Barua Kutoka kwa Baraza Linaloongoza
Ndugu Zetu Wapendwa:
Hizi ni nyakati zenye kusisimua kama nini! Na tuna furaha iliyoje! Tunafurahia kikweli kufanya kazi pamoja nanyi ndugu na dada wapendwa—“bega kwa bega”—katika kutoa ushahidi mkubwa zaidi kuwahi kutolewa kumhusu Baba yetu wa mbinguni, Yehova.—Sef. 3:9; Yoh. 14:12.
Ingawa tunafurahia kumtumikia Yehova, haimaanishi kuwa hatukabili matatizo makubwa. Katika mwaka wa utumishi uliopita, baadhi yenu mlipatwa na hali ngumu zilizosababishwa na matetemeko ya ardhi, mafuriko, vimbunga, na misiba mingine ya asili yenye kuhatarisha uhai. (Mt. 24:7) Wengi hupambana kila siku na uzee na pia magonjwa yanayodhoofisha mwili. Sote lazima tupambane na “maumivu ya taabu” yanayozidi kuongezeka. (Mt. 24:8) Katika nchi kadhaa, kutia ndani Armenia, Eritrea, na Korea Kusini, wengi wa ndugu zetu wametiwa gerezani kwa sababu ya imani yao.—Mt. 24:9.
Ni nini ambacho kimetusaidia kuwa na mtazamo unaofaa licha ya matatizo hayo? Andiko la mwaka wa 2010 limetukumbusha jambo moja muhimu: ‘Upendo huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.’ (1 Kor. 13:7, 8) Ndiyo, upendo wetu kwa mmoja na mwenzake—na pia upendo wetu kwa Yehova—hutuimarisha kuendelea kuvumilia.
Watu wengi wanaodai kuwa Wakristo wanashangaa kuona bidii yetu katika kazi ya kuhubiri ambayo tunaifanya bila kuacha. Ingawa huenda wasikubaliane na imani na mafundisho yetu, baadhi yao wamechochewa kusema, “Ninyi watu mnafanya kazi tunayopaswa kuwa tunafanya!” Ni nini kinachowawezesha Mashahidi wa Yehova kuendelea kuhubiri bila kuacha? Kwa mara nyingine tena, jibu ni upendo. Kama Baba yetu wa mbinguni, hatutaki mtu yeyote aangamizwe. (2 Pet. 3:9) Tamaa yetu kwamba wote wafikie toba inadhihirishwa na kilele kipya cha wahubiri 7,508,050 katika mwaka wa utumishi uliopita. Ni mashirika gani mengine ya kidini ambayo yana wahudumu wengi kadiri hiyo, ambao wanajitolea kwa upendo kuwasaidia wengine kiroho?
Tunatiwa moyo kuona unabii wa huu wa Isaya ukiendelea kutimizwa: “Itatukia katika siku za mwisho kwamba mlima wa nyumba ya Yehova utawekwa imara juu ya kilele cha milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote yatamiminika huko.” (Isa. 2:2-4) Kati ya watu wengi wanaomiminika katika nyumba ya Yehova kuna 294,368 waliobatizwa katika mwaka wa utumishi uliopita. Tunawakaribisha ndugu hao wenye thamani katika tengenezo letu. Upendo wetu wa Kikristo na utuchochee kuendelea kuwasaidia kupambana na mashambulio ya adui yetu Shetani Ibilisi.—1 Pet. 5:8, 9.
Kilele kipya cha watu 18,706,895 waliohudhuria Ukumbusho uliofanywa Jumanne (Siku ya 2), Machi 30, 2010 (30/3/2010), kinaonyesha kuwa kuna uwezekano wa mamilioni ya watu kujiunga nasi katika ibada ya Yehova. Tunafurahi kama nini kwamba Yehova bado hajauharibu ulimwengu huu mwovu! Kwa sasa, upendo wetu unatusaidia kuendelea kuvumilia.—2 The. 3:5.
Makusanyiko ya Wilaya, “Kaa Karibu na Yehova!” ya mwaka wa 2010 yaliimarisha uhusiano wetu pamoja na Baba yetu wa mbinguni, Yehova. Mengi ya makusanyiko hayo yalifanywa kotekote ulimwenguni. Maneno haya ya mtunga-zaburi ni ya kweli kabisa: “Wenye furaha ni watu ambao Mungu wao ni Yehova!” (Zab. 144:15) Hata hali ziwe namna gani wakati ujao, tuna uhakika kuwa ikiwa Yehova yuko upande wetu, hatupaswi kuogopa chochote. (Zab. 23:4) Hivi karibuni, Yehova ‘atazivunja kazi za Ibilisi’ kupitia Mwana wake. (1 Yoh. 3:8) Kwa kweli, tunatazamia siku hiyo kwa hamu! Lakini wakati huu, tuna kazi nyingi sana ya kufanya.—1 Kor. 15:58.
Muwe na hakika kwamba sikuzote tunawataja katika sala zetu “bila kuacha.” (Rom. 1:9) Na “[mjitunze] katika upendo wa Mungu, huku mkiingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo kwa kutazamia uzima wa milele.”—Yuda 21.
Tunawapenda nyote!
Ndugu zenu,
Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova