Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • rs uku. 161-uku. 168
  • Mageuzi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mageuzi
  • Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mtu Akisema—
  • Mageuzi Yajaribiwa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1994
  • Je, Fundisho la Mageuzi Linapatana na Biblia?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
  • Je, Uhai Wote Umetokana na Chanzo Kimoja?
    Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai
  • Uumbaji au Mageuzi?—Sehemu ya 2: Kwa Nini Uchunguze Nadharia ya Mageuzi?
    Vijana Huuliza
Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
rs uku. 161-uku. 168

Mageuzi

Maana: Mageuzi ni nadharia ya kwamba kiumbe hai cha kwanza kilitokana na kitu kisicho na uhai. Kisha inasemekana kwamba kilipoendelea kuzaa kiligeuka kikawa aina mbalimbali za viumbe hai, na mwishowe kikatokeza namna zote za mimea na wanyama ambao wamepata kuishi duniani. Inasemekana kwamba yote hayo yalitendeka bila Muumba kuingilia kati. Watu fulani hujaribu kuchanganya imani katika Mungu na mageuzi, wakisema kwamba Mungu aliumba kwa kutumia mageuzi, kwamba aliumba viumbe hai vya kwanza vilivyo duni kisha viumbe hai vya hali ya juu, kutia ndani mwanadamu, vikatokea kupitia mageuzi. Hilo si fundisho la Biblia.

Je, kweli fundisho la mageuzi ni la kisayansi?

Njia ya “kisayansi” ya kuthibitisha mambo ni hii: Chunguza yanayotukia; kwa kutegemea uchunguzi, tunga nadharia kuhusu jambo linaloweza kuwa la kweli; ijaribu nadharia hiyo kwa uchunguzi zaidi na kwa majaribio; kisha tazama uone ikiwa matarajio yanayotegemea nadharia hiyo yanatimizwa. Je, njia hiyo inafuatwa na wale wanaoamini na kufundisha mageuzi?

Mtaalamu wa nyota Robert Jastrow anasema hivi: “[Wanasayansi] wanaudhika kwa sababu hawana jibu la wazi, kwa sababu wanakemia hawajafaulu kamwe katika majaribio yao ya kutokeza uhai kiasili kutokana na vitu visivyo hai. Wanasayansi hawajui jinsi hilo lilivyotukia.”—The Enchanted Loom: Mind in the Universe (New York, 1981), uku. 19.

Mwanamageuzi Loren Eiseley alikiri hivi: “Baada ya kumdhihaki mwanatheolojia kwa kuwa anategemea hadithi na muujiza, sayansi ilijikuta katika hali mbaya iliyoilazimisha kujitungia hadithi yake: yaani, dhana ya kwamba eti jambo ambalo haliwezi kuthibitishwa kwamba linatokea leo hata baada ya jitihada nyingi, kwa kweli lilitukia zamani za kale.”—The Immense Journey (New York, 1957), uku. 199.

Kulingana na New Scientist: “Hesabu inayozidi kuongezeka ya wanasayansi, hasa hesabu inayoongezeka ya wanamageuzi . . . wanabisha wakisema kwamba nadharia ya mageuzi ya Darwin si nadharia ya kweli hata kidogo kisayansi. . . . Wengi wa wachambuzi hao wana masomo ya hali ya juu.”—Juni 25, 1981, uku. 828.

Mwanafizikia H. S. Lipson alisema: “Maoni pekee yanayokubalika ni uumbaji. Ninajua kwamba jambo hili ni mwiko kwa wanafizikia, kama lilivyo kweli kwangu mimi, lakini hatupaswi kukataa nadharia ambayo hatuipendi ikiwa inaungwa mkono na uthibitisho wa majaribio.” (Italiki zimeongezwa.)—Physics Bulletin, 1980, Buku la 31, uku. 138.

Je, wale wanaounga mkono mageuzi wanakubaliana? Mambo yanayofuata yanakufanya uoneje yale wanayofundisha?

Utangulizi wa chapa ya kitabu cha Darwin kinachoitwa Origin of Species (London, 1956) unasema hivi: “Kama tunavyojua, kuna tofauti kubwa ya maoni kati ya wanabiolojia, si juu ya visababishi vya mageuzi tu bali pia hata juu ya utaratibu wenyewe. Tofauti hiyo ipo kwa sababu ule uthibitisho hauridhishi wala hauruhusu uamuzi wowote ulio hakika. Kwa hiyo ni jambo zuri na linalofaa kuwajulisha watu ambao si wanasayansi kwamba wanasayansi hawakubaliani kuhusu mageuzi.”—Na W. R. Thompson, aliyekuwa mkurugenzi wa Commonwealth Institute of Biological Control, Ottawa, Kanada.

“Karne moja baada ya kifo cha Darwin, bado hatuna hata jambo dogo la kuonyesha au lenye kusadikisha kuhusu jinsi mageuzi yalivyotukia hasa—na katika miaka ya hivi karibuni hilo limesababisha mabishano mengi kuhusu suala hilo. . . . Wanamageuzi wenyewe hubishana waziwazi, huku kila kikundi [cha mageuzi] kikiomba kuwe na mabadiliko fulani mapya.”—C. Booker (mwandikaji wa The Times la London), The Star, (Johannesburg), Aprili 20, 1982, uku. 19.

Gazeti la kisayansi Discover lilisema: “Mageuzi . . . yanashambuliwa na Wakristo wenye imani kali, na pia yanatiliwa shaka na wanasayansi wenye kuheshimika. Wanasayansi wanaochunguza mabaki ya viumbe vya zamani wana maoni yanayotofautiana.”—Oktoba 1980, uku. 88.

Mabaki ya viumbe vya zamani yanaunga mkono maoni gani?

Darwin alikiri hivi: “Ikiwa viumbe mbalimbali . . . vilianza kuishi mara moja, jambo hilo litaiangamiza nadharia ya mageuzi.” (The Origin of Species, New York, 1902, Sehemu ya Pili, uku. 83) Je, uthibitisho unaonyesha kwamba “viumbe mbalimbali” vilianza kuishi mara moja, au je, unaonyesha ukuzi wa hatua kwa hatua, kama nadharia ya mageuzi inavyodai?

Je, mabaki ya kutosha ya viumbe vya zamani yamepatikana ili kufikia uamuzi unaofaa?

Porter Kier, mwanasayansi katika Smithsonian Institution anasema: “Kuna mabaki milioni mia moja ya viumbe vya zamani, na mabaki hayo yote yameorodheshwa na kutambulishwa, katika majumba ya makumbusho ulimwenguni.” (New Scientist, Januari 15, 1981, uku. 129) Kitabu A Guide to Earth History kinaongeza hivi: “Kwa kutumia mabaki ya viumbe vya zamani, sasa wataalamu wa viumbe vya zamani wanaweza kutueleza mengi kuhusu viumbe vya kale.”—(New York, 1956), Richard Carrington, Chapa ya Mentor, uku. 48.

Mabaki ya viumbe vya zamani yanaonyesha nini hasa?

Jarida Bulletin la Field Museum of Natural History la Chicago lilieleza hivi: “Nadharia ya Darwin ya [mageuzi] nyakati zote imehusianishwa sana na uthibitisho kutoka kwenye mabaki ya viumbe vya zamani, na huenda watu wengi hudhani kwamba mabaki hayo hutoa uthibitisho muhimu unaounga mkono ufafanuzi wa Darwin kuhusu jinsi uhai ulivyoanza. Kwa kusikitisha, jambo hilo si kweli kabisa. . . . rekodi ya mawe ya wakati huo haikuonyesha na ingali haionyeshi kwamba viumbe vilitokea kwa njia ya mageuzi ya hatua kwa hatua na vinaendelea kufanya hivyo leo.”—Januari 1979, Buku la 50, Na. 1, uku. 22, 23.

Gazeti A View of Life linaeleza hivi: “Tangu mwanzoni mwa kipindi cha Kambria na kuendelea kwa miaka milioni 10 hivi, vikundi vyote vikubwa vya wanyama wasio na uti wa mgongo viliibuka kwa mara ya kwanza kwa njia yenye kuvutia zaidi katika unamna-namna ambao haujawahi kuonekana katika dunia yetu.”—(California, 1981), Salvador E. Luria, Stephen Jay Gould, Sam Singer, uku. 649.

Alfred Romer, mtaalamu wa viumbe vya zamani aliandika hivi: “Chini ya hiki [kipindi cha Kambria], kuna matabaka manene ambapo tungetazamia kupata wazazi wa viumbe vya kipindi cha Kambria. Lakini hatuwapati humo; matabaka hayo ya zamani hayana uthibitisho wowote wa viumbe, na kwa ujumla inaweza kusemwa kwamba hali hiyo inapatana na lile wazo la uumbaji wa pekee mwanzoni mwa vipindi vya Kambria.”—Natural History, Oktoba 1959, uku. 467.

Harold Coffin, mtaalamu wa wanyama anaeleza hivi: “Ikiwa kwa kweli viumbe duni viligeuka hatua kwa hatua na kuwa viumbe vya juu zaidi, basi wazazi wa kale wa viumbe hivyo vilivyogeuka kabisa katika kipindi cha Kambria wanapaswa kupatikana; lakini hawajapatikana, na wanasayansi wanakubali kwamba hakuna tarajio la kuwapata kamwe. Kwa msingi wa mambo hakika pekee, kwa msingi wa yale ambayo kwa kweli yanapatikana udongoni, ile nadharia ya uumbaji wa ghafula ambapo viumbe vikubwa viliumbwa, inafaa zaidi.”—Liberty, Septemba/Oktoba 1975, uku. 12.

Carl Sagan, alikiri hivi kwa unyoofu katika kitabu chake Cosmos: “Uthibitisho wa mabaki ya viumbe vya zamani unapatana na lile wazo la kwamba kuna Mbuni Mkuu.”—(New York, 1980), uku. 29.

Je, inawezekana kwamba mageuzi yalitokana na mabadiliko makubwa ya ghafula katika chembe za urithi?

Jarida la Science Digest linasema hivi: “Wasahihishaji wa nadharia ya mageuzi wanaamini kwamba mabadiliko katika chembe kuu za urithi zinazotoa mwongozo huenda yakawa ndiyo msukumo ambao nadharia yao ya mabadiliko ya ghafula inahitaji.” Hata hivyo, gazeti hilo pia linamnukuu mtaalamu wa wanyama Mwingereza, Colin Patterson, akisema hivi: “Kukisia-kisia kunaruhusiwa. Sisi hatujui lolote kuhusu hizi chembe kuu za urithi zenye kutoa mwongozo.” (Februari 1982, uku. 92) Maana yake ni kwamba hakuna uthibitisho wa kuunga mkono nadharia hiyo.

The Encyclopedia Americana inakiri hivi: “Uhakika wa kwamba mabadiliko mengi katika chembe za urithi hukiathiri kiumbe, hufanya iwe vigumu kuupatanisha na maoni ya kwamba mabadiliko katika chembe za urithi ndicho chanzo cha mageuzi. Kwa kweli, viumbe vyenye chembe za urithi zilizobadilika, vinavyochorwa katika vitabu vya biolojia ni viumbe vyenye ulemavu na vyenye kasoro, nako kubadilika kwa chembe za urithi kunaonekana kuwa na athari mbaya badala ya kuboresha aina ya viumbe.”—(1977), Buku la 10, uku. 742.

Namna gani zile picha za “nyani-mtu” zilizo katika vitabu vya shule, ensaiklopidia na majumba ya makumbusho?

“Nyama na nywele za viumbe hivyo huchorwa au kuundwa kutokana na fikira za mtu. . . . Hatujui lolote kuhusu rangi ya ngozi; rangi na aina ya nywele, na jinsi zilivyoenea mwilini; umbo la viungo; na sura ya watu hao wa zamani za kale.”—The Biology of Race (New York, 1971), James C. King, uku. 135, 151.

“Mawazo mengi sana ya wachoraji hutegemea ubunifu badala ya uthibitisho. . . . Wachoraji hulazimika kubuni kitu fulani kati ya nyani na mwanadamu; kadiri kiumbe hicho kinavyosemwa kuwa cha zamani, ndivyo wanavyozidi kukifanya kiwe kama nyani zaidi.”—Science Digest, Aprili 1981, uku. 41.

“Kama vile tunavyojifunza polepole kwamba watu wa kale hawakuwa washenzi, vivyo hivyo lazima tufahamu kwamba watu wa zamani katika Enzi ya Barafu hawakuwa tu wanyama wasio na akili wala hawakuwa nusu-nyani wala hawakuwa washamba. Kwa hiyo jitihada zote za kuunda upya mtu wa Neanderthal au hata wa Peking ni upumbavu mtupu.”—Man, God and Magic (New York, 1961), Ivar Lissner, uku. 304.

Je, vitabu vya mafundisho havionyeshi kwamba mageuzi ni jambo hakika?

“Wanasayansi wengi hunaswa na kile kishawishi cha kulazimisha mambo bila uthibitisho, . . . tena na tena, suala la chanzo cha aina mbalimbali za viumbe limetolewa kana kwamba ni jambo lililosuluhishwa kabisa. Jambo hilo si kweli hata kidogo .  . . . Lakini mwelekeo wa kulazimisha mambo bila uthibitisho unaendelea kuwapo, nao unaiharibia sayansi sifa.”—The Guardian, London, Uingereza, Desemba 4, 1980, uku. 15.

Lakini je, ni jambo linalopatana na akili kuamini kwamba kila kitu duniani kiliumbwa katika siku sita?

Kuna vikundi fulani vya kidini vinavyofundisha kwamba Mungu aliumba kila kitu katika siku sita zenye saa 24 kila moja. Lakini Biblia haisemi hivyo.

Andiko la Mwanzo 1:3-31 linasimulia jinsi Mungu alivyotayarisha dunia ambayo tayari ilikuwapo ili iwe makao ya wanadamu. Linasema kwamba jambo hilo lilifanywa wakati wa kipindi cha siku sita, lakini halisemi kwamba hizo zilikuwa siku zenye saa 24 kila moja. Huenda mtu akasema kuhusu “siku ya babu” yake, akimaanisha muda wote wa maisha ya babu yake. Vivyo hivyo, pia, mara nyingi Biblia hutumia neno “siku” kumaanisha kipindi kirefu cha wakati. (Linganisha na 2 Petro 3:8.) Kwa hiyo neno “siku” katika Mwanzo sura ya 1 linaweza kumaanisha maelfu ya miaka.

Kwa maelezo zaidi, ona ukurasa wa 394.

Mtu Akisema—

‘Ninaamini mageuzi’

Unaweza kujibu: ‘Je, unaamini kwamba Mungu alihusika katika kuumba, au unaamini kwamba tangu mwanzo uhai ulitokea wenyewe tu? (Kisha endelea kulingana na maelezo ya mtu huyo.)’

Au unaweza kusema: ‘Haingefaa kukataa jambo ambalo limethibitishwa kikamili kisayansi, sivyo? . . . Hapa nina maelezo fulani ya wanasayansi ambayo ni yenye kupendeza kuhusu habari hii. (Tumia habari iliyo katika ukurasa wa 161, 162, chini ya kichwa, “Je, kweli fundisho la mageuzi ni la kisayansi?” au katika ukurasa wa 162, chini ya kichwa, “Je, wale wanaounga mkono mageuzi wanakubaliana? . . . ”)’

Pia unaweza kusema: ‘Kunapokuwa na uthibitisho thabiti kuhusu jambo fulani, tunapaswa kuliamini, sivyo? . . . Nakumbuka katika vitabu vyangu vya shule kwamba picha za mabaki ya viumbe vya zamani zilichorwa ili kuunga mkono mageuzi. Lakini tangu wakati huo nimesoma maelezo fulani yenye kupendeza sana ya wanasayansi kuhusu mabaki ya viumbe vya zamani. Sasa hivi nina baadhi ya maelezo hayo. (Tumia habari iliyo katika ukurasa wa 162-164, chini ya kichwa, “Mabaki ya viumbe vya zamani yanaunga mkono maoni gani?”)’

Pendekezo lingine: ‘Je, ni sawa nikisema kwamba wewe ni mtu anayependa kukabili maisha jinsi yalivyo kweli kweli? . . . Nami pia nina maoni kama yako.’ Kisha unaweza kuongezea: ‘Nikienda kutembea mashambani nami nikute nyumba iliyojengwa kwa mawe na mbao, inapaswa kuwa wazi kwangu kwamba kuna mtu aliyekuwako kabla yangu, naye akaijenga; sivyo? . . . Lakini, sasa, je, lingekuwa jambo la akili kwangu kukata shauri kwamba maua yanayokua kando ya nyumba yalitokea yenyewe tu? Ikiwa ningekuwa na maoni kama hayo, basi ninapaswa kutazama kwa uangalifu na kuona ubuni tata, kwa sababu ninajua ni kweli kwamba palipo na ubuni ni lazima pawe na mbuni. Hivi ndivyo Biblia inavyotuambia katika Waebrania 3:4.’

Au unaweza kujibu (mtu wa umri mkubwa zaidi): ‘Mojawapo ya mawazo ya msingi katika mageuzi ni kwamba mwanadamu yuko jinsi alivyo leo kwa sababu ya maendeleo yake, sivyo?’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Wewe umeishi kwa muda fulani. Je, unakumbuka jinsi mambo yalivyokuwa ulipokuwa mtoto? Je, kulikuwako uhalifu mwingi kama leo? . . . Je, ulilazimika kufunga mlango kwa kufuli nyakati zote? . . . Je, ungesema kwamba watu wakati huo waliwahangaikia zaidi jirani zao na wazee, kuliko wanavyofanya leo? . . . Kwa hiyo, ijapokuwa kumekuwako na maendeleo makubwa ya kiufundi, inaonekana kwamba wanadamu wenyewe wanapoteza baadhi ya sifa muhimu zaidi. Kwa nini?’ (2) ‘Naona kwamba mambo hayo ambayo tumejionea maishani yanapatana na yaliyoandikwa katika Biblia katika Waroma 5:12. . . . Basi, kwa kweli mambo yamekuwa yakiharibika.’ (3) ‘Lakini Biblia inaonyesha jinsi hali hiyo itakavyobadilika. (Dan. 2:44; Ufu. 21:3, 4)’

‘Ninaamini kwamba Mungu alimuumba mwanadamu kupitia mageuzi’

Unaweza kujibu: ‘Nimeongea na watu wengine walio na maoni kama yako. Je, nikisema kwamba wewe ni mtu aliye na imani thabiti katika Mungu, nitakuwa nimekosea? . . . Kwa hiyo unatanguliza imani katika maisha yako; imani inakufanya uchunguze mambo mengine, sivyo? . . . Hayo ndiyo maoni yangu pia.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Ninajua kwamba ikiwa yale ninayoamini ni kweli kabisa, hayatapingana na mambo ya sayansi yaliyothibitishwa. Wakati huohuo najua kwamba ungekuwa upumbavu kama ningedharau yale ambayo Neno la Mungu linasema, kwa sababu Mungu anajua mengi zaidi kuhusu kazi zake kuliko yeyote kati yetu. Ninavutiwa na yale ambayo Biblia, Neno la Mungu lililoongozwa na roho, linasema hapa katika Mwanzo 1:21 (kazia “kulingana na aina zake”).’ (2) ‘Kisha katika Mwanzo 2:7 tunaona kwamba Mungu alimuumba mtu, si kutokana na wanyama waliotangulia kuwako, bali kutokana na mavumbi.’ (3) ‘Na katika mstari wa 21 na 22 tunaona kwamba Hawa aliumbwa, si kutokana na mnyama, bali kutokana na ubavu wa Adamu.’

Au unaweza kusema: ‘(Mkiisha kuelewana, kama ilivyo hapo juu . . . ) Watu fulani husema kwamba Adamu anayetajwa katika Biblia alikuwa mtu wa kubuniwa tu. Lakini ikiwa maoni hayo ni ya kweli, tunapaswa kukata kauli gani?’ (1) ‘Basi, ona yanayosemwa hapa katika Waroma 5:19: “Kama vile kupitia kutotii kwa mtu mmoja [Adamu] wengi walifanywa watenda-dhambi, vivyo hivyo pia kupitia kutii kwa mtu mmoja [Yesu Kristo] wengi watafanywa kuwa waadilifu.” Vivyo hivyo, andiko la 1 Wakorintho 15:22 linasema: “Kama vile katika Adamu wote wanakufa, vivyo hivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.” Lakini ikiwa kwa kweli hakukuwako “mtu mmoja” aliyeitwa Adamu, basi mtu huyo hakutenda dhambi kamwe. Ikiwa hakutenda dhambi na kuwapitishia watoto wake dhambi, basi Kristo hakuhitaji kuutoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu. Ikiwa Kristo kweli hakuutoa uhai wake kwa ajili yetu, basi hatuna tazamio lingine la kuishi isipokuwa miaka michache ambayo tunayo sasa. Hilo lingemaanisha kwamba Ukristo hauna faida.’ (2) ‘Hata hivyo, Ukristo una kanuni za juu zaidi za maadili ambazo haziwezi kupatikana mahali pengine. Je, mafundisho bora zaidi kuhusu kweli na haki yangeweza kutokana na kitu fulani ambacho si cha kweli hata kidogo?’ (Ona pia ukurasa wa 25-27, chini ya kichwa, “Adamu na Hawa.”)

‘Lakini watu wenye elimu ya juu wanaamini mageuzi’

Unaweza kujibu: ‘Ni kweli, hata hivyo nimeona kwamba hata wale wanaosema kwamba wanaamini mageuzi huenda wakatofautiana kabisa na wengine wanaoamini mageuzi. (Taja mifano kutoka habari iliyo katika ukurasa wa 162.) Kwa hiyo, sisi wenyewe lazima tuchunguze uthibitisho ili tuone jambo tunalopaswa kuamini—mageuzi au uumbaji.’

Au unaweza kusema: ‘Hilo ni kweli. Hata hivyo nimeona kwamba kuna watu wengine wenye elimu ya juu ambao hawaamini mageuzi.’ Kisha unaweza kuongezea: (1) ‘Kwa nini watu wana maoni tofauti? Wote wana uthibitisho uleule. Je, huenda ikawa wana nia zinazotofautiana? Inawezekana kwamba ndivyo ilivyo.’ (2) ‘Unaweza kuamuaje utamwamini nani? Unapotazama kikundi kizima (na bila kumchambua mtu mmoja-mmoja), ni kikundi kipi unachoona kingekuwa chenye kusema ukweli zaidi—wale wanaoamini kwamba mtu aliumbwa na Mungu na hivyo wanamtegemea, au wale wanaosema kwamba walitokea wenyewe tu na hivyo wanajitegemea wenyewe?’ (3) ‘Hivyo, basi, sisi wenyewe tunahitaji kuchunguza uthibitisho ili tuone kama uumbaji au mageuzi hutoa majibu yenye kuridhisha zaidi maishani.’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki