Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • yb11 kur. 39-72
  • Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote
  • 2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
2011 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
yb11 kur. 39-72

Kuhubiri na Kufundisha Duniani Kote

HUENDA maneno ya Yesu yaliwashangaza wanafunzi wake wa karne ya kwanza. Alitabiri kwamba wangechukiwa na mataifa yote—wangeuawa na kutiwa katika dhiki. Isitoshe, wengi wangekwazika na kusalitiwa. Lakini Yesu akasema kwamba habari njema itahubiriwa katika dunia yote. (Mt. 24:9-14) Je, kazi hiyo ya kuhubiri ingefanikiwa licha ya upinzani ulimwenguni pote? Utapata jibu la swali hilo lenye kuchochea fikira katika kurasa zinazofuata.

Jumla Kuu za 2010

Ofisi za Tawi za Mashahidi wa Yehova: 116

Idadi ya Nchi Zinazoripoti: 236

Idadi ya Makutaniko: 107,210

Waliohudhuria Ukumbusho Ulimwenguni Pote: 18,706,895

Waliokula Mkate na Kunywa Divai Ulimwenguni Pote: 11,202

Kilele cha Wahubiri wa Ufalme: 7,508,050

Wastani wa Wahubiri Watendaji Kila Mwezi: 7,224,930

Asilimia ya Ongezeko Kupita 2009: 2.5

Idadi ya Waliobatizwa: 294,368

Wastani wa Mapainia Wasaidizi Kila Mwezi: 287,960

Wastani wa Mapainia Kila Mwezi: 844,901

Jumla ya Saa Zilizotumiwa Shambani: 1,604,764,248

Wastani wa Mafunzo ya Biblia Kila Mwezi: 8,058,359

Katika mwaka wa utumishi wa 2010, Mashahidi wa Yehova walitumia zaidi ya dola milioni 155 za Marekani kwa ajili ya mapainia wa pekee, wamishonari, na waangalizi wanaosafiri katika kazi yao ya kuhubiri.

◼ Ulimwenguni pote kuna wahudumu 20,062 waliowekwa rasmi kufanya kazi katika ofisi za tawi. Wote hao ni sehemu ya Kikundi cha Ulimwenguni Pote cha Watumishi wa Pekee wa Wakati Wote cha Mashahidi wa Yehova.

AFRIKA

IDADI YA NCHI 57

IDADI YA WATU 888,219,101

IDADI YA WAHUBIRI 1,222,352

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 2,596,614

KIKUNDI CHATAFUTA KWELI. Katika kijiji kidogo huko Madagaska, watu 80 waliamua kutoka katika Kanisa kubwa zaidi la Kiprotestanti nchini humo. Walijenga kanisa lao wenyewe na kuanza kutafuta dini ya kweli, wakichunguza kila dini iliyokuwa katika eneo hilo. Walikata kauli kwamba Wakatoliki hawakujifunza Biblia na kwamba kulikuwa na magombano katika Kanisa la Kilutheri. Walihisi kwamba Waprotestanti hawakufundisha kweli, na waumini wa Kanisa la Sabato walikuwa na miiko mingi. Kisha wakamfikia mmoja wa ndugu zetu na kumwomba awafundishe Biblia. Ndugu huyo alikubali mara moja.

Wahubiri wachache walipanga kuwatembelea watu hao waliopendezwa. Ndugu hao walipata watu 26 wamekusanyika ndani ya kanisa walilojenga, wakiwa tayari kusikiliza habari za Biblia. Wakitumia sura ya 15 ya kitabu Biblia Inafundisha, ndugu hao waliwafafanulia jinsi ya kupata dini inayokubaliwa na Mungu. Watu hao waliridhishwa na ufafanuzi huo. Ndugu hao walipowatembelea tena, walipata watu 73. Na katika ziara yao ya tatu, kulikuwa na watu 142!

UJUMBE WA SIMU ULIOTUMWA KWA MTU KIMAKOSA. Ili kumtia moyo mwanafunzi wake wa Biblia, Shahidi anayeitwa Menen, anayeishi Ethiopia, alimtumia andiko la mwaka wa 2009, kupitia simu yake ya mkononi. Hata hivyo, alibonyeza nambari fulani kimakosa, na ujumbe huo ukamfikia mtu mwingine. Mwanamke aliyepokea ujumbe huo aliusoma mara kadhaa: “‘Toa ushahidi kamili kuhusu habari njema.’—Matendo 20:24, NW.” Kwa sababu mwanamke huyo alimpenda Mungu, alikubaliana na ujumbe huo ingawa hakujua jinsi ambavyo angeutii. Pia alitatanishwa na herufi “NW” [Tafsiri ya Ulimwengu Mpya] mwishoni mwa andiko hilo. Majuma kadhaa baadaye, alikuwa bado anafikiria kuhusu andiko hilo. Mwishowe alimpigia simu yule aliyemtumia ujumbe huo. Dada huyo alishangaa kwamba ujumbe wake ulimfikia kimakosa, lakini akatumia nafasi hiyo kujibu swali la mwanamke huyo. Funzo la Biblia lilianzishwa, na linaongozwa mara mbili kwa juma.

MAPAINIA WENZI WACHANGA. Persis, anayeishi Kamerun, alianza kutumika akiwa mhubiri ambaye hajabatizwa alipokuwa na umri wa miaka sita. Ripoti yake ya kwanza ilionyesha mafunzo kumi ya Biblia. Mwandishi wa kutaniko alifikiri kuwa amekosea. Alipomwuliza, Persis alimwambia kwamba kwa kweli alikuwa na mafunzo kumi. Alimwuliza hivi pia: “Unahesabu saa jinsi gani kwa kuwa huna saa ya mkononi?” Alimjibu kwamba anajua kipindi cha mapumziko shuleni huwa ni saa moja. Alianza kuhubiri kipindi hicho kilipoanza na kumaliza kengele ilipopigwa. Kuhubiri kwake kwa ujasiri kuliwavutia mama na binamu yake ambao baadaye walikuja kuwa wahubiri ambao hawajabatizwa. Sasa akiwa na umri wa miaka kumi, Persis amebatizwa na anatumika akiwa painia-msaidizi akiwa bado shuleni. Tayari rafiki yake, Aasy, mwenye umri wa miaka minane ni mhubiri ambaye hajabatizwa. Mwanafunzi mmoja wa Biblia alisema hivi kuwahusu: “Kwenye mikutano, nilifurahi sana kuona watoto wakisalimu kila mtu, hasa walio wazee, kabla ya kwenda kuketi na wazazi wao. Sikuwahi kuona hilo katika kanisa letu. Ninajua kwamba watoto wanaolelewa hivyo watakuwa watu wazuri katika jamii wakati ujao.”

AMERIKA

IDADI YA NCHI 55

IDADI YA WATU 918,834,998

IDADI YA WAHUBIRI 3,673,750

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 3,967,184

HAKUBISHA MLANGO. Miriam, anayeishi nchini Bolivia, alisali kwa Mungu kwa juma moja. Sala yake ilisema hivi: “Tafadhali nisaidie nikufahamu, lakini sitaki msaada wa Mashahidi wa Yehova. Sitaki wabishe mlango wangu.”

Baadaye katika juma hilo alipigiwa simu. Painia wa pekee anayeitwa Candy alimwuliza Miriam ikiwa anaweza kumletea magazeti yetu baada ya saa moja. Alikubali. Saa moja baadaye Candy alikuwa mlangoni mwake. Miriam alifungua mlango huo ghafula na kumwamuru Candy aingie na kuketi. Kisha Miriam akaanza kutembea huku na huku akitikisa kichwa chake akiwa amekasirika. Candy akamwuliza ana tatizo gani. “Ninashangaa!” Miriam akamwambia. “Kwa zaidi ya juma moja, nimekuwa nikisali kwa Mungu aniongoze na kunielekeza, lakini nilimweleza waziwazi katika sala kwamba sitaki msaada wa Mashahidi wa Yehova ambao wanabisha mlango wangu kila wakati! Kisha ukapiga simu badala ya kubisha mlango! Tangu uliponipigia simu saa moja iliyopita, nimekuwa nikisali kwa Mungu kwamba usije kunitembelea. Lakini umekuja! Ninashangaa! Ni wazi kwamba anataka ninyi watu, ninyi Mashahidi wa Yehova, mnisaidie.” Funzo lilianzishwa mara moja.

WALIMWACHA AKIWA KARIBU KUFA. Zamani Pasensi alikuwa kiongozi maarufu wa kijiji, au kapiten, nchini Suriname na alikuwa mshiriki wa karibu wa granman, chifu, au mfalme, wa eneo lote la mto katika eneo la vijijini. Pasensi alitetea sana tamaduni za kienyeji. Aliwapinga Mashahidi wa Yehova kwa sababu aliwaona kuwa tisho kwa mambo ya kitamaduni.

Baada ya muda, kijana fulani akadai kwamba ana uwezo wa kuwatambua wanakijiji waliokuwa wachawi. Wafuasi wake wengi walimfuata kwenye mto wakitumia mitumbwi, na kuwapiga wale walioshtakiwa na kuchukua mali yao yote. Kijana huyo alilipwa pesa nyingi sana ili “awatakase” wale walioshtakiwa kuwa na roho mwovu. Pasensi alikuwa mmoja kati ya wengi walioshtakiwa kimakosa, naye alipigwa na kuachwa akiwa karibu kufa. Hata rafiki yake, yule granman, hangeweza kumsaidia, kwa kuwa aliogopa uhai na sifa yake ilikuwa hatarini iwapo angemsaidia mtu aliyeshtakiwa kuwa mchawi. Marafiki na watu wa ukoo hawakuruhusiwa kumsaidia. Hata hivyo, mwana-mkwe wa Pasensi alijipa ujasiri na kumpeleka katika kijiji kilichokuwa na Mashahidi wengi wa Yehova. Akina ndugu walizungumzia jambo hilo na ingawa walijua kwamba walikuwa wakijihatarisha, waliaamua kumsaidia. Walipanga kwamba Pasensi apelekwe kwa mtumbwi hadi kijiji cha karibu ambako kuna ndugu anayesimamia uwanja fulani wa ndege. Kutoka hapo, mpinzani huyo wa zamani alisafirishwa kwa ndege hadi jijini ili atibiwe.

Pasensi, alipopona majeraha yake, alichochewa sana na upendo alioonyeshwa na watu ambao hapo zamani aliwapinga. Alianza kujifunza Biblia na akabatizwa Desemba 2009. Sasa Pasensi ni mhubiri mwenye bidii wa habari njema, na ingawa ana umri wa miaka 80, alifanya upainia msaidizi mnamo Aprili 2010.

ALIFIKIRI KWAMBA ANAIJUA BIBLIA. Eric, mwanamume aliyekuwa amefuga ndevu alienda kwenye mkutano wa kutaniko huko Marekani akiwa na Biblia mkononi. Ndugu mmoja alipomsalimu, Eric alianza kuuliza maswali kuhusu imani yetu. Alikataa kuchukua kitabu Biblia Inafundisha, akipendelea kutumia Biblia peke yake. Alikuwa na ratiba ya kusoma kurasa 20 za Biblia kila siku, na alikuwa ameisoma Biblia yote mara nyingi sana hivi kwamba hangeweza kuzihesabu. Baada ya mkutano, aliendeleza mazungumzo pamoja na ndugu huyo kwa zaidi ya saa tatu. Mwishowe, Eric alisema, “Nimeudhika sana.” Ndugu huyo alipomwuliza sababu, Eric alijibu hivi: “Nilikuwa na uhakika kwamba ninayafahamu Maandiko vizuri. Hata hivyo, baada ya kuwatembelea nimetambua kwamba siyafahamu hata kidogo.” Kisha akakubali kitabu Biblia Inafundisha.

Siku iliyofuata, walijifunza kwa mara ya kwanza. Eric alikuwa amekesha usiku uliotangulia akisoma sura kumi za kwanza za kitabu Biblia Inafundisha. Alifikia mkataa gani? “Hatimaye nimeipata kweli!” Kwa siku tano kila juma, walijifunza kwa saa tatu au nne kwa siku. Alianza kutayarisha na kuhudhuria mikutano yote pamoja na familia yake yote. Baada ya juma moja, alikuwa ameandika barua za kujitenga na makanisa matatu, akanyoa ndevu zake, na akaazimia kwamba hatasherehekea sikukuu. Katika majuma mawili alijiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na katika majuma manne alikuwa mhubiri ambaye hajabatizwa. Alibatizwa mnamo Aprili 2010, miezi sita baada ya kukutana na Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza!

ABATIZWA AKIWA NA UMRI WA MIAKA SABA. Paola, anayeishi magharibi mwa Mexico, anaishi na babu na nyanya yake. Nyanya yake alianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova Paola alipokuwa na umri wa miaka mitano. Paola alisikiliza funzo hilo na kweli ikaingia katika moyo wake mchanga. Ingawa nyanya yake hakufanya maendeleo, Paola alianza kuhudhuria mikutano akiwa peke yake. Angemwomba babu au nyanya amsaidie kuvaa na kuvuka barabara ili afike kwenye Jumba la Ufalme.

Alipojifunza kusoma na kuandika, Paola alijiandikisha kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na akawa mhubiri. Kwa sababu alimpenda Yehova, alibatizwa akiwa na umri wa miaka saba. Alipoulizwa kwa nini yeye anahudhuria mikutano na kuhubiri kwa bidii ingawa haungwi mkono na watu wa familia, Paola ambaye sasa ana umri wa miaka kumi, alijibu hivi: “Mimi hufurahia sana hotuba kwa sababu zinanitia moyo niendelee kujifunza Biblia na kuepuka matatizo. Na ninahubiri kwa sababu ninataka kuwafundisha watu yale ambayo Yehova atawafanyia wakati ujao na kwa sababu Biblia inaweza kuwafanya wawe na furaha hata sasa.”

KUWAHUBIRIA WANAOPIGA SIMU KIMAKOSA. Katika Jamhuri ya Dominika, dada mmoja alikuwa akipigiwa simu nyingi kimakosa, nazo zilivuruga sana kazi yake. Baada ya siku chache, alijiambia, ‘Ninaweza kutumia nafasi hiyo kuhubiri.’ Alifanya hivyo jinsi gani? Alipopokea simu hizo kimakosa, alisema anasikitika kwamba mtu huyo amepiga namba yake kimakosa, lakini akaongezea hivi, “Acha nitumie nafasi hii kukuuliza, Je, leo umesoma Biblia?” Ingawa watu kadhaa walikata simu, wengine walijibu kwamba hawajasoma Biblia. Kisha aliwauliza, “Je, unajua kwa nini ni muhimu sana kufanya hivyo?” Ili awape jibu la Kimaandiko, aliwasomea Zaburi 1:1-3. Ofisa mmoja wa serikali alizungumza kwa muda mrefu na dada huyo na kumwambia kwamba yeye hana Biblia. Mipango ilifanywa ili apelekewe Biblia na vichapo fulani vya Biblia. Majuma mawili baadaye alipiga simu ili kumshukuru dada huyo kwa upendezi wake na kwa vichapo hivyo.

Alipopigiwa simu nyingine kimakosa, msichana mmoja alimwuliza dada yetu, “Je, wewe ni Shahidi wa Yehova?” Aliposema kwamba yeye ni Shahidi, msichana huyo alianza kulia, akaeleza kwamba yeye alikuwa mhubiri asiyetenda. Dada yetu alimtia moyo na akapanga ili mtu amsaidie kiroho. Sasa msichana huyo ni mhubiri anayetenda.

ASIA NA MASHARIKI YA KATI

IDADI YA NCHI 47

IDADI YA WATU 4,587,021,833

IDADI YA WAHUBIRI 652,251

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 601,306

“MWANAMKE MSAMARIA.” Ilikuwa siku yenye joto kali wakati wa kiangazi huko Kazakhstan. Mapainia wawili, ndugu na dada, walikuwa wakihubiri na wakamwona mwanamke akiteka maji katika kisima. Ndugu alimwomba maji ya kunywa, na alipokuwa akinywa, dada akamhubiria mwanamke huyo. Mwanamke huyo alionyesha upendezi na akawakaribisha mapainia hao nyumbani kwake ili aweze kujifunza mengi kuhusu yale waliyokuwa wakimwambia. Walizungumza kwa muda, na mapainia hao wakamwachia vichapo vya Biblia. Dada huyo aliahidi kwamba atarudi baada ya siku mbili.

Kama alivyoahidi, dada huyo alirudi, akiwa pamoja na mama yake, ambaye pia ni Shahidi. Walimpata mwanamke huyo akiwasubiri nje ya nyumba yake, akiwa ameshika vichapo alivyokuwa amemwachia. Alimpa dada huyo vichapo hivyo na kumwambia: “Vichapo hivi ni vya Mashahidi wa Yehova! Dini yenu ni ya Warusi!”

Mama ya dada huyo alimwuliza mwanamke huyo ikiwa anaweza kumsomea mstari kutoka katika Maandiko kabla ya kuondoka. Kwa kuwa alitaka kumwonyesha mwanamke huyo jina la Mungu katika Maandiko, alifungua Kutoka 3:15 na kusoma: “Yehova Mungu wa mababu zenu, Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaka na Mungu wa Yakobo, amenituma kwenu.” Akina dada hao walishangaa mwanamke huyo alipowakaribisha waingie ndani ya nyumba. Ni nini kilichomfanya abadili maoni yake upesi hivyo? Babu za mwanamke huyo waliitwa Abrahamu, Isaka, na Yakobo. Alijiambia kwamba ikiwa Yehova alikuwa ndiye Mungu wa mababu zake, basi hapaswi kuwafukuza Mashahidi wake. Walipomtembelea mara nyingine, walianzisha funzo la Biblia. Alitaka sana kujifunza kweli hivi kwamba funzo likaongozwa mara mbili kwa juma. Licha ya upinzani kutoka kwa wana wake, aliendelea kukua kiroho, na sasa yeye ni mhubiri ambaye hajabatizwa. Isitoshe, binti-mkwe wake na mama ya binti-mkwe huyo wanajifunza Biblia na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Kwa kuwa njia aliyopatikana mara ya kwanza inafanana na ile ya simulizi la Yohana 4:3-15, anajulikana kutanikoni kama “mwanamke Msamaria.”

“NINA MASWALI KADHAA.” Dada mmoja mwenye umri mkubwa nchini Saiprasi, ambaye ni painia, anaandika hivi: “Jumatano (Siku ya 3) moja asubuhi, nilikuwa ninajisikia vibaya, lakini badala ya kubaki nyumbani, nilitaka sana kuhubiri barabarani. Kwa hiyo, nilisali kwa Yehova nikimwomba ikiwa anaweza kunitumia mtu aliyekuwa na muda wa kuja aketi kando yangu kwenye benchi, ili nianzishe funzo la Biblia. Punde si punde kijana mmoja kutoka Nepal akaja. Nilikuwa nimeshika magazeti mkononi mwangu, na hata kabla ya kuanza kuzungumza naye, aliniuliza magazeti hayo yanahusu nini. Nilipomwambia kwamba yalitegemea Biblia, aliniambia hivi: ‘Mama, kwa kuwa nina muda fulani, je, ninaweza kuketi kando yako? Nina maswali kadhaa kuhusu Biblia ambayo ningependa kukuuliza.’

“Bila shaka, nilikubali kwa kuwa hilo ndilo nililokuwa nimemwomba Yehova! Mwanamume huyo akasema: ‘Swali langu la kwanza ni, Biblia inafundisha nini hasa?’ Nilishangaa sana hivi kwamba singeweza kuzungumza! Nilitoa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kutoka mfukoni na kumwonyesha. Alitazama kitabu hicho, akanitazama, na kuuliza, ‘Si kichwa cha kitabu hiki kinapatana kabisa na swali nililotoka tu kukuuliza?’ Kwa hiyo nikaanzisha funzo la Biblia papo hapo kwenye benchi bustanini! Sasa anajifunza Biblia kwa ukawaida na pia anahudhuria mikutano kwa ukawaida, na amesema kwamba angependa kujiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Nimejionea umuhimu wa kumtegemea Yehova kikamili ili anipe nguvu na uongozi ninaposhiriki katika huduma ya Kikristo, hata ingawa nyakati nyingine mimi hujihisi nikiwa nimechoka kimwili.”

BABU AMFUNDISHA ALIYEMWUA MJUKUU WAKE. Mjukuu wa Miguel aliuawa miaka kadhaa iliyopita. Mwuaji wake, Esmeraldo, alikamatwa lakini alikanusha shtaka hilo alipofikishwa mahakamani. Hata hivyo, kwa kutegemea uthibitisho uliotolewa, alifungwa gerezani.

Baadaye, mzee fulani alimwomba Miguel aandamane naye hadi kwenye gereza lilelile nchini Filipino ambako Esmeraldo alikuwa amefungwa. Miguel alisitasita akijua kwamba mwuaji wa mjukuu wake alikuwa humo. Hata hivyo, aliandamana naye na akashiriki kuwafundisha wafungwa fulani waliokuwa wakijifunza Biblia. Wakati wa funzo, alimwona Esmeraldo akija kumwelekea. Ili atulize hali ambayo huenda ingelipuka, Miguel alizungumza naye kwa upole akimwambia: “Esmer, sikuja hapa kubishana, bali nilikuja kuwaonyesha upendo watu kama wewe. Ona, tunajifunza Biblia na mtu huyu. Hungekuwa hapa ikiwa ungekuwa unajua Neno la Mungu. Tafadhali jifunze Biblia pamoja nasi.” Miguel alishangaa Esmeraldo alipoketi na kusikiliza sehemu ya funzo iliyosalia. Akiwa ameguswa na mambo aliyosikia, alimwambia Miguel waziwazi kwamba yeye ndiye aliyekuwa amemwua mjukuu wake. Kisha akamwomba msamaha.

Kwa kuwa hakuwa amesikia mazungumzo hayo ya faragha, mzee yule alipotazama na kuona ni kana kwamba walikuwa wakizungumza kwa urafiki, alimwambia Miguel ajifunze na Esmeraldo. Mwanzoni Miguel aliogopa, kwa kuwa alijua kwamba mtu huyo alikuwa amewaua watu wengine mbali na mjukuu wake, lakini akakubali. Esmeraldo alijitahidi sana kwa muda mrefu ili apatanishe maisha yake na viwango vya Mungu; lakini jitihada zake zenye subira zilikuwa na matokeo, na Februari 1, 2010, alibatizwa ili kuonyesha wakfu wake kwa Yehova. Ili aonyeshe kwamba amemsamehe Esmeraldo, Miguel anajaribu kuona ikiwa anaweza kufanya jambo lolote ili kifungo cha Esmeraldo kipunguzwe ili awe huru kuwaeleza wengine kweli za Biblia kwa ukamili zaidi.

ULAYA

IDADI YA NCHI 47

IDADI YA WATU 739,193,855

IDADI YA WAHUBIRI 1,575,094

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 830,888

MAMBO MAWILI ALIYOTAMANI KUTIMIZA. Nelena, mwenye umri wa miaka 19 na anayeishi nchini Bulgaria, alitamani kufanya mambo mawili—kubatizwa na kutumika akiwa painia-msaidizi. Hata hivyo, anaugua ugonjwa wa mfumo wa neva aliorithi, ambao kwa sasa hauna tiba. Yeye hutumia mashini fulani inayomsaidia kupumua, na hilo humzuia kutembea kwa uhuru. Ilikuwa vigumu kwake kutimiza jambo la kwanza alilotaka kufanya, yaani, kubatizwa, kwa sababu hali yake haikumruhusu kutoka nje ya nyumba ili ahudhurie kusanyiko. Kwa hiyo alipokuwa na umri wa miaka 18, hotuba ya Biblia ilitolewa nyumbani kwao, kisha akabatizwa kwenye beseni kubwa ya bafu.

Namna gani kuhusu tamaa yake ya kuwa painia-msaidizi? Katika majira ambayo hali ya hewa ni nzuri, anaweza kupumua kwa saa moja au zaidi bila kutumia mashini. Hivyo, yeye hufanya upainia msaidizi, na mhubiri mmoja humsukuma kwenye kiti cha magurudumu wanapohubiri nyumba kwa nyumba. Pia, Nelena huongoza funzo la Biblia kwa kutumia simu inayopigwa kupitia Intaneti. Nyakati nyingine, akina dada huongoza mafunzo ya Biblia nyumbani kwa Nelena, na hilo humsaidia kushiriki. Hivyo, Nelena alifanya upainia msaidizi mara tatu katika mwaka wa utumishi uliopita. Anasema hivi: “Ninafurahi sana kwa sababu nilitimiza mambo mawili niliyotamani kufanya. Kufanya hivyo kumenisaidia nimkaribie Yehova zaidi, Muumba wangu mpendwa.”

SIKU HIZI ANAFUNGA TAI. Dada mmoja nchini Armenia alidhihakiwa na wafanyakazi wenzake kwa sababu alikuwa Shahidi wa Yehova. Mfanyakazi mwenzake alikuwa na zoea la kumdhihaki, akisema kwamba “wale watu ambao hufunga tai” walikuwa wamemshawishi dada huyo kujiunga na dini yao. Dada huyo alijitahidi sana kuzungumza naye mara nyingi lakini hakubadili maoni yake, kwa hiyo dada huyo aliamua kupuuza dhihaka zake na kumwiga Yesu Kristo kwa ‘kutojibu.’ (Mt. 27:12) Hatimaye, mfanyakazi huyo aliachishwa kazi kwa sababu ya mwenendo wake mbaya na kwa kumsumbua dada yetu. Baada ya miezi kadhaa, mwanamume fulani alifika mahali ambapo dada huyo alikuwa akifanya kazi na kumtafuta. Kumbe alikuwa ni mtu yuleyule aliyekuwa amemkera sana kwa dhihaka zake. Dada huyo alishangaa sana kumwona. Ingawa alikuwa amewadhihaki Mashahidi kuwa wao hufunga tai, sasa yeye ndiye aliyekuwa amefunga tai na kubeba mkoba. Alimwambia hivi dada yetu: “Ninaomba msamaha kwa maneno yenye kuumiza niliyokuambia. Sasa ninajua kwamba nimeipata kweli.” Mwanamume huyo alikuwa amejifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, na licha ya upinzani kutoka kwa familia yake, alibatizwa na alikuwa akitumika akiwa painia wa kawaida.

“JE, UNAMJUA BI. NADIA?” Nadia ni painia katika kutaniko moja kaskazini mwa Italia. Mnamo Septemba 2009, alizungumza na mwanamume mmoja kwa kutumia simu iliyokuwa kwenye lango, lakini mwanamume huyo alimkatiza na kumweleza kwamba mke wake alikuwa amekufa na hivyo hakutaka kuzungumza naye wakati huo. Jumapili (Siku ya Yenga) iliyofuata, Nadia alirudi nyumbani kwa mwanamume huyo ili kumfariji na kumwonyesha tumaini la Biblia la ufufuo, lakini bado mwanamume huyo hakutaka kuzungumza naye wakati huo. Habari iliyokuwa imezungumziwa alasiri hiyo kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi ilitia ndani habari kumhusu dada mmoja aliyekuwa amemwandikia barua mtu fulani aliyekuwa amefiwa na mpendwa wake. Jambo hilo lilimfanya Nadia kufikiria kumhusu mwanamume huyo aliyekuwa amezungumza naye. Hivyo, aliamua kumwandikia barua ya kumfariji na kumweleza kuhusu tumaini la ufufuo. Siku mbili baadaye, aliituma barua ile.

Siku kadhaa baadaye, Nadia alikuwa akihubiri barabarani na kumsimamisha mwanamume mmoja aliyekuwa na umri wa miaka 70 hivi, ili amsomee andiko fulani la Biblia. Mwanamume huyo alimuuliza ikiwa alikuwa Shahidi wa Yehova, na Nadia alijibu, ‘Ndiyo.’ Mwanamume huyo alieleza kwamba alikuwa ametembelewa na Shahidi wa Yehova, ambaye alikuwa amemwachia barua iliyomgusa moyo sana. Kisha akauliza, “Je, unamjua Bi. Nadia?” Wote wawili wakiwa wameshangaa sana, Nadia alijijulisha kwake na kufanya mpango wa kumtembelea akiwa pamoja na mume wake. Mbali na kuanza kujifunza Biblia, mwanamume huyo sasa anahudhuria mikutano kwa ukawaida.

HAWAWEZI KUJIFUNZA NAO WOTE. Mashahidi wanne wa Yehova wanaishi katika mji wa Bujanovac kusini mwa Serbia. Watangazaji hao wa Ufalme walifurahi sana kuwa na hudhurio la watu 460 kwenye Ukumbusho katika mwaka wa 2010! Wazee kutoka kutaniko jirani wamefanya mipango ya kuongoza mikutano kwa ukawaida huko Bujanovac kwenye jengo la kukodi. Kwa wastani, zaidi ya watu 50 huhudhuria—wengi wao wana asili ya Kiromani. Kwa sababu watu wengi wanaitikia ujumbe wa Ufalme, mapainia wa pekee wanaohubiri katika eneo hilo hawawezi kuongoza mafunzo ya Biblia na wote wanaoonyesha upendezi. Kwa hiyo, wao hujifunza na wale tu wanaohudhuria mikutano yote wakiwa wamejitayarisha vizuri.

AMEISHI ZAIDI YA KARNE MOJA! Elin, ambaye ndiye mhubiri mwenye umri wa juu zaidi nchini Sweden, ana umri wa miaka 110—umri ambao Yoshua alifikia. (Yos. 24:29) Anaishi katika makao ya kuwatunza wazee na yeye hutumia kila nafasi kuzungumza na wageni au mtu yeyote anayekutana naye. Yeye huwaachia watu wengi vitabu. Wakati mmoja mzee fulani pamoja na binti yake walikuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba kwenye ujirani wao, nao walimhubiria msichana mmoja aliyesema kwamba alikuwa amehubiriwa na Elin na kuachiwa kitabu. Mazungumzo mazuri yalifuatia.a

ALIPATA VITABU KANISANI. Tatyana, anayeishi Belarus, alishangaa sana siku moja alipopigiwa simu na msichana mmoja asiyemjua. Msichana huyo alitaka kupata majibu ya Biblia kuhusu maswali aliyokuwa nayo. Mazungumzo yenye uchangamfu yalifuatia. Alipata wapi namba ya simu ya Tatyana? Msichana huyo alieleza kwamba alipoenda katika kanisa moja, alipata kitabu Biblia Inafundisha pamoja na Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya chini ya benchi na ndani yake vilikuwa vimeandikwa namba ya simu ya Tatyana. Ni nani aliyevipeleka vitabu hivyo kanisani? Vilipelekwa mle na mama ya msichana aliyejifunza Biblia pamoja na Tatyana. Ni wazi kwamba mama ya msichana huyo alitaka kumuuliza kasisi wa kanisa hilo ikiwa ilikuwa sawa kwa binti yake kusoma vitabu hivyo au la. Kwa sababu fulani, vitabu hivyo viliachwa mle kanisani. Msichana huyo aliviona na akaamua kuvichukua. Baada ya kuzungumza na Tatyana kwa simu, mazungumzo zaidi ya Biblia yalifuata.

KOTI LILILOPOTEA LAANZISHA MAZUNGUMZO. Elena, dada ambaye ni painia wa pekee, aliona koti zuri sana lililokuwa limeanguka kwenye barabara huko Minsk, Belarus. Koti hilo lilikuwa safi na halikuonekana kuwa limetupwa. Alipoliokota, alipata likiwa na dola 1,200 za Marekani mfukoni. Alipowatazama wapita njia, mara moja alimtambua mtu aliyekuwa ameangusha koti hilo bila kujua. Mwanamume huyo alionekana mwenye wasiwasi naye alikimbia huku na huku kana kwamba alikuwa akitafuta kitu. Ilimbidi Elena akimbie pia ili amfikie. Alikuwa mfanyabiashara kutoka Bangladesh, aliyekuwa akiishi huko Moscow. Alifurahi sana kupata koti lake likiwa na pesa zake. Pia, alitaka kujua ni kwa nini dada huyo alimrudishia kote lake, hata ikiwa ilimlazimu kukimbia ili amfikie. Alimweleza kwamba yeye ni Shahidi wa Yehova. Mwanamume huyo alimwambia kwamba siku mbili zilizopita, Mashahidi wawili walikuwa wamezungumza naye. Kwa muda wa dakika 30, alibishana nao na kutetea imani yake ya kidini. Kisha mwanamume huyo alimwuliza Elena jinsi ambavyo angemshukuru kwa kulirudisha koti lake. Dada huyo alimweleza kwamba hakutaka zawadi yoyote kwa sababu ya kulirudisha koti hilo, bali angeweza kuonyesha shukrani zake kwa kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova atakaporudi Moscow. Alikubali kufanya hivyo.

Oceania

IDADI YA NCHI 30

IDADI YA WATU 39,384,408

IDADI YA WAHUBIRI 101,483

IDADI YA MAFUNZO YA BIBLIA 62,367

KUKABILIANA NA MATATIZO YA USEMI. Hamish, mwenye umri wa miaka 23 ni ndugu aliyebatizwa, anayeishi Australia, na aliye na tatizo kubwa sana la usemi ambalo husababisha maneno yake kusikika yakiwa yamechanganyika au yasiyoeleweka au hata wakati mwingine anashindwa kabisa kuzungumza. Hata hivyo, tatizo hilo halijamfanya apunguze bidii yake ya kusema hadharani au kushiriki katika utumishi wa shambani. Kwa mfano, ili aweze kutoa hotuba katika Jumba la Ufalme, kwanza Hamish huchapa muhtasari wake kwenye kifaa cha elektroniki ambacho hugeuza maandishi yaliyochapwa kuwa maneno yanayosikika. Wakati anapotoa hotuba, yeye huweka kifaa hicho kwenye kinara cha msemaji na kutumia kibodi ili kuchagua mafungu au sentensi alizochapa awali na kuzicheza. Kisha maneno hayo yaliyobadilishwa hunaswa na kikuza sauti na kusikika kupitia mfumo wa sauti. Ikiwa sehemu yake inawahusisha wasikilizaji, yeye hutumia kifaa chake kuuliza maswali na kuwashukuru wasikilizaji kwa maelezo yao. Anaposhiriki katika utumishi wa shambani, yeye hutumia njia hiyohiyo kuwasiliana, na hivyo yeye hutayarisha sentensi kadhaa, maandiko yaliyonukuliwa, na kuchapa kwa haraka! Kwa kutumia njia hiyo, ameweza kupata ziara za kurudia zenye maendeleo. Tangu mwaka wa 2007, Hamish alipowekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma, amefanya upainia msaidizi mara kadhaa kila mwaka.

MASHINI YAKE YA KUCHAPA ILIKUWA IMEHARIBIKA. David, ambaye ni fundi wa kompyuta nchini New Caledonia, alipigiwa simu na mwanamke mmoja ambaye mashini yake ya kuchapa ilikuwa na matatizo fulani—haingeweza kuchapa ujumbe fulani. David alirekebisha tatizo hilo mara moja, lakini alishangaa sana kuona ujumbe uliochapwa kwenye karatasi, uliosema: “MSITUTEMBELEE. Yesu yuko nasi. Hatuhitaji dini nyingine yoyote.”

David alimuuliza mwanamke huyo: “Samahani, nilipokuwa nikirekebisha mashini yako, nilisoma ujumbe kwenye karatasi hii. Kwa nini uliandika ujumbe huu?”

Mwanamke huyo alijibu: “Ah, unajua kwamba Mashahidi wa Yehova hutembea hapa kila mwisho wa juma. Tumechoka kuwaona kwenye eneo hili. Ninakuhakikishia kwamba hakuna hata mmoja wao atakayeingia ndani ya nyumba hii.”

David aliuliza: “Je, unajua kwamba tayari umemkaribisha mmoja wao ndani ya nyumba yako?”

“Haiwezekani hata kidogo!” akajibu.

David alimwambia: “Mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova! Na ulinikaribisha ndani!” Mwanamke huyo alishangaa sana na pia akaaibika. Kwa heshima, David alimweleza kwa nini Mashahidi wa Yehova hutembelea watu nyumbani kwao. Walizungumza kwa muda wa saa mbili. Siku chache baadaye, David alimtembelea tena mwanamke huyo na mume wake. Walimweleza kwamba baada ya kufikiria kuhusu yale yaliokuwa yametendeka, walikuwa wamesadikishwa kwamba Mungu alikuwa amemwongoza David awatembelee. Kwa hiyo hawangeweza kumzuia! Sasa wao hupokea magazeti yetu kwa ukawaida.

KUTUMIA TRAKTI. Nathan, mwenye umri wa miaka 12, anaishi Australia. Yeye hubeba trakti za Biblia kwenye mkoba wake wa shule na kuwahubiria rafiki zake shuleni kwa ukawaida. Siku moja, alipokuwa akirudi nyumbani kutoka shule, alimwona mwanamke mmoja mzee akiwa amesimama nje ya nyumba yake. Mwanamke huyo alitabasamu, na hivyo Nathan pia akatabasamu na kumpa moja ya trakti zake. Kisha mwanamke huyo alimwambia kwamba mume wake alikufa miaka mitatu iliyopita. Kusikia hivyo, Nathan alimpa trakti Kuna Tumaini Gani kwa Wapendwa Waliokufa? Macho ya mwanamke yule yalijawa na machozi Nathan alipokuwa akimweleza kuhusu ufufuo wa wakati ujao ambapo atamwona mume wake tena katika Paradiso. “Lakini kuteseka kote kutaisha lini?” mwanamke huyo aliuliza. Nathan alitoa trakti nyingine inayosema, Kuteseka Kote Kutaisha Karibuni! Kisha mwanamke huyo alimwomba Nathan amweleze zaidi kuhusu mambo anayoamini. Hivyo akampa trakti nyingine inayosema, Mashahidi wa Yehova Wanaamini Nini? Baada ya hayo, Nathan aliondoka. Majuma kadhaa baadaye alimwona tena mwanamke yule akiwa amesimama nje ya nyumba yake. Alimwita Nathan na kumkumbatia, kisha akamwambia, “Wajua nini Nathan, baada ya kunipa zile trakti, wanawake wawili ambao ni Mashahidi walinitembelea, na sasa ninajifunza Biblia pamoja nao!”

MWALIKO MMOJA TU WA UKUMBUSHO. Michael alisaidia katika ujenzi wa ofisi mpya ya tawi katika Visiwa vya Solomon. Baada ya ujenzi kukamilika, aliamua kwenda kuwahubiria watu katika Kisiwa cha Mbanika kilicho mbali ambako alilelewa akiwa mtoto na ambako ndugu zake waliishi. Hakukuwa na Mashahidi katika kisiwa hicho. Pia hakuna meli inayosafiri huko kwa ukawaida, wala hakuna huduma za posta, na kuna simu moja tu inayotumika.

Alisafiri pamoja na Hansly, painia mchanga hadi kwenye Kisiwa cha Mbanika. Walipofika, walianza mara moja kujenga Jumba la Ufalme dogo wakitumia majani ya mnazi na kukaribisha watu kuhudhuria Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Kwa sababu walikuwa na mwaliko mmoja tu wa Ukumbusho, ndugu hao wawili waliwaonyesha watu mwaliko huo na kueleza umuhimu wa Ukumbusho.

Siku moja kabla ya Ukumbusho, ndugu hao walisafiri saa mbili kwa mtumbwi hadi ng’ambo ile nyingine ya kisiwa ili kukaribisha familia moja iliyoishi huko. Hata hivyo, walipata watoto wakiwa peke yao. Michael aliamua kuwaachia mwaliko ule mmoja tu aliokuwa nao. Alimpa binti mkubwa wa familia hiyo na kumwambia ampe baba yake.

Alasiri iliyofuata, Michael na Hansly walipokuwa wakijitayarisha kwa ajili ya Ukumbusho, waliiona familia hiyo ikija kwa mtumbwi. Baba yao alikuwa amesoma mwaliko huo na akaamua kwamba lazima Ukumbusho uwe ni tukio muhimu sana, na hivyo akasafiri pamoja na familia yake yote ili kuhudhuria. Jioni hiyo, watu 52 walihudhuria Ukumbusho. Michael na Hansly wanaendelea kuhubiri huko na pia kujifunza Biblia pamoja na wale waliohudhuria Ukumbusho.

[Maelezo ya Chini]

a Elin alikufa kabla ya kitabu cha mwaka kukamilishwa.

[Chati katika ukurasa wa 40-47]

RIPOTI YA MWAKA WA UTUMISHI WA 2010 YA MASHAHIDI WA YEHOVA ULIMWENGUNI POTE

(Ona nakala iliyochapishwa)

[Ramani katika ukurasa wa 48-50]

(Ona nakala iliyochapishwa)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki