Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • jr sura 6 kur. 67-80
  • “Tafadhali, Itii Sauti ya Yehova”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Tafadhali, Itii Sauti ya Yehova”
  • Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YULE ANAYESTAHILI UTII WETU
  • NI MUHIMU KUMTII YEHOVA
  • INGAWA YEHOVA HUSAMEHE KWA HIARI, KUNA MASHARTI
  • MTII YEHOVA KWA KURUDI KWAKE
  • UTII UNAWEZA KUKULINDA
  • WANAOMTII YEHOVA HAWAKO PEKE YAO
  • Je, Kila Siku Unauliza, “Yehova Yuko Wapi?”
    Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • “Siwezi Kunyamaza Kimya”
    Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • “Uwaambie Neno Hili”
    Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
  • “Nitaishibisha Nafsi Iliyochoka”
    Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
Pata Habari Zaidi
Mungu Asema Nasi Kupitia Yeremia
jr sura 6 kur. 67-80

SURA YA SITA

“Tafadhali, Itii Sauti ya Yehova”

1, 2. Mara nyingi wale wanaofuata “mwendo unaopendwa na wengi” huwa na mtazamo gani, na kwa nini tunapaswa kuwa tofauti?

WATU wengi leo hawapendi kutii. Wengi leo hata hawatui na kufikiria lililo sawa kabla ya kufanya maamuzi. Badala yake wanaongozwa na kanuni kama: ‘Fanya utakalo’ au ‘Fanya lolote maadamu usipatikane.’ Hilo huonekana wazi wakati ambapo madereva wanakataa kutii sheria za barabarani, wafanya-biashara wanakiuka sheria za uwekezaji, na maofisa wakuu wanavunja sheria ambazo huenda hata walishiriki kutunga. Hata katika siku za Yeremia, kulikuwa na watu waliofuata “mwendo [huo] unaopendwa na wengi,” ijapokuwa ni mwendo usiofaa na ni hatari.—Yer. 8:6.

2 Wale wanaotaka kupata kibali cha Mungu Mweza-Yote hawapaswi kufuata tu “mwendo unaopendwa na wengi.” Yeremia alionyesha waziwazi tofauti kati ya wale ambao ‘hawakutii sauti ya Yehova’ na wale waliotaka Kumtii. (Yer. 3:25; 7:28; 26:13; 38:20; 43:4, 7) Kila mmoja wetu anapaswa kujichunguza kuhusiana na jambo hilo. Kwa nini? Shetani anawashambulia vikali waabudu wa kweli wanaojitahidi kudumisha utimilifu. Yeye ni kama nyoka mwenye sumu kali anayevizia na kushambulia ghafula. Kuazimia kwetu kutii sauti ya Yehova hutusaidia kuepuka kuumwa na nyoka huyo mwenye sumu kali. Hata hivyo, tunaweza kuimarisha jinsi gani azimio letu la kumtii Yehova? Maandishi ya Yeremia yanaweza kutusaidia.

YULE ANAYESTAHILI UTII WETU

3. Kwa nini Yehova anastahili utii wetu?

3 Kwa nini Yehova anastahili utii wetu? Yeremia anaeleza sababu moja anapomwita “Mtengenezaji wa dunia kwa nguvu zake, Yeye anayeifanya imara nchi yenye kuzaa kwa hekima yake.” (Yer. 10:12) Yehova ndiye Mwenye Enzi Kuu. Ndiye tunayepaswa kumwogopa kuliko watawala wengine wote. Ana haki ya kutuagiza tutii amri zake za hekima, ambazo kwa kweli ni kwa ajili ya faida yetu ya milele.—Yer. 10:6, 7.

Picha katika ukurasa wa 69

Kunywa “maji yaliyo hai” kutoka kwa Yehova kutakuimarisha utii

4, 5. (a) Wayahudi walijifunza ukweli gani wakati wa ukame? (b) Ni kwa njia gani wakaaji wa Yuda waliyatumia vibaya “maji yaliyo hai” kutoka kwa Yehova? (c) Unaweza kunywa “maji yaliyo hai” kutoka kwa Mungu jinsi gani?

4 Mbali na kuwa Mwenye Enzi Kuu; Yehova ndiye Mtegemezaji wa uhai wetu. Wayahudi wa siku za Yeremia walijulishwa hilo waziwazi. Nchi ya Misri ilitegemea sana maji ya Mto Nile, lakini hali ilikuwa tofauti katika Nchi ya Ahadi. Kwa kiasi kikubwa, watu wa Mungu walitegemea mvua za msimu, nao walikuwa wakihifadhi maji katika matangi yaliyokuwa chini ya ardhi. (Kum. 11:13-17) Yehova tu ndiye angeweza kutokeza mvua ambayo ingelowesha udongo ili uweze kuzaa. Kwa upande mwingine, angeweza pia kuzuia mvua isinyeshe. Hivyo, katika siku za Yeremia, mara kwa mara Wayahudi wasiotii walikumbwa na ukame ambao ulifanya mashamba na mizabibu yao ikauke, pia visima na matangi yao yalikauka.—Yer. 3:3; 5:24; 12:4; 14:1-4, 22; 23:10.

5 Badala ya kuthamini “maji yaliyo hai” ambayo Yehova alikuwa akiwapa bure, Wayahudi hao walihangaikia maji halisi. Walifanya hivyo kwa kukataa kimakusudi kutii Sheria ya Mungu na kuyategemea mataifa yaliyowazunguka. Wayahudi hao walikuwa kama watu ambao wakati kuna upungufu wa maji, wanayatia katika matangi yaliyovunjika yasiyoweza kuhifadhi chochote. (Soma Yeremia 2:13; 17:13.) Bila shaka, tunaweza kujiepusha na msiba tukiepuka kufanya walivyofanya. Yehova anaendelea kutupa mwongozo wa kutosha kupitia Neno lake lililoongozwa na roho. Hata hivyo, ili “maji yaliyo hai” yatunufaishe, lazima tujifunze Neno la Mungu kwa ukawaida na kuishi kupatana nalo.

6. (a) Fafanua mtazamo wa Mfalme Sedekia kuhusu kumtii Yehova. (b) Kwa nini unafikiri mfalme huyo hakutenda kwa hekima?

6 Kadiri siku ya hukumu ya Mungu dhidi ya Yuda ilivyokuwa ikikaribia, ndivyo pia ilivyokuwa muhimu kuwa watiifu. Kila Myahudi aliyetaka kupata kibali na ulinzi wa Yehova, alipaswa kutubu na kuanza kumtii. Mfalme Sedekia pia alipaswa kufanya hivyo. Hakuwa na msimamo imara wa kutenda yaliyo sawa. Watu katika serikali yake walipomwambia wanataka Yeremia auawe, hakuwa na ujasiri wa kuwazuia. Kama tulivyoona katika sura iliyotangulia, nabii huyo aliokolewa na Ebed-meleki na baadaye akamsihi Sedekia: “Tafadhali, itii sauti ya Yehova.” (Soma Yeremia 38:4-6, 20.) Ni wazi kwamba, mfalme alipaswa kuamua ikiwa atamtii Mungu.

Kwa nini Yeremia aliwasihi Wayahudi tena na tena wamtii Mungu?

NI MUHIMU KUMTII YEHOVA

7. Ni hali gani zinazoweza kupima utii wako?

7 Kama ilivyokuwa katika siku za Yeremia, utii ni muhimu leo pia. Je, umeazimia kabisa kumtii Yehova? Ikiwa ungejikuta bila kukusudia katika kituo cha Intaneti chenye picha chafu, je, ungeendelea kutazama, au ungepinga kishawishi hicho na kuondoka mara moja katika kituo hicho? Namna gani ikiwa mfanyakazi au mwanafunzi mwenzako ambaye si mwamini angekuomba muwe na matembezi ya kirafiki? Je, ungekuwa na ujasiri wa kukataa? Je, vitabu vya waasi-imani au vituo vyao kwenye Intaneti hukusisimua au hukuchukiza? Katika hali hizo au nyinginezo, usisahau maneno ya andiko la Yeremia 38:20.

8, 9. (a) Kwa nini ni jambo la hekima kusikiliza wazee wanapokushauri? (b) Unapaswa kuwa na maoni gani wazee wanapokushauri tena na tena?

8 Mara nyingi Yehova alimtuma Yeremia kwa watu Wake akiwa na ujumbe mbalimbali, kama vile: “Geukeni, tafadhali, kila mmoja kutoka katika njia yake mbaya, na mfanye njia zenu na matendo yenu kuwa mema.” (Yer. 7:3; 18:11; 25:5, soma Yeremia 35:15.) Vivyo hivyo, wazee Wakristo leo hufanya yote wawezayo ili kuwasaidia waamini wenzao walio katika hatari ya kiroho. Wazee wanapokushauri kuhusu mwenendo fulani usiofaa au mbaya unaopaswa kuepuka, wasikilize. Lengo lao ni kama la Yeremia.

9 Nyakati nyingine, huenda wazee wakakukumbusha kanuni za Kimaandiko ambazo tayari wamekuonyesha. Kumbuka kwamba si rahisi kwao kutoa shauri lilelile tena na tena, isitoshe, huwa vigumu kwao hata zaidi hasa ikiwa yule anayehitaji msaada anaonyesha mtazamo kama wa Wayahudi wa siku za Yeremia. Jitahidi kuona jitihada za mara kwa mara za wazee kuwa njia ya Yehova ya kukuonyesha upendo. Pia, kumbuka kwamba Yeremia hangehitaji kurudia maonyo yake tena na tena ikiwa watu wangechukua hatua inayofaa. Kwa hiyo, ili kuepuka kushauriwa tena na tena tunapaswa kufuata shauri mara tu tunapolipokea.

Picha katika ukurasa wa 70

Wazee wanapojaribu kukusaidia, sikiliza

INGAWA YEHOVA HUSAMEHE KWA HIARI, KUNA MASHARTI

10. Kwa nini msamaha wa Yehova una masharti?

10 Hata tujaribu namna gani, hatuwezi kamwe kumtii Yehova kikamilifu katika mfumo huu. Tunathamini kwamba yuko tayari kutusamehe tunapokosea. Hata hivyo, kuna masharti. Kwa nini? Kwa sababu Yehova anachukia dhambi. (Isa. 59:2) Hivyo, anataka kuhakikisha kwamba tunastahili msamaha wake.

11. Kwa nini mtu anayefanya dhambi sirini hatakosa kupata adhabu?

11 Kama vile ambavyo tumeona, Wayahudi wengi wa siku za Yeremia walikuwa na mazoea ya kutomtii Mungu na kutumia vibaya subira na rehema yake. Je, mtumishi wa Mungu leo anaweza kuwa na mtazamo kama huo? Ndiyo, ikiwa anapuuza vikumbusho vya Yehova na kuanza kufanya dhambi. Katika visa fulani, hilo limetendeka waziwazi, kwa mfano wakati mtu anapoingia katika ndoa ya uzinzi. Lakini hata kama dhambi haijulikani na wanadamu, yule anayekataa kumtii Yehova yuko hatarini. Huenda mtu mnafiki akasema, ‘Hakuna atakayejua.’ Hata hivyo, ukweli ni kwamba Mungu anatazama ndani ya akili na mioyo na anaweza kuona kinachofanywa sirini. (Soma Yeremia 32:19.) Ni nini kinachopaswa kufanya ikiwa kwa kweli mtu amekosa kumtii Mungu?

12. Wakati mwingine wazee hulazimika kufanya nini ili kulinda kutaniko?

12 Wayahudi wengi walidharau msaada ambao Yehova aliwapa tena na tena kupitia Yeremia. Vivyo hivyo, huenda mtu ambaye amefanya dhambi nzito leo akakataa kutubu, na kukataa msaada wa wazee. Katika hali hiyo, wazee watafuata mwongozo wa Kimaandiko wa kulinda kutaniko kwa kumtenga na ushirika mkosaji huyo. (1 Kor. 5:11-13; ona sanduku “Kuishi Bila Sheria,” katika ukurasa wa 73.) Hata hivyo, je, hilo linamaanisha kwamba huo ndio mwisho wa mambo, kwamba mtu huyo hawezi kamwe kumrudia Yehova? Hapana. Ingawa Waisraeli waliasi kwa muda mrefu, bado Mungu aliwaambia: “Rudini, ninyi wana waasi. Nitaiponya hali yenu ya uasi.” (Yer. 3:22)a Yehova anawaalika wakosaji wamrudie. Na si kuwaalika tu, bali anawaagiza wafanye hivyo.

KUISHI BILA SHERIA

Wayahudi waliishi maisha ya aina gani baada ya Yerusalemu kuharibiwa? Yeremia anatueleza kifupi kwenye Maombolezo 2:9. Kuta za Yerusalemu zilikuwa zimebomolewa, huenda hata malango ya jiji hilo. Isitoshe, ‘hawakuwa na sheria.’ Je, Yeremia alimaanisha kwamba watu waliookoka uharibifu huo walikuwa umati wenye fujo? Yaelekea alimaanisha kwamba wamepoteza ulinzi wa kiroho na hali nzuri waliyokuwa wakifurahia wakati ambapo makuhani waaminifu na manabii walikuwa wakiwafundisha Sheria ya Mungu. Sasa manabii wa uwongo waliowategemea hawakuwa na ‘maono’ ya kweli, au mwongozo, kutoka kwa Yehova; “maono” yao yalikuwa ya ubatili.—Omb. 2:14.

Huenda mtu ambaye ametengwa na ushirika wa kutaniko la Kikristo akajiona hivyo. Anakosa ushirika wenye upendo wa ndugu na dada zake wa kiroho na wazee wanaomjali. Amepoteza mwongozo wa kiroho. Katika ulimwengu ‘usio na sheria’ kutoka kwa Yehova, huenda anahisi kuwa amepata hasara kubwa. Vyovyote vile, anaweza kurudi na kupata kibali cha Yehova na kufurahia baraka nyingi tena. (2 Kor. 2:6-10) Hata hivyo, kumtii Yehova na kuendelea kuishi kupatana na sheria ni bora kuliko kuishi bila sheria.

Kwa nini tunapaswa kumwomba Mungu msamaha tunapokosea?

MTII YEHOVA KWA KURUDI KWAKE

13. Mtu anayetaka kumrudia Yehova, anapaswa kutambua nini?

13 Kulingana na maneno ya Yeremia, mtu anayetaka kumrudia Mungu anapaswa kujiuliza: ‘Nimefanya nini?’ Kisha kwa kutegemea kanuni za Kimaandiko, anapaswa kukubali kwa unyoofu ukweli wa mambo. Wayahudi ambao hawakutubu katika siku za Yeremia walikwepa swali hilo. Hawakukiri uzito wa dhambi zao, na kwa sababu hiyo Yehova hangeweza kuwasamehe, naye hakuwasamehe. (Soma Yeremia 8:6.) Tofauti nao, mtenda-dhambi anayetubu hutambua kwamba kwa kutomtii Yehova, ameleta suto juu ya jina la Mungu na juu ya kutaniko la Kikristo. Mtu mwenye toba ya kweli huhuzunishwa sana na madhara ambayo huenda amewasababishia wasio na hatia. Anapaswa kukumbuka kwamba ili Yehova azingatie ombi lake la kutaka msamaha, lazima kwanza akiri madhara yote ambayo yamesababishwa na matendo yake mabaya. Hata hivyo, kumrudia Mungu kunatia ndani mengi zaidi.

14. Ni kwa njia gani mtu anaweza ‘kurudi kabisa kwa Yehova’? (Tia ndani sanduku “Toba Ni Nini?”)

14 Mtu mwenye toba ya kweli huchunguza nia, tamaa, na mazoea yake. (Soma Maombolezo 3:40, 41.) Atachunguza udhaifu mbalimbali alio nao, kama vile uhusiano wake na watu wa jinsia tofauti, matumizi ya pombe au sigara, matumizi ya Intaneti, au shughuli za kibiashara. Kama vile mwanamke nyumbani anavyosugua kona zilizofichika jikoni kwake ili kudumisha nyumba ikiwa safi, mtu anayetubu anapaswa kujitahidi sana kusafisha mawazo yake na mambo anayofanya faraghani. Anapaswa ‘kurudi kabisa kwa Yehova’ kwa kutimiza matakwa ya Mungu na kufuata viwango Vyake. Baadhi ya Wayahudi katika siku za Yeremia walimrudia Yehova kwa “uwongo.” Walijifanya wanajuta lakini hawakubadili kamwe mioyo au maisha yao. (Yer. 3:10) Tofauti nao, mtu anayeomba msamaha kikweli hajaribu kumdanganya Yehova na kutaniko Lake. Badala ya kujaribu kuepuka aibu au kutaka tu kuendeleza ushirika pamoja na watu wa ukoo au wengine katika kweli, anataka kuacha kabisa mwenendo mbaya ili astahili kupata msamaha na kibali cha Mungu.

TOBA NI NINI?

Katika Biblia, maneno ya Kiebrania na Kigiriki yanayotafsiriwa toba hurejelea mtazamo wa mtu; kama vile mtu anapobadili maoni kuhusiana na mwenendo mbaya aliokuwa nao au ana mwelekeo wa kuufuata. Maneno hayo pia yanafafanua hisia za mtu kama huyo, kama vile majuto na faraja. (2 Sam. 13:39; Ayu. 42:6) Biblia inaonyesha waziwazi kwamba toba ya kweli inahusisha matendo yanayochochewa na hisia zenye nguvu kutoka moyoni. Ili kupata msamaha wa Yehova, wote wanaotubu dhambi zao wanapaswa kuonyesha toba ya aina hiyo.—Yer. 31:18, 19.

15. Mtu anayetubu kikweli hutoa sala za aina gani kwa Mungu?

15 Sala ni sehemu muhimu ya toba. Katika nyakati za kale, lilikuwa jambo la kawaida watu kuinua mikono kuelekea mbinguni wanaposali. Leo, mtu anayetubu kikweli anaposali, ‘anainua moyo wake pamoja na mikono yake kwa Mungu aliye mbinguni,’ kama Yeremia alivyosema. (Omb. 3:41, 42) Majuto humchochea mkosaji mwenye toba kutenda kulingana na ombi lake la msamaha. Sala zake ni za unyoofu, zinatoka moyoni.

Picha katika ukurasa wa 75

‘Kwa nini sikusikiliza?’

16. Kwa nini ni jambo la hekima kumrudia Mungu?

16 Ni wazi kwamba mkosaji anayekiri kikweli makosa yake huenda akahitaji kushinda kiburi chake. Lakini jambo kuu ni hili: Yehova anataka wakosaji wamrudie. Mungu anapoona moyo wa mwanadamu wenye huzuni ya kweli, moyo wake utamchochea kuchukua hatua. Anaanza kuwa na “msukosuko” wa hisia zenye upendo kwa sababu anataka kuwasamehe wote wanaotubu dhambi zao, kama vile alivyowasamehe Waisraeli waliorudi kutoka uhamishoni. (Yer. 31:20) Inatia moyo kama nini kujua kwamba Mungu anawapa amani na tumaini wale wanaomtii! (Yer. 29:11-14) Kwa mara nyingine tena wanaweza kutumikia pamoja na watumishi wengine waaminifu wa Mungu.

UTII UNAWEZA KUKULINDA

17, 18. (a) Warekabi walikuwa nani? (b) Kama ukurasa wa 77 unavyoonyesha, wanajulikana kwa kufanya nini?

17 Kumtii Yehova katika kila jambo ni ulinzi. Mfano wa Warekabi wa siku za Yeremia unathibitisha hilo. Karne mbili hivi mapema, babu yao Mkeni, Yehonadabu, ambaye alimuunga mkono Yehu, aliwapa amri kadhaa. Amri moja ilihusu kutokunywa divai. Ingawa muda mrefu ulikuwa umepita tangu Yehonadabu afe, Warekabi waliendelea kumtii. Akitaka kupima utii wao, Yeremia aliwapeleka katika chumba cha kulia katika hekaluni, akaweka divai mbele yao na kuwasihi wanywe. Walimwambia: “Hatutakunywa divai.”—Yer. 35:1-10.

18 Kwa Warekabi, kumtii babu yao aliyekufa zamani kulikuwa jambo muhimu. Waabudu wa kweli wanapaswa kutii hata zaidi amri za Mungu aliye hai. Utii wa Warekabi ulimpendeza Yehova, nao walikuwa tofauti kabisa na Wayahudi walioasi. Mungu aliwaahidi Warekabi ulinzi wakati wa msiba uliokuwa unakaribia. Namna gani leo? Je, hatungetazamia kwamba Yehova atawahakikishia wale wanaomtii kabisa ulinzi wakati wa dhiki kubwa?—Soma Yeremia 35:19.

Picha katika ukurasa wa 77

Kwa nini kutubu dhambi nzito ni sehemu muhimu ya utii? Utii unaweza kumsaidia jinsi gani mtu asihitaji kutubu?

WANAOMTII YEHOVA HAWAKO PEKE YAO

19. Mungu anaweza kukupa ulinzi gani ukimtii?

19 Yehova hakuwalinda watu wake nyakati za zamani tu. Hata leo, Yehova huwalinda wanaomtii dhidi ya hatari ya kiroho. Kama vile ukuta mrefu ulivyoyalinda majiji ya zamani yasishambuliwe, sheria ya Mungu inawalinda wale wanaojifunza sheria hiyo na kuitumia. Je, utakaa ndani ya ukuta huo wenye ulinzi wa sheria za Mungu za maadili? Uwe na hakika kwamba mambo yatakuendea vema ukifanya hivyo. (Yer. 7:23) Mambo mengi yaliyoonwa yanathibitisha ukweli huo.​—Ona sanduku “Kumtii Yehova Ni Ulinzi,” katika ukurasa wa 78.

20, 21. (a) Unaweza kuwa na uhakika gani unapomtumikia Yehova? (b) Mfalme Yehoyakimu alitenda jinsi gani aliposikia ujumbe wa Mungu kupitia Yeremia?

20 Iwe wako kazini au shuleni, au ni wenye mamlaka, wapinzani hufanya iwe vigumu kumtumikia Mungu. Hata hivyo, unaweza kuwa na hakika kwamba ikiwa unamtii Yehova katika kila hali, atakusaidia hata utakapokuwa katika hali ngumu zaidi. Usisahau kwamba Mungu aliahidi kumtegemeza Yeremia wakati ambapo angepata upinzani mkali, na Yehova alitimiza ahadi yake. (Soma Yeremia 1:17-19.) Moja kati ya pindi ambazo msaada wa Mungu ulionekana wazi ni katika siku za Mfalme Yehoyakimu.

21 Si wengi kati ya watawala wa Israeli waliowapinga wasemaji wa Mungu kwa hasira kama alivyofanya Yehoyakimu. Hilo linaonekana wazi katika kisa cha nabii Uriya, aliyeishi wakati mmoja na Yeremia. Mfalme mwovu, Yehoyakimu, alituma watu wamfuate mpaka nchi jirani. Uriya, nabii wa Yehova aliporudishwa, mfalme alimuua kwa upanga. (Yer. 26:20-23) Katika mwaka wa nne wa utawala wa Yehoyakimu, Yehova alimwamuru Yeremia aandike maneno yote ambayo alikuwa amemwambia kufikia wakati huo kisha ayasome kwa sauti hekaluni. Yehoyakimu alichukua kitabu cha kukunjwa cha Yeremia na kumwagiza afisa wa makao ya mfalme amsomee. Alipokuwa akikisoma, mfalme alikirarua kitabu hicho na kukitupa ndani ya moto, ingawa baadhi ya wakuu walimsihi asifanye hivyo. Kisha akatuma watu wakawakamate Yeremia na Baruku. Ikawaje? ‘Yehova aliendelea kuwaficha.’ (Yer. 36:1-6; soma Yeremia 36:21-26.) Yehova hakumruhusu Yehoyakimu awadhuru wanaume hao wawili waaminifu.

KUMTII YEHOVA NI ULINZI

Kijana mmoja Shahidi nchini Hispania amefaidika sana kwa kumtii Yehova. Anasema: “Msichana fulani shuleni alitaka tuwe marafiki. Alikuwa mrembo sana, hata hivyo, nilijua kwamba kuna hatari kufanya urafiki na mtu asiyempenda Yehova.

“Wakati huohuo, wanafunzi wenzangu walikuwa wakinishinikiza niende kwenye karamu ya mwisho wa muhula. Nilipotumia Biblia kuwaeleza ni kwa nini siwezi kujiunga nao, walianza kunitukana. Nilijiona kuwa sifai. Nilizungumza na mzee wa kutaniko letu. Akaniuliza, ‘Watu ambao hawaheshimu maoni yako na viwango vyako vya maadili wanaweza kuwa rafiki zako wa kweli?’ Maneno yake yalinipa nguvu na kunisaidia kushinda shinikizo la wanafunzi wenzangu.

“Nafurahi kwamba sikwenda. Kwenye karamu hiyo, msichana mmoja alibakwa. Usiku huohuo, wanafunzi watatu walijeruhiwa vibaya katika msiba wa barabarani kwa sababu yule aliyekuwa akiliendesha gari alikuwa amelewa. Ikiwa ningeenda kwenye karamu hiyo, huenda ningekuwa katika gari hilo pamoja nao. Namshukuru Yehova kwa kunipa nguvu za kumtii licha ya kushinikizwa na marafiki shuleni.”

22, 23. Mfano wa Shahidi mmoja huko Asia ya kati unaonyesha utegemezo wa Mungu jinsi gani?

22 Yehova akiona inafaa, anaweza pia kuwaficha watumishi wake leo wasipatwe na madhara. Hata hivyo, mara nyingi yeye huwapa ujasiri na hekima ili wamtii na kuendelea kuhubiri habari njema. Mama mmoja, ambaye tutamwita Gulistan, analea watoto wanne pasipo mwenzi. Yehova amemtegemeza. Kwa muda, yeye tu ndiye aliyekuwa Shahidi katika eneo kubwa la Asia ya kati ambamo wenye mamlaka wanapinga kazi ya kuhubiri. Kutaniko la karibu liko umbali wa zaidi ya kilomita 400, hivyo Gulistan hapati nafsi ya kushirikiana na Wakristo wakomavu. Licha ya upinzani na matatizo mengine, yeye huhubiri nyumba kwa nyumba na hupata watu wengi wenye kupendezwa. Kulingana na ripoti moja ya hivi karibuni, amekuwa akiongoza mafunzo ya Biblia 20 hivi na anatunza kikundi kinachozidi kukua cha kondoo wa Yehova.

23 Kama Yehova alivyomsaidia Yeremia na Mashahidi wengine kama Gulistan, yuko tayari kukusaidia wewe na watumishi wake watiifu. Azimia kumtii yeye kuwa Mtawala kuliko wanadamu. Ukifanya hivyo, upinzani na vizuizi vingine havitakuzuia kumsifu Mungu wa pekee wa kweli mbele ya watu walio katika eneo lenu.—Yer. 15:20, 21.

24. Utii una faida gani leo?

24 Hatuwezi kupata furaha na uradhi wa kweli maishani tusipomtegemea Muumba wetu. (Yer. 10:23) Baada ya kujifunza yale ambayo Yeremia aliandika kuhusu utii, je, kuna njia ambazo unaweza kumruhusu Yehova aongoze hatua zako zaidi? Amri zake ndizo tu zinazoweza kutuongoza kupata furaha na mafanikio kamili. Yehova anatusihi hivi: ‘Tiini sauti yangu, ili iwe vema kwenu.’​—Yer. 7:23.

Katika uhusiano wako na Mungu, unaweza kutumia jinsi gani mambo ambayo umejifunza katika kitabu cha Yeremia kuhusu utii?

a Yehova alikuwa akizungumza na taifa la kaskazini la Israeli. Watu wa ufalme huo wa makabila kumi walikuwa uhamishoni kwa miaka 100 hivi Yeremia alipotangaza ujumbe huo. Alikiri kwamba hata kufikia siku zake, bado taifa hilo halikuwa limetubu. (2 Fal. 17:16-18, 24, 34, 35) Hata hivyo, watu mmoja-mmoja wangeweza kupata tena kibali cha Mungu, na hata kurudi kutoka uhamishoni.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki