacho Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. Kufikia Aprili 1996, Halmashauri ya Uandikaji ya Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova ilikuwa imekubali utangazaji wa kitabu Ujuzi katika lugha zaidi ya 140, na kufikia wakati huo nakala zacho 30,500,000 zilikuwa zimechapwa tayari katika lugha 111. Kitabu hicho kiliandikwa na lengo la kusaidia wanafunzi wa Biblia wajifunze vya kutosha kuhusu Neno na makusudi ya Mungu ili waweze kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Kwa kuwa watangazaji wa Ufalme hawatakuwa wakiongoza funzo la Biblia nyumbani pamoja na mwanafunzi yuleyule kwa miaka mingi, wanaweza kuongoza mafunzo pamoja na watu wengi zaidi au kuongeza kushiriki kwao katika kazi ya kuhubiri nyumba hadi nyumba na namna nyinginezo za huduma. (Matendo 5:42; 20:20, 21) Kwa sababu ya kufahamu wajibu wao wa kutoa hesabu kwa Mungu, wao huelekeza uangalifu kwenye maonyo ya kimungu. (Ezekieli 33:7-9) Lakini kusudi lao kuu ni kumheshimu Yehova na kusaidia wengi iwezekanavyo wajifunze juu ya habari njema katika ule wakati mfupi unaobaki bado wa mfumo huu mwovu wa mambo.

Kutoa Hesabu Nzuri Tukiwa Familia

13. Kwa nini familia zinazomwogopa Mungu ziwe na funzo la Biblia la familia la kawaida?

13 Kila mtu mmoja-mmoja na familia anayekubali Ukristo wa kweli ana wajibu wa kutoa hesabu kwa Mungu na kwa hiyo apaswa “kukaza mwendo [“mbele kwenye ukomavu,” NW]” na kuwa ‘thabiti katika imani.’ (Waebrania 6:1-3; 1 Petro 5:8, 9) Kwa kielelezo, wale ambao wamejifunza kitabu Ujuzi na wamebatizwa wanahitaji kukamilisha ujuzi wao wa Kimaandiko kwa kuhudhuria mikutano kwa ukawaida na pia kwa kusoma Biblia na vichapo vingine vya Kikristo. Familia zinazomwogopa Mungu zapaswa pia kuwa na funzo la familia la kawaida, kwa maana hiyo ni njia ya maana ya ‘kukesha, kusimama imara katika imani, kufanya kiume, kuwa hodari.’ (1 Wakorintho 16:13) Ikiwa wewe ni kichwa cha nyumba, una wajibu hasa kwa Mungu kuhakikisha kwamba familia yako inalishwa vizuri kiroho. Sawa na vile chakula cha kimwili chenye lishe kinavyochangia afya ya asili, ndivyo chakula cha kiroho kilicho kingi na cha ukawaida kinavyohitajiwa ikiwa wewe na familia yako mtaendelea kuwa “wazima katika imani.”—Tito 1:13.

14. Ushahidi uliotolewa na msichana Mwisraeli aliyefundishwa vizuri ulikuwa na tokeo jipi?

14 Ikiwa kuna watoto katika nyumba yako, Mungu atapendezwa na hesabu yako ukiwapa maagizo timamu ya kiroho. Kufundisha huko kutawanufaisha, sawa na vile kulivyomnufaisha msichana mdogo Mwisraeli aliyetekwa na Wasiria katika siku za nabii wa Mungu, Elisha. Alikuwa kijakazi wa mke wa Naamani, mkuu wa jeshi la Siria, aliyekuwa na ukoma. Ingawa msichana huyo alikuwa mchanga, alimwambia bibi-mwenyeji wake hivi: “Laiti bwana wangu angekuwa pamoja na yule nabii aliyeko Samaria! maana angemponya ukoma wake.” Kwa sababu ya ushuhuda wake, Naamani alienda Israeli, akautii hatimaye mwelekezo wa Elisha wa kuoga mara saba katika Mto Yordani, na akasafishwa ukoma. Zaidi ya hayo, Naamani akawa mwabudu wa Yehova. Hilo bila shaka lilimsisimua kama nini yule msichana mdogo!—2 Wafalme 5:1-3, 13-19.

15. Kwa nini ni jambo la maana kwa wazazi kuwapa watoto wao mazoezi mazuri ya kiroho? Toa kielezi.

15 Si rahisi kuwalea watoto wenye kumhofu Mungu katika ulimwengu huu usio na adili unaokaa katika nguvu ya Shetani. (1 Yohana 5:19) Hata hivyo, tangu utoto wa Timotheo, nyanya yake Loisi, na mama yake Eunike, walimfundisha Maandiko kwa mafanikio. (2 Timotheo 1:5; 3:14, 15) Kujifunza Biblia pamoja na watoto wako, kwenda pamoja nao kwenye mikutano ya Kikristo kwa ukawaida, na hatimaye kuandamana nao katika huduma, yote hayo ni sehemu ya kigezo cha mazoezi ambacho ni lazima utoe hesabu kwa Mungu juu yacho. Mkristo mmoja katika Wales, ambaye sasa yumo katika miaka yake ya 80, akumbuka kwamba katika miaka ya mapema ya 1920, baba yake alienda pamoja naye alipotembea kilometa 10 juu ya mlima (safari ya kwenda na kurudi ya kilometa 20) ili kugawanya trakti za Biblia kwa wana-kijiji katika bonde la karibu. “Baba yangu aliikaza kweli kikiki moyoni mwangu, katika matembezi hayo,” asema kwa shukrani.

Wazee Hutoa Hesabu—Jinsi Gani?

16, 17. (a) Wanaume wazee wenye ukomavu katika Israeli la kale walikuwa na mapendeleo yapi? (b) Kwa kulinganisha na hali katika Israeli la kale, kwa nini mengi zaidi yanatakwa kwa wazee Wakristo leo?

16 “Kichwa chenye mvi ni taji ya utukufu, kama kikionekana katika njia ya haki,” akasema Sulemani mwenye hekima. (Mithali 16:31) Lakini si umri wa kimwili tu unaomtayarisha mtu kwa ajili ya daraka katika kutaniko la watu wa Mungu. Wanaume wazee wenye ukomavu kiroho katika Israeli la kale walitumikia wakiwa waamuzi na maofisa wa kusimamia haki na kudumisha amani, utaratibu mzuri, na afya ya kiroho. (Kumbukumbu la Torati 16:18-20) Ingawa ndivyo ilivyo kwa habari ya kutaniko la Kikristo, mengi zaidi yanatakwa kwa wazee kadiri mwisho wa mfumo huu wa mambo ukaribiavyo. Kwa nini?

17 Waisraeli walikuwa ‘watu wachaguliwa’ waliokombolewa na Mungu kutoka Misri. Kwa kuwa waliipokea Sheria kupitia mpatanishi wao Musa, wazao wao walizaliwa katika taifa lililowekwa wakfu na walifahamu amri za Yehova. (Kumbukumbu la Torati 7:6, 11) Hata hivyo, leo hakuna mtu anayezaliwa katika taifa lililowekwa wakfu, na ni wachache kwa kulinganisha wanaokua katika familia zinazomwogopa Mungu zinazofahamu vizuri kweli ya Kimaandiko. Wale hasa ambao wameanza hivi majuzi ‘kwenda katika kweli’ huenda wakahitaji maagizo juu ya jinsi ya kuishi kulingana na kanuni za Kimaandiko. (3 Yohana 4) Wazee waaminifu wana daraka lililoje basi ‘washikapo kielelezo cha maneno yenye uzima’ na kuwasaidia watu wa Yehova!—2 Timotheo 1:13, 14.

18. Ni lazima wazee wa kutaniko wawe tayari kutoa msaada wa aina gani, na kwa nini?

18 Mtoto mchanga anayejifunza kutembea huenda akajikwaa na kuanguka. Hana usalama na anahitaji msaada na uhakikishio wa wazazi. Mtu aliyejiweka wakfu kwa Yehova anaweza vilevile kujikwaa au kuanguka kiroho. Hata mtume Paulo aliona ni lazima kushindana ili kufanya lililo sawa au jema machoni pa Mungu. (Warumi 7:21-25) Wachungaji wa kundi la Mungu wanahitaji kutoa msaada wenye upendo kwa Wakristo ambao wamekosea lakini ni wenye toba kikweli. Wazee walipomtembelea mwanamke mmoja aliyejiweka wakfu aliyekuwa amefanya kosa zito, alisema hivi mbele ya mume wake aliyejiweka wakfu: “Najua mtanitenga na ushirika!” Lakini alianza kulia machozi alipoambiwa kwamba wazee walitaka kujua ni msaada gani uliohitajiwa ili kuirudisha hali ya kiroho ya familia. Kwa sababu ya kufahamu kwamba ni lazima watoe hesabu, wazee walifurahi kusaidia mwamini mwenzao mwenye toba.—Waebrania 13:17.

Endelea Kutoa Hesabu Nzuri

19. Twaweza kuendeleaje kutoa hesabu nzuri kwa Mungu kujihusu wenyewe?

19 Wazee wa kutaniko na watumishi wa Mungu wengine wote wanahitaji kuendelea kutoa hesabu nzuri kwa Yehova kuhusu wao wenyewe. Hiyo yawezekana tukishikamana na Neno la Mungu na kufanya mapenzi yake. (Mithali 3:5, 6; Warumi 12:1, 2, 9) Twataka hasa kuwafanyia mema wale ambao katika imani ni jamaa zetu. (Wagalatia 6:10) Hata hivyo, mavuno yangali mengi, na wafanyakazi wangali wachache. (Mathayo 9:37, 38) Kwa hiyo na tuwafanyie wengine mema kwa kupiga mbiu ya ujumbe wa Ufalme kwa bidii yenye kuendelea. Yehova atapendezwa na hesabu yetu tukitimiza wakfu wetu, tukifanya mapenzi yake, na kupiga mbiu ya habari njema kwa uaminifu.

20. Twajifunza nini kutokana na kufikiria mwendo wa Nehemia?

20 Kwa hiyo na tuendelee kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana. (1 Wakorintho 15:58) Na twafanya vema kumfikiria Nehemia, aliyejenga upya ukuta wa Yerusalemu, akatekeleza Sheria ya Mungu, na kuendeleza kwa bidii ibada ya kweli. Alisali kwamba Yehova Mungu amkumbuke kwa ajili ya mema aliyokuwa amefanya. Na uthibitike kuwa mwenye kujitoa vivyo hivyo kwa Yehova, na apendezwe na hesabu yako.

Majibu Yako Ni Nini?

◻ Ni kielelezo kipi kilichowekwa na Nehemia?

◻ Kwa nini ujuzi hutufanya tuwe na wajibu wa kutoa hesabu kwa Mungu?

◻ Twaweza kutoaje hesabu yenye kukubalika kwa Yehova katika huduma yetu?

◻ Familia zaweza kufanya nini ili kutoa hesabu nzuri kwa Mungu?

◻ Wazee Wakristo hutoaje hesabu?

[Picha katika ukurasa wa 18]

Sawa na Paulo, twaweza kutoa hesabu nzuri kwa Mungu tukiwa wapiga-mbiu wa Ufalme

[Picha katika ukurasa wa 19]

Je, watoto wako, wako imara katika imani kama yule msichana mdogo Mwisraeli katika nyumba ya Naamani?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki