Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • bt sura 11 kur. 85-92
  • “Kujawa na Shangwe na Roho Takatifu”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Kujawa na Shangwe na Roho Takatifu”
  • “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Wawekeni kando kwa Ajili ya Kazi’ (Mdo. 13:1-12)
  • ‘Neno la Kitia Moyo’ (Mdo. 13:13-43)
  • “Tunawageukia Mataifa” (Mdo. 13:44-52)
  • Barnaba Yule “Mwana wa Faraja”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Kigezo Chenye Kupuliziwa Roho cha Kazi ya Mishonari ya Kikristo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Watu wa Yehova Waimarishwa Katika Imani
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • “Wakizungumza kwa Ujasiri kwa Mamlaka ya Yehova”
    “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
bt sura 11 kur. 85-92

SURA YA 11

“Kujawa na Shangwe na Roho Takatifu”

Paulo anatuwekea mfano mzuri wa kushughulika na watu wakali, wasiotaka kusikiliza

Matendo 13:1-52

1, 2. Safari ya Barnaba na Sauli ina tofauti gani na zile safari nyingine za umishonari, na safari hiyo itasaidiaje kutimiza andiko la Matendo 1:8?

NI SIKU ya shangwe sana katika kutaniko la Antiokia. Kati ya manabii na walimu wote, Barnaba na Sauli ndio waliochaguliwa na roho takatifu kwenda kutangaza habari njema katika sehemu za mbali.a (Mdo. 13:1, 2) Ni kweli kwamba wanaume wanaostahili walitumwa wakati uliopita. Hata hivyo, wakati huo wamishonari hao walienda maeneo ambayo Ukristo ulikuwa umetia mizizi. (Mdo. 8:14; 11:22) Sasa, Barnaba na Sauli—pamoja na Yohana Marko, atakayewahudumia—wanatumwa nchi ambazo watu wengi hawajasikia kamwe habari njema.

2 Miaka 14 hivi iliyopita, Yesu aliwaambia wafuasi wake: “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, katika Yudea yote na Samaria, na mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Kuwekwa rasmi kwa Barnaba na Sauli kuwa wamishonari kutachangia sana kutimizwa kwa unabii huo wa Yesu!b

‘Wawekeni kando kwa Ajili ya Kazi’ (Mdo. 13:1-12)

3. Kwa nini haikuwa rahisi kusafiri katika karne ya kwanza?

3 Kuna maendeleo mengi sana katika ulimwengu wa leo. Kwa muda wa saa moja au mbili, watu wanaweza kusafiri mbali sana kwa kutumia magari na ndege. Hali hii ni tofauti na ile ya karne ya kwanza W.K. Siku hizo, watu walitembea kwa miguu katika barabara mbaya. Kwa siku nzima mtu angeweza kusafiri kilomita 30 hivi, na safari hiyo ilikuwa yenye kuchosha sana.c Ingawa Barnaba na Sauli walitazamia kwa hamu kwenda kwenye mgawo wao, bila shaka walijua kwamba watalazimika kufanya jitihada nyingi na kujinyima mengi.​—Mt. 16:24.

SAFARI KATIKA SIKU ZA MITUME

Zamani, kusafiri kwa kutumia barabara kulichukua muda mrefu, kulichosha, na kugharimu pesa nyingi kuliko kusafiri kwa mashua. Hata hivyo, ili kufika sehemu nyingi, njia pekee ilikuwa kutembea kwa miguu.

Msafiri angeweza kutembea kilomita 30 hivi kwa siku. Angekumbana na hali ngumu kama vile jua kali, mvua, baridi, au kushambuliwa na wezi. Mtume Paulo alisema kwamba aliposafiri, ‘mara nyingi alikabili hatari za kutokana na mito, hatari za kutokana na wezi.’​—2 Kor. 11:26.

Milki ya Roma ilikuwa na barabara nyingi nzuri za mawe. Kando ya barabara kuu, kulikuwa na nyumba za wageni kila baada ya umbali wa safari ya siku moja hivi kwa miguu. Karibu nusu ya safari, kulikuwa na hoteli ambazo mtu angeweza kupata chakula au mahitaji mengine ya msingi. Waandishi wa enzi hizo walitaja kwamba hoteli na nyumba hizo za wageni zilikuwa chafu, zilijaa watu, viroboto na zilikuwa na joto sana. Hazikuheshimika na zilipendwa na watu wanaotenda mambo mabaya. Mara nyingi, wahudumu wa sehemu hizo waliwaibia wasafiri na walitoa huduma za ukahaba.

Bila shaka Wakristo waliepuka sehemu hizo kadiri walivyoweza. Hata hivyo, waliposafiri kwenda sehemu ambazo hawakuwa na watu wa ukoo au marafiki, walilazimika kukaa humo.

4. (a) Barnaba na Sauli walichaguliwaje, na waabudu wenzao waliitikiaje? (b) Tunawezaje kuwaunga mkono wale wanaopewa mapendeleo ya kitheokrasi?

4 Lakini, kwa nini roho takatifu iliagiza moja kwa moja Barnaba na Sauli wawekwe kando ‘kwa ajili ya kazi’? (Mdo. 13:2) Biblia haisemi. Hata hivyo, tunajua kwamba roho takatifu ilielekeza wanaume hao wachaguliwe. Hatusomi popote kwamba manabii na walimu huko Antiokia walipinga uamuzi huo bali waliunga mkono kabisa uamuzi huo. Wazia jinsi Barnaba na Sauli walivyohisi wakati ndugu zao wa kiroho bila wivu wowote ‘walipofunga na kusali na kuweka mikono juu yao, na kuwaacha waende.’ (Mdo. 13:3) Sisi pia, tunapaswa kuwaunga mkono wale wanaopata mapendeleo ya kitheokrasi, kutia ndani wanaume wanaowekwa rasmi kuwa waangalizi katika kutaniko. Badala ya kuwaonea wivu, tunapaswa ‘kuwafikiria kwa njia inayozidi ile ya kawaida katika upendo kwa sababu ya kazi yao.’​—1 The. 5:13.

5. Eleza jinsi kisiwa cha Kipro kilivyohubiriwa.

5 Baada ya kutembea hadi Seleukia, bandari iliyokuwa karibu na Antiokia, Barnaba na Sauli walisafiri kwa mashua hadi kisiwa cha Kipro, umbali wa kilomita 200 hivi.d Kwa kuwa alikuwa mzaliwa wa Kipro, bila shaka Barnaba alikuwa na hamu kubwa ya kutangaza habari njema katika eneo la nyumbani kwao. Walipofika Salami, jiji lililokuwa kwenye ufuo wa mashariki wa kisiwa hicho, wanaume hao hawakupoteza wakati wowote. Mara moja, “wakaanza kulitangaza neno la Mungu katika masinagogi ya Wayahudi.”e (Mdo. 13:5) Barnaba na Sauli walisafiri kutoka upande mmoja hadi upande wa pili wa Kipro, wakihubiri katika majiji makubwa yaliyokuwa njiani. Ikitegemea barabara waliyopitia, huenda wamishonari hao walitembea kilomita 160 hivi!

MASINAGOGI YA WAYAHUDI

Neno “sinagogi” linamaanisha “kukusanya pamoja.” Mwanzoni, neno hilo lilimaanisha kusanyiko au kutaniko la Wayahudi na baadaye likapata maana mpya yaani mahali au jengo lililotumiwa kwa ajili ya kusanyiko hilo.

Inaaminika kwamba masinagogi yalianza kutumiwa wakati wa ile miaka 70 Wayahudi walipokuwa uhamishoni Babiloni au muda mfupi baada ya kutoka huko. Masinagogi yalikuwa mahali pa kutoa elimu, kuabudu, kusoma na kufafanua Maandiko, na kuchochea watu kiroho. Katika karne ya kwanza W.K., kila mji katika maeneo ya Palestina ulikuwa na sinagogi. Majiji makubwa, kama Yerusalemu, yalikuwa na masinagogi kadhaa.

Hata hivyo, si Wayahudi wote waliorudi Palestina baada ya uhamisho wa Babiloni. Wengi walihamia nchi nyingine ili kufanya biashara. Kufikia karne ya tano hivi K.W.K., Wayahudi walikuwa wakiishi katika wilaya zote 127 za Milki ya Uajemi. (Esta 1:1; 3:8) Baada ya muda, wakaanza kuishi katika majiji yaliyozunguka Bahari ya Mediterania. Wayahudi hao walioishi katika maeneo hayo wakaanza kujenga masinagogi.

Katika masinagogi, Sheria ilisomwa na kufafanuliwa kila Sabato. Kulikuwa na jukwaa la kusomea lililozungukwa na viti katika pande tatu. Mwanamume yeyote Myahudi aliyekuwa mwamini angeweza kusoma, kuhubiri, au kuwahimiza wengine katika sinagogi.

6, 7. (a) Sergio Paulo ni nani, na kwa nini Bar-Yesu alijaribu kumzuia asisikilize habari njema? (b) Sauli alishughulikiaje upinzani wa Bar-Yesu?

6 Katika karne ya kwanza, ibada ya uwongo ilikuwa imeenea sana Kipro. Hilo lilionekana wazi Barnaba na Sauli walipofika Pafo, kwenye ufuo wa magharibi wa kisiwa hicho. Huko walikutana “na mwanamume Myahudi aliyeitwa Bar-Yesu, ambaye alikuwa mlozi na nabii wa uwongo, [naye] alikuwa pamoja na liwali Sergio Paulo, mwanamume mwenye akili.”f Katika karne ya kwanza, Waroma wengi wenye kuheshimika—hata ‘wanaume wenye akili,’ kama Sergio Paulo—waliwaendea walozi au wanajimu kutafuta msaada wa kufanya maamuzi mazito. Hata hivyo, Sergio Paulo alivutiwa sana na ujumbe wa Ufalme naye “alitamani kulisikia neno la Mungu.” Hilo halikumpendeza Bar-Yesu, ambaye jina lake la cheo lilikuwa Elima, yaani, “Mlozi.”​—Mdo. 13:6-8.

7 Bar-Yesu aliupinga ujumbe wa Ufalme. Njia pekee ambayo angeweza kutumia ili kudumisha cheo chake kikubwa akiwa mshauri wa Sergio Paulo ilikuwa ni kwa “kumzuia yule liwali asiwe mwamini.” (Mdo. 13:8) Hata hivyo, Sauli hakumruhusu mlozi huyo amkengeushe Sergio Paulo. Alifanya nini? Masimulizi yanasema: “Sauli, aitwaye pia Paulo, akiwa amejaa roho takatifu, akamtazama kwa makini [Bar-Yesu] na kumwambia: “Ewe mtu uliyejaa kila aina ya upunjaji na kila aina ya ulaghai, wewe mwana wa Ibilisi, wewe adui wa kila jambo la uadilifu, je, hutaacha kuzipotosha njia za Yehova zilizo sawa? Tazama! mkono wa Yehova uko juu yako, nawe utakuwa kipofu, hutaona nuru ya jua kwa kipindi fulani.” Mara moja akaangukiwa na ukungu mzito na giza, naye akazunguka akitafuta mtu wa kumshika mkono ili amwongoze.”g Matokeo? “Yule liwali alipoona jambo lililotokea, akawa mwamini kwa sababu alistaajabishwa na fundisho la Yehova.”​—Mdo. 13:9-12.

Ndugu ameshika Biblia iliyofunguliwa, akitetea kweli mbele ya hakimu mahakamani.

Kama Paulo, tunaitetea kweli kwa ujasiri hata tukikabili upinzani

8. Tunawezaje kuiga ujasiri wa Paulo?

8 Paulo hakumwogopa Bar-Yesu. Vivyo hivyo, hatupaswi kuogopa wapinzani wanapojaribu kuvuruga imani ya wale wanaopendezwa na ujumbe wa Ufalme. Ni kweli kwamba maneno yetu yanapaswa kuwa “yenye neema sikuzote, yaliyokolezwa chumvi.” (Kol. 4:6) Hata hivyo, hatuwezi kuacha hali ya kiroho ya mtu anayependezwa iwe hatarini kwa sababu tu tunataka kuepuka ubishi. Wala hatupaswi kuogopa kufichua dini za uwongo kama za Bar-Yesu, ambazo zinaendelea ‘kupotosha njia za Yehova zilizo sawa.’ (Mdo. 13:10) Kama Paulo, na tuendelee kutangaza kweli kwa ujasiri na kuichochea mioyo ya watu wanyoofu. Ingawa huenda tusione waziwazi utegemezo wa Mungu, kama ilivyokuwa katika kisa cha Paulo, tuna uhakika kwamba Yehova atatumia roho yake takatifu kuwavuta watu wanaostahili kwenye ile kweli.​—Yoh. 6:44.

‘Neno la Kitia Moyo’ (Mdo. 13:13-43)

9. Paulo na Barnaba waliweka mfano gani mzuri unaoweza kuigwa na wale wanaosimamia kutaniko leo?

9 Inaonekana kulikuwa na badiliko fulani wanaume hao walipoondoka Pafo kuelekea Perga, pwani ya Asia Ndogo, umbali wa kilomita 250 hivi kupitia baharini. Katika Matendo 13:13 kikundi hicho, kinaitwa cha “Paulo na wenzake.” Inaonekana tangu wakati huo, Paulo ndiye aliyesimamia kikundi hicho. Hata hivyo, hakuna jambo lolote linaloonyesha kwamba Barnaba alianza kumwonea wivu Paulo. Badala yake, wanaume hao wawili waliendelea kumtumikia Mungu bega kwa bega. Paulo na Barnaba wanawawekea mfano mzuri wale wanaosimamia kutaniko leo. Badala ya kujitafutia makuu, Wakristo wanakumbuka maneno haya ya Yesu: “[Ninyi] nyote ni ndugu.” Pia alisema: “Yeyote anayejiinua atanyenyekezwa, na yeyote anayejinyenyekeza atainuliwa.”​—Mt. 23:8, 12.

10. Eleza jinsi safari ya kutoka Perga kuelekea Antiokia ya Pisidia ilivyokuwa.

10 Walipofika Perga, Yohana Marko aliwaacha Paulo na Barnaba, akarudi Yerusalemu. Haieleweki kwa nini aliondoka. Paulo na Barnaba waliendelea na safari kutoka Perga hadi Antiokia ya Pisidia, jiji lililokuwa katika wilaya ya Galatia. Safari hiyo haikuwa rahisi, kwa kuwa Antiokia ya Pisidia iko mita 1,100 juu ya usawa wa bahari. Mara nyingi njia za milimani zilikuwa na wanyang’anyi. Isitoshe, huenda Paulo alikuwa na matatizo ya afya pia.h

11, 12. Alipotoa hotuba katika sinagogi huko Antiokia ya Pisidia, Paulo alitumia njia gani ili kuwavutia wasikilizaji wake?

11 Wakiwa Antiokia ya Pisidia, Paulo na Barnaba waliingia katika sinagogi siku ya Sabato. Masimulizi hayo yanasema: “Baada ya kusoma hadharani Sheria na Manabii, maofisa wasimamizi wa sinagogi wakawatuma watu kwao, wakisema: ‘Wanaume, akina ndugu, ikiwa mna neno lolote la kuwatia moyo watu, lisemeni.’” (Mdo. 13:15) Basi Paulo akasimama na kuanza kuzungumza.

12 Paulo alianza hotuba yake kwa kusema: “Wanaume, Waisraeli nanyi wengine mnaomwogopa Mungu.” (Mdo. 13:16) Watu hao waliomsikiliza Paulo walikuwa Wayahudi na wageuzwa imani. Paulo alitumia njia gani ili kuwavutia watu hao ambao hawakutambua jukumu la Yesu katika kusudi la Mungu? Paulo alianza kwa kusimulia historia ya Wayahudi. Alieleza jinsi Yehova ‘alivyowainua watu hao walipokuwa wakiishi wakiwa wageni katika nchi ya Misri’ na jinsi ambavyo baada ya kuachiliwa huru, Mungu ‘aliwavumilia huko nyikani’ kwa miaka 40. Pia, Paulo alisimulia jinsi Waisraeli walivyomiliki Nchi ya Ahadi na jinsi ambavyo Yehova ‘aliwapa nchi yao iwe urithi wao.’ (Mdo. 13:17-19) Inasemekana kwamba Paulo alikuwa akirejelea Maandiko fulani yaliyokuwa yamesomwa kwa sauti muda mfupi uliopita kulingana na desturi za Sabato. Ikiwa ndivyo, huo ni mfano mzuri unaoonyesha kwamba Paulo alijua jinsi ya kuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote.”​—1 Kor. 9:22.

13. Tunaweza kufanya nini ili kuwavutia watu tunaowahubiria?

13 Sisi pia tunapaswa kujitahidi kuwavutia watu tunaowahubiria. Kwa mfano, kujua dini ya mtu kunaweza kutusaidia kuchagua habari zitakazompendeza. Pia, tunaweza kunukuu Maandiko ambayo huenda mtu huyo anajua. Huenda tukapata matokeo mazuri kwa kumwomba mtu huyo asome Biblia yake mwenyewe. Jitahidi kuchochea mioyo ya watu unaozungumza nao.

14. (a) Paulo alianza kuzungumzia habari njema kuhusu Yesu jinsi gani, naye alitoa onyo gani? (b) Umati ulifanya nini baada ya kusikia maneno ya Paulo?

14 Kisha, Paulo akazungumzia ukoo wa wafalme wa Israeli uliomtokeza “mwokozi, yaani, Yesu” ambaye alitayarishiwa njia na Yohana Mbatizaji. Halafu akaeleza jinsi Yesu alivyouawa na kufufuliwa. (Mdo. 13:20-37) “Acheni ijulikane kwenu,” Paulo akasema, “kwamba kupitia mtu huyo mnatangaziwa msamaha wa dhambi . . . kila mtu anayeamini anatangazwa kuwa bila hatia kupitia mtu huyu.” Naye akawaonya: “Jihadharini ili msipatwe na mambo haya yanayosemwa katika Manabii: ‘Tazameni, ninyi wenye dharau, na mshangae na kuangamia, kwa sababu ninafanya kazi fulani katika siku zenu, kazi ambayo hamtaiamini kamwe hata mtu yeyote akiwaeleza kirefu.’” Matokeo yalikuwa yenye kushangaza. Biblia inasema: “Watu wakawasihi wazungumzie mambo hayo Sabato iliyofuata.” Isitoshe, baada ya kusanyiko la sinagogi kumalizika, “Wayahudi wengi na wageuzwa imani waliomwabudu Mungu wakawafuata Paulo na Barnaba.”​—Mdo. 13:38-43.

“Tunawageukia Mataifa” (Mdo. 13:44-52)

15. Baada ya Paulo kutoa hotuba, ni nini kilichotokea Sabato iliyofuata?

15 Sabato iliyofuata, “karibu jiji lote” lilikusanyika ili kumsikiliza Paulo. Hilo halikuwafurahisha Wayahudi fulani, nao wakaanza “kupinga wakikufuru mambo ambayo Paulo alikuwa akisema.” Paulo na Barnaba wakawaambia hivi kwa ujasiri: “Ilikuwa lazima neno la Mungu lihubiriwe kwenu kwanza. Kwa kuwa mnalikataa na kujiona hamstahili uzima wa milele, tazameni! tunawageukia mataifa. Kwa maana Yehova ametuamuru kwa maneno haya: ‘Nimewachagua muwe nuru ya mataifa, na muwe wokovu mpaka miisho ya dunia.’”​—Mdo. 13:44-47; Isa. 49:6.

Paulo na Barnaba wakitupwa nje ya jiji la Antiokia ya Pisidia na wapinzani wenye hasira.

“Wakaanza kuwatesa Paulo na Barnaba . . .  Nao wanafunzi wakaendelea kujawa na shangwe na roho takatifu.”—Matendo 13:50-52

16. Wayahudi walifanya nini waliposikia maneno makali ya wamishonari hao, nao Paulo na Barnaba walifanya nini upinzani ulipotokea?

16 Watu wa Mataifa waliokuwa wakisikiliza walishangilia, na “wote waliokuwa na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele wakawa waamini.” (Mdo. 13:48) Baada ya muda mfupi, neno la Yehova likaenea nchini kote. Hata hivyo, Wayahudi waliitikia kwa njia tofauti. Wamishonari hao waliwaambia kwamba ingawa walikuwa wa kwanza kutangaziwa Neno la Mungu, walimkataa Masihi na hivyo hawangeweza kuepuka hukumu kali ya Mungu. Wayahudi hao wakawachochea wanawake mashuhuri na wakuu wa jiji hilo, “nao wakaanza kuwatesa Paulo na Barnaba na kuwatupa nje ya mipaka yao.” Paulo na Barnaba walifanya nini? “Wakawakung’utia mavumbi yaliyokuwa kwenye miguu yao na kwenda Ikoniamu.” Je, huo ndio mwisho wa Ukristo katika Antiokia ya Pisidia? Hapana! Wanafunzi waliobaki “wakaendelea kujawa na shangwe na roho takatifu.”​—Mdo. 13:50-52.

17-19. Tunawezaje kuiga mfano mzuri uliowekwa na Paulo na Barnaba, na ni kwa njia gani kufanya hivyo kutatuletea shangwe?

17 Tunaweza kujifunza jambo muhimu kutokana na hatua ambayo wanaume hao walichukua upinzani ulipotokea. Hatuachi kamwe kuhubiri, hata wakati watu mashuhuri ulimwenguni wanapojaribu kutuzuia tusitangaze ujumbe wetu. Pia, kumbuka kwamba watu wa Antiokia walipoukataa ujumbe, Paulo na Barnaba ‘walikung’uta mavumbi kutoka miguuni mwao.’ Hawakufanya hivyo kwa sababu ya hasira, bali walitaka kuonyesha kwamba hawana lawama. Wamishonari hao walitambua kwamba hawangeweza kuwalazimisha watu wakubali ujumbe wao. Hata hivyo, watu hao hawangeweza kuwazuia kuhubiri. Paulo na Barnaba hawakupunguza bidii yao badala yake walienda Ikoniamu, na kuendelea kuhubiri!

18 Namna gani wanafunzi waliobaki Antiokia? Ni kweli kwamba lilikuwa eneo gumu. Hata hivyo, shangwe yao haikutegemea matokeo waliyopata. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!” (Luka 11:28) Hivyo ndivyo wanafunzi waliobaki Antiokia ya Pisidia walivyofanya.

19 Kama walivyofanya Paulo na Barnaba, na tukumbuke kwamba jukumu letu ni kuhubiri habari njema, iwe watu watasikiliza au la. Hata ikiwa watu tunaowahubiria hawapendezwi, tusisahau jinsi hali ilivyokuwa katika karne ya kwanza. Tukiithamini kweli tuliyo nayo, na kukubali kuongozwa na roho takatifu, sisi pia tunaweza kuwa na shangwe, hata tukikabili upinzani.​—Gal. 5:18, 22.

BARNABA—“MWANA WA FARAJA”

Yosefu, Mlawi, mzaliwa wa Kipro, alijulikana sana katika kutaniko la Yerusalemu. Mitume walimpatia jina lingine, lililopatana na utu wake. Walimwita Barnaba, yaani, “Mwana wa Faraja.” (Mdo. 4:36) Barnaba alipoona waamini wenzake wana uhitaji fulani, hakusita kuwasaidia.

Barnaba akitoa mchango wa mifuko miwili ya sarafu.

Siku ya Pentekoste, mwaka wa 33 W.K., wanafunzi wapya 3,000 walibatizwa. Inawezekana wengi kati yao walisafiri kwenda Yerusalemu kwa ajili ya sherehe hiyo na hawakupanga kukaa katika jiji hilo kwa muda mrefu. Kutaniko lilihitaji pesa na vitu vingine ili kuhudumia umati huo. Kwa hiyo, Barnaba akauza sehemu ya shamba na kuwaletea mitume mchango wa pesa.​—Mdo. 4:32-37.

Barnaba alikuwa mwangalizi Mkristo mkomavu, na sikuzote alikuwa tayari kuwasaidia wengine. Wanafunzi wengine wote walipomwogopa Sauli wa Tarso aliyejulikana kuwa mtesaji, Barnaba alimsaidia. (Mdo. 9:26, 27) Barnaba alikubali kwa unyenyekevu Paulo alipompa shauri zito yeye na Petro kuhusu jinsi Wakristo Wayahudi na wa Mataifa wanavyopaswa kujiendesha. (Gal. 2:9, 11-14) Mifano hiyo michache inaonyesha kwamba kwa kweli Barnaba aliishi kulingana na jina lake, yaani “Mwana wa Faraja.”

a Ona Sanduku lenye kichwa “Barnaba—‘Mwana wa Faraja.’”

b Kufikia wakati huo, makutaniko yalikuwa yameenea sehemu za mbali sana kama vile Antiokia ya Siria—lililokuwa kilomita 550 hivi kaskazini mwa Yerusalemu.

c Ona sanduku lenye kichwa “safari katika siku za mitume.”

d Katika karne ya kwanza, meli zingeweza kusafiri kilomita 150 hivi kwa siku ikitegemea upepo. Safari hiyo ingechukua muda mrefu zaidi ikiwa hali ya hewa ni mbaya.

e Ona Sanduku lenye kichwa “Masinagogi ya Wayahudi.”

f Kisiwa cha Kipro kilikuwa chini ya utawala wa Roma. Mkuu wa kisiwa hicho alikuwa liwali.

g Tangu wakati huo na kuendelea, Sauli alianza kuitwa Paulo. Watu fulani husema kwamba alijipa jina hilo la Kiroma kwa heshima ya Sergio Paulo. Hata hivyo, kwa kuwa aliendelea kuitwa Paulo hata alipoondoka Kipro, lazima kulikuwa na sababu nyingine, kwamba Paulo, “mtume wa mataifa,” aliamua kwamba tangu wakati huo na kuendelea atatumia jina lake la Kiroma. Huenda pia alitumia jina Paulo kwa sababu matamshi ya Kigiriki ya jina lake la Kiebrania, Sauli, yanafanana sana na neno la Kigiriki lenye maana mbaya.​—Rom. 11:13.

h Miaka kadhaa baadaye Paulo aliwaandikia barua Wagalatia. Katika barua hiyo, Paulo alisema: “kwa sababu ya ugonjwa wa kimwili kwamba nilipata nafasi yangu ya kwanza ya kuwatangazia habari njema.”​—Gal. 4:13.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki