Norway
KNUD PEDERSON HAMMER, akiwa amesimama kwenye sitaha ya meli, alijawa na furaha nyingi alipoitazama pwani ya Norway. Awali, alihudumu katika Kanisa moja la Baptisti huko North Dakota, Marekani. Lakini mwaka mmoja mapema, Knud alikuwa amejiunga na Wanafunzi wa Biblia (ambao sasa ni Mashahidi wa Yehova). Sasa, katika mwaka wa 1892, alikuwa anarudi katika nchi alimozaliwa ili kuwahubiria marafiki na watu wa ukoo.
Wengi kati ya watu milioni mbili walioishi Norway walikuwa washiriki wa Kanisa la Kilutheri la Serikali. Knud alitamani sana kuwasaidia watu wanyoofu wa Norway kumjua Mungu wa kweli, Yehova, na pia kuwasaidia waelewe kwamba Mungu huyo mwenye upendo hawaadhibu watenda dhambi katika moto wa mateso. Alitaka pia kuwafundisha kuhusu Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo utakaoigeuza dunia kuwa paradiso.
Meli ilipokaribia pwani, Knud alitazama kwa makini nchi hii maridadi—nchi nyembamba yenye milima mirefu iliyofunikwa kwa theluji, mikono-bahari yenye kupendeza na misitu mikubwa. Alitambua kwamba haingekuwa rahisi kufikia maeneo yenye watu wachache sana na ambayo yalikuwa na madaraja na barabara chache tu. Ingawa watu wengi wa Norway waliishi katika miji iliyokuwa ikipanuka siku baada ya siku, wengine waliishi katika maeneo ya mashambani, vijiji vya wavuvi, au katika visiwa vingi katika pwani ya Norway. Matokeo ya kazi ya Knud ya kuhubiri, na vilevile ukuzi wa ibada safi nchini Norway licha ya matatizo, yanaimarisha imani na kuwachochea watu wa Mungu kila mahali.
MBEGU YA UFALME YAZAA MATUNDA
Ingawa watu fulani walipendezwa na ujumbe wake, Knud hakukaa sana Skien, jiji la nyumbani. Alilazimika kurudi kwa familia yao nchini Marekani. Hata hivyo, mnamo 1899, alirudi tena Norway baada ya kuombwa na Charles T. Russell aliyekuwa msimamizi wa kazi ya Wanafunzi wa Biblia wakati huo. Ndugu Russell alitaka Knud aanzishe kutaniko nchini Norway. Knud alibeba nakala kadhaa za mabuku mawili ya kwanza ya vitabu Millennial Dawn (baadaye viliitwa Studies in the Scriptures), ambayo yalikuwa yametafsiriwa katika mchanganyiko wa Kinorway na Kidenishi. (Wakati huo, maandishi ya Kinorway yalifanana na ya Kidenishi, na machapisho yangeweza kusomwa nchini Denmark na Norway.) Knud aliwahubiria watu wengi na kuwaachia vitabu, lakini baada ya muda alilazimika kurudi Marekani tena.
Mwaka uliofuata, Ingebret Andersen, ambaye aliishi karibu na jiji la Skien, alipata kitabu The Plan of the Ages, ambacho huenda kilikuwa mojawapo ya nakala ambazo Knud alileta Norway. Kwa muda mrefu, Ingebret alipendezwa na habari kuhusu kuja kwa Kristo kwa “mara ya pili,” na sasa yeye na mke wake Berthe, walivutiwa na mambo waliyosoma. Punde si punde, Ingebret akaanza kuhubiri. Hata alienda kwenye mikutano ya kidini ili kuwaambia watu kuhusu Utawala wa Miaka Elfu wa Kristo. Baadaye, aliwatembelea watu waliopendezwa, na muda si muda kukawa na kutaniko la angalau Wanafunzi wa Biblia kumi jijini Skien.
Knud alipoambiwa na mtu wa ukoo kuhusu kutaniko hilo dogo jijini Skien, alirudi Norway mwaka wa 1904 kumtafuta Ingebret. Alisimama barabarani na kumuuliza mwanamume fulani, “Je, unamfahamu Ingebret Andersen?” Mwanamume huyo akajibu, “Ndiyo, ni mimi.” Knud alisisimka sana hivi kwamba alifungua mkoba wake papo hapo katikati ya barabara, na akaanza kumwonyesha Ingebret vitabu alivyokuwa navyo. Ingebret naye alifurahi kukutana na Knud na kuona machapisho hayo mengi.
Knud aliwaambia kwa shauku waamini wenzake wa Norway kuhusu tengenezo na kazi ya kuhubiri. Kufikia wakati aliporudi kwa familia yake, ambayo kwa sasa waliishi Kanada, kutaniko la Skien lilikuwa limetiwa moyo sana kusonga mbele.
KUYAFIKIA MAENEO MENGINE YA NORWAY
Kazi ya kuhubiri nchini Norway ilipata nguvu zaidi mwaka wa 1903 wakati makolpota (wahubiri wa wakati wote) watatu wenye bidii walipofika kusaidia. Watatu hao walikuwa Fritiof Lindkvist, Viktor Feldt, na E. R. Gundersen. Fritiof aliamua kuishi jijini Kristiania (ambalo sasa ni Oslo), na mwaka wa 1904 nyumba yake ilifanywa ofisi ya Watch Tower Society, ambapo maagizo ya machapisho na maandikisho ya Zion’s Watch Tower yalishughulikiwa.
Mwishoni mwa mwaka wa 1903, Ndugu Gundersen alipokuwa anahubiri eneo la Trondheim, alizungumza na Lotte Holm, ambaye alikubali machapisho. Baadaye mwanamke huyo alienda nyumbani huko Narvik, eneo lililo juu ya Mzingo wa Aktiki, na akawa mhubiri wa kwanza kaskazini mwa Norway. Baada ya hapo, Viktor Feldt alienda Narvik, akawahubiria wanaume fulani wawili na wake zao, na wote wakawa Wanafunzi wa Biblia. Walimtafuta Lotte na baada ya muda mfupi, wakawa wanakutana pamoja kujifunza Biblia. Hallgerd, dada ya Lotte, pia alikubali kweli na baadaye wote wawili wakawa mapainia wenye bidii katika sehemu mbalimbali nchini Norway.
Ndugu Feldt na Gundersen walikuwa na matokeo mazuri sana walipohubiri Bergen mwaka wa 1904 na 1905. Gazeti la Zion’s Watch Tower la Machi 1, 1905 liliripoti hivi: “Mhubiri mashuhuri wa kanisa la Free Mission la [Bergen] amesadikishwa kabisa na nuru iliyo wazi, na sasa anawaeleza wengine kuhusu Injili yote na iliyo ya kweli.”
Mhubiri huyo alikuwa Theodor Simonsen, ambaye baadaye alifukuzwa kutoka Kanisa la Free Mission kwa sababu ya kufundisha kweli nzuri mpya ambazo alijifunza katika machapisho yetu. Hata hivyo, Wanafunzi wa Biblia walimkaribisha Ndugu Simonsen. Watu wa Yehova walimpenda Theodor sana na pia alikuwa msemaji mzuri. Mwishowe, Ndugu Theodor aliamua kuishi Kristiania ambapo kulikuwa na kutaniko lililokuwa likiongezeka.
BAADHI YA MAPAINIA WA KWANZAKWANZA
Mwaka wa 1905 hivi, kulikuwa na makutaniko ya Wanafunzi wa Biblia katika majiji manne, yaani, Skien, Kristiania, Bergen, na Narvik. Bila kukawia, wahubiri kadhaa wenye bidii wakaanza kufanya upainia na kupeleka habari njema katika maeneo mengine ya Norway. Mapainia hao wa kwanzakwanza walikuwa wa malezi yasiyo ya kawaida.
Dada painia wa kwanza alikuwa Helga Hess. Alikuwa yatima aliyeishi jijini Bergen, ambapo alianza kufundisha watoto mambo ya dini katika shule ya Jumapili akiwa na umri wa miaka 17. Alipomsikia Theodor Simonsen katika kanisa la Free Mission akisema mambo aliyokuwa amesoma katika mojawapo ya vitabu vya Wanafunzi wa Biblia, alivutiwa sana na akaanza kusoma vitabu hivyo. Akaacha kazi, na mwaka wa 1905, akiwa na umri wa miaka 19, akaenda kuhubiri habari njema jijini Hamar na Gjøvik.
Siku moja katika mwaka wa 1908, Andreas Øiseth alikuwa akikata miti katika shamba la familia yao karibu na Kongsvinger, wakati painia fulani alipomhubiria na kumwachia kitabu The Divine Plan of the Ages. Andreas, ambaye alikuwa na miaka 20 hivi, alipendezwa na mambo aliyosoma na akaagiza machapisho zaidi. Baada ya miezi kadhaa, aliwaachia ndugu zake wadogo usimamizi wa shamba lao na kuanza upainia. Kwa miaka minane iliyofuata, alihubiri karibu kila sehemu ya nchi. Kwanza, alielekea kaskazini akisafiri kwa baiskeli katika majira ya kiangazi, na wakati wa baridi kali alitumia kigari cha kujisukuma kwa mguu juu ya theluji. Alipofika Tromsø, alielekea kusini, akahubiri eneo lote la pwani mpaka Kristiania.
Anna Andersen kutoka eneo la Rygge, karibu na Moss, alikuwa pia mmoja wa mapainia wa kwanzakwanza. Kwa miaka mingi alikuwa ofisa wa Jeshi la Wokovu na alijitoa kuwasaidia maskini. Mwaka wa 1907 hivi, alisoma baadhi ya machapisho yetu na kugundua kwamba amepata kweli. Katika mji wa Kristiansund, alikutana na Hulda Andersen (baadaye Øiseth), ofisa mwingine wa Jeshi la Wokovu ambaye pia alipendezwa na Biblia. Muda si muda, wanawake hao wawili wakaanza safari ndefu kuelekea kaskazini kwa meli ya mvuke iliyosafiri kando-kando ya pwani hadi Kirkenes, karibu na mpaka wa Urusi. Walishuka katika kila bandari na kuwaachia watu machapisho. Anna alianza upainia katika mwaka wa 1912 hivi. Kwa miaka mingi, alisafiri kwa mashua na baiskeli, na akapeleka machapisho katika karibu miji yote nchini Norway. Alikaa kwa muda mjini Kristiansand, ambapo alilisaidia sana kutaniko.
Karl Gunberg alikuwa ofisa katika jeshi la wanamaji kabla ya kuwa Mwanafunzi wa Biblia. Alianza upainia mwaka wa 1911 hivi akiwa na miaka 30 na kitu, na alijitegemeza kwa kufundisha watu jinsi ya kujua mwelekeo wanaposafiri majini au hewani. Ingawa Karl alionekana mkali, alikuwa mtu mzuri na mcheshi. Alihubiri kotekote nchini Norway mpaka alipozeeka, na ujuzi wake aliopata akiwa mwanajeshi na mwalimu wa mambo ya usafiri ulisaidia sana katika kueneza habari njema kama tutakavyoona.
KUIMARISHA AKINA NDUGU
Oktoba 1905, ndugu wa Kristiania walifurahi sana kuwa na kusanyiko lao la kwanza. Watu 15 hivi walihudhuria na 3 wakabatizwa. Mnamo 1906, kusanyiko lingine lilifanywa jijini Bergen, na kuanzia 1909, makusanyiko yalifanywa kila mwaka, na wasemaji walitoka Denmark, Finland, na Sweden. Wengine kati ya wasemaji hao waliyatembelea makutaniko wakiwa mapilgrimu, ambao sasa wanaitwa waangalizi wanaosafiri.
Jambo lililowafurahisha sana akina ndugu katika miaka hiyo ni ziara za Ndugu Russell. Mwaka wa 1909 aliyatembelea majiji ya Bergen na Kristiania. Ndugu na dada walithamini sana pendeleo la kukutana naye na kusikiliza hotuba zake. Wengi walipata habari kuhusu ziara ya pili ya Ndugu Russell mnamo 1911 na hivyo ndugu 61 waliokusanyika, wakafurahi kuona hudhurio la watu 1,200 hivi wakati wa hotuba ya watu wote aliyotoa!
Miaka mitatu baadaye, Ndugu Russell alimwomba Henry Bjørnestad awatembelee ndugu wa Norway na Sweden kwa ukawaida akiwa mwangalizi wa kwanza kutoka Norway.
KUFANYA KAZI KWA BIDII ZAIDI KABLA YA 1914
Kifaa kizuri cha kuhubiri kilitolewa mnamo 1910 kwa njia ya mfululizo wa trakti Peoples Pulpit. Trakti hizo ziliwasaidia wengi wa Wanafunzi wa Biblia kushiriki kibinafsi katika kazi ya kuhubiri. Wakiwa na hamu kubwa ya kufunua makosa ya dini na kueleza kweli za Biblia, ndugu na dada walisambaza maelfu ya trakti hizo bila malipo na mara nyingi wakaziambatanisha na magazeti ya habari.
Wanafunzi wa Biblia walingoja kwa hamu kuona mambo ambayo yangetukia mwaka wa 1914. Kitabu The Time Is at Hand (buku la pili la Millennial Dawn,) kilieleza kwamba nyakati za Mataifa zingeisha 1914, kipindi ambacho kingekuwa na mchafuko na matatizo. Kisha, Ufalme wa Mungu ungeanza kutawala. Pia, Wanafunzi wa Biblia walitazamia kwamba warithi pamoja na Kristo wangeenda mbinguni wakati huo.
Jambo hilo lilizungumziwa sana. Kwa mfano, jioni moja mnamo Julai 1914, Karl Kristiansen alikuwa akicheza muziki pamoja na kikundi cha wanamuziki cha Skien. Wakati wa mapumziko, aliwaambia watu waliokuwa karibu naye hivi: “Baada ya majuma machache, jambo fulani litatokea. Kwanza kutakuwa na vita, kisha mageuzi, kisha mchafuko, na hatimaye Ufalme wa Mungu utakuja.” Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilipozuka muda mfupi baada ya hapo, watu walimwendea Karl wakitaka kujua zaidi.
Mjini Arendal, kulikuwa na Mwanafunzi wa Biblia mmoja tu katika mwaka wa 1914. Siku moja, dada huyo alikutana na Mia Apesland barabarani na kumwambia kwamba kulingana na Biblia, kungekuwa na vita katika majira ya kupukutika kwa majani mwaka wa 1914. “Hilo likitukia, nitakuwa mwamini,” Mia akajibu. Muda mfupi baadaye, Mia alipoona mambo ambayo dada huyo alisema yakitukia, akawa mwamini kama alivyoahidi. Mia, dada aliyemhubiria, na wengine wachache wakaanzisha Kutaniko la Arendal.
MAENDELEO, KISHA MATATIZO
Matazamio ya mwaka wa 1914 ya Wanafunzi wa Biblia hayakutimia yote kama walivyotarajia. Hata hivyo, waliendelea kuhubiri kwa bidii. Kuanzia Desemba 1914 mpaka 1915 sinema yenye kuvutia iliyoitwa “Photo-Drama of Creation,” ilitumiwa kutoa ushahidi mzuri kwa watu wengi huko Kristiania, Bergen, Trondheim, Skien, Arendal, na Kristiansand.
Hata hivyo, matatizo yalizuka muda mfupi baadaye. Fritiof Lindkvist, ambaye alikuwa amesimamia kazi kwa miaka kumi hivi, alianza kufuata maoni yake mwenyewe, na kufikia 1916, aliacha kushirikiana na tengenezo. Kwa hiyo, ndugu kutoka Sweden na Denmark wakachukua daraka hilo kwa miaka michache iliyofuata. Mnamo 1921, Enok Öman alipewa jukumu la kusimamia kazi nchini Norway, na alifanya hivyo mpaka 1945.
Kulikuwa pia na msukosuko kidogo mnamo 1916 C. T. Russell alipokufa na mahali pake kama msimamizi wa kazi ya Wanafunzi wa Biblia pakachukuliwa na J. F. Rutherford. Kwa sababu ya kutotimia kwa matazamio fulani ya 1914 na pia mabadiliko ya usimamizi, wengi waliacha kushirikiana na tengenezo. Kutaniko la Bergen hasa liliathiriwa sana kwa kuwa ni ndugu mmoja tu na dada saba waliobaki kutanikoni kufikia 1918. Mjini Trondheim, wengi waliacha kushirikiana na kutaniko na kikundi fulani jijini Kristiania kikasambaratika. Lakini, wale walioshikamana na tengenezo walifurahia baraka nyingi za Yehova muda mfupi baadaye.
NGUVU MPYA
Mnamo 1918, Ndugu Rutherford alitoa hotuba yenye kusisimua yenye kichwa, “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe.” Kuanzia 1920 mpaka 1925, hotuba hiyo yenye kuchochea ilitolewa ulimwenguni pote. A. H. Macmillan kutoka makao makuu jijini New York alikuja Norway kutoa hotuba hiyo katika majiji kadhaa. Huko Kristiania, ukumbi wa chuo kikuu ulijaa kabisa hivi kwamba wengi walikosa nafasi. Hata hivyo, Ndugu Öman alisimama mlangoni juu ya sanduku fulani na kutangaza: “Mkirudi baada ya muda wa saa moja na nusu, Macmillan atatoa hotuba hiyo tena!” Na kwa hakika, watu walijaa tena katika jumba hilo na Ndugu Macmillan akatoa hotuba hiyo kwa mara ya pili. Kwa miaka kadhaa iliyofuata, ndugu wa Norway walitoa hotuba hiyo kotekote nchini. Maelfu ya watu walisikiliza kwa makini uthibitisho wa Kimaandiko kwamba wengi wataokoka Har–Magedoni na kuishi milele katika dunia paradiso. Wengi pia walipokea ujumbe kupitia kijitabu Millions Now Living Will Never Die!
Tangu 1922 mpaka 1928, Wanafunzi wa Biblia walisambaza mamia ya maelfu ya trakti zenye maazimio ambayo yalifikiwa katika makusanyiko, kama vile, Mwito kwa Viongozi wa Ulimwengu, Onyo kwa Wakristo wote, na Makasisi Washtakiwa. Wengi wa Wanafunzi wa Biblia walianza kuhubiri kwa kusambaza trakti hizo.
Lakini ukuzi ulichukua muda. Ijapokuwa wahubiri wenye bidii na mapainia walihubiri bila kuacha, wengine walihitaji msaada ili kushiriki zaidi katika kazi ya kuhubiri. Isitoshe, bado hakukuwa na machapisho katika Kinorway bali yalipatikana tu katika lugha za Kidenishi, mchanganyiko wa Kidenishi na Kinorway au Kiswedi. Ni nini kingefanywa ili kuchochea bidii katika kazi?
Jarida Bulletin (sasa Huduma Yetu ya Ufalme) la Kinorway la Aprili 1925 lilikuwa na tangazo hili lenye kufurahisha: “Tunawatangazia nakala ya kwanza ya The Golden Age katika Kinorway. Mnaweza kutuma maandikisho ya gazeti hilo.” Hiyo ilikuwa nakala ya Machi 1925 ya The Golden Age (sasa Amkeni!). Punde si punde, Golden Age la Kinorway lilikuwa likisomwa na wengi nchini Norway na Denmark. Kufikia 1936, Golden Age la Kinorway lilipobadilishwa jina na kuitwa Ny Verden (Ulimwengu Mpya), kulikuwa na watu 6,190 walioandikisha gazeti hilo.
USIMAMIZI BORA NA JENGO JIPYA
Wanafunzi wa Biblia zaidi ya 500 kutoka nchi mbalimbali za Skandinavia walihudhuria kusanyiko lililofanywa Mei 1925, huko Örebro, Sweden. Katika kusanyiko hilo, Ndugu Rutherford alitangaza kwamba Ofisi ya Ulaya Kaskazini ingefunguliwa jijini Copenhagen, Denmark. William Dey kutoka London angesimamia kazi ya watu wa Mungu nchini Denmark, Norway, Sweden, Finland, na nchi za Baltiki. Lakini, kila nchi ingekuwa na ndugu mwenyeji anayesimamia kazi, na Enok Öman aliendelea kusimamia kazi nchini Norway.
William Dey, mzaliwa wa Scotland, alikuwa mwenye nguvu na alifanya mengi ili kuharakisha kazi ya kuhubiri. Alikuwa stadi wa kupanga mambo na aliwatia moyo akina ndugu kupitia uchangamfu wake na mfano mzuri katika huduma. Miezi ya Septemba na Oktoba 1925, alisafiri kotekote nchini Norway kuratibu utendaji wa makutaniko kulingana na miongozo kutoka makao makuu. Alitumia mkalimani kwa kuwa alizungumza Kiingereza. Ndugu Dey alisimamia kazi katika Ofisi ya Ulaya Kaskazini mpaka wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu.
Kwa muda fulani, akina ndugu walikuwa wakitafuta mahali pazuri kwa ajili ya ofisi ya Norway. Mnamo 1925, ndugu mmoja aliyekuwa amerithi kiasi fulani cha pesa alinunua nyumba ya ghorofa mbili jijini Oslo na akawauzia Wanafunzi wa Biblia karibu nusu ya bei aliyoinunua. Nyumba hiyo ilipatikana kwa wakati unaofaa kabisa! Jengo hilo lilitumika mpaka 1983.
TENGENEZO LA MASHAHIDI WENYE BIDII
Katika mwaka wa 1931, watumishi wa Mungu duniani pote walipiga hatua muhimu sana katika historia. Walichukua jina jipya, yaani, Mashahidi wa Yehova. Ndugu Öman aliandika, “Tulikubali jina letu jipya kwa kusimama na kusema ‘Ja’ [Ndio] kwa sauti kubwa sana.” Ndugu walifurahi sana kuwa na jina la Kimaandiko, na waliazimia kuishi kulingana na jina hilo.
Ilikuwa wazi kwamba Yehova alibariki bidii ya kazi nchini Norway. Idadi ya wahubiri iliongezeka kutoka wastani wa 15 mwaka wa 1918 na kufikia 328 katika 1938. Watu wa Yehova hawakuwa tu Wanafunzi wa Biblia; walikuwa mashahidi wenye bidii.
Mmoja wao ni Even Gundersrud, mshiriki wa Kutaniko la Skien aliyebatizwa mwaka wa 1917. Mwanzoni, mke wake alificha viatu vya Even ili kumzuia asihudhurie mikutano. Lakini hilo halikumzuia. Alienda mikutanoni hata bila viatu! Pindi fulani, alimfungia katika chumba cha kulala lakini Even akatoka kupitia dirishani. Hakuna chochote mke wake angefanya ili kumzuia Even asihudhurie mikutano. Ijapokuwa hayo yote, Even aliendelea kumwonyesha fadhili. Mwanamke huyo akaanza kuona aibu kwamba mume wake anaenda jijini bila viatu. Akaanza kuandamana naye ili ajionee kile kilichomfanya Even aithamini sana mikutano. Hatimaye, yeye pia akawa Shahidi wa Yehova.
Kama Kutaniko la Skien, makutaniko yalikuwa na bidii sana wakati huo. Ndugu wa Skien walihubiri sana katika majiji yaliyokuwa karibu, miji, na maeneo ya mashambani. Wakati wa miisho-juma, walisafiri kwa malori yaliyokuwa wazi nyuma au mashua, wakihubiri na kupanga mikutano. Baada ya muda mfupi, vikundi na makutaniko mapya yakaanzishwa katika eneo hilo. Makutaniko mengine pia yalikuwa na bidii sana ya utendaji wa kiroho.
MAENDELEO KATIKA ENEO LA BERGEN
Mmoja wa wahubiri katika eneo la Bergen alikuwa Torkel Ringereide. Katika mwaka wa 1918 alipata broshua iliyochapishwa na Wanafunzi wa Biblia. Akamtafuta Dahl, ndugu pekee katika kutaniko la Bergen wakati huo. Ndugu Dahl alifanya mikutano nyumbani mwake na washiriki wengine wa kutaniko hilo ambao walikuwa dada saba. Mmoja wao ni Helga Hess, aliyetajwa mapema na ambaye sasa alikuwa amerudi Bergen. Torkel alijiunga na kutaniko hilo dogo na akamwoa Helga mwaka wa 1919.
Torkel alijulikana kwa ujasiri na sauti yake yenye nguvu. Kwa miaka mingi, ni yeye tu aliyetoa hotuba kutanikoni. Kwa kawaida, alitoa hotuba kila Jumapili, akifunua waziwazi unafiki wa makasisi na mafundisho yao ya uwongo. Mara nyingi, hotuba hizo zilitangazwa kwenye magazeti ya habari, na idadi ya watu waliohudhuria ilizidi ile ya Wanafunzi wa Biblia katika eneo hilo.
Torkel aliwatia moyo wasikilizaji wawaeleze wengine kweli walizojifunza. Mnamo 1932, Nils Raae alisikia mwito wa Torkel. Kwa mwaka mmoja, Nils alikuwa amejua kweli lakini alisita kuhubiri. Wakati huo, kutaniko lilitaka kuanza kampeni kubwa ya kuwaachia watu kijitabu The Kingdom, the Hope of the World, na Torkel alitoa hotuba kuhusu umuhimu wa kushiriki katika huduma. Nils alisema: “Hotuba hiyo ilikuwa nzuri ajabu na ilinisisimua sana.” Kumalizia hotuba yake, Torkel alinukuu maneno ya Yehova kwenye Isaya 6:8: “Nitamtuma nani, na ni nani atakayeenda kwa ajili yetu?” Kisha akasema: “Acheni sote tujibu kama alivyojibu Isaya: ‘Mimi hapa! Nitume mimi’!” Hicho ndicho kichocheo ambacho Nils na mke wake walihitaji. Bila kukawia, wakaanza kuhubiri.
Ndugu na dada waliwatembelea sana Torkel na Helga. Nyakati zote walizungumzia kweli za Biblia na hivyo waliwatia moyo sana wahubiri wapya na wachanga. Mara nyingi, wahubiri wa Bergen walitumia mashua na malori kwenda kuhubiri katika maeneo yaliyowazunguka. Baadaye, walikutana kueleza mambo yaliyoonwa na kufurahia ushirika pamoja.
WAHUBIRI WENYE BIDII WA OSLO
Katika miaka ya 1920 na 1930, kazi ya kuhubiri ilikuwa ikiendelea vizuri sana katika eneo la Oslo. Olaf Skau, aliyebatizwa mwaka wa 1923 alikuwa mmoja wa wahubiri katika eneo hilo. Aliwekwa rasmi kuwa mwelekezi wa utumishi kutanikoni mwaka wa 1927 na kwa miaka mingi alitumika akiwa mwangalizi mwenye kujali na ambaye alitafuta njia za kuboresha huduma. Alipanga kazi jijini Oslo na pia akapanga safari za miisho-juma za kwenda kuhubiri nje ya jiji kwa basi au lori. Alikaa macho hadi usiku wa manane akichora ramani na kupanga safari za utumishi.
Wahubiri kutoka Oslo walihubiri pia katika miji, majiji na maeneo ya mashambani. Walihubiri Halden, Fredrikstad, Hamar, Kongsvinger, Drammen, na Hønefoss. Kwa kawaida, walifika kwenye eneo saa 3 asubuhi na kuhubiri nyumba kwa nyumba mchana kutwa. Mara nyingi walifanya mikutano pia. Utendaji huo ulisaidia kuanzisha vikundi na makutaniko mapya na ulithaminiwa sana na ndugu na dada wachache walioishi katika maeneo hayo. Katika mojawapo ya kampeni hizo mwaka wa 1935, wahubiri 76 kutoka Oslo waliwaachia watu vijitabu 13,313, wastani wa vijitabu zaidi ya 175 kwa kila mhubiri!
Esther, mke wa Olaf aliugua ugonjwa wa yabisi na alitumia kiti cha magurudumu. Licha ya hayo, nyumba yao haikukosa wageni. Kwa kawaida, Olaf ndiye aliyepika na alitambulika sana kwa upishi bora wa mabawa ya kuku. Lakini, Mashahidi wengi wanakumbuka zaidi mambo yenye kujenga kiroho, mazungumzo ya Biblia yenye kusisimua, na maswali ya Biblia waliyokuwa nayo nyumbani mwa Ndugu Skaus. “Sikuzote tuliondoka kwake tukiwa tumejengwa kiroho,” asema Ragnhild Simonsen.
“MWELEKEO UNAOFAA KWA AJILI YA UZIMA WA MILELE”
Kitambo, watu walipenda dini zaidi na walikuwa na ujuzi zaidi wa Biblia kuliko sasa. Wengi walipendezwa na mazungumzo ya Biblia na kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, ‘wale waliokuwa na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele wakawa waamini.’—Mdo. 13:48.
Mfano wa watu kama hao ni Durdei Hamre. Mnamo 1924, alipokea kijitabu fulani ambacho alisoma usiku wote. Alisema hivi baadaye, “Nilienda kulala nikiwa Mpentekoste, nikaamka nikiwa Shahidi wa Yehova.”
Katikati ya miaka ya 1920, mmoja kati ya ndugu wanane wa familia ya Fjelltvedt, alisikiliza hotuba ya watu wote kuhusu moto wa mateso na akapata kijitabu kilichozungumzia jambo hilo. Mambo aliyosoma yalimsadikisha kwamba fundisho la moto wa mateso ni la uwongo. Muda mfupi baadaye, familia yao ilipokusanyika katika shamba lao, aliwaeleza ndugu zake saba na dada watatu mambo aliyokuwa amejifunza. Walizungumzia kijitabu hicho mpaka usiku wa manane. Punde baadaye, ndugu na dada zake wote na wengi wa wenzi wao wa ndoa wakawa Wanafunzi wa Biblia. Baadaye, wengi wa watoto wao na wajukuu wao wakawa wahubiri wenye bidii, na wengine wakapeleka kweli katika maeneo mengine.
Uthamini wa mambo ya kiroho wa watu wa Norway ulionekana wazi mnamo 1936 wakati M. A. Howlett kutoka makao makuu jijini New York alipokuja kutoa hotuba makusanyikoni jijini Bergen na Oslo. Huko Bergen, watu 810, kutia ndani wahudumu fulani wa dini na askofu mmoja, walisikiliza hotuba ya watu wote. Kati ya wasikilizaji hao wote, Mashahidi walikuwa 125 tu. Nako jijini Oslo, kulikuwa na Mashahidi 140 tu miongoni mwa watu 1,014 waliosikiliza hotuba ya watu wote!
‘WANAANZA KUKUSANYWA!’
Mashahidi wa Yehova walifurahi sana mwaka wa 1935 walipoelewa wazi utambulisho wa “umati mkubwa” unaotajwa katika Ufunuo 7:9-17. Walifurahi kujua kwamba waabudu wa Mungu walio na tumaini la kuishi katika dunia paradiso wangeweza kujiweka wakfu na kumtumikia Yehova pamoja na mabaki ya watiwa mafuta. Tangu mwaka huo na kuendelea, kazi kubwa zaidi katika historia ya wanadamu ikaanza,yaani, kukusanywa kwa umati mkubwa wa waabudu wa kweli ambao wataokoka “ile dhiki kuu.”
Mwaka wa 1935, mapainia fulani wenye tumaini la kwenda mbinguni walihubiri sehemu fulani ya mashambani karibu na Lillehammer. John Johansen mwenye umri wa miaka 10 alisikiliza kwa makini mapainia hao walipoeleza familia yao kuhusu kusudi la Mungu la kuifanya dunia kuwa paradiso. Alipokuwa na umri wa miaka 13, John alitamani sana kuwaeleza wengine kuhusu tumaini lake zuri hivi kwamba akaomba mkoba wa baba yake na kwenda kuwahubiria majirani akiwa peke yake! Sasa, zaidi ya miaka 70 baadaye, John, akiwa na mke wake Edith, anaendelea kuhubiri kwa bidii na kufurahia kwamba amechangia katika ongezeko kubwa la Mashahidi wapya kwa miaka hiyo yote.
Siku moja, mwaka wa 1937, Olaf Rød akiwa kwake nyumbani pamoja na ndugu mmoja walizungumza kuhusu umati mkubwa. Hakukuwa na Mashahidi wengine katika eneo hilo la Haugesund na hivyo waliwaza jinsi kazi kubwa ya kukusanya umati mkubwa ingefanywa. Ghafula, mlango ukabishwa. Olaf akafungua mlango na kumwona Alfred Trengereid. Alfred alikuwa amesoma nakala ya Mnara wa Mlinzi na kuvutiwa na yale aliyosoma. Bila kukawia, alipanda mashua yake na kwenda Haugesund ili apate vitabu kutoka kwa Olaf, kwa kuwa alijua Olaf ni Shahidi. Olaf alishangaa sana. ‘Sasa, wanaanza kukusanywa!’ Olaf akawaza. Na kwa kweli walikusanywa, ingawa si kwa njia ileile wala kwa wakati uleule. Alfred na wengine kutoka eneo la kwao waliokubali habari njema za Ufalme wakawa Mashahidi.
MASHUA ZASAIDIA KUKUSANYA UMATI MKUBWA
Kazi ya kuhubiri ilipoanza nchini Norway, ilionekana kwamba ingekuwa vigumu kuwafikia watu walioishi kwenye visiwa vingi sana vya nchi hiyo, na maeneo mengine ya pwani yaliyo mbali. Hivyo, mnamo 1928, ofisi ya tawi ilinunua mashua yenye injini, ambayo ingewatosha mapainia wawili au watatu na yenye nguvu inayoweza kuabiri pwani ya Norway iliyochongoka sana. Lakini nani angekuwa nahodha wa mashua hiyo? Karl Gunberg, painia mwenye uzoefu alijitolea. Ujuzi wake alipokuwa katika jeshi la wanamaji na pia akiwa mwalimu wa mambo ya usafiri ulimsaidia sana. Mashua ya kwanza iliyoitwa Elihu, ilianza safari huko Oslo, ikaelekea kaskazini huku ikitia nanga katika bandari mbalimbali. Hata hivyo, usiku mmoja wa majira ya baridi kali ya mwaka wa 1929, kulitokea dhoruba kubwa iliyoiharibu mashua hiyo karibu na Stavanger. Wote walishukuru kwamba ndugu katika mashua hiyo walifika ufuoni salama.
Mnamo 1931 ndugu walipata mashua nyingine waliyoiita Ester. Kwa mara nyingine tena, Karl akashika usukani akisaidiwa na ndugu wengine wawili. Ester ilitumiwa magharibi na kaskazini mwa Norway kwa miaka saba iliyofuata. Mwaka wa1932, Karl alihisi kwamba “amezeeka na hivyo hawezi kuendelea na safari hizo.” Kwa hiyo, akamwachia Johannes Kårstad usukani na akatumika akiwa painia katika eneo la mashariki mwa Norway. Mwaka wa 1938, mashua iliyoitwa Ruth ilichukua mahali pa Ester na ikatumiwa mpaka 1940, wakati kazi ya kuhubiri kwa mashua ilipokoma kwa sababu ya Vita vya Pili vya Ulimwengu. Wahubiri hao wa kutumia mashua walihubiri maeneo mengi na kuwaachia watu machapisho mengi. Katika mwaka wa 1939, Andreas Hope na Magnus Randal waliotumia mashua Ruth, waliripoti kwamba kwa mwaka mmoja tu, waliwaachia watu zaidi ya vitabu 16,000, vijitabu, magazeti, na watu 2,531 wakasikiliza hotuba kwenye gramafoni mara 1,072.
Kando na matokeo mazuri ya kiroho, ndugu hao pia waliona mandhari zenye kupendeza. Andreas Hope alisema, “Kila siku tulielekea kaskazini tukiingia na kutoka ndani ya mikono-bahari na kuzunguka rasi refu. Mandhari ilikuwa maridadi sana.” Wakati wa majira ya baridi kali, wakiwa upande wa kaskazini ya Mzingo wa Aktiki waliona “uzuri wa ajabu wa mianga ya kaskazini [aurora borealis].” Na wakati wa kiangazi, waliduwazwa na “uangavu wa jua la usiku wa manane.”
DADA PAINIA MWENYE BIDII
Katika miaka ya 1930, idadi ya mapainia iliongezeka haraka. Wakiwa na vitu vichache maishani, walihubiri maeneo mengi, wakiwaeleza watu habari njema na kuwaachia machapisho. Jitihada na bidii yao iliweka msingi wa ukuzi wa wakati ujao.
Kwa mfano, Solveig Løvås (baadaye Stormyr), kutoka Oslo, alitamani sana kujua kweli na alihudhuria mikutano mbalimbali ya kidini. Siku moja, alihudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova na akatambua kwamba amepata kweli ya Biblia. Alibatizwa mwaka wa 1933, na miaka miwili baadaye akaenda kufanya upainia kaskazini mwa Norway. Ingawa alichechemea kidogo kwa sababu ya polio, kwa miaka sita tu alihubiri katika majiji mengi, miji, vijiji vya wavuvi, na kwa jamii ndogo-ndogo kuanzia kusini ya Bodø mpaka Kirkenes. Maelfu walikubali machapisho ya Biblia. Kwa mwaka mmoja tu, Solveig alipata maandikisho 1,100 ya magazeti yetu!
Mmoja aliyependezwa sana na ujumbe wa Solveig ni seremala anayeitwa Dag Jensen wa kijiji cha Hennes katika eneo la Vesterålen. Kwa miaka mingi alipata machapisho yetu kutoka kwa watu wengine waliopendezwa. Solveig alipokutana naye, alifanya mipango ili Dag apate andikisho la magazeti yetu, kisha akaenda kuhubiri katika maeneo mengine. Dag alianza kuhubiri akiwa peke yake na kuwaazima machapisho watu waliopendezwa.
Kisiwani Andøya, Solveig aliwafikia wavuvi fulani wenye miraba minne katika kibanda chao kidogo. Aliwatolea ushahidi mzuri, wakasikiliza hotuba kwenye gramafoni, na kuwaeleza kuhusu maandikisho ya magazeti. Frits Madsen, alipendezwa na akaandikisha magazeti yetu. Solveig alipomaliza eneo hilo, alielekea kwingine. Huo ndio ulikuwa mtindo wakati huo—mapainia walihubiri, wakapata watu wanaopendezwa, wakawaachia machapisho na kupata maandikisho ya magazeti, na kisha, wakaelekea eneo lingine. Ni nini kingefanywa ili kuwasaidia watu wanaopendezwa?
KUWACHUNGA KONDOO WA MUNGU
Mpango mpya kwa ajili ya waangalizi wanaosafiri ulianzishwa Januari 1939. Norway iligawanywa katika kanda au mizunguko minne. Waangalizi wa mzunguko (wakati huo waliitwa watumishi wa kanda) waliagizwa watumie muda mwingi zaidi kila mahali kuliko walivyofanya awali. Walikazia hasa kuyasaidia makutaniko, kupanga makutaniko mapya, na kuwasaidia watu wanaopendezwa waanze kuhubiri. Andreas Kvinge aliwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa Mzunguko namba 4, uliokuwa na urefu wa kilomita 2,600 kuanzia Florø mpaka Kirkenes. Eneo hilo lote lilikuwa na makutaniko matatu tu—Trondheim, Namsos, na Narvik. Lakini alipaswa kutembelea wahubiri na vikundi vilivyokuwa maeneo ya mbali, na vilevile watu walioandikisha magazeti.
Andreas na mke wake Sigrid, walitumia baiskeli kuelekea kaskazini. Alijitahidi kuwasaidia wahubiri na waliopendezwa kufanya maendeleo ya kiroho. Mapainia kama Solveig Løvås walitoa habari zaidi kuwahusu watu waliopendezwa na ambao walihitaji msaada wa kiroho. Kwa mfano, Solveig alimweleza Andreas kuhusu Dag Jensen wa Hennes na Frits Madsen wa kisiwa cha Andøya.
Alipokutana na Dag mara ya kwanza mwaka wa 1940, “alikuwa ananyoa ndevu na uso wake ulijaa sabuni,” asema Andreas. “Sitasahau kamwe macho yake yaliyong’aa. Alisahau kabisa kwamba alikuwa ananyoa.” Andreas alimsaidia Dag kufanya maendeleo ya kiroho. Dag alikuwa na bidii sana na punde si punde, akamsaidia mke wake Anna, wengi wa rafiki zake, na pia watu wa ukoo, kujifunza kweli.
Huko Bleik, kisiwani Andøya, Andreas alimtafuta Frits Madsen. Kwa msaada wa Andrea, Frits na mke wake wakawa Mashahidi wa kwanza katika kutaniko lililoanzishwa huko baadaye. Katika sehemu nyingine nyingi, Andreas na mke wake waliwatembelea watu ambao walikuwa wamehubiriwa na Solveig na mapainia wengine wenye bidii. Andreas na waangalizi wengine wa mzunguko walipanga mikutano na kuanzisha makutaniko. Kama ilivyokuwa katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, wahubiri fulani nchini Norway walipanda, na wengine wakatia maji, lakini “Mungu akaendelea kuikuza” kwa njia kubwa.—1 Kor. 3:6.
VITA VYA PILI VYA ULIMWENGU VYATIKISA NORWAY
Mnamo Aprili 1940, majeshi ya Ujerumani yaliivamia Norway, na hivyo nchi hiyo ikalazimika kujiunga na vita vya pili vya ulimwengu. Baada ya siku 62 tu, nchi yote ikawa chini ya Ujerumani ya Wanazi. Kufikia wakati huo, miji mingi ilikuwa imevamiwa kwa makombora. Siku chache baada ya uvamizi kuanza, askari wa Gestapo walimkamata Enok Öman aliyekuwa mwangalizi wa tawi na kumweka kizuizini kwa juma moja. Walimhoji kifupi na kumwachilia. Majuma kadhaa baadaye, askari hao wakamchukua tena ili wamhoji.
Ndugu waliogopa kwamba Wanazi wangewapeleka kwenye kambi za mateso kama ilivyokuwa nchini Ujerumani. Hata hivyo, Wanazi hawakufanya hivyo, na wahubiri waliendelea kuhubiri kwa bidii. Kwa kweli, watu walisikiliza habari njema vizuri zaidi kwa sababu ya vita, na mafunzo mengi ya Biblia (ambayo wakati huo yaliitwa mafunzo ya kigezo) yakaanzishwa. Hata hivyo, waliendelea kupokea gazeti la Mnara wa Mlinzi katika Kidenishi, huku lile la Consolation (Ny Verden) likiendelea kuchapishwa katika Kinorway. Bado walifanya mikutano na makusanyiko na jambo la kushangaza ni kwamba idadi ya wahubiri iliongezeka.
KUNYANG’ANYWA VITABU, KUKAMATWA, NA KISHA MARUFUKU
Matatizo yalikuwa njiani. Kwa mara nyingine tena, polisi wa Ujerumani walikuja kwenye ofisi ya tawi, wakaitisha machapisho na kumhoji Ndugu Öman. Mwishoni mwa 1940, polisi hao waliwanyang’anya akina ndugu kitabu Enemies, kwa sababu ya maelezo yake kuhusu utawala wa Kifashisti na wa Wanazi. Mapema mwaka wa 1941, polisi walikamata na kuwahoji mapainia kadhaa. Wakati mwingine, Wanazi wa Ujerumani na wa Norway walihudhuria mikutano ili kufanya upelelezi. Kisha, Wanazi wakaja ofisini na kuchukua akiba yote ya vijitabu viwili, Fascism or Freedom na Government and Peace.
Mnamo Julai 1941, Gestapo walianza jitihada za kusimamisha kazi ya kuhubiri kotekote nchini Norway. Polisi watano Wajerumani walikuja Betheli, wakachukua machapisho yaliyobaki na kuwapeleka Wanabetheli wote kwenye makao makuu ya polisi ili kuwahoji. Ndugu Öman alipaswa kuripoti kwa polisi kila siku, na alifanya hivyo kwa majuma 12.
Wakiwa wamejipanga vizuri, Gestapo walivamia nyumba za ndugu wenye majukumu na kuchukua machapisho yote ya Watch Tower Society. Waliwaambia akina ndugu kwamba wangepelekwa katika kambi za mateso iwapo hawangeacha kuhubiri. Gestapo waliwakamata ndugu na dada kadhaa na kuwazuia wengine kwa siku chache.
Huko Moss, polisi walienda kwa Sigurd Roos na kuchukua machapisho yake. Wakamkamata Sigurd, mke wake, na ndugu mwingine. Polisi hao waliwaamuru waache kuhubiri na kutumia jina Yehova. Wahubiri hao walieleza kwamba hawawezi kamwe kuacha kuhubiri kumhusu Yehova na Ufalme wake. Hatimaye, polisi wakasema: “Hatuwezi kuwanyang’anya imani yenu.” Baada ya saa chache, wahubiri hao wenye imani thabiti wakaachiliwa.
Wanazi pia walienda kwa Olaf Skau, jijini Oslo. Waliipekua nyumba yake na kuchukua Biblia, machapisho, gramafoni, na wakafunga kabisa kabati lake la vitabu. Maofisa hao hawakupata kadi za rekodi ya wahubiri zilizokuwa zimefichwa ndani ya oveni. Baadaye walirudi na lori ili kubeba machapisho. Aliyesimamia polisi hao alikuwa Luteni Klaus Grossmann, Mnazi aliyeogopwa sana. Alipoulizwa na Olaf kuhusu kile ambacho wangefanya na machapisho hayo, alisema kwamba wangeyasaga-saga.
“Kwani hamwogopi Yehova?” akauliza Ndugu Skau.
Luteni huyo akajibu kwa kejeli, “Yehova anapaswa kujichunga sana!” Wanazi walipojisalimisha miaka minne baadaye, Grossmann akajiua.
Gestapo walimkamata Andreas Kvinge huko Bodø Julai 1941 na kumwuliza mahali walikokuwa Mashahidi wa kaskazini mwa Norway. Andreas alijibu kwa unyoofu, “Sijui wako wapi leo.” Wazia jinsi Andreas alivyohisi wakati maofisa hao walipotawanya sakafuni vitu vilivyokuwa mkobani mwake, yaani, karatasi zenye orodha ya majina na anwani za makutaniko, watumishi wa makutaniko, na watu wanaopendezwa. Jambo la kupendeza ni kwamba, hakuna ofisa hata mmoja aliyejishughulisha kusoma karatasi hizo. Tamaa yao kubwa ilikuwa ni kumfanya Andreas atie sahihi taarifa ya kukubali marufuku dhidi ya Mashahidi wa Yehova na kazi ya kuhubiri.
Andreas aliwaambia, “Tunajua kwamba kazi yetu imepigwa marufuku, kwa hiyo ninaweza kutia sahihi taarifa hii. Lakini, hata mkitukataza kufanya mikutano na kuwapa watu magazeti na vitabu, tutaendelea kuwaeleza watu kuhusu Ufalme wa Mungu tukitumia Biblia.” Hatimaye, Gestapo walimwachilia Andreas walipoona kwamba hatalegeza msimamo wake.
Mwishowe, Wanazi wenye mamlaka walichukua jengo lililotumiwa kama ofisi ya tawi. Waliwaruhusu Ndugu na Dada Öman kubaki lakini wakawaagiza Wanabetheli hao wengine waondoke.
KUKUTANA PAMOJA WAKATI WA MARUFUKU
Kwa sababu ya jitihada za Wanazi za kuwakomesha Mashahidi wa Yehova, ndugu waliendeleza utendaji wao wa kitheokrasi kisiri. Baadhi ya akina ndugu waliwatembelea ndugu na dada ili kuwatia moyo. Søren Lauridsen, ambaye awali alitumika Betheli kwa muda fulani, alitembelea ndugu wa Norway kusini. Naye Andreas Kvinge aliendelea kuwatembelea Mashahidi wa kaskazini mwa Norway, huku akifanya vibarua mara kwa mara ili kuficha utendaji wake. Mnamo 1943, Magnus Randal, ambaye awali alitumia mashua Ruth, alipata anwani kadhaa kutoka kwa Ndugu Öman na kuelekea kaskazini kwa baiskeli, umbali wa kilomita 1,200, mpaka Bodø ili kuwatia moyo ndugu na dada.
Ingawa wenye mamlaka waliwakataza kukutana, ndugu na dada waliendelea kukutana wakiwa vikundi-vikundi ili kutiana moyo. Kwa kawaida, vikundi vilikutana katika nyumba za watu lakini wakati mwingine wangekutana kisiri wakiwa wengi. Walifurahi sana mwaka wa 1942 watu 280 walipohudhuria Ukumbusho uliofanywa katika maeneo mawili tofauti jijini Oslo, na 90 wakashiriki kula mkate na kunywa divai.
Vilevile, Mashahidi walikusanyika kisiri katika mashamba ya mbali au katika misitu midogo. Kusanyiko kubwa zaidi kati ya hayo, lilifanywa katika msitu fulani karibu na kijiji cha Ski mwaka wa 1943. Ndugu na dada 180 hivi kutoka eneo la mkono-bahari wa Oslo walihudhuria. Wakati wa mapumziko, askari-jeshi Wajerumani wakiwa juu ya farasi wakatokea ghafula. Ndugu wangefanya nini?
Ndugu mmoja ambaye alizungumza Kijerumani aliongea nao na wakamwambia kwamba walitaka kwenda kuogelea lakini wamepotea njia. Akina ndugu hawakusita kuwaonyesha njia.
Walipokuwa wakiondoka, mmoja wao aliuliza wenzake, “Unafikiri ni kwa nini watu hao wamekusanyika?”
“Nafikiri hicho ni kikundi cha wanakwaya,” mwenzake akajibu. Hakuna ndugu au dada aliyetaka kurekebisha maoni yao. Wote walifurahi kuona wapanda-farasi hao wakitokomea msituni.
KUFANYA KAZI KISIRI
Wahubiri wengi walificha machapisho katika sehemu zisizo za kawaida. Machapisho yalizikwa na kufukuliwa yalipohitajiwa. Ndugu Skau, aliyefanya kazi ya vifaa vya umeme, alificha katoni ya vitabu nyuma ya transfoma kazini mwake. Ndugu Øiseth alificha machapisho katika mzinga wa nyuki, naye Ndugu Kvinge akaficha yake ndani ya pipa la viazi.
Kwa kuhofia kwamba depo ya vitabu jijini Harstad ingegunduliwa, Lotte Holm alienda huko kuondoa makatoni yote ya vitabu. Alipanda mashua, akapanga makatoni hayo vizuri, na kuketi juu yake. Safari ilipoanza, Lotte alishangaa kuona askari-jeshi wengi Wajerumani kwenye mashua na akasumbuka sana akilini alipofikiria jinsi ambavyo angepakua makatoni hayo bila kugunduliwa. Hata hivyo, alitaabika bure. Mashua ilipotia nanga, askari-jeshi hao walimhurumia mwanamke huyo mzee aliyekuwa na mizigo mingi mizito na hivyo wakamsaidia kupakua makatoni hayo na hata wakayabeba mpaka nyumbani kwake. Hawakujua jinsi tendo lao la fadhili lilivyowanufaisha Mashahidi wakati huo.
Licha ya marufuku, ndugu waliendelea kupata nakala za karibuni zaidi za Mnara wa Mlinzi kisiri, kutoka Sweden na Denmark. Walitafsiri makala za funzo katika Kinorway na kusambaza kotekote nchini nakala walizochapa. Kulikuwa na mfumo wa usambazaji na ndugu walisafiri kwa gari-moshi, baiskeli, au mashua ili kuhakikisha waabudu wa kweli nchini kote wamepata chakula cha kiroho kwa wakati wake.
WALIENDELEA KUHUBIRI
Wakati wa vita, hali fulani ilitokea ambayo ilidhibitika kuwa jaribu kwa ndugu na dada wa Norway. Kazi yetu ilipopigwa marufuku mwezi wa Julai 1941, ndugu waliombwa wawe waangalifu ili wasikasirishe mamlaka ya Wanazi. Hivyo, wengi waliwahubiria isivyo rasmi marafiki, watu wa ukoo, na watu waliokuwa wamezungumza nao awali. Hata hivyo, ndugu fulani hawakupenda njia hiyo ya kuhubiri na wakaona ni sawa kuhubiri nyumba kwa nyumba wakitumia Biblia tu. Ingawa hawakukubaliana kuhusu njia inayofaa ya kuhubiri, wote walikuwa na hamu kubwa ya kumtumikia Yehova kwa uaminifu licha ya upinzani.
Ndugu wangefanya nini? Yaelekea suluhisho halingepatikana upesi kwa sababu vita vilizuia mawasiliano kati yao na makao makuu jijini New York. Je, ndugu wangeruhusu tofauti hizo zidhoofishe imani yao? Au wangeendelea kuhubiri kadiri ya uwezo wao huku wakimngojea Yehova ashughulikie mambo kupitia tengenezo lake?
Ni wazi kwamba Yehova alibariki utumishi wao wa uaminifu kwa sababu wakati wa vita, kulikuwa na ongezeko sawa na lile walilokuwa nalo miaka mitano kabla ya vita. Licha ya vita, marufuku, na njia tofauti za kuhubiri, kilele cha wahubiri kiliongezeka kutoka 462 mwaka wa 1940 mpaka 689 mwaka wa 1945. Jambo lililowafanya washangilie.
WAUNGANISHWA KATIKA UTUMISHI WA YEHOVA
Vita vilipokoma mwaka wa 1945, William Dey alikuja Norway mwezi wa Julai na Agosti kuwasaidia ndugu kupanga upya utendaji wao. Ndugu Dey alipanga mikutano huko Oslo, Skien, na Bergen na akawasihi ndugu wote washirikiane katika jitihada zao. Alitaja kwamba Yehova amewabariki, wamepata ongezeko, na wanaweza kusonga mbele wakiwa na uhakika wa mwongozo wa Yehova.
Mnamo Septemba 1945, Nathan H. Knorr, wa makao makuu aliwasiliana na Marvin F. Anderson, Mmarekani mwenye asili ya Denmark, aliyekuwa na umri wa miaka 28. Awali Anderson alitumika Betheli ya New York lakini wakati huo alikuwa mwangalizi wa mzunguko nchini Marekani. Ndugu Knorr alimwuliza Ndugu Anderson kama angekubali kwenda Norway kushughulikia mambo fulani na kuishi huko “kwa miaka kadhaa.” Anderson alikubali, ijapokuwa angefika huko baada ya miezi kadhaa.
Hata hivyo, Ndugu Knorr na Ndugu Henschel walienda Norway mnamo Desemba 1945. Mwongozo waliotoa kwa upendo uliwasaidia ndugu kupendana zaidi na kudumisha umoja. Wakati huohuo, Ndugu Knorr alitangaza kuwa Ndugu Dey angechukua mahali pa Ndugu Öman kama msimamizi wa tawi. Mwezi mmoja baadaye, Ndugu Anderson aliwasili, na akawekwa rasmi kuwa msimamizi wa tawi mwezi wa Februari. Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, watumishi wa Yehova kotekote nchini Norway walizidisha bidii yao katika huduma wakiwa na nguvu mpya, na uhakikisho wa baraka za Yehova.
TENGENEZO LA YEHOVA LASONGA MBELE
Kufikia wakati ambapo Marvin Anderson alifika Norway, ofisi ya tawi ilikuwa na utendaji mwingi. Mnamo Septemba 1945, wahubiri walipokea kijitabu kimoja katika Kinorway na vingine vinne katika Kiswedi. Mwezi uliofuata, gazeti la Mnara wa Mlinzi la Oktoba 1, 1945, lilichapishwa katika Kinorway na baadaye machapisho mengine.
Jambo fulani lenye kuchekesha linaonyesha umuhimu wa kuwa na machapisho katika Kinorway. Kijitabu kimoja cha Kiswedi kilikuwa na kichwa Hopp—neno la Kiswedi linalomaanisha “tumaini.” Hata hivyo, katika Kinorway, neno “hopp” linamaanisha “ruka.” Ilibidi wahubiri waeleze kwamba ujumbe wao wa tumaini haukuhitaji wasomaji waruke!
Ndugu Anderson alipowekwa kuwa mwangalizi wa tawi mwaka wa 1946, ofisi ya tawi ilikuwa ndogo sana, hivyo aliishi katika chumba kimoja na ndugu wengine watano. Wakaaji wasio Mashahidi waliokuwa wakiishi katika jengo hilo tangu enzi za Nazi walihamishwa ili kupata nafasi kwa ajili ya familia ya Betheli iliyokuwa ikiongezeka.
Ndugu Anderson alikuwa na bidii sana katika mgawo wake mpya. Jengo la ofisi lilifanyiwa marekebisho na vifaa vipya vikanunuliwa, kutia ndani matbaa inayoendeshwa kwa mguu. Mwaka wa 1946 shule yenye kusisimua ilianzishwa makutanikoni, yaani, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Hatimaye, ndugu wengi zaidi wangeweza kuzoezwa kutayarisha na kutoa hotuba, na baada ya muda mfupi wengi wakastahili kutoa hotuba za watu wote.
Makusanyiko ya kwanza baada ya vita yalifanywa Oslo, Bergen, na Trondheim mwezi wa Septemba na Oktoba 1946. Kwa jumla, katika sehemu hizo tatu, watu 3,011 walihudhuria hotuba ya watu wote yenye kichwa “Mkuu wa Amani,” na 52 wakabatizwa—idadi kubwa kwelikweli ikizingatiwa kwamba wakati huo kulikuwa na wahubiri 766 tu nchini Norway.
Mnamo Desemba 1946, kazi ya kuyazungukia makutaniko ilianzishwa tena baada ya kukatizwa kwa zaidi ya miaka mitano. Ndugu kadhaa vijana, ambao baadhi yao walikuwa wametumika Betheli, waliwekwa rasmi kuwa waangalizi wanaosafiri (waliokuwa wakiitwa watumishi wa akina ndugu). Mojawapo ya kusudi lao kuu lilikuwa kuwazoeza wahubiri katika huduma ya nyumba kwa nyumba, na walijaribu sana kuhubiri na wengi iwezekanavyo katika kila kutaniko. Gunnar Marcussen, mmoja wa waangalizi vijana wakati huo, aeleza kwamba katika makutaniko fulani alihubiri na kati ya wahubiri 50 na 70 wakati wa ziara ya juma moja. Hatua kwa hatua, wahubiri walipata uzoefu katika kuwasilisha ujumbe wa Ufalme na wakaacha kutumia kadi za kutoa ushahidi na gramafoni, zilizokuwa zimetumiwa tangu miaka ya 1930. Walizingatia pia kufanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Biblia.
KUWACHOCHEA WAHUBIRI WAWE MAPAINIA
Baada ya vita, wahubiri walitiwa moyo wafanye upainia ili kusaidia idadi kubwa ya watu waliopendezwa na ujumbe wa Ufalme. Hivyo, wahubiri wengi walioacha upainia kazi yetu ilipokuwa imepigwa marufuku mwaka wa 1941, wakarudia utumishi wa wakati wote. Ingawa hali ya uchumi ilikuwa ngumu, kufikia mwishoni mwa mwaka wa 1946, kulikuwa na jumla ya mapainia 47 nchini Norway.
Svanhild Neraal, alikuwa mmoja wa mapainia hao. Dada huyo alisafiri upande wa kaskazini hadi jimbo la Finnmark mwaka wa 1946. Svanhild alikuwa amefanya upainia huko mwaka wa 1941 akiwa na Solveig Løvås na walijionea miji ya Kirkenes na Vardø ikilipuliwa na mabomu. Svanhild hakuwasahau watu wenye kupendezwa ambao yeye na Solveig walihubiria huko, kwa hiyo akaamua kurudi Kirkenes, mji uliokuwa umeharibiwa na vita. Svanhild alipohamia eneo hilo bila kujua mahali atakapoishi, wenyeji walifikiri kwamba amerukwa na akili.
Hata hivyo, Svanhild alimtegemea Yehova, na wakati wa majira ya kwanza ya baridi kali, alilala jikoni kwenye sakafu katika nyumba ndogo ambamo watu wengine watano waliishi. Hali zilikuwa mbaya sana baada ya vita na alivumilia mambo mengi magumu. Mara nyingi, akiwa ananyeshewa, alisubiri mashua ambazo zilichelewa au hata kutowasili kabisa.
Svanhild alifurahia mambo mengi alipowahubiria Wasami. Aliposhindwa kuwafikia katika maeneo yao ya mbali kwa basi, alitumia mashua au baiskeli. Wasami ni wakarimu na mara nyingi walimkaribisha ndani ya mahema yao yaliyotengenezwa na ngozi ya mbawala na kumsikiliza kwa makini alipowahubiria kwa msaada wa mkalimani. Wakati wa chakula, walimkaribisha kwa mlo wa nyama ya mbawala. Baadaye, baadhi ya watu waliohubiriwa na Svanhild waliikubali kweli.
Kjell Husby, aliyekuwa anatumika Betheli wakati huo, alisema kwamba nyakati zote ofisi ya tawi ilijua mahali ambapo Svanhild alikuwa hasa kwa sababu ya anwani za maandikisho aliyotuma. Kwa miaka mitatu aliyoishi Finnmark, alipata maandikisho 2,000 ya Mnara wa Mlinzi na kuwaachia watu vitabu 2,500!
“WAVUVI WA WATU”
Baada ya vita, wahubiri pia walishiriki kwa shangwe katika kazi ya kuhubiri na wakapata matokeo yenye kutia moyo. Wakati wa vita, Dag Jensen, aliyetajwa awali, aliwahubiria marafiki na watu wa ukoo katika kijiji kidogo cha Hennes mjini Vesterålen. Wengi walipendezwa na wakajifunza Biblia wakitumia vitabu vyetu. Vita vilipokoma mwaka wa 1945, Dag akabatizwa. Mwaka uliofuata, kutaniko lilipoanzishwa Hennes, watu 16 walibatizwa nyumbani kwa Dag. Miaka mitano baadaye, kutaniko hilo lilikuwa na karibu wahubiri 50, na katika mwaka wa 1971, Dag aliripoti kwamba zaidi ya wahubiri 20 kutanikoni walikuwa wameanza upainia.
Wengine walichochewa na upendo wa Dag kwa Yehova na bidii yake katika huduma. “Dag alipoingia katika nyumba yoyote,” akumbuka Åshild Rønning, aliyelelewa katika kutaniko hilo, “hungekosa kuona furaha na shangwe yake. Sifa zake ziliwavutia wengi.” Sikuzote Dag aliwatia moyo watoto, hasa walipokuwa na migawo katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. “Alifanya tuhisi kwamba tuliyofanya yalikuwa muhimu,” asema Åshild. Kutokana na kutiwa moyo kwa njia hiyo, Åshild alianza upainia mwaka wa 1962 na amepata shangwe ya kuwahubiria wengine “habari njema yenye utukufu ya Mungu mwenye furaha,” Yehova.—1 Tim. 1:11.
Ni nini kilichowafanya wengi katika sehemu hiyo wakubali kweli na kuwa Mashahidi wenye bidii? Ingawa wengi kutoka jamii hiyo ndogo hawakuwa wafuasi wa dini, walimwamini Mungu na waliiamini Biblia. Isitoshe, Mashahidi wengi walijulikana katika jamii kuwa vichwa vizuri vya familia ambao waliungwa mkono na wake zao washikamanifu. Mmoja wa kichwa cha familia ni Arnulf Jensen, mpwa wa Dag, aliyebatizwa mwaka wa 1947. Alifanya kazi ya uvuvi, na katikati ya juma alienda baharini kwa siku kadhaa kuvua samaki akitumia mashua yake. Lakini kila Ijumaa jioni, alirudi nyumbani, hata kama samaki walikuwa wengi na wavuvi wengine wangetaka kuendelea kuvua ili wapate pesa nyingi zaidi. Arnulf alihakikisha kwamba alikuwa nyumbani mwishoni mwa juma ili kuhudhuria mikutano na kushiriki katika kazi ya kuhubiri pamoja na mke wake na watoto wao wanane, ambao wote walichukua msimamo imara kwa ajili ya kweli. Mara nyingi, siku za Jumamosi na Jumapili, akina ndugu walitimiza utume wao wa kuwa “wavuvi wa watu,” wakitumia mashua ya Arnulf kufanya kazi ya uvuvi wa kiroho katika maeneo ya mbali.—Marko 1:16-18.
“TUNATIMIZA KAZI MUHIMU”
Mazoezi ambayo wamishonari hupata katika Shule ya Gileadi huko New York yamewasaidia sana akina ndugu nchini Norway. Hans Peter Hemstad na Gunnar Marcussen, waliohitimu kutoka Gileadi mwaka wa 1948, walikuwa wanafunzi wa kwanza kutoka Norway. Walitumwa Norway na kutumika katika kazi ya kuzungukia makutaniko na pia Betheli, mwanzoni wakiwa waseja na baadaye wakiwa pamoja na wake zao. Tangu 1948 hadi 2010, wahubiri 45 hivi kutoka Norway walihitimu kutoka Shule ya Gileadi. Zaidi ya nusu yao walitumwa Norway na wametumikia wakiwa wahubiri wa wakati wote au waangalizi wanaosafiri au washiriki wa familia ya Betheli.
Andreas Hansen kutoka Denmark na Kalevi Korttila kutoka Finland walikuwa miongoni mwa wamishonari wa kwanza-kwanza kutoka Shule ya Gileadi waliotumwa Norway. Mwaka wa 1951 walitumwa Finnmark Mashariki, ambako walihubiri eneo kubwa kwa mashua, baiskeli, na kwa viatu vya kuteleza kwenye theluji. Mara nyingi walizungumza na watu waliokuwa wamehubiriwa na Svanhild Neraal miaka kadhaa mapema. Kwa sababu hiyo, baada ya mwaka mmoja tu, idadi ya wahubiri katika eneo lao ikaongezeka kutoka 3 hadi 15!
Kjell Martinsen kutoka eneo la Hennes, huko Vesterålen, alihitimu kutoka Gileadi mwaka wa 1953 na kupewa mgawo nchini Norway. Akiwa na umri wa miaka 22, aliyazungukia makutaniko katika majimbo ya Vestfold na Telemark. Ingawa aliogopa kutumika akiwa mwangalizi anayesafiri kwa sababu ya umri wake mdogo, anakumbuka jinsi alivyokaribishwa kwa shauku na ushirikiano mzuri aliopata kutoka kwa ndugu waliokuwa na uzoefu zaidi. Kjell alitumika akiwa mwangalizi wa mzunguko mpaka mwaka wa 2001 wakati yeye na mke wake, Jorunn, walipoamua kuishi Svolvær katika wilaya ya Lofoten ambapo Kjell alitumika akiwa painia.
Karen Christensen kutoka Denmark alifanya upainia mwaka wa 1950 katika mji wa Egersund na Kongsvinger, ambako hakukuwa na makutaniko. Alisafiri kwa baiskeli ili kuhubiri katika maeneo hayo. Baada ya kuhitimu kutoka Gileadi mwaka wa 1954, alitumwa Kongsberg. Mwaka wa 1956 aliolewa na Marvin Anderson na wametumika Betheli tangu wakati huo. Karen amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 60. Anasema: “Sisi ni watu wa kawaida tu, lakini tunatimiza kazi muhimu.”
HATUA KUBWA ZA KISHERIA
Kuanzia mwaka wa 1948 hadi 1951, kulikuwa na ongezeko kubwa. Mwaka wa 1951, idadi ya wastani ya wahubiri iliongezeka kwa asilimia 29 kufikia kilele cha wahubiri 2,066. Hata hivyo, wakati huohuo watumishi wa Yehova nchini Norway walikabili matatizo fulani ya kisheria.
Kesi iliyowavutia wengi ilihusiana na kuhubiri barabarani kwa kutumia gazeti la Mnara wa Mlinzi. Mnamo Novemba 1949, wahubiri fulani waliotoa ushahidi barabarani jijini Oslo walikamatwa na kupelekwa katika kituo cha polisi, kisha wakaachiliwa baada ya saa chache. Wakiwa na ujasiri, Mashahidi hao walihubiri barabarani tena mwisho-juma uliofuata. Kisha, mnamo Desemba 6, 1949, wote waliohubiri barabarani jijini Oslo walikamatwa. Waliambiwa kwamba hawaruhusiwi kuwapa watu magazeti barabarani bila idhini ya polisi. Polisi walidai kwamba kazi yao ilisababisha msongamano na usumbufu na kuzuia utaratibu wa uendeshaji magari. Wahubiri saba kati yao walihojiwa na kupelekwa mahakamani ambapo walihitajika kulipa faini ndogo au kukaa siku tatu gerezani.
Kwa kuwa hicho hakikuwa kisa cha kupata kibali cha polisi tu bali kilitia ndani haki ya kueleza imani yao ya kidini kwa uhuru, akina ndugu walikata rufani kwa Mahakama Kuu Zaidi ya Norway. Mwakilishi wa habari wa Mashahidi wa Yehova, John Roos alisema katika gazeti la Dagbladet kwamba kazi yetu ya kuhubiri barabarani haijawahi kamwe kusababisha usumbufu wowote. Aliongeza: “Ikiwa kazi ya kuhubiri inafanywa barabarani bila usumbufu, kuzuia magari, au kusababisha msongamano wa watu, je, kuna sababu yoyote ya kupata idhini ya polisi? Au raia yeyote ana haki ya kuhubiri kwa sababu ya uhuru wa kidini?” Wakiwa wanasubiri uamuzi wa Mahakama Kuu Zaidi, Mashahidi waliendelea kuhubiri barabarani licha ya kukamatwa mara nyingi na kutozwa faini kubwa. Wahubiri fulani walikamatwa mara kumi hivi.
Mnamo Juni 17, 1950, Mahakama Kuu Zaidi ilibatilisha uamuzi wa mahakama ya mji, na wahubiri wakaachiliwa huru! Uamuzi huo na maamuzi mengine mazuri yalithibitisha kwamba Mashahidi wa Yehova wana haki ya kisheria nchini Norway ya kuwapa watu machapisho yanayotegemea Biblia barabarani na nyumba kwa nyumba, bila kuomba idhini kutoka kwa polisi.
MAKUSANYIKO YA KUKUMBUKWA
Katika miaka ya 1950 na 1960, makusanyiko mengi yasiyosahaulika yaliimarisha tengenezo na kuwasaidia Mashahidi kuwa na uhusiano wa karibu. Nathan H. Knorr na Milton G. Henschel, wa makao makuu, walikuwa miongoni mwa wasemaji waliotoa hotuba katika kusanyiko la kitaifa lililofanywa huko Lillehammer mwaka wa 1951. Wahudhuriaji walitoka kotekote nchini. Walifurahi kuona watu 89 wakibatizwa na 2,391 wakisikiliza hotuba ya watu wote! Katika miaka iliyofuata, wajumbe kutoka Norway walifurahi kuhudhuria makusanyiko ya kimataifa katika jiji la London na New York. Kisha, mnamo 1955, Mashahidi 2,000 hivi kutoka Norway walihudhuria kusanyiko la kimataifa jijini Stockholm, nchini Sweden.
Kusanyiko la kimataifa la mwaka wa 1965 lenye kichwa “Neno la Kweli” lililofanywa katika uwanja wa michezo wa Ullevål, jijini Oslo lilikuwa la pekee sana. Hata hivyo, kulikuwa na tatizo fulani. Timu ya kandanda ya Norway ilikuwa icheze na timu nyingine ya kitaifa katika uwanja huohuo jioni iliyotangulia programu. Umati wa Mashahidi ulisubiri nje ya malango hadi mashabiki wa kandanda walipoondoka, kisha wakaingia ili kutayarisha uwanja huo kwa ajili ya kusanyiko. Walifanya kazi usiku kucha wakisafisha, kuondoa taka, na kujenga mahema ya vyakula. Pia, walijenga majukwaa, kibanda cha muziki, na kwa ajili ya mapambo, wakajenga bohari, na vibanda vingine vitatu, vyote vikiwa na paa za nyasi. Gazeti la Dagbladet lilisema: “Muujiza wakati wa usiku. Uwanja wa michezo wa Ullevål umebadilishwa na kuwa mahali patulivu penye kuvutia . . . Bidii yenye kustaajabisha ya Mashahidi wa Yehova.”
Akina ndugu na dada wa Norway waliwakaribisha manyumbani mwao wajumbe zaidi ya 7,000, wengi wao kutoka nchi ya Denmark. Mahema yalijengwa katika uwanja fulani nje ya jiji. Yalifaa hali ya hewa ilipokuwa nzuri. Hata hivyo, wajumbe 6,000 waliokaa katika mahema hayo hawatasahau kamwe mvua iliyonyesha na kufanya uwanja huo ujae matope siku za kwanza za kusanyiko hilo. Kila mtu alifurahi hali ya hewa ilipobadilika siku mbili za mwisho. Licha ya hali mbaya ya hewa, wenyeji na wageni walifurahia ushirika wa Kikristo, na programu hiyo ya wakati unaofaa iliwaburudisha. Walishangilia sana kuona watu 199 wakibatizwa, na kilele cha wahudhuriaji 12,332 wakati wa hotuba ya watu wote iliyotolewa na Ndugu Knorr!
“KUHUBIRI NI SEHEMU MUHIMU SANA YA MAISHA YETU”
Mbali na kuhubiri nyumba kwa nyumba na barabarani, ndugu na dada wengi wamekuwa na matokeo mazuri wanapohubiri isivyo rasmi. Mwaka wa 1936, Konrad Flatøy, aliyekuwa mchochea-makaa katika merikebu moja, alimpa mfanyakazi mwenzake kijitabu. Mfanyakazi huyo, Paul Bruun, alikubali kijitabu hicho na kukisoma usiku huohuo.
Paul alisema: “Mara moja niligundua kwamba hii ndiyo kweli, na kijitabu hicho kilinionyesha tofauti kati ya dini ya kweli na ya uwongo.” Kadiri Paul alivyoendelea kujifunza zaidi, ndivyo alivyoanza kuwahubiria wengine. Wakati wa vita, alimfunza Biblia baharia mmoja aliyependezwa na kweli. Baharia huyo alipoendelea kupata ujuzi zaidi, aliamua kwamba hatatumia bunduki zilizokuwa ndani ya merikebu. Wenye mamlaka walipopata kujua msimamo wake, walimwamuru Paul aache kumfundisha Biblia. Paul alikataa na kwa sababu hiyo, yeye na baharia huyo wakaachwa katika pwani ya London. Mwezi mmoja baadaye, merikebu hiyo iligongwa na kombora la chini ya maji na ikazama. Baadaye, baharia huyo alibatizwa, naye Paul akaalikwa kuhudhuria Shule ya Gileadi. Alipohitimu mwaka wa 1954, akatumwa atumike akiwa mmishonari nchini Ufilipino. Baadaye, alirudi Norway na kutumika akiwa mwangalizi anayesafiri pamoja na mke wake, Grethe.
Katika mwaka wa 1948, Holger Abrahamsen alifanya kazi ya kuwapeleka na kuwarudisha wafanyakazi kutoka katika meli kubwa ya kutoa vitu chini ya maji katika bandari ya Narvik. Holger alizoea kusema: “Kuhubiri ni sehemu muhimu sana ya maisha yetu, hatuwezi kuishi bila kuhubiri.” Hivyo, Holger alitumia kila fursa kuwahubiria abiria wake. Mmoja wa abiria hao, Olvar Djupvik, alipendezwa na akamwambia mchumba wake, Anne Lise, kuhusu tumaini la Paradiso. Wote walibatizwa na baadaye wakawalea wana wao wanne katika kweli. Hermann, mmoja wa wana hao, akawa mmishonari nchini Bolivia pamoja na mke wake, Laila. Baadaye, walirudi Norway, na sasa Hermann ni mwangalizi anayesafiri.
KUTUNZA KONDOO WA YEHOVA
Katika miaka ya 1960 na 1970, marekebisho muhimu ya kitengenezo yalifanywa katika ofisi ya tawi na makutanikoni. Roar Hagen alichukua mahali pa Marvin Anderson aliyekuwa mwangalizi wa ofisi ya tawi. Kisha, mwaka wa 1969, Thor Samuelsen akawekwa rasmi kuwa mwangalizi wa ofisi ya tawi. Mwaka wa 1976, Halmashauri ya Tawi ikawekwa rasmi, na Thor Samuelsen, Kåre Fjelltveit, na Niels Petersen wakawa washiriki wa kwanza wa halmashauri hiyo.
Mnamo Oktoba 1972, mabaraza ya wazee yaliwekwa rasmi kuyachunga makutaniko kiroho. Wanaume wakomavu makutanikoni walisaidiwa kusitawisha sifa za kustahili ili kuwachunga wapya wengi walioikubali kweli ya Biblia. Tangu wakati huo, Yehova amewabariki sana watu wake wanapoendelea kutumikia kwa ushikamanifu chini ya usimamizi wake wenye upendo.
WASAMI WAKUBALI HABARI NJEMA
Kwa miaka mingi, mapainia wengi pamoja na wahubiri wengine wamewahubiria Wasami, kutia ndani wachungaji wa mbawala katika nyanda za mlima Finnmarksvidda. Ingawa Wasami wengi huzungumza Kinorway, wakati mwingine wahubiri wamelazimika kutumia wakalimani. Mmoja wa Mashahidi wa kwanza kuhubiri kwa mapana na marefu katika Kisami alikuwa Aksel Falsnes, mwenye asili ya Sami na aliyezungumza Kisami, Kinorway, na Kifini. Dada yake aliyeishi kusini mwa Norway, ambaye alikuwa amejifunza kweli, alimtumia kitabu chetu kimoja alichokisoma kwa hamu kubwa. Hakukuwa na Mashahidi katika eneo la Troms, ambamo aliishi, lakini katika mwaka wa 1968 mapainia kadhaa pamoja na mwangalizi wa mzunguko walimtembelea Aksel na kumsaidia kufanya maendeleo ya kiroho.
Aksel alikuwa mhubiri mwenye bidii. Mara nyingi aliibeba baiskeli yake katika mtumbwi wake mapema asubuhi, akavuka mkono wa bahari, na kisha akatumia baiskeli kutembelea jamii moja hadi nyingine. Kwa kuwa alijua Kisami, Aksel aliwahubiria Wasami kwa mafanikio katika sehemu za mbali za Finnmark.
Aksel alikuwa mtu mkakamavu, na alisafiri sana akitumia viatu vya kuteleza kwenye theluji ili kufika maeneo ya mbali. Kwa mfano, wakati fulani mwishoni mwa majira ya baridi kali, alisafiri kwa kuteleza kwenye theluji kutoka Karasjok akipitia nyanda za mlima hadi Kautokeino na kisha akaelekea Alta. Kile tu alichoweza kubeba ni mfuko wa kubeba mgongoni uliokuwa na vitu vichache vya kibinafsi pamoja na machapisho kadhaa. Baada ya majuma machache, alifika Alta, kwa rafiki zake, akiwa amesafiri umbali wa kilomita 400 akitumia viatu vya kuteleza kwenye theluji!
Mwanzoni mwa miaka ya 1970, Wasami kadhaa waliikubali kweli. Mjini Hammerfest, mwanamke mmoja Msami pamoja na mume wake walianza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Baada ya muda mfupi, baadhi ya watu wake wa ukoo walioishi Alta wakapendezwa pia. Arne na Marie Ann Milde, waliokuwa mapainia wa pekee huko Alta, wakaanza kujifunza Biblia na watu hao wanyoofu na mara nyingi watu 10 au 12 walihudhuria funzo. Hatimaye, karibu nusu ya watu hao wakawa Mashahidi.
Hartvig Mienna, painia Msami huko Alta, ambaye hutumia kigari kinachoendeshwa juu ya theluji ili kuwafikia watu walio mbali asema: “Si rahisi kuhubiri katika eneo la Wasami. Maeneo yao yako mbali sana na wengi wanashikilia desturi zao. Lakini wao ni wakarimu sana, na tumefanikiwa kuanzisha mafunzo kadhaa ya Biblia.”
MIAKA AMBAYO MENGI YALITARAJIWA
Kulikuwa na idadi iliyozidi kuongezeka ya wahubiri kuanzia katikati ya miaka ya 1960 hadi katikati ya miaka ya 1970. Hata hivyo, imani ya baadhi ya akina ndugu ilijaribiwa kuhusiana na matarajio ya mwaka wa 1975. Dhiki kuu ilipokosa kuja mwaka wa 1975, watu fulani waliacha tengenezo, na kati ya mwaka wa 1976 na 1980, idadi ya wahubiri ikapungua kidogo. Wengine waliotamaushwa walipunguza utendaji wao wa Kikristo kwa muda. Hata hivyo, wengi walikuwa na maoni gani kuhusiana na utumishi wao kwa Yehova?
“Kulikuwa na matarajio na msisimko kuhusiana na mwaka wa 1975,” akiri Hans Jakob Lilletvedt, “lakini imani yangu haikutegemea mambo hayo.”
“Hatukujiweka wakfu kwa Yehova tukiwa na tarehe hususa akilini, kwa hiyo tuliendelea na utendaji wetu bila kufanya mabadiliko yoyote,” walisema John na Edith Johansen, Mashahidi wa muda mrefu.
“Nitamtumikia Yehova milele, si hoja ikiwa mwisho utakuja mwaka wa 1975 au baadaye,” akasema Lea Sørensen.
OFISI YA TAWI MPYA
Kazi ilizidi kuongezeka katika ofisi ya tawi kuelekea mwishoni mwa miaka ya 1970. Hivyo, kulikuwa na uhitaji wa kuongeza idadi ya Wanabetheli, vyumba vya makao, na sehemu ya kufanyia kazi. Hivyo, mwaka wa 1979, Baraza Linaloongoza likaidhinisha mipango ya kujenga ofisi ya tawi mpya nje ya jiji la Oslo. Kuelekea mwishoni mwa mwaka wa 1980, akina ndugu walipata mahali panapofaa katika eneo la Ytre Enebakk, kilomita 30 hivi kutoka katikati mwa jiji la Oslo.
Ili kupunguza gharama za ujenzi, wajitoleaji walialikwa kujenga jengo hilo. Haikuwa rahisi kupata vifaa vya ujenzi, kuandaa vyakula na makao kwa ajili ya watu 100 hivi na kupangia mradi mzima.
Jumla ya ndugu na dada zaidi ya 2,000 ‘walijitoa kwa hiari,’ kutia ndani ndugu waliotoka nchi nyingine. (Zab. 110:3) Wengi walisaidia kwa kutoa viazi, mboga, matunda, mikate, mayai, samaki, mavazi na vifaa. Wengine walikata miti msituni huku wengine wakiipasua na kutengeneza mbao. Wengine wengi walisaidia kwa kuchanga pesa na kutoa mikopo bila riba.
Baadhi ya wafanyakazi stadi walisaidia kwa muda mfupi tu, hivyo kazi nyingi ilifanywa na wajitoleaji wasio na ustadi. John Johnson aliyesimamia kazi zote za kuweka umeme, aeleza jinsi yeye na wasimamizi wengine wa ujenzi walivyohisi kuwa hawastahili. John anasema: “Wajitoleaji walijifunza kufanya kazi na wakaifanya vizuri sana. Ilipendeza kuona jinsi matatizo yalivyotatuliwa. Ilikuwa wazi kwamba Yehova Mungu alikuwa anaongoza ujenzi huo.”
Kwa sababu ya bidii ya wajitoleaji, ukarimu wa akina ndugu na dada, na baraka za Yehova, kazi iliendelea vizuri. Ujenzi ulianza mapema mwaka wa 1981, na mnamo Mei 19, 1984, wakati wa ziara ya Milton Henschel wa Baraza Linaloongoza, ofisi hiyo mpya ya tawi ikawekwa wakfu. Mradi huo wa ujenzi ulikuwa chanzo cha umoja na shangwe kubwa kwa akina ndugu nchini Norway. Katika miaka iliyofuata, baada ya mradi huo wa ujenzi, wajitoleaji wengi wa ujenzi walijiandikisha kuwa mapainia wasaidizi au wa kawaida.
KUHARAKISHA KAZI YA UJENZI WA MAJUMBA YA UFALME
Mwaka wa 1928, ndugu wanne wa familia ya Fjelltvedt walijenga jumba la kwanza kwa ajili ya waabudu wa Yehova katika kitongoji kimoja huko Bergen. Kufikia mwanzoni mwa miaka ya 1980, makutaniko mengi yalikuwa yamejenga au kununua Majumba yao ya Ufalme. Hata hivyo, bado makutaniko mengi yalifanya mikutano katika majumba ya kukodisha yasiyofaa. Wakati wa ujenzi wa ofisi ya tawi, ndugu fulani walizungumzia jinsi ambavyo wangeweza kuharakisha ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Walijua kwamba vikundi fulani vya akina ndugu nchini Marekani na Kanada walikuwa wakijenga Majumba ya Ufalme kwa muda mfupi sana, nao wakajiuliza, ‘Ikiwa akina ndugu huko wanaweza kujenga kwa msaada wa Yehova, kwa nini tusifanye hivyo?’
Ndugu fulani walichora ramani na kufanya matayarisho hususa yaliyohitajiwa, na kisha wakajenga Jumba la Ufalme la majaribio mjini Askim mwaka wa 1983. Baada ya hapo, mwaka wa 1984, walijenga Majumba ya Ufalme matatu kwa muda mfupi katika mji wa Rørvik, Steinkjer, na Alta. Walifanyaje hivyo? Kwa kutayarisha misingi mapema na kuwapanga wajitoleaji kwa uangalifu sana—walio stadi na wasio stadi—hivi kwamba hatua mbalimbali za ujenzi zingeweza kumalizika kwa muda wa siku chache tu.
Kwa kipindi cha miaka kumi, Majumba ya Ufalme 80 hivi ya kujengwa kwa muda mfupi yalikamilika nchini Norway. Baadaye, akina ndugu wa Norway walisafiri kwenda Iceland kusaidia kujenga Majumba ya Ufalme matatu. Ingawa makutaniko mengi nchini Norway sasa yana Majumba yao ya Ufalme, bado kuna kazi nyingi ya kufanywa. Majumba ya Ufalme ya zamani yanahitaji kufanyiwa ukarabati, mengine yanahitaji kupanuliwa, na bado mengine mapya yanahitaji kujengwa.
“AKINA NDUGU WAMEIMARISHWA”
Ujenzi wa Majumba ya Ufalme umeandaa mahali pa ibada panapofaa na penye kuvutia, na kutoa ushahidi mzuri katika jamii. Kwa mfano, ndugu watatu walikutana na maofisa wa mji wa Fredrikstad ili kufanya mipango ya ujenzi wa Jumba la Ufalme katika mwaka wa 1987. Maofisa hao walicheka ndugu hao walipowaeleza kuwa watamaliza ujenzi wa jumba hilo kwa muda wa siku tatu. Lakini hata katika siku ya kwanza, yaani, Ijumaa, maofisa hao waliona wazi kwamba Mashahidi watakamilisha jumba hilo kama walivyopanga. Siku ya Jumamosi, ofisa mmoja alileta bendi yake ya wacheza-tarumbeta kwenye eneo la ujenzi ili kuwatumbuiza wafanyakazi waliojitolea, kama njia ya kuwaomba msamaha kwa sababu ya kutilia shaka mpango wao hapo awali. Mwanamke mmoja aliyeshuhudia ujenzi wa Jumba la Ufalme la Arendal mwaka wa 1990 alisema: “Inashangaza kwamba ninyi Mashahidi mnaweza kujenga haraka sana. Lakini linaloshangaza hata zaidi ni kuwaona watu hawa wote wenye tabasamu na furaha.”
Leo, chini ya mpango wa Halmashauri ya Ujenzi ya Mkoa, kuna halmashauri mbili zinazosimamia ujenzi wa Majumba ya Ufalme kotekote nchini Norway. Pia, ndugu na dada wamejitolea kwa ajili ya miradi ya ujenzi iliyo mikubwa na inayohusisha mambo mengi. Kwa mfano, mwaka wa 1991 na 1992, ndugu walilazimika kupanua ofisi ya tawi. Na mwaka wa 1994, wakajenga Jumba la Kusanyiko maridadi jijini Oslo. Mnamo 2003, kikundi cha wajenzi kilijenga Jumba kubwa la Ufalme mjini Bergen, linaloweza kutumiwa kwa ajili ya mikutano ya kutaniko na vilevile makusanyiko.
Miradi hii hutokeza ushirikiano na umoja na hivyo huwa na matokeo mazuri kwa watumishi wa Yehova. “Hilo limeyasaidia makutaniko kuwa na umoja hata zaidi,” asema ndugu ambaye amesaidia katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme tangu mwaka wa 1983. “Undugu umeimarishwa—vifungo imara vya urafiki vimefanyizwa, na tumeweza kufanya kazi pamoja vizuri zaidi.”
UTENDAJI WAONGEZEKA BETHELI
Baada ya ofisi ya tawi mpya kukamilika, wafanyakazi waliongezwa na mengi zaidi yalitimizwa kwa ajili ya kazi ya kuhubiri nchini Norway. Kwa mfano, machapisho mengi yametafsiriwa katika Kinorway. Hatua kubwa ilifikiwa mwaka wa 1996, Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilipochapishwa katika Kinorway. (Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilikuwa tayari imetolewa mwaka wa 1991.) Sasa, karibu machapisho yote yanayochapishwa na Mashahidi wa Yehova yanapatikana katika Kinorway, kutia ndani mabuku ya Insight on the Scriptures.
Majengo mapya ya ofisi ya tawi yalitia ndani pia studio ya kurekodia iliyohitajika sana. Kuanzia miaka ya 1960, drama za makusanyiko zilirekodiwa katika Majumba ya Ufalme na katika dari na sehemu ya chini ya ardhi ya jengo la awali la ofisi ya tawi. Haikuwa rahisi kurekodi, na mara nyingi kazi ilikatizwa kwa sababu ya kelele za magari. Lakini studio ya kurekodia iliyo katika majengo mapya imerahisisha utengenezaji wa drama, video, na muziki wa kuimbwa wa nyimbo zetu za Ufalme. Pia, ofisi ya tawi hurekodi magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! katika Kinorway, vilevile Biblia nzima na vitabu vingine vimerekodiwa kwenye CD na kwenye Tovuti ya www.jw.org.
KUTUMIKIA WALIKOHITAJIWA ZAIDI
Ingawa wahubiri wa kutaniko huhubiri katika ujirani wao, wahubiri na mapainia wengi wamefikia maeneo yasiyogawiwa mtu hadi sehemu za kaskazini huko Longyearbyen, katika visiwa vya Svalbard. Wahubiri wengine wamehamia maeneo tofauti ya mbali ili kuhubiri habari njema na inapowezekana, kuanzisha makutaniko.
Finn na Tordis Jenssen walipofunga ndoa mwaka wa 1950, walijua kwamba wahubiri walihitajika Hammerfest, mojawapo ya miji iliyo kaskazini zaidi ulimwenguni. Hawakuwa na pesa nyingi; lakini walikuwa na baiskeli, nguvu, na azimio la moyoni. Hivyo wakaanza safari kwa baiskeli zao kutoka Bodø hadi Hammerfest, safari ya kilomita 900 hivi. Walipokaribia nusu ya safari kwa fadhili, marafiki fulani waliwapa pesa ili wakamilishe safari yao kwa mashua. Mjini Hammerfest, Finn na Tordis walihubiri kwa bidii na kuwaalika watu kwenye hotuba za watu wote ambazo Finn alitoa kila mwisho wa juma. Yehova alibariki jitihada zao na baada ya muda mfupi, wakaanzisha kutaniko dogo.
Mmoja wa wasemaji katika kusanyiko la wilaya lililofanywa Trondheim mwaka wa 1957 aliwatia moyo wahubiri wafikirie kuhamia maeneo yenye uhitaji wa wahubiri. Viggo na Karen Markussen, walioishi Stavanger, walikuwa wakisikiliza kwa makini, kisha Viggo akamgusa Karen kwa kiwiko. Mara moja Karen akatambua maana ya mguso huo. ‘Karibuni tutaondoka Stavanger,’ akawaza. Lakini binti zao wenye umri kati ya miaka 11 na 14 na ambao ni wahubiri wangeonaje jambo hilo?
Akina Markussen walipozungumzia hotuba hiyo baada ya kusanyiko, familia nzima ilikubali kwamba inaweza kutumika katika maeneo yenye uhitaji. Ofisi ya tawi ilipokea maombi yao na kuwaomba wahamie Brumunddal, ambapo hakukuwa na kutaniko. Hivyo, katika mwaka wa 1958, Viggo na Karen, wakauza nyumba yao ya kisasa, Viggo akauza duka lake la samani, na familia nzima ikahamia nyumba ya mbao karibu na mji wa Brumunddal. Yehova alibariki roho yao ya kujidhabihu, na katika miaka iliyofuata, watu wengi waliojifunza nao wakakubali kweli. Kufikia wakati binti zao walipoanza kujitegemea na Viggo kuwekwa kuwa mwangalizi wa mzunguko, kulikuwa na kutaniko dogo la wahubiri 40 hivi wenye bidii mjini Brumunddal.
Akina ndugu waseja wamejitahidi pia kufanya mengi katika kazi ya kuhubiri kwa kuhamia maeneo ambayo hayakuwa na makutaniko. Mwaka wa 1992, kikundi cha akina ndugu mapainia, wengi wao wakiwa na umri wa miaka 19 hivi, walihamia mji wa Måløy, katika eneo la Nord Fjord, kuwatembelea watu wenye kupendezwa waliopatikana huko. Walihubiri kwa bidii na mara moja wakaanza kufanya mikutano katika nyumba ya kukodisha walimoishi. Mwanamke mmoja waliyejifunza naye alikuwa mkarimu sana hivi kwamba akawa kama mama yao. Baadaye, mzee wa kutaniko na mke wake walihamia Måløy na kutaniko likaanzishwa. Ndugu hao vijana walifurahia sana mgawo wao, kuongoza mafunzo mengi, kushughulikia migawo mingi ya kutaniko, na kuliimarisha kutaniko hilo jipya. Mmoja wao alisema: “Hiyo ilikuwa safari ya kiroho yenye kusisimua na fursa ya kukua kiroho.” Kwa sababu ya bidii yao na ya wahubiri wengine, sasa kuna wahubiri 30 hivi katika Kutaniko la Nord Fjord, na wanaongoza mafunzo ya Biblia kati ya 50 na 60.
KUHUBIRI KATIKA LUGHA NYINGINEZO
Katika kipindi cha miaka 20 au zaidi iliyopita, kumekuwa na ongezeko kubwa la wahamiaji nchini Norway. Hivyo, makutaniko yamejitahidi sana kuwahubiria katika lugha zao au lugha nyingine wanazoelewa. Kutaniko la kwanza la lugha ya kigeni nchini Norway lilianzishwa mwaka wa 1986, na liliitwa Kutaniko la Kilatini la Oslo kwa sababu lilikuwa na watu waliozungumza Kihispania na Kireno, wengi wao kutoka Amerika ya Latini. Karibu wakati huohuo, wahubiri fulani walianzisha mpango rasmi wa kuwahubiria watu wanaozungumza Kiingereza jijini Oslo. Walipata watu wengi waliopendezwa, hasa kutoka Afrika na Asia. Waliwapata baadhi yao walipokuwa wakihubiri barabarani na wakawapata wengine katika maeneo ya kuwapokea wakimbizi. Pia, walitumia vitabu vya orodha ya namba za simu ili kutafuta watu walio na majina ya kigeni ambao huenda wakazungumza Kiingereza. Mafunzo mengi ya Biblia yalianzishwa na mnamo 1990, Kutaniko la Kiingereza la Oslo likaanzishwa.
Tangu wakati huo, wahubiri wengi nchini Norway wamejitahidi kujifunza lugha za kigeni. Wahubiri hao na wengine wenye asili ya kigeni, wameanzisha vikundi au makutaniko kwa ajili ya watu wanaozungumza Kiajemi, Kiarabu, Kichina, Kihispania, Kiingereza, Kipolishi, Kipunjabi, Kirusi, Kiserbo-Kroatia, Kitagalog, Kitamili, na Kitigrinya.
Jitihada za kuwahubiria viziwi zimekuwa na matokeo mazuri pia. Kuna maelfu kadhaa ya viziwi wanaotumia Lugha ya Ishara ya Norway, nalo tengenezo linajitahidi kuwasaidia. Katika miaka ya 1970, akina ndugu walianza kutumia lugha ya ishara katika mikutano na makusanyiko fulani, na tangu wakati huo, wahubiri kadhaa wamejifunza lugha ya ishara. Vikundi vya lugha ya ishara vimeanzishwa katika makutaniko kadhaa, na mwaka wa 2008, kutaniko la kwanza la lugha ya ishara lilianzishwa jijini Oslo. Kotekote nchini Norway, kuna wahubiri 25 hivi walio viziwi na ambao wanatumia machapisho ambayo yametafsiriwa katika Lugha ya Ishara ya Norway na yanapatikana katika DVD.
HALMASHAURI ZA UHUSIANO NA HOSPITALI
Kwa kuwa Mashahidi wa Yehova hawakubali kutiwa damu mishipani, wakati mwingine imekuwa vigumu kwa wagonjwa ambao ni Mashahidi kupata matibabu wanayohitaji na wanayokubali. Ili kuwasaidia Mashahidi walio katika hali kama hizo na kuwapa habari kuhusu matibabu ya badala, tengenezo lilianzisha Halmashauri za Uhusiano na Hospitali (HLC) nchini Norway mwaka wa 1990. Tangu 1990 hadi 2010, washiriki wa HLC jijini Oslo walifanya mikutano 70 hivi pamoja na wafanyakazi wa hospitali katika hospitali za eneo lao na wakasaidia katika visa zaidi ya 500. Bidii yao imewasaidia kuwasiliana na madaktari wengi wanaokubali maoni yetu, na habari za kitiba ambazo HLC imeandaa zimewachochea madaktari wengi kutumia njia za badala. Pia, msaada wa Vikundi vya Kutembelea Wagonjwa unathaminiwa sana na wagonjwa na familia zao.
Mambo yaliyompata Helen, dada mchanga ambaye ni painia, yanaonyesha umuhimu wa mpango wa HLC. Katika mwaka wa 2007 Hellen alikuwa mgonjwa sana na akapelekwa katika hospitali fulani ya kwao. Kiwango cha damu yake kilipungua sana, na wafanyakazi wa hospitali wakamshinikiza akubali kutiwa damu mishipani, wakimwambia kwamba hiyo tu ndiyo njia inayoweza kuokoa uhai wake. Kwa msaada wa mshiriki mmoja wa HLC, alipelekwa kwenye hospitali nyingine iliyo kubwa na yenye vifaa vingi. Helen na mama yake walipowasili, ndugu wa HLC alikuwa amefika kuwapokea, kuwatia moyo, na kuwasaidia kupata matibabu yanayofaa. Madaktari wa hospitali hiyo walikubali kumtibu Helen kwa kutumia mbinu inayochochea kutengenezwa kwa chembe nyekundu za damu. Baada ya siku chache, kiwango cha damu yake kilikuwa kimeongezeka na hakuwa hatarini. Sasa Helen ana afya nzuri, na anashukuru sana kwamba hospitali iliheshimu msimamo wake thabiti. Helen na mama yake wanasema: “Hatutasahau kamwe kuona jinsi tengenezo la Yehova linavyofanya kazi na jinsi akina ndugu na dada walivyotusaidia na kusali kwa ajili yetu.”
KUKABILI MASHAMBULIZI YENYE CHUKI KUTOKA KWA VYOMBO VYA HABARI
Kati ya mwaka wa 1989 na 1992, magazeti, redio, televisheni, na magazeti mbalimbali yalitoa habari mbaya kuhusu Mashahidi nchini Norway ili kuwaharibia jina. Mojawapo ya sababu za mashambulizi hayo ni ushikamanifu wetu kwa yale ambayo Biblia inasema kuhusu jinsi ya kuwatendea waliotengwa na ushirika. (1 Kor. 5:9-13; 2 Yoh. 10) Kwa sababu ya kuenezwa kwa maoni hayo mabaya, Mashahidi walikabili hali ngumu kutoka kwa watu wa familia, kazini, shuleni, na walipohubiri. Ingawa wafuasi wa Yesu hawashangazwi na dhihaka wanazopata, haikuwa rahisi kukabiliana na hali hiyo.—Mt. 5:11, 12.
“Hicho kilikuwa kipindi kigumu,” asema ndugu mmoja, “hata hivyo kilikuwa chenye manufaa pia. Kilinifanya nifikirie msingi wa Kimaandiko wa imani yangu. Imani yangu iliimarishwa nilipofikiria kuhusu chakula kizuri cha kiroho tunachopata kutoka kwa mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Matokeo ni kwamba ninahisi kuwa tumeimarishwa kukabiliana na majaribu ya imani.”
“Ilisisimua kuona ujasiri wa akina ndugu na dada wakati huo,” akumbuka mwangalizi mmoja wa mzunguko. “Tulitambua kwamba jambo bora ambalo tungefanya ni kujitoa zaidi katika utumishi wa shambani, kutia ndani kutoa ushahidi barabarani. Inapendeza kwamba Mashahidi wengi walifanya hivyo.”
Tofauti na maoni yasiyofaa yaliyoenezwa na vyombo vya habari, ona jinsi mtu fulani aliyekuwa ametengwa hapo awali alivyohisi kuhusu mwongozo wa Biblia kuhusiana na kutenga na ushirika. Fred asema: “Nilipotengwa na ushirika nikiwa na umri wa miaka 20, nilianza kuyafikiria maisha yangu kwa uzito. Sikufurahia kutengwa na ushirika, hata hivyo, kulikuwa na matokeo mazuri. Ni kana kwamba Yehova alikuwa akiniambia: ‘Mwanangu, sasa ni lazima ujirekebishe! Usipofanya hivyo, utapatwa na mabaya.’ Hilo lilikuwa somo muhimu lililonisaidia kuacha mazoea yangu yenye dhambi. Badala ya kujishughulisha na raha, nilianza kuichukua kweli kwa uzito. Niliona kwamba baadhi ya rafiki zangu walifanya maendeleo ya kiroho, na hilo likanisaidia kurekebisha njia zangu.” Inafurahisha kwamba Fred alitubu, akabadili njia zake, na akarudishwa. Sasa yeye ni mzee wa kutaniko.
“TAYARI KWA AJILI YA SIKU YA YEHOVA”
Licha ya kwamba watu wengi katika eneo wanafuatia vitu vya kimwili na ni wenye ubaridi, watumishi wa Yehova wameendelea kutanguliza utendaji wa kiroho unaoimarisha imani, kama vile kusoma Biblia kila siku na kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Wahubiri wengi wameongeza huduma yao kwa kujiandikisha kuwa mapainia wa kawaida. Ndugu mmoja alieleza hisia za wengi aliposema: “Ikiwa siko tayari kwa ajili ya siku ya Yehova kesho, basi sitakuwa tayari itakapokuja. Tunapaswa tu kuendelea kusonga mbele. Itakuja siku moja.” Bila shaka, mtazamo kama huo umechangia ongezeko la hatua kwa hatua tangu mwaka wa 2001.
Shule ya Mazoezi ya Kihuduma (sasa Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja) imechochea makutaniko na kuwapa ndugu wengi elimu nzuri ya kitheokrasi. Mwanafunzi mmoja akumbuka: “Fursa ya kujifunza Biblia kwa kina kwa majuma manane, ilinisaidia kuielewa kweli kwa njia ambayo sikuwa nimewahi kuielewa. Kila kitu katika Biblia kimekuwa wazi na halisi zaidi kwangu!” Katika miaka 20 iliyopita, zaidi ya wahitimu 60 wamesaidia kuyaimarisha makutaniko na kuchochea utendaji zaidi.
WATOTO WA WAZAZI MASHAHIDI
Kwa miaka mingi, wengi waliobatizwa kuwa Mashahidi wa Yehova, walijifunza kweli za Biblia kutoka kwa wazazi wao. Baadhi ya wahubiri nchini Norway ni wa kizazi cha tatu, cha nne, au hata cha tano cha Mashahidi. Ivan Gåsodden, mwana wa mjukuu wa Ingebret Andersen, Mwanafunzi wa Biblia wa kwanza huko Skien, asema: “Mara nyingi nimefikiria jinsi lilivyo pendeleo kuzaliwa katika familia iliyotanguliza utumishi wa Yehova. Kilichonisaidia kuchukua msimamo upande wa kweli ni funzo la kibinafsi, kusoma Biblia kwa ukawaida, na marafiki wazuri waliokuwa na miradi kama yangu.” Wana wa Ivan, André na Richard, pia wanauthamini sana urithi wao wa kiroho.
“Ninashukuru sana kulelewa katika familia yenye vizazi vingi vya Mashahidi,” asema painia Bente Bu, mjukuu wa Magnus Randal, ambaye alitumika katika mashua iliyoitwa Ruth. “Kuanza maisha yangu kwa njia hiyo kulinisaidia kuepuka matatizo mengi, na ninataka kutumia maisha yangu kwa faida ya wengine.”
Baadhi ya wale waliokuwa dhaifu kiroho walipokuwa vijana, sasa, wakiwa watu wazima, ni Mashahidi wa Yehova wenye bidii. Kwa mfano, Thomas na Serine Fauskanger kutoka Bergen, walilelewa na wazazi Wakristo, lakini hawakufanya maendeleo ya kiroho haraka. Ni nini kilichowasaidia kubadili maoni yao kuhusu kumwabudu Yehova?
“Mwaka wa 2002 ndugu kijana aliyekuwa amehudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma alikuja katika kutaniko letu,” aeleza Thomas. “Alinisaidia kushiriki katika huduma na kufuatia miradi ya kiroho.”
Thomas alipokuwa na umri wa miaka 25, alimwoa Serine, na mwaka wa 2007 wakahamia Båtsfjord, Finnmark, ili kujiunga na wenzi wa ndoa mapainia kuwasaidia watu wenye kupendezwa katika eneo hilo. Baada ya muda mfupi, Thomas na Serine pia wakawa mapainia. Mwaka wa 2009, kwa miezi mitatu walihubiri eneo lisilogawiwa mtu katika kijiji cha wavuvi cha Kjøllefjord, ambapo walianzisha mafunzo ya Biblia zaidi ya 30 wakiwa pamoja na wahubiri wengine walioandamana nao. Kisha, Thomas na Serine wakahamia karibu na kijiji cha Kjøllefjord ili kuwasaidia watu wenye kupendezwa. Sasa wao husafiri kwa saa tatu na nusu hivi kwenda na saa hizohizo kurudi ili kuwasaidia watu hao. Wana shughuli nyingi, lakini Serine anasema: “Maisha yangu ni rahisi na yenye furaha sasa. Tuna vitu vichache, lakini bila matatizo mengi.”
KUTAZAMIA WAKATI UJAO WAKIWA NA IMANI KWA YEHOVA
Maisha yamebadilika sana tangu Mwanafunzi wa Biblia, Knud P. Hammer na wengine walipoanza kuhubiri nchini Norway. Mwanzoni, watumishi wa Yehova walikuwa tofauti kwa sababu walifundisha kweli za Biblia katika jamii ya kidini yenye makanisa mengi yaliyo na uvutano mwingi na mafundisho ya uwongo. Kwa miaka mingi, watu wengi wanyoofu walifurahia kujifunza Biblia na kuchukua msimamo upande wa ibada ya kweli.
Sasa maoni ya watu wa Norway kuhusu dini yamebadilika. Ni watu wachache wanaomwamini Mungu, na inaonwa kuwa jambo lisilofaa kudai kwamba kuna dini moja tu ya kweli. Wakati na jitihada nyingi zinahitajika ili kuwasaidia watu wanaopendezwa wapate ujuzi wa Biblia na kujenga imani yao katika Mungu na Biblia. Kwa kawaida inachukua muda mrefu kujifunza kuishi kulingana na viwango vya Biblia. Hata hivyo, Yehova anaendelea kuwavuta watu wanyoofu, iwe wanaishi katika vijiji vya wavuvi vilivyo mbali au katika majengo ya kisasa katika miji iliyo na watu wengi.—Yoh. 6:44.
Kama ilivyo ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova nchini Norway wanathamini “pendeleo la kumtolea utumishi mtakatifu bila woga,” Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova. (Luka 1:74) Wanapoendelea kuwatafuta watu wenye mioyo minyoofu, wanajionea mandhari ya kiparadiso iliyo maridadi, tulivu, na yenye kustaajabisha kama ile ambayo Muumba anakusudia kwa dunia yote. Waabudu wa Yehova nchini Norway pamoja na ndugu na dada zao washikamanifu duniani pote, wanasubiri kwa hamu siku ambayo Ufalme wa Mungu utatimiza mapenzi ya Mungu katika kila pembe ya dunia yetu maridadi.—Dan. 2:44; Mt. 6:10.
[Blabu katika ukurasa wa 106]
Hilo halikumzuia—alienda mikutanoni hata bila viatu!
[Blabu katika ukurasa wa 111]
“Nilienda kulala nikiwa Mpentekoste, nikaamka nikiwa Shahidi wa Yehova”
[Blabu katika ukurasa wa 122]
“Hatuwezi kuwanyang’anya imani yenu”
[Blabu katika ukurasa wa 157]
‘Mwanangu, sasa ni lazima ujirekebishe! Usipofanya hivyo, utapatwa na mabaya’
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 90]
Maelezo Mafupi Kuhusu Norway
Nchi
Norway inajulikana kwa mikono-bahari maridadi na milima yenye kustaajabisha na vilevile maelfu ya visiwa. Bila kuhesabu visiwa vya Svalbard vilivyo katikati ya Norway barani na Ncha ya Kaskazini, nchi hiyo ni kubwa kidogo kuliko Italia. Ingawa kunaweza kuwa na baridi kali nchini Norway, hasa katika eneo la Aktiki, sehemu kubwa ya nchi hii ina joto la kadiri ikilinganishwa na nchi nyingine zilizo katika maeneo kama hayo kwa sababu ya mawimbi yenye joto na mfumo upepo kutoka bahari ya Atlantiki.
Watu
Wengi wa wakaaji milioni tano ni wenyeji wa Norway, na asilimia 10 hivi ni wahamiaji. Wasami (waliojulikana kama Lapp) bado wanajitegemeza kwa kuvua samaki, kuwinda na vilevile kufuga mbawala.
Lugha
Kinorway ndiyo lugha rasmi na huandikwa kwa njia mbili—Nynorsk, na Bokmål inayotumiwa na watu wengi sana na inakaribiana na Kidenishi.
Kazi
Viwanda vya mafuta na gesi ndio vyanzo vikuu vya mapato nchini. Samaki huuzwa katika nchi za nje kwa wingi. Ni asilimia 3 tu ya ardhi nchini Norway inayotumiwa kukuza mimea.
Chakula
Samaki, nyama, viazi, mkate, na mazao ya maziwa ni vyakula vya kawaida nchini Norway. Chakula kinachopendwa sana ni Fårikål (mchuzi wa nyama ya kondoo na kabichi). Kwa sababu ya ongezeko la wahamiaji katika miaka ya karibuni, chakula hicho sasa kinapendwa hata na watu wa mataifa mengine.
[Sanduku/Picha katika ukurasa za 95, 96]
Alijitolea Kabisa Kumtumikia Yehova
THEODOR SIMONSEN
ALIZALIWA 1864
MWANAFUNZI WA BIBLIA TANGU 1905
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Awali alikuwa mhubiri wa kanisa la Free Mission lakini baadaye akawa mwangalizi anayesafiri.
◼ THEODOR aliposoma machapisho yetu na kutambua kwamba fundisho la moto wa mateso linapingana na Biblia, alianza kufunua uwongo wa fundisho hilo kupitia hotuba zake katika kanisa la Free Mission—jambo lililowafurahisha wengi waliohudhuria. Lakini siku moja, baada ya kutoa hotuba fulani, alipewa karatasi iliyoandikwa, “Hiyo ndiyo hotuba yako ya mwisho hapa!”
Theodor alitoa hiyo hotuba ya mwisho katika kanisa la Free Mission mwaka wa 1905, na akawa Mwanafunzi wa Biblia mwaka huohuo. Baadaye, alitoa hotuba nyingi kwa mamia ya Wanafunzi wa Biblia waliozithamini sana. Theodor alifanya kazi ya kupaka nyumba rangi ili kuitegemeza familia yake kifedha huku akitumia miisho-juma kuhubiri na kufundisha. Kwa kuwa alikuwa mtulivu, mwenye ujuzi mwingi wa Biblia, na alitoa hoja zake kwa njia yenye kueleweka, Theodor alithibitika kuwa mwalimu stadi. Pia, alikuwa na sauti nzuri ya kuimba na kwa kawaida alianza na kumaliza hotuba zake kwa kuimba huku akipiga zeze.
Mwaka wa 1919, hali ya familia yake iliporuhusu, alianza kutumika akiwa mwangalizi anayesafiri. Alitumika katika mgawo huo hadi mwaka wa 1935, akitembelea makutaniko huko Norway, Denmark, na Sweden. Ilikuwa kazi ya kuchosha iliyohusisha kutia moyo makutaniko na vikundi vilivyo mbali na pia kutoa hotuba katika miji ambayo haikuwa na Wanafunzi wa Biblia. Kwa mfano: Wakati wa safari moja ya miezi 12, alipaswa kutembelea maeneo 190 kati ya Kristiansand iliyo upande wa kusini na Tromsø iliyo upande wa kaskazini. Siku hizo, waangalizi wanaosafiri walikaa mahali fulani kwa siku moja au mbili tu kisha wakaondoka na kwenda kwingine kwa kutumia aina yoyote ya usafiri uliopatikana.
Hata ingawa hakukuwa na Wanafunzi wa Biblia katika sehemu nyingi alizotembelea, watu wengi wenye kupendezwa walijitokeza alipotoa hotuba. Kwa mfano, alipotembelea Bodø mwaka wa 1922, alihubiri na kuwaalika watu kwa hotuba ya watu wote akiwa pamoja na Anna Andersen, painia ambaye pia alikuwa ametembelea eneo hilo. Johan na Olea Berntsen, waliokuwa miongoni mwa waliosikiliza hotuba yake, walipendezwa sana. Baada ya hotuba waliwaalika Theodor na Anna nyumbani kwao ili kujibu maswali yao ya Biblia. Kwa sababu hiyo, familia ya Berntsen wakawa Wanafunzi wa kwanza wa Biblia huko Bodø.
Sauti ya Theodor ilitumiwa katika hotuba zilizorekodiwa katika Kinorway kwenye gramafoni miaka ya 1930. Alitumika kwa uaminifu hadi alipokufa mwaka wa 1955 akiwa na tumaini la kwenda mbinguni.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 102]
‘Alitembea Pamoja na Mungu’
ENOK ÖMAN
ALIZALIWA 1880
ALIBATIZWA 1911
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alitumika akiwa mwangalizi wa tawi tangu 1921 hadi 1945.
◼ ENOK alipokuwa kijana huko Sweden, simulizi la Biblia la jinsi Enoko ‘alivyoendelea kutembea pamoja na Mungu wa kweli’ lilimgusa moyo sana. (Mwa. 5:22) Enok alitaka kutenda kama Enoko anayetajwa katika Biblia. Hata hivyo, alijua kabisa maana ya kutembea na Mungu alipokuwa na umri wa miaka wa 31 baada ya kusoma buku la kwanza la Studies in the Scriptures. Alibatizwa na kuwa Mwanafunzi wa Biblia, kisha akawa painia. Baadaye alitumika katika ofisi ya tawi nchini Sweden.
Mwaka wa 1917, Enok alitumwa Norway ili atumike katika ofisi ya tawi, na katika mwaka wa 1921, akapata mgawo wa kusimamia kazi nchini Norway. Wakati huo ofisi ya Watch Tower Society ilikuwa katika chumba kimoja cha jengo fulani ambapo Dada Maria Dreyer alikuwa na nyumba na duka la kurembesha miguu. Enok alipomwoa Maria mwaka wa 1922, nyumba ya Maria ikatumiwa kama ofisi ya tawi. Walifanya kazi pamoja Betheli hadi Maria alipokufa mwaka wa 1944. Mnamo 1953, Enok alioa tena na kuanza utumishi wa painia tena. Nyakati zote, alikazia akili tumaini lake la kwenda mbinguni, na hilo lilimsaidia “kutembea pamoja na Mungu” kwa uaminifu mpaka alipokufa mwaka wa 1975.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 110]
“Alikuwa Mwenye Shauku na Mwenye Kutia Moyo”
WILHELM UHRE
ALIZALIWA 1901
ALIBATIZWA 1949
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Mhubiri mwenye bidii licha ya kuwa na ugonjwa unaodhoofisha misuli.
◼ WILHELM alikuwa na ugonjwa wa misuli ambao ulifanya miguu yake ipooze na ikawa vigumu kwake kuongea. Hata hivyo, mara tu aliposikia habari njema katikati ya miaka ya 1930, alianza kuwaeleza wengine kuhusu kweli nzuri alizokuwa anajifunza. Alitumia baiskeli yenye magurudumu matatu alipoenda kuhubiri na alienda kwenye bandari ya Sortland huko Vesterålen kwa ukawaida ili kuwachezea watu hotuba za Biblia kwenye gramafoni na kuwapa machapisho. Wilhelm alibatizwa baadaye katika mwaka wa 1949 kwa sababu alikuwa mlemavu na aliishi katika eneo la mbali. Hata hivyo, alikuwa mhubiri mwenye bidii. Wengi waliosafiri sehemu za pwani walijifunza kweli kutoka kwake, na baadhi yao wakawa Mashahidi wa Yehova.
Wilhelm alipozeeka, aliishi katika makao ya kuwatunzia wazee huko Tromsø. Akisaidiwa na wahubiri wengine, aliendelea kuhubiri kupitia barua. Kwa sababu alijiendesha kwa njia nzuri, aliwatia moyo wengine kutia ndani wafanyakazi katika makao hayo. Alipokufa, meneja wa makao hayo alisema: “Sikuzote tulifurahi kuingia chumbani mwake. Kwa sababu ya imani yake, alikuwa mwenye shauku na mwenye kutia moyo.”
[Sandku/Picha katika ukurasa wa 113]
Alitimiza Ahadi Yake
JOHANNES KÅRSTAD
ALIZALIWA 1903
ALIBATIZWA 1931
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alitumika katika mashua za mapainia kwa miaka minane.
◼ MWAKA wa 1929, Johannes alilazwa hospitalini kwa sababu ya ugonjwa wa kifua kikuu. Akiwa huko alianza kusoma Biblia na kumwahidi Mungu kuwa atamtumikia akipona.
Muda mfupi tu kabla ya kuondoka hospitalini, Johannes alifurahia sana kusoma baadhi ya vitabu vya Wanafunzi wa Biblia. Baadaye, akapokea vitabu zaidi, akasoma kila kitabu mara nne au tano, na punde si punde, Johannes akaanza kuwahubiria wengine kweli mpya alizojifunza. Mara tu alipopona kabisa, alienda Bergen na kumtembelea Ndugu Ringereide, aliyemtia moyo aanze upainia. Ingawa Johannes alikuwa ameanza tu kuhubiri, hakusita kujiandikisha kuwa painia.
Kuanzia 1931 hadi 1938, alitumia mashua ya mapainia inayoitwa Ester, na kisha akafanya upainia kwa mwaka mmoja hivi akitumia mashua Ruth, akisafiri kandokando ya pwani kuelekea upande wa kaskazini hadi Tromsø. Mwaka wa 1939, Johannes akiwa mwangalizi anayesafiri katika sehemu ya mashariki ya Norway alipata mgawo wa kutumika Betheli kwa muda. Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, alimwoa Sigrid na wakafanya upainia pamoja. Mwaka 1995, alipokuwa Fredrikstad, Johannes alikufa akiwa na tumaini la kwenda mbinguni.
[Sanduku/Picha katika ukuras wa 132]
Kuhubiri Katika Sehemu Tambarare
RANDI HUSBY
ALIZALIWA 1922
ALIBATIZWA 1946
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Amekuwa katika utumishi wa wakati wote tangu 1946.
◼ WAZAZI wa Randi walibatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova katika mwaka 1938 na baadaye, Randi akaamua kumtumikia Yehova. Mwaka 1946, alikubali mwaliko wa kutumika Betheli, na huko akakutana na ndugu mmoja kijana aliyeitwa Kjell Husby. Randi na Kjell wakachumbiana, wakaoana, na kuanza utumishi wa upainia. Walifurahia kushiriki utendaji mbalimbali wa kiroho katika utumishi wa wakati wote hadi kifo cha Kjell mwaka wa 2010.
Katika miaka ya hivi karibuni, matatizo ya miguu yamefanya iwe vigumu kwa Randi kupanda ngazi au sehemu zenye mwinuko. Lakini anaweza kutembea vizuri katika sehemu iliyo tambarare naye huonekana mara nyingi akihubiri barabarani na madukani huko Trondheim. Ili kuwahubiria habari njema wote anaokutana nao, Randi huhakikisha amebeba machapisho katika lugha zisizopungua nane. Pia, rafiki za Randi kutanikoni humbeba kwa gari na kumpeleka kwa watu ambao hupokea magazeti ya karibuni kutoka kwake kwa ukawaida.
Randi hana nguvu za kufanya mengi kama alivyofanya hapo zamani. Lakini anaendelea kupata shangwe na uradhi kutokana na utumishi wake wa nafsi yote, akijua kwamba Yehova ‘hatasahau kazi yake na upendo alioonyesha kwa ajili ya jina lake.’—Ebr. 6:10.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 149, 150]
Alijionea Jinsi Neno la Mungu Linavyobadili Maisha
VIKTOR UGLEBAKKEN
ALIZALIWA 1953
ALIBATIZWA 1981
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Hapo awali alikuwa mhalifu, alidhibitiwa na roho waovu, na alitumia dawa za kulevya.
◼ VIKTOR alianza kutumia bangi na madawa mengine alipokuwa kijana na hatua kwa hatua, akajiingiza katika maisha ya uhalifu. Alipendezwa na Biblia, na mwaka wa 1979, baada ya kuchoshwa na maisha yake ya uhalifu, alijiuliza iwapo Neno la Mungu lingeweza kumsaidia. Hata hivyo, uchunguzi aliofanya katika dini mbalimbali ulimwacha akiwa katika hali ya kufadhaika na kukosa uradhi.
Hatimaye, akiwa ameshuka moyo sana, Viktor akafikiria kujiua. Kisha, akapokea barua kutoka kwa binamu yake huko Bergen, ambaye alikuwa ameanza kujifunza na Mashahidi wa Yehova. Viktor alihamia Bergen na kujiunga na binamu yake katika funzo hilo. Mwanzoni, alijaribu kuthibitisha kwamba Mashahidi hawakuwa wakifundisha kweli. Lakini kwa sababu alipendezwa na mazingira, alifurahia kujifunza kwamba Mungu ‘atawaharibu wale wanaoiharibu dunia’ na atageuza sayari yetu iwe paradiso.—Ufu. 11:18.
Mara moja Viktor akaanza kuhudhuria mikutano pamoja na binamu yake, na akavutiwa sana na jinsi alivyokaribishwa na kuonyeshwa fadhili katika Jumba la Ufalme na katika nyumba za Mashahidi. Yale aliyosikia na kujionea yalimsadikisha kuwa alipaswa kubadili maisha yake na kuacha kutumia dawa za kulevya. Viktor alisali kwa bidii na kutoka moyoni na akajionea mwenyewe jinsi Neno la Mungu na roho takatifu hubadili maisha.—Luka 11:9, 13; Ebr. 4:12.
Haikuwa rahisi kwa Viktor kufanya mabadiliko ili astahili kubatizwa. Ni kwa msaada wa Mungu tu ndipo alipoweza kujitoa chini ya udhibiti wa roho waovu na akaacha kutumia dawa za kulevya licha ya kwamba alikuwa amerudia zoea hilo mara mbili. Alisaidiwa na mzee wa kutaniko aliyemhakikishia kwamba ‘kama vile baba anavyowaonyesha wanawe rehema, ndivyo ambavyo Yehova anawaonyesha rehema wale wanaomwogopa.’ (Zab. 103:13) Viktor aliendelea kukua kiroho na akabatizwa mwaka wa 1981. Bado ilibidi afungwe gerezani kwa uhalifu aliokuwa amefanya awali, lakini muda mfupi baada ya kuachiliwa, akaanza upainia. Tangu wakati huo, amefurahia kuwasaidia wengi kuwa watumishi wa Yehova. Amepata matokeo hasa anapohubiri katika magereza, na wawili kati ya wafungwa aliojifunza nao wamekuwa Mashahidi.
Viktor sasa ni kichwa cha familia mwenye kutegemeka na mzee wa kutaniko. Anaendelea kutumika akiwa painia pamoja na mke wake, Tone, na mwana wao. “Utumishi ni mojawapo ya mambo yaliyonibadili,” asema Viktor. “Namshukuru sana Yehova kwamba ninaweza kuwapa wengine hazina za kiroho zenye thamani.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 152]
Alitaka Kufanya Jambo Bora Zaidi
TOM FRISVOLD
ALIZALIWA 1962
ALIBATIZWA 1983
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Mchezaji kandanda aliyetaka kumtumikia Yehova.
◼ AKIWA na umri wa miaka 20, Tom alikuwa na fursa ya kupata kazi nzuri sana ya kuchezea mojawapo ya timu bora zaidi ya kandanda nchini Norway. Mama yake alikuwa tayari mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Siku moja, painia fulani aliyemtembelea mama yake alimuuliza Tom ikiwa angependa kujifunza Biblia. Tom alikubali lakini akamwambia kwamba hakuwa na nia ya kuwa Shahidi.
Tom aliguswa moyo na jinsi alivyokaribishwa kwa shauku alipoanza kuhudhuria mikutano. Pia, wakati wa programu, aliona kila mtu akifungua na kusoma Biblia. Tom akakata kauli, “Lazima iwe ni Biblia inayowafanya watu hawa wawe wazuri hivi.”
Hatimaye, Tom alitambua kwamba amepata kweli na akaamua kumtumikia Yehova. Lakini angefanya nini ili kushawishi timu yake ya kandanda imruhusu avunje mkataba wake ilhali alikuwa mmoja wa wachezaji wao wazuri? La kushangaza ni kwamba alipowaeleza wasimamizi wake kuwa alitaka kutumia maisha yake kufuatilia jambo bora zaidi kuliko kandanda, walimruhusu avunje mkataba wake.
Tom alibatizwa mwaka 1983 na akaanza upainia mwaka wa 1985. Mnamo 1987, alihamia Hammerfest pamoja na Viktor Uglebakken ili kusaidia eneo lenye uhitaji mkubwa. Baadaye, Tom aliwekwa rasmi kuwa mwangalizi wa mzunguko, na sasa anatumika Betheli pamoja na mke wake, Kristina.
[Chati/Picha katika ukurasa wa 162, 163]
MFUATANO WA MATUKIO—Norway
1890
1892 Knud Pederson Hammer aanza kuhubiri nchini Norway.
1900
1900 Kutaniko la kwanza laanzishwa.
1904 Ofisi yafunguliwa Kristiania (Oslo).
1905 Kusanyiko la kwanza lafanywa Kristiania.
1909 na 1911 C. T. Russell atembelea Norway.
1910
1914 Mwangalizi anayesafiri wa kwanza awekwa rasmi.
1914-1915 “Photo-Drama of Creation” yavutia umati mkubwa.
1920
1920-1925 “Mamilioni Wanaoishi Sasa Hawatakufa Kamwe!” yatolewa kote nchini.
1925 Gazeti The Golden Age (Amkeni!) lachapishwa katika Kinorway.
1928-1940 Mashua zilizotumiwa kuhubiria jamii zilizo pwani.
1930
1940
1940-1945 Waendelea kuhubiri licha ya upinzani wakati wa vita.
1945 Gazeti la Mnara wa Mlinzi lachapishwa katika Kinorway.
1948 Wamishonari wa kwanza waliozoezwa Gileadi wawasili.
1950
1950 Mahakama Kuu Zaidi yaruhusu machapisho yatumiwe katika kazi ya kuhubiri.
1960
1965 Kusanyiko la kimataifa lafanywa jijini Oslo.
1970
1980
1984 Ofisi mpya ya tawi yawekwa wakfu.
1990
1990 Halmashauri za Uhusiano na Hospitali zawekwa rasmi.
1994 Jumba la Kusanyiko lawekwa wakfu huko Oslo.
1996 Biblia nzima Tafsiri ya Ulimwengu Mpya yatolewa katika Kinorway.
2000
2010
2011 Vilele vipya vya mapainia wa kawaida na wasaidizi, wahubiri, na wahudhuriaji wa Ukumbusho.
[Grafu/Picha katika ukurasa wa 159]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Jumla ya Wahubiri
Jumla ya Mapainia
10,000
8,000
6,000
4,000
2,000
1920 1935 1950 1965 1980 1995 2010
[Ramani katika ukurasa wa 91]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
SWEDEN
STOCKHOLM
Örebro
Ghuba ya Bothnia
FINLAND
HELSINKI
Ghuba ya Finland
BAHARI YA BALTIKI
DENMARK
COPENHAGEN
NORWAY
OSLO
Kjøllefjord
Båtsfjord
Vardø
Kirkenes
Karasjok
Hammerfest
Alta
Finnmarksvidda
Kautokeino
Troms
Harstad
Narvik
Sortland
Hennes
Svolvær
Bodø
Rørvik
Namsos
Steinkjer
Trondheim
Kristiansund
Måløy
Florø
Bergen
Haugesund
Stavanger
Egersund
Kristiansand
Arendal
Skien
Kongsberg
Drammen
Hønefoss
Gjøvik
Lillehammer
Brumunddal
Hamar
Kongsvinger
Ski
Askim
Moss
Halden
Fredrikstad
Mkono-Bahari wa Oslo
BAHARI YA KASKAZINI
BAHARI YA NORWAY
Kisiwa cha Andøya
Bleik
Visiwa vya Svalbard
Longyearbyen
Mikoa
Finnmark
Tromsø
Telemark
Vestfold
[Picha katika ukurasa wa 88]
Knud Pederson Hammer
[Picha katika ukurasa wa 88, 89]
Reine, Norway kaskazini
[Picha katika ukurasa wa 92]
Kutaniko la Skien mwaka wa 1911, pamoja na Ingebret na Berthe Andersen
[Picha katika ukurasa wa 93]
Viktor Feldt
[Picha katika ukurasa wa 94]
Hallgerd Holm (1), Theodor Simonsen (2), na Lotte Holm (3)
[Picha katika ukurasa wa 98]
Mapainia wa kwanzakwanza: (1) Helga Hess, (2) Andreas Øiseth, (3) Karl Gunberg, (4) Hulda Andersen, na (5) Anna Andersen
[Picha katika ukurasa wa 100]
“Peoples Pulpit”
[Picha katika ukurasa wa 104]
“Golden Age” katika Kinorway
[Picha katika ukurasa wa 106]
Even Gundersrud
[Picha katika ukurasa wa 107]
Mara nyingi, wahubiri wa Kutaniko la Skien walisafiri kwa malori yaliyokuwa wazi nyuma walipoenda kuhubiri katika maeneo yaliyokuwa karibu na jiji hilo
[Picha katika ukurasa wa 108]
Torkel Ringereide
[Picha katika ukurasa wa 109]
Olaf Skau
[Picha katika ukurasa wa 114]
Karl Gunberg alikuwa nahodha wa mashua iliyoitwa “Elihu”
[Picha katika ukurasa wa 115]
Johannes Kårstad alikuwa nahodha wa mashua iliyoitwa “Ester”
[Picha katika ukurasa wa 116]
Andreas Hope na Magnus Randal walitumika katika mashua iliyoitwa “Ruth”
[Picha katika ukurasa wa 117]
“Aurora borealis,” kaskazini mwa Norway
[Picha katika ukurasa wa 118]
Solveig Løvås
[Picha katika ukurasa wa 119]
Andreas na Sigrid Kvinge
[Picha katika ukurasa wa 124]
Kukusanyika kisiri msituni karibu na kijiji cha Ski
[Picha katika ukurasa wa 127]
Marvin Anderson na mke wake, Karen
[Picha katika ukurasa wa 128]
Matbaa inayoendeshwa kwa mguu
[Picha katika ukurasa wa 129]
Kusanyiko la wilaya la 1946, mjini Bergen
[Picha katika ukurasa wa 130]
Svanhild Neraal, mwaka wa 1961
[Picha katika ukurasa wa 133]
Mara nyingi mashua ya Arnulf ilitumiwa kwa ajili ya utumishi
[Picha katika ukurasa wa 135]
Gunnar Marcussen (1) na Hans Peter Hemstad (2) walikuwa wanafunzi wa kwanza kutoka Norway kuhitimu Shule ya Gileadi
[Picha katika ukurasa wa 138]
Kambi ya mahema kwa ajili ya kusanyiko la kimataifa lenye kichwa “Neno la Kweli”
[Picha katika ukurasa wa 139]
Paul Bruun
[Picha katika ukurasa wa 142]
Hartvig Mienna na wahubiri wengine wakitumia magari yanayoendeshwa juu ya theluji wanapowahubiria Wasami
[Picha katika ukurasa wa 144]
Ujenzi wa ofisi ya tawi ulianza mwaka wa 1981
[Picha katika ukurasa wa 145]
Ofisi ya tawi leo
[Picha katika ukurasa wa 147]
Jumba la Kusanyiko la Oslo
[Picha katika ukurasa wa 160]
Mafundisho ya Biblia katika familia yametokeza vizazi vingi vya watumishi wa Yehova