Myanmar (Burma)
IKIWA katikati ya nchi kubwa zaidi za Asia, India na China, Myanmar ni nchi yenye mambo mengi yanayovutia.a Yangon (zamani Rangoon), ndilo jiji kubwa zaidi, kuna majengo makubwa ya ghorofa, maduka mengi, na msongamano wa magari. Hata hivyo nje ya jiji la Yangon kuna vijiji vingi ambako nyati hutumiwa kulima, watu wanastaajabishwa na wageni, na muda unapimwa kwa kupita kwa majira.
Myanmar ya leo inatukumbusha jinsi bara la Asia lilivyokuwa. Kuna mabasi ya zamani yanayoyumba-yumba katika barabara zenye mashimo na kuyapita magari ya kukokotwa na ng’ombe yanayosafirisha mazao hadi sokoni na wachungaji wa mbuzi wanachunga mbuzi wao malishoni. Wengi wa wanaume wa Myanmar bado wanavaa sketi za kitamaduni zinazofungwa kiunoni (lungi). Wanawake wanapaka usoni mchanganyiko laini unaotengenezwa kutokana na magome ya mti (thanaka) ili kujiremba. Watu wanapenda sana dini. Wafuasi wa Budha wanawaheshimu zaidi watawa wao kuliko watu mashuhuri na kila siku wanakandika dhabihu za karatasi za dhahabu kwenye sanamu inayong’aa ya Budha.
Watu wa Myanmar ni wapole, wenye kujali, na wadadisi. Kuna makabila makubwa nane na karibu makabila madogo-madogo 127 nchini Myanmar. Kila kabila lina lugha, mavazi, chakula, na utamaduni wake. Watu wengi wanaishi katika nyanda pana ya kati inayorutubishwa na mto mkubwa wa Ayeyarwady (Irrawaddy), wenye urefu wa kilomita 2,170, chanzo chake kikianzia kwenye barafu za Himalaya na kuishia kwenye maji moto ya Bahari ya Andaman. Mamilioni zaidi wanaishi kwenye mwambao mkubwa wa delta iliyo pwani na mwishoni mwa nyanda za juu zinazopakana na Bangladesh, China, India, Laos, na Thailand.
Kwa miaka 100 hivi, Mashahidi wa Yehova nchini Myanmar wamekuwa na imani isiyoyumba-yumba na uvumilivu. Wakati wa vurugu zenye jeuri na misukosuko ya kisiasa, wamedumisha msimamo wao wa kutojiingiza katika mambo ya kisiasa. (Yoh. 17:14) Licha ya hali ngumu, upinzani wa kidini, na mawasiliano hafifu kati yao na ndugu zao ulimwenguni pote, watu wa Yehova wamehubiri habari njema za Ufalme wa Mungu bila kuchoka. Habari ifuatayo inaonyesha masimulizi yao yenye kutia moyo.
Kazi ya Kuhubiri Yaanza
Katika mwaka wa kihistoria wa 1914, Waingereza wawili walishuka katika bandari ya Yangon yenye joto kali. Hendry Carmichael na painia mwenzake walisafiri kutoka India wakiwa na mgawo mgumu wa kuanzisha kazi ya kuhubiri nchini Burma. Eneo lao lilitia ndani nchi nzima.
Wakianzia jijini Yangon, muda si muda Hendry na mwandamani wake walikutana na wanaume wawili Waingereza-Wahindi ambao walipendezwa kikweli na ujumbe wa Ufalme.b Bertram Marcelline na Vernon French waliacha mara moja kushirikiana na dini zinazodai kuwa za Kikristo na wakaanza kuwahubiria isivyo rasmi marafiki wao. Baada ya muda mfupi, karibu watu 20 walikuwa wakikutana kwa ukawaida kwenye nyumba ya Bertram ili kujifunza Biblia kwa kutumia gazeti la Mnara wa Mlinzi.c
Wahubiri jijini Yangon, mwaka 1932
Mnamo 1928, painia mwingine Mwingereza kutoka India, George Wright, alitembelea Burma na kutalii kwa miezi mitano akigawa machapisho mengi ya Biblia. Bila shaka, mbegu hizo za kweli zilitia ndani kijitabu kilichotolewa mwaka 1920 Millions Now Living Will Never Die!—kijitabu cha kwanza kati ya machapisho yetu ya Kikristo kutafsiriwa katika lugha ya Kiburma.
Miaka miwili baadaye, mapainia Claude Goodman na Ronald Tippin waliwasili jijini Yangon na kupata kikundi kidogo cha akina ndugu waliokuwa wakifanya mikutano kwa uaminifu lakini wakihubiri bila utaratibu. “Tuliwatia moyo akina ndugu wahubiri kila Jumapili,” akasema Claude. “Ndugu mmoja aliuliza ikiwa wengine wanaweza kuhubiri kwa niaba yake, halafu atupatie pesa sisi mapainia. Ron akamwambia: “Hakuna shaka, isipokuwa tu iwe unataka wengine wapate uzima wa milele kwa niaba yako.’” Kikundi kilihitaji kitia moyo hicho kilichotolewa kwa njia ya wazi. Baada ya muda mfupi, Claude na Ronald wakapata waandamani wengi wa kuhubiri nao.
“Rachel, Nimeipata Kweli!”
Mwaka huohuo, Ron na Claude walikutana na Sydney Coote, msimamizi wa kituo cha treni jijini Yangon. Sydney alikubali vitabu vilivyoitwa seti ya upinde wa mvua, mkusanyiko wa vitabu vyetu kumi vyenye rangi zinazong’aa. Baada ya kusoma sehemu mbalimbali za kitabu kimoja, Sydney akamwita mke wake na kumwambia, “Rachel, nimeipata kweli!” Muda mfupi baadaye familia nzima ya Coote ilikuwa ikimtumikia Yehova.
Sydney alikuwa mwanafunzi mwenye bidii wa Maandiko. Binti yake Norma Barber, mmishonari wa muda mrefu ambaye sasa anatumikia katika ofisi ya tawi ya Uingereza, anaeleza hivi: “Baba yangu alikusanya marejeo ya maandiko katika kitabu chake mwenye. Wakati wowote alipopata andiko linaloelezea fundisho la Biblia, aliliandika kwenye kitabu chake chini ya kichwa kinachohusu andiko hilo. Alikiita kitabu hicho Where Is It?”
Sydney Coote (katikati) alikuwamwanafunzimwenye bidii waMaandiko; yeye na mke wake, Rachel (kushoto), waliwahubiria wengine ujumbe wa Biblia
Si kwamba Sydney alitaka kujifunza Biblia tu bali pia alitaka kuwaambia wengine ujumbe wa Biblia. Kwa hiyo, aliiandikia ofisi ya tawi ya India akiuliza ikiwa kulikuwa na Mashahidi wowote nchini Burma. Baada ya muda mfupi, alipokea sanduku kubwa lenye machapisho na orodha ya majina. “Baba alimwandikia barua kila mtu aliyekuwa katika orodha hiyo, akimwalika atutembelee kwa siku moja,” anasema Norma. “Akina ndugu watano au sita walikuja nyumbani kwetu na kutuonyesha jinsi ya kuhubiri isivyo rasmi. Wazazi wangu hawakupoteza muda wowote, waligawa machapisho hayo kwa marafiki na majirani. Pia waliwatumia barua na machapisho watu wetu wote wa ukoo.”
Daisy D’Souza, dada ya Sydney aliyekuwa akiishi Man-dalay, alipopokea barua ya Sydney na kijitabu The Kingdom, the Hope of the World, alijibu mara moja akiomba Biblia na machapisho zaidi. “Mama yangu alifurahia sana kusoma kijitabu hicho hivi kwamba alikisoma karibu usiku kucha,” anasema binti yake Phyllis Tsatos. “Kisha akatukusanya watoto wote sita kwa ajili ya tangazo lenye kushangaza: ‘Ninaachana na Kanisa Katoliki, kwa sababu nimeipata kweli!’” Baadaye, mume wa Daisy na watoto pia waliikubali kweli. Leo, watu wa vizazi vinne vya familia ya D’Souza wanamtumikia Yehova Mungu kwa uaminifu.
Mapainia Jasiri
Mwanzoni mwa miaka ya 1930, mapainia jasiri walikuwa wakitangaza habari njema kandokando ya reli ya kaskazini inayotoka Yangon hadi Myitkyina, mji ulio karibu na mpaka wa China. Pia walihubiri Mawlamyine (Moul-mein) na Sittwe (Akyab), miji ya pwani iliyo mashariki na magharibi mwa Yangon. Matokeo yake, makutaniko madogo yalianzishwa haraka jijini Mawlamyine na Mandalay.
Mwaka 1938 usimamizi wa kazi ya kuhubiri nchini Burma ulihamishwa kutoka tawi la India kwenda tawi la Australia, na mapainia kutoka Australia na New Zealand walianza kuwasili nchini Burma. Wafanyakazi hao wenye bidii walitia ndani Fred Paton, Hector Oates, Frank Dewar, Mick Engel, na Stuart Keltie. Akina ndugu hao walikuwa mapainia wenye bidii kwelikweli.
Frank Dewar
Fred Paton anaeleza hivi: “Kwa miaka minne niliyokuwa nchini Burma, nilihubiri katika maeneo mengi ya nchi hiyo. Wakati huo wote, niliugua malaria, homa ya matumbo, kuhara damu, na matatizo mengine ya kiafya. Baada ya kuhubiri siku nzima, mara nyingi sikuwa na mahali pa kulala. Hata hivyo, siku zote Yehova aliniandalia mahitaji yangu na kunisaidia kuvumilia kwa nguvu za roho yake.” Frank Dewar, mwanaume jasiri kutoka New Zealand, anasema: “Nilikabiliana na majambazi, waasi, na maofisa wenye kuogopesha. Lakini nilitambua kwamba kuwa mtulivu, mpole, mnyenyekevu, na mwenye kukubali maoni ya wengine, kulifanya hata vikwazo vikubwa vitoweke. Baada ya muda mfupi, watu wengi walitambua kwamba Mashahidi wa Yehova si watu hatari.”
Mapainia hao walikuwa tofauti kabisa na wageni waliokuwa wakiishi nchini humo, ambao kwa kawaida waliwatendea wenyeji kwa njia isiyofaa. Mapainia hao waliwatendea watu kwa heshima na upendo. Mfikio wao wa fadhili uliwavutia Waburma wanyenyekevu, ambao wanapendelea mazungumzo ya upole na busara badala ya mazungumzo ya moja kwa moja na malumbano. Kupitia maneno na matendo yao, mapainia hao walionyesha kwamba Mashahidi wa Yehova ndio Wakristo wa kweli.—Yoh. 13:35.
Kusanyiko la Kihistoria
Miezi kadhaa baada ya mapainia kuwasili, ofisi ya tawi ya Australia ilipanga kufanya kusanyiko jijini Yangon. Mahali pa kufanyia kusanyiko palikuwa kwenye Ukumbi wa Jiji la Yangon, jengo kubwa linalopendeza lenye ngazi za maru-maru na milango mikubwa ya shaba. Wajumbe wa kusanyiko walitoka Thailand, Malasia, na Singapore, naye Alex MacGillivray, mtumishi wa ofisi ya tawi ya Australia, alikuja na kikundi cha akina ndugu kutoka Sydney.
Kukiwa na dalili za vita kutokea, kichwa cha hotuba “Vita vya Ulimwengu Wote Viko Karibu” kilichotangazwa kwa mapana na marefu kilisababisha watu wengi sana wapendezwe. “Sijawahi kuona ukumbi ukijaa haraka kadiri hiyo,” alisema Fred Paton. “Nilipofungua milango ya mbele, umati wa watu ulisukumana kwenye ngazi na ndani ya ukumbi. Kwa muda usiozidi dakika kumi, zaidi ya watu 1,000 walikuwa wamejaa kwenye ukumbi wenye viti 850.” “Tulilazimika kufunga milango ya mbele kwa sababu ya umati uliokuwa ukiongezeka, tukiwaacha watu wengine 1,000 nje,” akaongeza Frank Dewar. “Licha ya milango kufungwa, vijana fulani hodari walijipenyeza na kuingia kupitia milango midogo ya pembeni.”
Akina ndugu walisisimka si tu na upendezi mkubwa ulioonyeshwa bali pia watu waliohudhuria, ambao walitia ndani watu kutoka makabila mbalimbali. Mpaka wakati huo, wenyeji wachache sana walikuwa wameonyesha upendezi katika kweli, kwa kuwa wengi wao walikuwa waumini wa Budha. Wenyeji waliodai kuwa Wakristo—wengi wao wakiwa Wakayin (Wakaren), Wakachin, na Wachin—waliishi katika maeneo ya mbali ambayo haikuwa rahisi kufikiwa na habari njema. Ilionekana kwamba eneo hilo la wenyeji lilikuwa tayari kwa ajili ya mavuno. Baada ya muda mfupi “umati mkubwa” kutoka katika mataifa mbalimbali uliotabiriwa katika Biblia ungetia ndani pia makabila mengi yaliyo nchini Burma.—Ufu. 7:9.
Wanafunzi wa Kwanza Wakayin
Wanafunzi wa kwanza Wakayin, Chu May “Daisy” (kushoto) na Hnin May “Lily” (kulia)
Mnamo 1940 painia aliyeitwa Ruby Goff alikuwa akihubiri mjini Insein, mji mdogo ulio katika viunga vya jiji la Yangon. Akiwa amepata upendezi mdogo siku hiyo, Ruby alisali, “Yehova, tafadhali niruhusu nipate angalau ‘kondoo’ mmoja kabla sijarudi nyumbani.” Katika nyumba iliyofuata, alikutana na Hmwe Kyaing, Mkayin aliyekuwa Mbaptisti, ambaye alikuwa tayari kusikiliza ujumbe wa Ufalme. Muda mfupi baadaye, Hmwe Kyaing na binti zake, Chu May (Daisy) na Hnin May (Lily), walikuwa wakijifunza Biblia na kufanya maendeleo mazuri ya kiroho. Ingawa Hmwe Kyaing alikufa muda mfupi baadaye, Lily, binti yake mdogo, alikuja kuwa Mkayin wa kwanza kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Daisy pia alibatizwa.
Lily na Daisy walikuja kuwa mapainia wenye bidii na kuacha kumbukumbu isiyosahaulika. Leo, mamia ya vizazi vyao na mafunzo yao ya Biblia wanamtumikia Yehova nchini Myanmar na nchi za ng’ambo.
Matatizo Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu
Mnamo 1939, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilianza kupiganwa barani Ulaya, madhara yake yakienea duniani kote. Wakati vita hivyo vikiendelea, viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo nchini Burma walizidi kuishinikiza serikali ya kikoloni ipige marufuku machapisho yetu. Ili kukabiliana na hali hiyo, Mick Engel, aliyekuwa akitunza depo ya machapisho jijini Yangon, alienda kwa ofisa wa Marekani mwenye cheo cha juu, na akapewa kibali cha kusafirisha karibu tani mbili za machapisho kwa kutumia lori la jeshi kutoka Burma hadi China.
Fred Paton na Hector Oates walichukua machapisho na kuyasafirisha hadi Lashio, mji ulio karibu na mpaka wa China. Walipokutana na ofisa aliyekuwa akiongoza msafara uliokuwa ukielekea China, ofisa huyo alilipuka kwa hasira! “Mnasema nini?” akafoka. “Ninawezaje kuwapa nafasi ya thamani kwenye malori yangu kwa ajili ya trakti zenu zisizofaa kitu wakati sina nafasi hata kidogo kwa ajili ya mahitaji ya haraka ya jeshi na vifaa vya kitiba, ambavyo vipo hapa nje vikioza?” Fred alitua kidogo, kisha akatoa kibali kutoka kwenye mkoba wake, na akamwambia ofisa huyo kwamba lingekuwa jambo zito sana ikiwa atapuuza agizo kutoka kwa maofisa wa Yangon. Papo hapo, mwongozaji huyo akawapa lori dogo, dereva na vifaa ambavyo akina ndugu walihitaji. Walisafiri karibu kilomita 2,400 ili kufika Chongqing (Chungking), kusini ya kati ya China, mahali ambapo waligawa machapisho hayo yenye thamani na hata walimhubiria Chiang Kai-shek, rais wa serikali ya Kitaifa ya China.
Hatimaye, mnamo Mei 1941, serikali ya kikoloni nchini India iliwasiliana na Yangon, na kuziagiza mamlaka za eneo hilo kukamata machapisho yetu. Ndugu wawili waliokuwa wakifanya kazi katika ofisi ya mawasiliano waliona ujumbe huo na mara moja wakamjulisha Mick Engel. Mick aliwasiliana na Lily na Daisy nao wakafanya haraka kwenda depo, ambako waliondoa makatoni 40 ya machapisho yaliyobaki na kuyaficha kwenye nyumba mbalimbali jijini Yangon. Wenye mamlaka walipofika, machapisho yote yalikuwa yameondolewa.
Mnamo Desemba 11, 1941, siku nne baada ya Japani kushambulia Pearl Harbor, mabomu ya Wajapani yalianza kuangushwa katika ardhi ya Burma. Mwisho-juma huo kikundi kidogo cha Mashahidi kilikusanyika kwenye jengo dogo juu ya Kituo cha Treni cha Kati jijini Yangon. Baada ya mazungumzo ya Kimaandiko, Lily akabatizwa bafuni kwenye beseni kubwa la kuogea.
Majuma kumi na mbili baadaye, jeshi la Wajapani liliingia Yangon na kukuta karibu wakazi wote wameondoka jijini. Zaidi ya watu mia moja elfu walikimbia kuelekea India. Maelfu walikufa njiani, kwa sababu ya njaa, uchovu, na ugonjwa. Sydney Coote, ambaye alikimbia na familia yake, alikufa karibu na mpaka wa India kutokana na malaria iliyopanda kichwani. Ndugu mmoja alipigwa risasi na wanajeshi wa Japani, wakati ndugu mwingine alimpoteza mke na familia yake, nyumba yao ilipolipuliwa na bomu.
Ni Mashahidi wachache tu waliobaki nchini Burma. Lily na Daisy walihamia Pyin Oo Lwin (Maymyo), mji mtulivu ulio pande za mlimani karibu na Mandalay, ambako walipanda mbegu za kweli ambazo baadaye zilizaa matunda. Shahidi wa tatu, Cyril Gay, aliishi Thayarwaddy, kijiji kidogo kilicho kilomita hivi kaskazini mwa Yan-gon, mahali alikoishi kipindi chote cha vita.
Shangwe ya Kukutana Tena
Vita ilipoisha, wengi wa akina ndugu na dada ambao walikimbilia India walianza kurudi Burma. Kufikia Aprili 1946 Kutaniko la Yangon lilikuwa na wahubiri watendaji nane. Mwishoni mwa mwaka, kutaniko lilipokua kufikia wahubiri 24, akina ndugu waliamua kufanya kusanyiko.
Kusanyiko la siku mbili lilifanywa kwenye shule moja mjini Insein. “Nilirudi kutoka India na kupewa mgawo wa kutoa hotuba ya dakika sitini,” anakumbuka Theo Syriopoulos, ambaye alijifunza kweli jijini Yangon mwaka 1932. “Mpaka kufikia wakati huo, nilikuwa nimetoa hotuba mbili tu za dakika tano kwenye mikutano nchini India. Hata hivyo, kusanyiko lilifanikiwa na zaidi ya watu 100 walihudhuria.”
Majuma machache baadaye, kiongozi wa kabila la Kayin ambaye alipendezwa na kweli alilipa kutaniko kipande cha ardhi huko Ahlone, eneo lililo kandokando ya mto karibu na katikati ya jiji la Yangon. Akina ndugu walijenga mahali hapo Jumba la Ufalme la mianzi na kuweka viti kwa ajili ya watu mia moja hivi. Kutaniko lilifurahi sana. Akina ndugu na dada waliokoka vita, imani yao ikiwa imeimarishwa na walikuwa tayari na wenye hamu ya kuendelea kuhubiri.
Wamishonari wa Kwanza wa Gileadi Wawasili
Juu: Wamishonari wa kwanza wa Gileadi Hubert Smedstad, Robert Kirk, Norman Barber, na Robert Richards.
Mapema mwaka wa 1947, kikundi cha akina ndugu wenye shauku kilikusanyika katika bandari ya Yangon ili kumkaribisha Robert Kirk, mmishonari wa kwanza aliyezoezwa Gileadi kuingia nchini Burma. Muda mfupi baadaye, wamishonari watatu zaidi waliwasili—Norman Barber, Robert Richards, na Hubert Smedstad—pamoja na Frank Dewar, ambaye alikuwa akipainia nchini India wakati wa vita.
Wamishonari waliwasili katika jiji lililokuwa limeharibiwa na vita. Majengo yasiyo na idadi yalikuwa yameharibiwa na mabomu. Maelfu ya watu waliishi kwenye vibanda vya mianzi vilivyochakaa pembezoni mwa barabara. Watu walipika, walifua, na kuishi mitaani. Hata hivyo, wamishonari walikuja kufundisha kweli za Biblia, kwa hiyo walibadilikana kulingana na hali na wakawa na mengi ya kufanya katika huduma.
Mnamo Septemba 1, 1947, ofisi ya tawi ya Watch Tower Society ilianzishwa kwenye nyumba ya wamishonari katika Barabara ya Signal Pagoda, karibu na katikati ya jiji. Robert Kirk alipewa mgawo wa kusimamia ofisi ya tawi. Muda mfupi baadaye, Kutaniko la Yangon lilihama kutoka kwenye jumba la mianzi la Ahlone na kuhamia kwenye jengo la ghorofa katika Mtaa wa Bogalay Zay. Ghorofa hilo lilikuwa karibu na jengo la ofisi za Usimamizi, jengo la kifahari la serikali ya kikoloni ya Uingereza—utawala ambao siku zake zilikuwa zikihesabika!
Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe Vyaanza!
Mnamo Januari 4, 1948, Waingereza waliikabidhi mamlaka serikali mpya ya Burma. Baada ya miaka 60 ya utawala wa kikoloni, Burma ikawa huru. Hata hivyo, nchi ilikuwa ikipigana vita vya wenyewe kwa wenyewe.
Makabila mbalimbali yalipigana ili kuanzisha majimbo huru, wakati majeshi ya watu binafsi na magenge ya wahalifu yakishindana ili kupata maeneo ya kutawala. Mapema mwaka wa 1949, majeshi ya waasi yalidhibiti maeneo mengi ya nchi, na mapigano yakatokea kwenye viunga vya jiji la Yangon.
Wakati mapigano yakipamba moto, akina ndugu walihubiri kwa tahadhari sana. Ofisi ya tawi ilihamishwa kutoka kwenye Barabara ya Signal Pagoda na kupelekwa katika jengo kubwa la ghorofa kwenye Mtaa wa 39, eneo lenye usalama lililokuwa na ofisi nyingi za ubalozi. Jengo hilo lilikuwa mwendo wa dakika tatu tu kutoka ilipo ofisi kuu ya posta.
Jeshi la Burma liliimarisha mamlaka yake hatua kwa hatua, likiwafukuzia waasi milimani. Kufikia katikati ya miaka ya 1950, serikali ilikuwa imetwaa tena udhibiti wa maeneo mengi ya nchi. Hata hivyo, Vita vya Wenyewe kwa Wenyewe havikuisha. Vimeendelea kwa njia moja au nyingine hadi leo.
Kuhubiri na Kufundisha kwa Kiburma
Hadi kufikia katikati ya miaka ya 1950, akina ndugu nchini Burma walihubiri kwa kiasi kukubwa kwa Kiingereza, lugha iliyozungumzwa na wasomi katika miji mikubwa na majiji. Hata hivyo, mamilioni ya watu hawakuongea lugha nyingine zaidi ya Kuburma (Myanmar), Kikayin, Kikachin, au lugha nyingine za kienyeji. Wangewezaje kuhubiriwa habari njema?
Mnamo 1934, Sydney Coote alipanga mwalimu wa shule Mkayin atafsiri vijitabu mbalimbali katika Kiburma na Kikayin. Baadaye, wahubiri wengine walitafsiri kitabu “Mungu na Awe wa Kweli” na vijitabu kadhaa katika Kiburma. Kisha, mwaka 1950, Robert Kirk alimwomba Ba Oo atafsiri makala za funzo kwenye Mnara wa Mlinzi katika Kiburma. Tafsiri zilizoandikwa kwa mkono zilipangwa na kuchapishwa na kampuni ya uchapishaji ya Yangon na wale waliohudhuria mikutano ya kutaniko walipewa makala hizo. Baadaye, ofisi ya tawi ya Burma ilinunua mashine ya kuchapa ili kazi ya kutafsiri ifanywe kwa haraka zaidi.
Ba Oo (kushoto) alitafsiri makala za funzo kwenye Mnara wa Mlinzi katika Kiburma
Watafsiri hao wa mapema walikabili hali ngumu nyingi. “Nilifanya kazi mchana ili kuiruzuku familia yangu na kisha nilitafsiri makala usiku nikitumia mwanga hafifu wa balbu ya umeme,” anakumbuka Naygar Po Han, ambaye aliendelea na kazi ya kutafsiri baada ya Ba Oo kutoweza kuendelea kufanya kazi hiyo. “Habari iliyotafsiriwa ni lazima iwe haikuwa sahihi sana kwa sababu ujuzi wangu wa Kiingereza ulikuwa mdogo sana. Hata hivyo, tulitaka sana magazeti yetu yawafikie watu wengi iwezekanavyo.” Robert Kirk alipomwomba Doris Raj atafsiri Mnara wa Mlinzi katika Kiburma, alishindwa kuzuia hisia zake hivi kwamba akaangua kilio. “Nilikuwa na elimu ya msingi tu na sikuwa na uzoefu wowote wa kutafsiri,” anaeleza Doris. “Hata hivyo, ndugu Kirk alinitia moyo nijaribu. Kwa hiyo, nilisali kwa Yehova na kuanza kazi.” Leo, miaka 50 hivi baadaye, bado Doris anafanya kazi akiwa mtafsiri katika Betheli ya Yangon. Naygar Po Han, sasa ana miaka 93, yeye pia yuko Betheli na bado ana shauku katika kuendeleza kazi ya Ufalme.
Mwaka 1956, Nathan Knorr alitangaza kutolewa kwa Mnara wa Mlinzi katika Kiburma
Mwaka 1956, Nathan Knorr kutoka makao makuu ya ulimwenguni pote alitembelea Burma na kutangaza kutolewa kwa Mnara wa Mlinzi katika Kiburma. Pia, aliwahimiza wamishonari wajifunze lugha hiyo ili kwamba wahubiri kwa mafanikio zaidi. Wakitiwa moyo na himizo lake, wamishonari waliongeza jitihada zao katika kujifunza Kiburma. Mwaka uliofuata, Frederick Franz, mjumbe mwingine kutoka makao makuu ya ulimwenguni pote, alikuwa msemaji wa hotuba ya msingi katika kusanyiko la siku tano lililofanywa kwenye Ukumbi wa Taasisi ya Reli jijini Yangon. Aliwatia moyo akina ndugu kupanua kazi ya kuhubiri hadi mbali zaidi kwa kuwatuma mapainia kwenye majiji na miji ya mbali. Eneo la kwanza kunufaika na mapainia hao wapya lilikuwa mji mkuu wa zamani wa Burma ambao pia ni jiji la pili kwa ukubwa, Mandalay.
Matokeo ya Kazi ya Kuhubiri Jijini Mandalay
Mapema mwaka wa 1957, mapainia wa pekee wapya sita waliwasili jijini Mandalay na kuungana na wenzi wapya wa ndoa Robert Richards, ambaye alikuwa mmishonari, na mke wake Mkayin, Baby, ambao tayari walikuwa jijini humo. Mapainia waliona kwamba jiji hilo ni eneo gumu. Mandalay ni kituo kikubwa cha dini ya Budha na karibu nusu ya watawa wa Kibudha huishi katika jiji hilo. Hata hivyo, mapainia walitambua kwamba kama ilivyokuwa katika Korintho la kale, Yehova alikuwa na ‘watu wengi katika jiji hilo.’—Mdo. 18:10.
Mmoja wa watu hao alikuwa Robin Zauja, mwanafunzi Mkachin mwenye umri wa miaka 21, ambaye anakumbuka hivi: “Siku moja asubuhi na mapema, Robert na Baby Richards walikuja nyumbani kwangu na kujitambulisha kuwa wao ni Mashahidi wa Yehova. Walisema kwamba walikuwa wakitangaza habari njema nyumba kwa nyumba, wakitii amri ya Yesu ya kuhubiri. (Mt. 10:11-13) Walinieleza ujumbe wao na wakanipa anwani yao, pamoja na magazeti na vitabu kadhaa. Jioni ya siku hiyo nilichukua kitabu kimoja na kukisoma usiku kucha na kufikia asubuhi nilikuwa nimekimaliza. Siku hiyohiyo, nilienda nyumbani kwa Robert na kumuuliza maswali mengi kwa saa kadhaa. Alijibu kila swali kwa kutumia Biblia.” Baada ya muda mfupi Robin Zauja akawa Mkachin wa kwanza kukubali kweli. Baadaye, alitumikia kaskazini mwa Burma kwa miaka mingi akiwa painia wa pekee, na kuwasaidia karibu watu mia moja wajifunze kweli. Wawili kati ya watoto wake sasa wanatumikia katika Betheli ya Yangon.
Mwanafunzi mwingine mwenye bidii alikuwa Pramila Galliara, msichana mwenye umri wa miaka 17 ambaye alikuwa ametoka tu kujifunza kweli jijini Yangon. “Baba yangu, mshiriki wa dini ya Jain, alipinga vikali imani yangu mpya,” anasema Pramila. “Mara mbili alichoma Biblia yangu na machapisho ya Biblia, na mara nyingi alinipiga mbele ya watu. Pia alinifungia ndani ya nyumba ili nisihudhurie mikutano ya Kikristo, na hata alitishia kuiteketeza nyumba ya Ndugu Richards! Hata hivyo, alipoona kwamba hawezi kuvunja imani yangu, polepole aliacha kunipinga.” Baada ya kuacha masomo yake ya chuo kikuu, Pramila alikuja kuwa painia mwenye bidii na baadaye alifunga ndoa na mwangalizi wa mzunguko Dun-stan O’Neill. Kuanzia wakati huo, amewasaidia watu 45 waingie katika kweli.
Wakati kazi ikisonga mbele jijini Mandalay, ofisi ya tawi iliwatuma wamishonari au mapainia katika majiji na miji mingine pia, kutia ndani Pathein (Bassein), Kalaymyo, Bhamaw, Myitkyina, Mawlamyine, na Myeik (Mer-gui). Ni wazi kwamba Yehova alibariki kazi hiyo, kwani makutaniko imara yalianzishwa katika miji yote hiyo.
Wamishonari Wafukuzwa!
Kazi ya kuhubiri ilipokuwa ikiendelea kupanuka, nchi iliendelea kushuhudia mizozo ya kikabila na ya kisiasa. Mwishowe, mnamo Machi 1962 jeshi liliipindua serikali. Mamia ya maelfu ya Wahindi na Waingereza-Wahindi walifukuzwa na kupelekwa India na Bangladesh (zamani iliitwa Pakistan Mashariki), na wageni wanaozuru wangeweza kupata kibali cha kukaa kwa saa 24 tu. Burma ilifanya iwe vigumu kwa raia wake kuwasiliana na watu wa mataifa mengine.
Akina ndugu walikuwa wakishuhudia mabadiliko hayo wakiwa na wasiwasi mwingi. Serikali ya kijeshi ilitoa uhakikisho wa uhuru wa ibada, ikiwa tu dini ingejitenga na siasa. Kama ilivyotarajiwa, wamishonari wa dini zinazodai kuwa za Kikristo waliendelea kujiingiza katika mambo ya kisiasa. Hatimaye, ilipofika Mei 1966, serikali ilikuwa imevumilia vya kutosha, hivyo, iliagiza wamishonari wote wa kigeni waondoke nchini humo! Wamishonari Mashahidi walikuwa waangalifu sana ili wasijihusishe katika siasa; hata hivyo, wao pia baada ya muda mfupi walifukuzwa.
Akina ndugu wenyeji walishtushwa lakini hawakuvunjika moyo. Walijua kwamba Yehova Mungu yupo pamoja nao. (Kum. 31:6) Hata hivyo, bado akina ndugu fulani walijiuliza jinsi ambavyo kazi ya Ufalme ingeendelea.
Baada ya muda mfupi, Yehova alianza kuelekeza mambo. Mara moja, Maurice Raj, aliyekuwa mwangalizi wa mzunguko hapo awali na ambaye kwa kadiri fulani alipata mazoezi katika ofisi ya tawi, aliwekwa rasmi ili asimamie ofisi ya tawi. Ingawa ni Mhindi, Maurice hakufukuzwa pamoja na Wahindi wengine. “Miaka kadhaa mapema, nilijaza ombi la kuwa raia wa Burma,” anaeleza. “Hata hivyo, sikuwa na kyats 450d zilizohitajika ili kulipia hati ya uraia, kwa hiyo niliamua kusubiri. Kisha siku moja nilipokuwa nikipita katika ofisi ya kampuni iliyoniajiri miaka iliyopita, bosi wangu wa awali aliniona. Akaniita kwa sauti: ‘Raj, njoo uchukue pesa zako. Ulipoondoka, ulisahau kuchukua pesa zako ulizokuwa ukitengewa kwa ajili ya malipo ya uzeeni.’ Zilikuwa jumla ya kyats 450.
“Nilipokuwa nikiondoka katika ofisi hiyo, niliwaza jinsi ambavyo ningetumia kyats 450. Lakini kwa kuwa zilikuwa pesa kamili nilizohitaji kulipia hati yangu ya uraia, nilihisi kwamba yalikuwa mapenzi ya Yehova nitumie pesa hizo kwa kusudi hilo. Uamuzi huo ulikuwa na faida kubwa. Wahindi wengine walipofukuzwa nchini Burma, mimi nilibaki, niliweza kusafiri bila vizuizi, kuingiza machapisho nchini, na kufanya mambo mengine muhimu yanayohusiana na kazi ya kuhubiri, nilifanya yote hayo kwa sababu nilikuwa raia wa Burma.”
Maurice pamoja na Dunstan O’Neill, walipanga ziara ya kuzunguka nchi nzima ili kuyatia moyo makutaniko na vikundi vilivyo mbali. “Tuliwaambia akina ndugu: ‘Msihofu, Yehova yupo pamoja nasi. Ikiwa sisi ni washikamanifu kwake, atatusaidia,’” anasema Maurice. “Na kwa kweli, Yehova alitusaidia! Muda mfupi baadaye mapainia wa pekee wapya waliwekwa rasmi, na kazi ya kuhubiri iliongezeka kwa kasi hata zaidi.”
Leo, miaka 46 baadaye, Maurice, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi, bado anasafiri kotekote nchini Myanmar ili kuyaimarisha makutaniko. Kama mzee Kalebu wa kale, bado ana bidii ileile kwa ajili ya kazi ya Mungu.—Yos. 14:11.
Kazi ya Kuhubiri Yafika Katika Jimbo la Chin
Moja ya maeneo ya kwanza kupata mapainia wa pekee lilikuwa Jimbo la Chin, eneo lenye milima linalopakana na Bangladesh na India. Eneo hilo lina watu wengi wanaodai kuwa Wakristo, kwa sababu ya wamishonari Wabaptisti waliofika wakati wa utawala wa kikoloni wa Uingereza. Hivyo, watu wengi wa Chin wanaiheshimu sana Biblia na watu wanaofundisha Biblia.
Kuelekea mwisho wa mwaka 1966, Lal Chhana, mwanajeshi wa zamani ambaye sasa ni painia wa pekee, aliwasili Falam, uliokuwa mji mkubwa zaidi katika Jimbo la Chin. Akiwa huko aliungana na Dunstan na Pramila O’Neill na Than Tum, mwanajeshi mwingine wa zamani ambaye alikuwa amebatizwa karibuni. Wafanyakazi hao wenye bidii walipata familia kadhaa zinazopendezwa na baada ya muda mfupi wakaanzisha kutaniko dogo lakini lenye bidii.
Mwaka uliofuata, Than Tum alihamia Hakha, mji ulio kusini mwa Falam, ambako alianza kupainia na akaanzisha kikundi kidogo. Baadaye aliendelea kuhubiri kotekote katika Jimbo la Chin na kusaidia kuanzisha makutaniko huko Vanhna, Surkhua, Gangaw, na katika maeneo mengine. Leo, miaka 45 baadaye, Than Tum bado ni painia wa pekee mwenye bidii katika kijiji chake cha nyumbani, Vanhna.
Than Tum alipoondoka Hakha, Donald Dewar, painia wa pekee mwenye umri wa miaka 20 alichukua mahali pake. Kwa kuwa wazazi wa Donald, Frank na Lily (zamani Lily May) Dewar, walikuwa wamefukuzwa karibuni, mdogo wa Donald, Samuel mwenye umri wa miaka 18, aliungana naye. “Tuliishi kwenye kibanda kidogo cha bati ambacho kilikuwa na joto kali wakati wa kiangazi na kiliganda wakati wa baridi kali,” anasema Donald. “Hata hivyo, upweke ndilo jambo lililokuwa gumu hata zaidi. Kwa kawaida nilihubiri peke yangu na ilikuwa vigumu sana kuongea lugha ya wenyeji, Kihakha Chin. Mimi na Samuel tu, na nyakati fulani mhubiri mwingine mmoja au wawili ndio tuliohudhuria mikutano. Polepole nikavunjika moyo na hata nikawa nafikiria kuacha mgawo wangu.
“Karibu wakati huohuo, nilisoma simulizi lenye kuchochea katika Kitabu cha Mwaka kuhusu ndugu zetu nchini Malawi ambao walibaki waaminifu chini ya mateso makali.e Kisha nikajiuliza, ‘Ikiwa siwezi kuvumilia upweke, nitawezaje kuvumilia mateso?’ Nilimweleza Yehova mahangaiko yangu katika sala na nikaanza kujihisi nafuu. Pia, nilipata nguvu kwa kusoma na kutafakari Biblia na makala zilizo kwenye Mnara wa Mlinzi. Nilipotembelewa bila kutarajia na ndugu Maurice Raj na Dunstan O’Neill, nilihisi kana kwamba nilikuwa nikiona malaika wawili! Polepole nilipata shangwe tena.”
Baadaye, alipokuwa akitumikia akiwa mwangalizi anayesafiri, Donald alitumia mfano wake mwenyewe kuwatia moyo Mashahidi wengine walio kwenye maeneo ya mbali. Pia, jitihada zake huko Hakha zilizaa matunda. Sasa, Hakha wanafurahia kuwa na kutaniko kubwa na huandaa kwa ukawaida makusanyiko ya pekee, mzunguko na wilaya. Wawili kati wahubiri ambao walihudhuria mikutano huko Hakha, Johnson Lal Vung na Daniel Sang Kha, walikuja kuwa mapainia wa pekee wenye bidii ambao walisaidia kutangaza habari njema katika maeneo mengi zaidi ya Jimbo la Chin.
‘Kupanda Milima’
Jimbo la Chin lipo kati ya mita 900 hadi 1,800 kutoka usawa wa bahari kukiwa na vilele fulani vilivyoinuka hadi mita 3,000. Milima mingi imefunikwa na misitu minene iliyojaa miti mirefu ya mivule, misonobari maridadi, maua ya waridi yenye rangi mbali mbali, na maua mazuri ya okidi. Eneo hilo lina mapori makubwa yanayofanya usafiri uwe mgumu. Miji katika eneo hilo imeunganishwa na barabara za vumbi zilizopindapinda ambazo zinafanya iwe vigumu kusafiri katika kipindi cha mvua na mara nyingi zinaharibiwa na maporomoko ya udongo. Vijiji vingi vya mbali vinaweza kufikika kwa miguu tu. Hata hivyo, vikwazo hivyo, havijawazuia watumishi wa Yehova, ambao wameazimia kuwahubiria habari njema watu wengi kadiri iwezekanavyo.
Aye Aye Thit, ambaye alitumikia pamoja na mume wake katika Jimbo la Chin, anakumbuka hivi: “Nililelewa kwenye maeneo tambarare ya Delta ya Ayeyarwady na nilipendezwa sana na uzuri wa Milima ya Chin. Nilifurahia sana kupanda mlima kwa mara ya kwanza, hata hivyo tukiwa kileleni nilizimia kwa sababu ya kukosa hewa. Baada ya kupanda milima kadhaa baadaye, nilikuwa nimechoka sana hivi kwamba nilifikiri ningekufa. Hatimaye, nilijifunza jinsi ya kupanda milima—kwa kupumzika na kutumia nguvu zangu vizuri. Baada ya muda mfupi niliweza kutembea hadi kilomita 32 kwa siku katika safari ya siku sita au zaidi.”
Kushoto: Washiriki wa Kutaniko la Matupi walitembea Kilomita 270 ili kuhudhuriamakusanyiko ya Kikristomjini Hakha
Kwa miaka mingi, akina ndugu katika Jimbo la Chin wamekuwa wakitumia njia mbalimbali za usafiri, kutia ndani nyumbu, farasi, baiskeli, na hivi karibuni, pikipiki, malori ya abiria, na magari yanayoendeshwa kwa magurudumu manne. Lakini wengi wao, hutembea. Kwa mfano, ili kufika kwenye vijiji vilivyo karibu na Matupi, mapainia wa pekee Kyaw Win na David Zama walisafiri kilomita nyingi sana wakipanda milima na mabonde. Ili kwenda kuhudhuria makusanyiko ya Kikristo mjini Hakha, mji ulio umbali wa zaidi ya kilomita 270, Kutaniko la Matupi lilitembea kwa siku sita hadi nane ili kufika Hakha na siku sita hadi nane kurudi. Wakiwa njiani waliimba nyimbo za Ufalme ambazo zilisikika kwenye milima hiyo maridadi.
Safari hizo ngumu zilihatarisha maisha ya akina ndugu kwa sababu ya hali mbaya ya hewa ya milimani, mbu wengi, na kila aina ya wadudu hatari, hasa wakati wa majira ya mvua. “Nilipokuwa nikitembea msituni, niliona wadudu wanaonyonya damu wakipanda miguuni mwangu,” anakumbuka Myint Lwin, mwangalizi wa mzunguko. “Nilipokuwa nikiwatoa, wawili zaidi wakanipanda. Nikarukia juu ya mti uliokuwa umeanguka, lakini kundi la wadudu hao wakaanza kupanda juu ya gogo hilo. Nilikimbia kwa woga katikati ya msitu huo. Mwishowe nilipofika barabarani, nilikuwa nimejaa wadudu hao.”
Kulia: Mwangalizi wa wilaya Gumja Naw na mke wake, Nan Lu, walitembelea makutaniko yaliyokuwa milimani katika Jimbo la Chin
Hata hivyo, wasafiri katika Jimbo la Chin walivumilia mengi zaidi ya wadudu hao wanaonyonya damu. Nchini Myanmar pia kuna nguruwe-pori, dubu, chui, simbamarara, na kulingana na vyanzo fulani vya habari, kuna aina mbalimbali za nyoka wenye sumu kuliko nchi nyingine yoyote ulimwenguni. Walipokuwa wakipanda milima ili kutembelea makutaniko katika Jimbo la Chin, mwangalizi wa wilaya Gumja Naw na mke wake, Nan Lu, waliwasha moto wakati wa usiku ili kuwafukuza wanyama-pori!
Wahubiri hao wenye bidii hawatasahaulika. “Walimtumikia Yehova kwa nguvu zao zote,” anasema Maurice Raj. “Hata baada ya kuondoka Jimbo la Chin, walikuwa tayari kurudi. Kwa kweli, jitihada zao zilimtukuza Yehova!” Leo, licha ya kuwa moja ya maeneo yenye watu wachache sana nchini Myanmar, Jimbo la Chin lina makutaniko saba na vikundi kadhaa.
“Hakuna ‘Kondoo’ Mjini Myitkyina”
Mwaka 1966 mapainia wa pekee kadhaa waliwasili mjini Myitkyina, mji mdogo ambao umepangwa vizuri ulio kwenye kona ya mto Ayeyarwady katika Jimbo la Kachin, karibu na China. Miaka sita mapema, Robert na Baby Richards walihubiri kidogo mahali hapo. Waliripoti hivi: “Hakuna ‘kondoo’ mjini Myitkyina.” Hata hivyo, mapainia hao wapya waliwapata watu wenye njaa ya kupata kweli.
Mmoja kati ya watu hao alikuwa Mya Maung, Mbaptisti mwenye umri wa miaka 19 ambaye alikuwa akisali kwa Mungu akiomba msaada wa kuielewa Biblia. Anakumbuka hivi: “Mapainia waliponitembelea katika sehemu yangu ya kazi na kuniomba nijifunze nao Biblia, nilikuwa na shangwe nyingi sana. Nilihisi kwamba sala zangu zilikuwa zimejibiwa. Mimi na mdogo wangu, San Aye, tulikuwa tukijifunza mara mbili kwa juma, na tulifanya maendeleo ya kiroho haraka.
“Tulisaidiwa na mwalimu mzuri sana—Wilson Thein. Badala tu ya kutuambia jambo la kufanya, alituonyesha jinsi ya kufanya! Kupitia vipindi vya mazoezi na maonyesho, tulijifunza jinsi ya kutumia Biblia vizuri, kuhubiri kwa ujasiri, kushinda upinzani, kuandaa na kutoa hotuba kutanikoni. Wilson Thein alitusikiliza tulipokuwa tukifanya mazoezi ya kila hotuba na kutupa mapendekezo ya jinsi ya kuboresha. Mazoezi hayo yalituchochea tujitahidi kufikia malengo yetu ya kiroho.
“Mwaka 1968, mimi na San Aye tulianza kupainia, hiyo ikafanya kuwe na jumla ya mapainia nane katika mji wa Myitkyina. Wanafunzi wetu wa kwanza wa Biblia walitia ndani mama yetu na wadogo zetu saba, ambao hatimaye wote walikubali kweli. Pia, tulikuwa tukihubiri katika miji na vijiji vilivyo kandokando ya reli inayotoka Myitkyina kwenda Mandalay, safari ya siku moja hadi tatu. Mbegu tulizopanda baadaye zilizaa matunda. Leo, miji iliyo kandokando ya reli, Namti, Hopin, Mohn-yin, na Katha ina makutaniko makubwa.”
Alipokuwa akihubiri kwenye eneo la biashara mjini Myitkyina, San Aye alikutana na Phum Ram, Mkachin Mbaptisti ambaye alifanya kazi serikalini. Phum Ram alikubali kweli kwa moyo wote na akahamia Putao, mji mdogo ulio chini ya milima ya Himalaya. Akiwa huko aliwahubiria watu wake wengi wa ukoo, na baada ya muda mfupi watu 25 walikuwa wakihudhuria mikutano ya Kikristo. Akiwa painia, Phum Ram alimsaidia mke na watoto wake saba na watu wake wengi wa ukoo wajifunze kweli. Sasa anatumikia akiwa painia na mzee wa kutaniko mjini Myitkyina.
Mabehewa ya Treni Yakosewa
Mashahidi wanaondoka Yangon kwenda Myitkyina katika treni waliyokodi ili kuhudhuria kusanyikomwaka 1969
Ukuzi wa kiroho wa haraka katika Jimbo la Kachin uliichochea ofisi ya tawi hivi kwamba ikapanga kufanya Mkusanyiko wa Kimataifa wenye kichwa “Amani Duniani” mwaka 1969 mjini Myitkyina badala ya Yangon, mahali ambapo makusanyiko yalifanyika kwa ukawaida. Ili kusafirisha wajumbe kutoka Yangon kwenda Myitkyina, zaidi ya kilomita 1,100 upande wa kaskazini, ofisi ya tawi ililiomba Shirika la Reli la Burma liwakodishie mabehewa sita ya treni. Ombi hilo halikuwa la kawaida kabisa. Jimbo la Kachin ndilo lililokuwa kitovu cha uasi, na safari za kuingia na kutoka jimboni humo zilidhibitiwa vikali sana. Hata hivyo, kwa kustaajabisha mamlaka ya reli ilikubali ombi lao.
Kikundi cha wazee katika Mkusanyiko wa Kimataifa wa “Amani Duniani” mwaka 1969 katika mji wa Myitkyina. (Mstari wa nyuma) Francis Vaidopau, Maurice Raj, Tin Pei Than, Mya Maung, (mstari wa katikati) Dunstan O’Neill, Charlie Aung Thein, Aung Tin Shwe, Wilson Thein, San Aye, (mstari wa mbele) Maung Khar, Donald Dewar, David Abraham, Robin Zauja
Katika siku ambayo treni iliyobeba wajumbe wa kusanyiko iliratibiwa kufika mjini Myitkyina, Maurice Raj na kikundi cha akina ndugu walienda kwenye kituo cha treni ili kuwakaribisha wajumbe. Maurice anaeleza: “Tulipokuwa tukingoja, msimamizi wa stesheni alikuja haraka mahali tulipokuwa na kutuambia kwamba ujumbe ulikuwa umewasili muda mfupi uliopita, uliosema kwamba wenye mamlaka wamekata mabehewa sita ya treni yaliyokuwa na wajumbe wetu, wameyaacha yakiwa yamekwama katikati ya Mandalay na Myitkyina. Ilionekana kwamba, treni isingeweza kupandisha mlima na mabehewa hayo.
“Tungefanya nini? Jambo la kwanza lililotujia akilini lilikuwa kubadili tarehe ya kusanyiko. Lakini kufanya hivyo kungemaanisha kujaza tena fomu nyingi za kuomba kibali, jambo ambalo lingechukua majuma kadhaa! Tulipokuwa tukisali kwa bidii kwa Yehova, mara treni ikaingia stesheni. Hatukuamini macho yetu—mabehewa yote sita yalijaa ndugu zetu! Walikuwa wakitabasamu na kupunga mikono. Tulipouliza jambo lililokuwa limetokea, mmoja wao alisema, ‘walikata mabehewa sita, lakini si mabehewa yetu!’”
Kusanyiko la Myitkyina lilifanikiwa kwa njia ya pekee sana. Wakati wa programu, machapisho mapya matatu yalitolewa katika Kiburma na matano katika Kiingereza. Miaka mitatu mapema wamishonari walipokuwa wamefukuzwa, kuingia kwa chakula cha kiroho nchini Burma kulipungua polepole. Sasa polepole hiyo ikageuka na kuwa mafuriko!
Kuwafundisha Wanaga
Miezi minne baada ya kusanyiko la Myitkyina, ofisi ya tawi ilipokea barua kutoka kwa karani wa posta mjini Khamti, mji ulio kandokando ya mto chini ya milima mirefu kaskazini-magharibi mwa mpaka wa Burma na India. Eneo hilo linakaliwa na jamii ya Wanaga, mkusanyiko wa makabila mbalimbali ambayo wakati fulani yaliogopwa sana kwa sababu ya kuwakata watu vichwa. Katika barua yake, karani huyo, Ba Yee, aliyekuwa Msabato zamani, aliomba msaada wa kiroho. Mara moja ofisi ya tawi iliwatuma mapainia wa pekee wawili, Aung Naing na Win Pe.
Win Pe anaeleza hivi: “Kwenye uwanja wa ndege wa Khamti, tuliogopa sana tulipowaona mashujaa wakali wa Naga wakiwa wamesimama huku wamejifunga mashuka tu kiunoni. Kisha Ba Yee alikuja haraka mahali tulipokuwa ili kutusalimu na akatupeleka mara moja tukakutane na watu fulani waliopendezwa. Baada ya muda mfupi tulikuwa tukijifunza na watu watano.
Biak Mawia (mstari wa nyuma, kulia kabisa) na Kutaniko la Khamti wakati kazi ya kuhubiri ikianzishwa katikamaeneo ya Naga
“Hata hivyo, wenye mamlaka walifikiri kimakosa kwamba tulikuwa wachungaji wa Kibaptisti ambao walishirikiana na vikundi vya waasi. Licha ya kuwahakikishia kwamba hatukuwa tukijihusisha na mambo ya kisiasa, walituamuru tuondoke katika eneo hilo chini ya mwezi mmoja tangu tulipowasili.”
Miaka mitatu baadaye, maofisa wapya walipoingia madarakani, Biak Mawia, painia mwenye umri wa miaka 18, aliendeleza kile ambacho mapainia wa awali walikiacha. Baada ya muda mfupi, Ba Yee alijiuzulu kazi yake katika ofisi ya posta na akaanza kupainia. Kisha mapainia wengine kadhaa wakawasili. Kikundi hicho chenye bidii baada ya muda mfupi kilianzisha kutaniko mjini Khamti na vikundi vidogo kadhaa kwenye vijiji vya karibu. Biak Mawia anakumbuka hivi: “Akina ndugu na dada wa Naga walikuwa watu wasio na elimu na hawakujua kusoma wala kuandika. Hata hivyo, walilipenda Neno la Mungu na walikuwa wahubiri wenye bidii ambao walitumia kwa ustadi picha zilizo kwenye machapisho yetu. Pia, walikariri Maandiko mengi na walijifunza kuimba nyimbo za Ufalme kutoka moyoni.”
Leo, makusanyiko ya wilaya yanafanywa kwa ukawaida mjini Khamti, wajumbe wanaohudhuria wanatoka mbali zaidi katika maeneo yote ya kusini hadi kufikia mji wa Homalin, safari ya saa 15 kwa boti.
Upinzani Katika Eneo la “Pembe Tatu ya Dhahabu”
Wakati huohuo, upande mwingine wa nchi, kazi ilikuwa ikipanuka hadi kufika kwenye nyanda za juu zinazopakana na China, Laos, na Thailand. Hapo ndipo kitovu cha Pembe Tatu ya Dhahabu, eneo zuri lenye milima mikunjo na mabonde yenye rutuba yaliyoharibiwa na uzalishaji wa afyuni (dawa za kulevya), uasi, na shughuli nyingine zisizo halali. Mapainia waliopeleka kweli katika eneo hilo lenye misukosuko walikuwa wenye busara na hadhari. (Mt. 10:16) Hata hivyo, kazi yao ya kuhubiri ilipingwa na kikundi fulani—Viongozi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo!
Mapainia Robin Zauja na David Abraham walipowasili Lashio, mji wenye shughuli nyingi katika Jimbo la Shan, mara moja viongozi wa dini wa eneo hilo waliwatangaza kuwa waasi. Robin alisema: “Tulikamatwa na kupelekwa gerezani, tukiwa huko tuliwaonyesha askari hati zetu za uhudumu. Baada ya muda mfupi, mkuu wa jeshi aliingia ndani. ‘Hujambo Bw. Zauja,’ akasema kwa sauti. ‘Naona Mashahidi wa Yehova wameingia Lashio!’ Mkuu huyo, mwanafunzi mwenzangu wa zamani, akatuachia huru mara moja.”
Mapainia hao wawili wakaanza tena kazi na baada ya muda mfupi wakaanzisha kutaniko kubwa kiasi. Kisha wakajenga Jumba la Ufalme. Miaka miwili baadaye, waliitwa makao makuu ya serikali ya mji wa Lashio kwenye mkutano uliokuwa na zaidi maofisa 70 wa jeshi, viongozi wa makabila, na viongozi wa dini. Robin anakumbuka hivi: “Viongozi wa dini wakiwa na hasira walitushutumu kwamba sisi tuliwachochea watu waache mapokeo ya dini zao. Mwenyekiti wa mkutano alipotaka tutoe jibu, nilimwomba ikiwa ningeweza kutumia Biblia wakati wa kujitetea. Alikubali. Haraka haraka nilitoa sala kimyakimya na kisha nikaeleza maoni ya Biblia kuhusu mapokeo ya uwongo ya dini, utumishi wa kijeshi, na sherehe za kizalendo. Nilipomaliza, mwenyekiti alisimama na kutangaza kwamba sheria ya Burma iliruhusu dini zote kuabudu kwa uhuru. Tuliachiliwa huru na tukaruhusiwa kuendelea kuhubiria, jambo lililowavunja moyo sana viongozi wa dini.”
Baadaye, huko Mongpaw, kijiji kidogo karibu na mpaka wa China, kikundi cha Wabaptisti wenye hasira kilichoma Jumba la Ufalme. Kitendo hicho kibaya kiliposhindwa kuwaogopesha Mashahidi wa eneo hilo, kikundi hicho chenye hasira kilichoma nyumba ya painia wa pekee na kuanza kuwatisha akina ndugu na dada kwenye nyumba zao. Akina ndugu waliwashtaki kwa kiongozi wa eneo hilo, lakini kiongozi huyo aliwaunga mkono Wabaptisti hao. Hatimaye, serikali iliingilia kati na kuwapa akina ndugu kibali cha kujenga Jumba la Ufalme jipya—si nje ya kijiji mahali lilipokuwa awali, bali katikati kabisa ya kijiji!
Upande wa mbele zaidi kusini, Leiktho, kijiji kilicho eneo la mbali milimani katika Jimbo la Kayin, kinachopakana na Pembetatu ya Dhahabu, Gregory Sarilo, alipingwa vikali sana na Kanisa Katoliki. “Kasisi wa kanisa aliagiza wafuasi wake waharibu bustani yangu ya mboga,” anaeleza Gregory. “Kisha wakanipa zawadi za vyakula, hata hivyo, rafiki yangu mmoja alinitahadharisha kwamba chakula hicho kilikuwa na sumu. Siku moja, wafuasi wa kasisi huyo waliniuliza ni njia gani ambayo ningepita siku inayofuata. Siku iliyofuata nilipita njia tofauti na hivyo kuepuka jitihada zao za kutaka kunivizia na kuniua. Nilipotoa taarifa ya majaribio hayo ya kutaka kuniua, mamlaka ilimwagiza vikali kasisi huyo na wafuasi wake kwamba waachane kabisa na mimi. Yehova alinilinda dhidi ya wale ‘walioiwinda nafsi yangu.’”—Zab. 35:4.
Kudumisha Msimamo wa Kutojiingiza Katika Siasa
Kwa miaka mingi, utimilifu wa ndugu na dada nchini Burma umejaribiwa kwa kiwango kikubwa. Mara kwa mara vita vya kikabila na misukosuko ya kisiasa vilitahini msimamo wao wa Kikristo wa kutojiingiza katika mambo ya kisiasa.—Yoh. 18:36.
Katika mji wa kusini wa Thanbyuzayat, unaojulikana kwa kituo cha treni kilichojengwa wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, painia wa pekee Hla Aung aliwahi kujikuta katikati ya mapigano yaliyokuwa yakiendelea kati ya vikosi vya waasi na vya serikali. Anaeleza hivi: “Wanajeshi wa serikali walivamia vijiji usiku na kuwakamata wanaume na kuondoka nao wakiwa wamewaelekezea mitutu ya bunduki ili wakafanye kazi ya kubeba mizigo. Wengi wao hawakuonekana tena. Usiku mmoja, wanajeshi walianza kuvamia kijiji chetu wakati mimi na Donald Dewar tulipokuwa tukizungumza ndani ya nyumba yangu. Mara moja, mke wangu akapiga kelele ili kututahadharisha, jambo lililotuwezesha kukimbilia msituni. Baada ya tukio hilo, nilijenga mahali pa siri pa kujificha ndani ya nyumba yangu, ambapo ningeweza kujificha haraka ikiwa tungevamiwa tena.”
Painia wa pekee Rajan Pandit alipowasili huko Dawei, mji ulio kusini ya Thanbyuzayat, mara moja alianza kuongoza mafunzo ya Biblia katika kijiji cha jirani ambacho kilikuwa ngome ya waasi. Anaeleza hivi: “Nilipokuwa nikirudi kutoka katika kijiji hicho, nilikamatwa na kupigwa na wanajeshi wakinituhumu kwamba nilikuwa nikishirikiana na waasi. Nilipowaeleza kwamba mimi ni Shahidi wa Yehova, walitaka kujua nilifikaje Dawei. Niliwaonyesha tiketi yangu ya ndege—ambayo nilikuwa nimeitunza kama kumbukumbu. Tiketi hiyo ilionyesha kwamba nilifika kwa ndege, usafiri ambao kwa kawaida haukutumiwa na waasi. Hawakuendelea kunipiga na baadaye waliniachilia. Hata hivyo, wanajeshi hao walimhoji mtu mmoja niliyekuwa nikijifunza naye Biblia, ambaye aliwathibitishia kwamba tulikuwa tumejifunza Biblia tu. Baada ya tukio hilo, wanajeshi hao hawakuendelea kunisumbua na hata baadhi yao nikawa nikiwapelekea magazeti kwa ukawaida.”
Nyakati nyingine maofisa wa mji walijaribu kuwashinikiza akina ndugu walegeze msimamo wao wa kutojiingiza katika mambo ya kisiasa ili wapige kura katika uchaguzi au washiriki katika sherehe za kitaifa. Wakati maofisa huko Zalun, mji ulio kando ya mto karibu kilometa 130 kaskazini ya Yangon, walipowalazimisha akina ndugu kupiga kura, akina ndugu walisimama imara, wakitumia Biblia kuthibitisha msimamo wao. (Yoh. 6:15) Maofisa hao wakawasiliana na wenye mamlaka mkoani. Lakini wenye mamlaka mkoani walijua vizuri kwamba Mashahidi wa Yehova hawajiingizi katika mambo ya kisiasa. Mara moja akina ndugu wakaondolewa katika mpango wa uchaguzi.
Watoto 23 waliokuwa Mashahidi huko Khampat, mji ulio katika mpaka wa Burma na India, walipokataa kuiinamia bendera ya taifa, mwalimu mkuu aliwafukuza shule. Kisha akawaita wazee wawili wa kutaniko mbele ya kundi la maofisa, lililotia ndani hakimu wa mji huo na kamanda wa jeshi. Paul Khai Khan Thang mmoja wa wazee hao anasema hivi: “Tulipokuwa tukiwaeleza sababu zinazotegemea Maandiko, baadhi ya maofisa walionyesha uhasama kwelikweli. Kisha tukawaonyesha nakala ya agizo la serikali linalosema kwamba Mashahidi wa Yehova wameruhusiwa ‘kusimama kimya na kwa adabu wakati wa kushushwa na kupandishwa kwa bendera.’ Maofisa hao walipigwa na butwaa. Baada ya kimya cha muda fulani, kamanda wa jeshi akamwamuru mwalimu mkuu awarudishe shuleni wanafunzi waliofukuzwa. Pia, mwalimu mkuu huyo akagawa nakala ya agizo hilo katika kila idara shuleni.”
Leo, maofisa wa ngazi za juu katika serikali ya Myanmar wanajua msimamo wa Mashahidi wa Yehova wa kutojiingiza katika mambo ya kisiasa. Kwa kuendelea kushikilia kwa uimara kanuni za Biblia, Mashahidi wa Yehova wametoa ushahidi mzuri, kama tu Yesu Kristo alivyotabiri.—Luka 21:13.
Wanajeshi Wakubali Kuwa Wakristo
Katika muda wote wa historia yenye msukosuko ya Myanmar, raia wake wengi wametumikia jeshini au kupigana wakiwa waasi. Kama ilivyokuwa kwa Kornelio ofisa wa jeshi la Roma katika karne ya kwanza, baadhi yao ni ‘watu wenye kumheshimu na kumwogopa Mungu.’ (Mdo. 10:2) Baada ya kujifunza kweli, wanajitahidi kuishi kulingana na viwango vya uadilifu vya Yehova.
Mmoja wa watu hao ni Hlawn Mang, ofisa wa zamani wa cheo cha chini katika jeshi ambaye alijifunza kweli alipokuwa akifanya kazi huko Mawlamyine. Anasema hivi: “Nilitaka kuanza kuhubiri mara moja. Lakini nilipokuwa karibu kujiuzulu, niligundua kwamba nimefikiriwa kupandishwa cheo na kupelekwa masomoni chini ya udhamini wa jeshi kwenye shule iliyo katika nchi tajiri ya Magharibi! Hata hivyo, niliazimia kushiriki katika kazi ya Mungu. Kwa mshangao wa wakubwa zangu, niliwasilisha barua yangu ya kujiuzulu na nikaanza kumtumikia Yehova. Leo, karibu miaka 30 baadaye, bado nina hakika kwamba nilifanya uamuzi unaofaa. Hakuna kinachoweza kulinganishwa na pendeleo la kumtumikia Mungu wa kweli!”
Aik Lin (kushoto) na Sa Than Htun Aung (kulia) walipambana katika mapigano kadhaa makali ya msituni wakiwa pande mbili zinazozozana
La Bang Gam, alikuwa akiendelea kupata nafuu katika hospitali ya jeshi alipoonyeshwa kitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikanaf na Robin Zauja. Kitabu hicho kilimsisimua sana La Bang Gam hivi kwamba akaomba abaki nacho. Lakini, kwa kuwa Robin alikuwa na nakala moja tu, alikubali kumwazimisha La Bang Gam kwa usiku mmoja tu. Robin aliporudi siku iliyofuata, La Bang Gam akamwambia: “Chukua kitabu chako. Sasa nina nakala yangu mwenyewe!” Alikesha usiku kucha akinakili kwa mkono kitabu chote chenye kurasa 250 na kukiandika kwenye madaftari kadhaa! Muda mfupi baadaye, La Bang Gam aliacha jeshi na alitumia kitabu chake cha “Paradiso” kuwasaidia wengine wengi wajifunze kweli.
Katika Jimbo la Shan lenye milima, Sa Than Htun Aung, kapteni katika jeshi la Burma, na Aik Lin, kamanda katika Jeshi la Muungano wa Jimbo la Wa, walipambana katika mapigano kadhaa makali ya msituni wakiwa pande mbili zinazozozana. Pande hizo mbili zilipozungumza kuhusu kusitisha mapigano, wote wawili wakaanza kuishi katika Jimbo la Shan. Baadaye bila yule mwingine kujua, kila mmoja akajifunza kweli, akajiuzulu kazi ya jeshi, na kubatizwa. Maadui hawa wa zamani walikutana kwenye kusanyiko la mzunguko, na wakakumbatiana kwa uchangamfu wakiwa ndugu Wakristo! Wakiwa wamewekwa huru kutoka katika minyororo ya chuki, sasa walikuwa wameunganishwa katika vifungo vya upendo kwa msaada wa nguvu zenye kuweka huru za Neno la Mungu.—Yoh. 8:32; 13:35.
Kujadiliana na “Watu wa Namna Zote”
Kati ya 1965 na 1976, idadi ya wahubiri nchini Burma iliongezeka kwa zaidi ya asilimia 300. Wengi wa watu hao wapya walioitikia vizuri jitihada za kuhubiri za Mashahidi walitoka katika dini zinazodai kuwa za Kikristo. Hata hivyo, akina ndugu walijua kuwa mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Tim. 2:4) Hivyo basi, kuanzia katikati ya miaka ya 1970 na kuendelea, waliongeza jitihada ya kuwahubiria waumini wa dini nyingine nyingi za Burma, kutia ndani Wabudha, Wahindu, na watu wanaoabudu vitu vya asili.
Ni jambo la kawaida kuwaona watawa wa Kibudha wakiwa wamevaa mavazi yao ya kitamaduni
Kulikuwa na changamoto nyingi. Wabudha hawaamini kwamba kuna Mungu au Muumba, Wahindu wanaabudu mamilioni ya miungu, na Waburma wanaoabudu vitu vya asili wanahofu viumbe wa roho wenye nguvu wanaoitwa nat. Dini hizi huamini uchawi, uaguzi, na kuwasiliana na pepo. Ingawa waamini wengi wa dini hizi wanaiona Biblia kuwa kitabu kitakatifu, kwa kawaida wanajua machache au hawajui lolote kuhusu watu wanaotajwa katika Biblia, historia, utamaduni, na mafundisho ya Biblia.
Hata hivyo, akina ndugu waliamini kwamba kweli zenye nguvu zinazopatikana katika Neno la Mungu zinaweza kuugusa moyo wa mwanadamu yeyote. (Ebr. 4:12) Walihitaji tu kuitegemea roho ya Mungu na kutumia “ufundi wa kufundisha,” yaani, kutoa hoja zenye kusadikisha ambazo zinaweza kufikia mioyo ya watu na kuwachochea kufanya mabadiliko katika maisha yao.—2 Tim. 4:2.
Kwa mfano, fikiria jinsi Rosaline, painia wa pekee wa muda mrefu anavyojadiliana anapozungumza na Wabudha. Anaeleza hivi: “Wabudha wanapofundishwa kwamba kuna Muumba, mara nyingi huuliza, ‘Lakini ni nani aliyemuumba Muumba?’ Wabudha wanaamini kwamba baada ya kufa wanadamu huzaliwa upya wakiwa wanyama, kwa hiyo, ninatumia mfano wa wanyama wao vipenzi kuhojiana nao.
“‘Je, unafikiri mnyama kipenzi anajua kwamba yule anayemmiliki yupo?’ Ninauliza.
“‘Ndiyo.’
“‘Lakini, je, anajua ikiwa ana kazi, amefunga ndoa, au historia ya yule anayemmiliki?’
“‘Hapana.’
“‘Vivyo hivyo, kwa kuwa wanadamu ni tofauti na Mungu, ambaye ni Roho, je, tutarajie kujua kila jambo kuhusu kuwapo kwa Mungu au chanzo chake?’
“‘Hapana.’”
Kujadiliana kwa njia hiyo kumewasadikisha Wabudha wengi wenye mioyo minyoofu wafikirie uthibitisho zaidi unaoonyesha kwamba kuna Mungu. Bila shaka, watu wanakubali kweli si kwa sababu akina ndugu wanahojiana nao kwa njia inayopatana na akili tu, bali pia kwa sababu ya kuonyeshwa upendo wa kweli wa Kikristo. Ohn Thwin, ambaye alikuwa Mbudha anasema hivi: “Nilipolinganisha fundisho la dini yangu ya Budha kuhusu Nirvana na ahadi ya Biblia kuhusu Paradiso duniani, niliona kwamba fundisho hilo linavutia zaidi. Lakini kwa sababu niliamini kwamba barabara mbalimbali huelekeza watu katika kweli, sikuona uhitaji wa kutenda kulingana na mambo niliyojifunza. Kisha nikaanza kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Nilifarijika sana kutokana na upendo nilionyeshwa na akina ndugu. Upendo huo ulinichochea kutenda kulingana na kile nilichojua kuhusu kweli.”
Kikundi cha Mashahidi nchini Burma,mwaka 1987
Naam, inahitaji busara na uvumilivu kuwasaidia watu wabadili maoni yao ya kidini. Kumar Chakarabani alikuwa na miaka kumi wakati baba yake, ambaye ni Mhindu mwenye msimamo mkali, alipomruhusu Mwanabetheli Jimmy Xavier amfundishe Kumar kusoma. Kumar anakumbuka hivi: “Baba alimwonya anifundishe kusoma tu, si dini. Hivyo, Jimmy akamweleza kwamba Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia ndicho kitabu bora sana cha kuwafundishia watoto kusoma. Pia, kila baada ya kunifundisha kusoma, Jimmy alizungumza na Baba, akipendezwa naye kibinafsi. Baba yangu alipoanza kuuliza maswali kuhusu mambo ya dini, kwa busara Jimmy alimwambia: ‘Biblia ina majibu. Acha tuyatafute pamoja.’ Baada ya muda, baba na watu wengine 63 katika familia yetu wakaikubali kweli na kuwa Mashahidi wa Yehova pia.”
Kufanya Makusanyiko Wakati wa Maasi
Katikati ya miaka ya 1980, hali ya kisiasa nchini Burma ilizidi kuwa mbaya. Hatimaye, mnamo 1988, makumi ya maelfu ya watu wakaandamana barabarani wakiilalamikia serikali. Hata hivyo, jeshi lilidhibiti haraka maandamano hayo, na sehemu kubwa ya nchi ikawa chini ya utawala wa kijeshi.
“Wenye mamlaka waliweka sheria kali ya kutotembea wakati fulani, na vikusanyiko vya watu zaidi ya watano vilipigwa marufuku,” anakumbuka Mwanabetheli Kyaw Win. “Tulijiuliza ikiwa tunapaswa kuacha mipango ya makusanyiko yetu ya wilaya. Lakini tukiwa na imani kwa Yehova, tulimfikia kamanda wa jeshi katika eneo la Yangon na kumwomba ruhusa ya kufanya kusanyiko litakalohudhuriwa na watu 1,000. Siku mbili baadaye tulipata kibali cha kufanya kusanyiko! Tulipoonyesha kibali hicho kwa wenye mamlaka wa maeneo mengine, mara moja waliruhusu makusanyiko yafanyike katika maeneo yao pia. Kwa msaada wa Yehova makusanyiko yote yalifanyika!”
Bila Kuacha Kuhudhuria Mikutano ya Kikristo
Baada ya maasi ya mwaka 1988, hali za kiuchumi nchini Burma zilizidi kuwa mbaya. Hata hivyo, ndugu na dada walionyesha imani thabiti kwa Mungu na kuendelea kutanguliza Ufalme katika maisha yao.—Mt. 6:33.
Kwa mfano, mfikirie Cin Khan Dal, ambaye aliishi pamoja na familia yake katika kijiji cha mbali huko Sagaing. “Tulitaka kuhudhuria kusanyiko la wilaya ambalo lingefanywa huko Tahan, umbali wa siku mbili kwa boti na lori,” anaeleza. “Lakini hakukuwa na mtu wa kuwatunza kuku wetu tutakapokuwa tumeondoka. Hata hivyo, tulimtumaini Yehova na kuhudhuria kusanyiko. Tuliporudi nyumbani, tukakuta kuku 19 wamepotea—hiyo ilikuwa hasara kubwa sana. Hata hivyo, mwaka mmoja baadaye, kuku wetu wachache waliongezeka hadi kufikia kuku zaidi ya 60. Ingawa kuku wengi kijijini walikufa kwa sababu ya ugonjwa mwaka huo, hakuna kuku wetu hata mmoja aliyekufa.”
Wanandoa wengine ambao walibaki macho kiroho ni Aung Tin Nyunt na mke wake, Nyein Mya, ambao waliishi na watoto wao tisa katika kijiji kidogo cha Kyonsha, kilometa 64 kaskazini-magharibi ya Yangon. Aung Tin Nyunt anaeleza: “Mara nyingi, familia yetu ilikula ubwabwa tu na mboga za majani. Hatukuwa na pesa wala kitu chochote cha kuuza. Hata hivyo, hatukuvunjika moyo. Niliiambia familia yangu: ‘Yesu hakuwa na mahali pa kulaza kichwa chake. Kwa hiyo, hata ikiwa nitapaswa kulala chini ya mti au kufa kwa sababu ya njaa, nitaendelea kumtumikia Mungu kwa uaminifu.’
“Hata hivyo, siku moja hatukuwa na chakula kabisa nyumbani mwetu. Mke na wanangu walinitazama wakiwa na nyuso zenye wasiwasi. ‘Msiwe na hofu,’ nikawahakikishia. ‘Mungu atatusaidia.’ Baada ya kushiriki katika utumishi wa shambani asubuhi, nikaenda na wanangu kuvua. Lakini tukapata samaki wa mlo mmoja tu. Tukaacha vikapu vyetu vya kuvulia mtoni, karibu na mahali palipokuwa na mayungiyungi mengi, nikawaambia hivi wanangu: ‘Tutarudi baadaye, baada ya mkutano.’ Alasiri ya siku hiyo kulikuwa na upepo mkali. Tuliporudi, tuligundua kwamba samaki wengi walikuwa chini ya yale mayungiyungi, walijificha kwa sababu ya upepo. Hivyo, tukashusha vikapu vyetu na kuvua samaki wengi, ambao tuliwauza na kununua chakula cha juma zima.”
Mara kwa mara, watumishi wa Yehova nchini Myanmar wameshuhudia kutimizwa kwa ahadi hii ya Mungu yenye kuchangamsha moyo: “Sitakuacha wala kukutupa hata kidogo.” Kwa hivyo wanasema hivi: “Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu anaweza kunitenda nini?”—Ebr. 13:5, 6.
Maendeleo Katika Kazi ya Uchapishaji
Tangu mwaka 1956, watu nchini Myanmar wamefaidika kutokana na chakula cha kiroho kinachopatikana kwa ukawaida katika toleo la Mnara wa Mlinzi katika Kimyanmar (Kiburma). Licha ya vita vya wenyewe kwa wenyewe vilivyokuwa vikiendelea, misukosuko ya kijamii, na hali ngumu za kiuchumi, hakuna toleo hata moja lililokosekana. Gazeti hilo lilichapishwa jinsi gani?
Kwa miaka mingi, ofisi ya tawi ilituma nakala kadhaa zilizochapwa za makala za gazeti lililotafsiriwa kwa mkaguzi wa machapisho wa serikali. Mkaguzi huyo alipoidhinisha makala hizo, ofisi ya tawi ingetuma ombi la kununua karatasi za kuchapishia. Baada ya kupata karatasi, ndugu angezichukua karatasi hizo na nakala za gazeti lililoidhinishwa hadi kwa mtu aliyefanya biashara ya uchapishaji, ambaye alichapa kila ukurasa kwa mkono—herufi baada ya herufi—katika herufi za lugha ya Kimyanmar (Kiburma). Kisha ndugu huyo angehakiki gazeti hilo, halafu mchapishaji huyo angechapisha gazeti hilo kwa kutumia mashine iliyochakaa. Nakala za gazeti zilipelekwa tena kwa mkaguzi, ambaye angeidhinisha kuchapishwa kwa gazeti hilo. Bila shaka, mzunguko huo mrefu ulichukua majuma mengi, na pia, ubora wa karatasi na kazi iliyochapishwa haikuwa nzuri.
Mnamo 1989, ofisi ya tawi ilipokea mfumo mpya wa kuchapishia ambao ulibadili kabisa utendaji wao. Ukiwa umebuniwa na kutengenezwa katika makao makuu ya ulimwenguni pote, mfumo huo Multilanguage Electronic Phototypesetting System (MEPS) ulitumia programu za kompyuta ili kupanga makala katika lugha 186 na kisha baadaye kuchapishwa, programu hiyo ilitia ndani Kimyanmar!g
“Bila shaka, Mashahidi wa Yehova ndio waliokuwa watu wa kwanza kupanga na kuchapisha machapisho kwa kutumia kompyuta nchini Myanmar,” anasema Mya Maung, ambaye alifanya kazi katika ofisi ya tawi. “Mfumo wa MEPS, ambao ulitumia herufi za hali ya juu za Kimyanmar zilizobuniwa katika ofisi yetu, ulileta mabadiliko makubwa katika nyanja ya uchapishaji. Watu hawakuelewa jambo tulilofanya ili kutokeza herufi safi kadiri ile!” MEPS pia ilituwezesha kuwa na njia mpya za kuchapa ambazo ziliboresha sana machapisho yetu. Zaidi ya hayo, MEPS ilituwezesha kuwa na picha na michoro ya hali ya juu, jambo lililofanya gazeti la Mnara wa Mlinzi lizidi kuvutia.
Mnamo 1991 serikali ya Myanmar iliruhusu kuchapishwa kwa gazeti la Amkeni! jambo hilo liliwafurahisha sana akina ndugu. Na hata watu kwa ujumla walifurahi pia! Ofisa wa cheo cha juu katika Wizara ya Habari alieleza kile ambacho watu wengi kwa ujumla walikuwa wakihisi: “Gazeti la Amkeni! liko tofauti sana na magazeti mengine ya kidini. Linazungumzia mambo mengi yenye kuvutia na linaeleweka kwa urahisi. Ninalipenda sana.”
Kwa zaidi ya miaka 20 iliyopita, idadi ya magazeti yanayochapishwa na ofisi ya tawi kila mwezi imeongezeka kutoka nakala 15,000 hadi nakala zaidi ya 141,000, hilo ni ongezeko la karibu asilimia 900! Sasa ni jambo la kawaida kuyaona magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! jijini Yangon na yanapendwa na watu kotekote nchini Myanmar.
Ofisi Mpya ya Tawi Yahitajika
Baada ya maasi ya mwaka 1988, mamlaka ya kijeshi iliomba mashirika ya kijamii na ya kidini nchini Myanmar yajisajili serikalini. Bila shaka, ofisi ya tawi iliitikia mara moja. Miaka miwili baadaye, mnamo Januari 5, 1990, serikali ililiandikisha rasmi shirika la “Jehovah’s Witnesses (Watch Tower) Society” nchini Myanmar.
Majengo ya Betheli yalikuwa madogo sana. Dada alipiga pasi akiwa ameketi sakafuni
Kufikia wakati huo, akina ndugu walikuwa wameihamisha ofisi ya tawi kutoka Mtaa wa 39 hadi katika jengo la ghorofa mbili lililokuwa katika eneo la nusu eka katika Barabara ya Inya, kwenye eneo la watu matajiri kaskazini mwa jiji. Hata hivyo, jengo hilo jipya lilikuwa dogo. Viv Mouritz, ambaye wakati huo alitembelea Myanmar akiwa mwangalizi wa eneo la dunia, anasema: “Washiriki 25 wa familia ya Betheli walifanya kazi katika mazingira magumu. Jikoni hakukuwa na stovu—dada alipika chakula akitumia jiko la kawaida la umeme. Hakukuwa na mashine za kufulia nguo, hivyo dada mmoja alifua nguo kwenye shimo lililokuwa sakafuni. Akina ndugu walitaka kununua stovu na mashine ya kufulia, hata hivyo, vifaa hivyo havingeweza kuingizwa nchini Myanmar.”
Ni wazi kwamba, akina ndugu walihitaji ofisi kubwa hata zaidi. Kwa hiyo, Baraza Linaloongoza liliidhinisha pendekezo la kubomoa jengo hilo lenye ghorofa mbili na kujenga jengo lenye ghorofa nne kwa ajili ya ofisi na makazi. Hata hivyo, kabla akina ndugu hawajaanza kazi hiyo, walipaswa kushinda vipingamizi vikubwa. Kwanza, walihitaji kupata idhini kutoka kwa maofisa sita wa ngazi mbalimbali serikalini. Pili, makampuni ya ujenzi nchini Myanmar ambayo hayakuwa na ujuzi wa kujenga kwa kutumia vyuma, hayangeweza kufanya kazi hiyo. Tatu, Mashahidi wanaojitolea kutoka nchi nyingine hawangeweza kuingia nchini Myanmar. Na hatimaye, vifaa vya ujenzi havikupatikana nchini Myanmar, wala havingeweza kuagizwa kutoka nchi nyingine. Kwa kweli, ilionekana kwamba mradi huo haungefanikiwa. Kama kawaida, akina ndugu walimtegemea Yehova. Ikiwa yalikuwa ni mapenzi ya Yehova, ofisi ya tawi ingejengwa tu!—Zab. 127:1.
‘Si kwa Nguvu, Bali kwa Roho Yangu’
Kyaw Win, kutoka Idara ya Sheria katika ofisi ya tawi, anaeleza hivi: “Maombi yetu ya ujenzi yalishughulikiwa bila shida kwenye ofisi tano kati ya zile sita za serikali, kutia ndani ofisi ya Wizara ya Mambo ya Dini. Kisha Halmashauri ya Kuendeleza Jiji la Yangon ikadai kwamba jengo la ghorofa nne lingekuwa refu sana, hivyo wakalikataa ombi letu. Tulipotuma ombi letu kwa mara nyingine, likakataliwa tena. Halmashauri ya Tawi ilinitia moyo niendelee kuwa mvumilivu. Hivyo, nilisali kwa Yehova kwa bidii na kutuma ombi hilo kwa mara ya tatu. Ombi hilo likakubaliwa!
“Kisha tukaenda Wizara ya Uhamiaji. Maofisa wizarani hapo walituambia kwamba wageni wanaruhusiwa kuingia nchini Myanmar kwa vibali vya kutalii vya siku saba tu. Lakini tulipowaambia wajenzi wetu wenye uzoefu kutoka nchi za nje watawafundisha wenyeji mbinu mpya zaidi za ujenzi, waliwapa wajitoleaji wetu vibali vya miezi sita!
“Kisha tukaenda katika Wizara ya Biashara na kugundua kwamba kuna agizo la kutoingiza kitu chochote. Hata hivyo, tulipowataarifu maofisa kuhusu mradi wetu wa ujenzi, wakatupa kibali cha kuingiza vifaa vya ujenzi vyenye thamani ya zaidi ya dola milioni moja za Marekani. Vipi kuhusu ushuru wa kuingiza vifaa hivyo? Tulipoenda Wizara ya Fedha tukaruhusiwa kuingiza vifaa hivyo bure! Katika njia hizo na nyingine nyingi, tulishuhudia ukweli wa maneno haya ya Mungu: ‘“Si kwa jeshi, wala kwa nguvu, bali kwa roho yangu,” Yehova wa majeshi amesema.’”—Zek. 4:6.
Ndugu wageni na wenyeji walifanya kazi pamoja
Mnamo 1997, wajenzi wakafika katika eneo la ujenzi. Akina ndugu nchini Australia walichangia karibu vifaa vyote vya ujenzi, vifaa vingine vilitoka Malasia, Singa-pore, na Thailand. Bruce Pickering, ambaye alisimamia ujenzi huo, anaeleza: “Akina ndugu kutoka Australia walitengeneza fremu yote ya chuma wakiwa Australia kisha wakasafiri hadi Myanmar ili kuiunganisha. Jambo la kushangaza ni kwamba hawakukosea hata shimo moja!” Wajitoleaji wengine walitoka Fiji, Marekani, New Zealand, Uingereza, Ugiriki, na Ujerumani.
Kwa mara ya kwanza katika kipindi cha miaka 30, ndugu wenyeji waliweza kushirikiana kwa uhuru na ndugu na dada wengi kutoka nchi nyingine. “Tulifurahi sana; ilikuwa kama ndoto,” anakumbuka Donald Dewar. “Hali ya kiroho, upendo, na roho ya kujidhabihu ya wajitoleaji ilitutia moyo sana.” Ndugu mwingine anaongeza hivi: “Pia, tulijifunza mbinu mpya za ujenzi. Wahubiri ambao walikuwa wamezoea kutumia mishumaa tu walijifunza kutandaza nyaya kwa ajili ya taa za umeme. Wengine ambao walikuwa wamezoea kutumia tu vipepeo vya mkono walijifunza kuweka viyoyozi. Hata tulijifunza kutumia vifaa vya umeme!”
Betheli ya Myanmar
Wajitoleaji kutoka ng’ambo nao waliguswa sana na imani na upendo wa ndugu na dada wa Myanmar. “Akina ndugu walikuwa maskini, lakini wakarimu sana,” anasema Bruce Pickering. “Wengi wao walitukaribisha katika nyumba zao kwa ajili ya chakula ambacho kingetosha familia zao kwa siku kadhaa. Kielelezo chao kilitukumbusha jambo la maana zaidi katika maisha, yaani, familia, uhusiano pamoja na Mungu, undugu wetu, na baraka za Mungu.”
Mnamo Januari 22, 2000, majengo mapya ya ofisi yaliwekwa wakfu katika programu ya pekee iliyofanywa katika Ukumbi wa Taifa wa Michezo ya Kuigiza. Ndugu wenyeji walisisimuka kuwa na ndugu John E. Barr wa Baraza Linaloongoza aliyetoa hotuba ya wakfu.
Kujenga Majumba Mapya ya Ufalme
Kazi ya ujenzi wa ofisi ya tawi ilipokuwa inakaribia kumalizika, akina ndugu walianza kufikiria kwa uzito jambo lingine lililohitaji uangalifu wa haraka—Majumba ya Ufalme. Mnamo 1999, Nobuhiko na Aya Koyama waliwasili kutoka Japani. Nobuhiko alisaidia kuanzisha Dawati la Ujenzi wa Majumba ya Ufalme katika ofisi ya tawi. Nobuhiko anakumbuka hivi: “Tulianza kukagua mahali pa kukutanikia pa makutaniko mengi nchini Myanmar, jambo lililotia ndani kusafiri kwa basi, ndege, pikipiki, baiskeli, boti, na kwa miguu. Mara nyingi tulihitaji vibali vya serikali ili tuweze kusafiri kwa kuwa wageni hawakuruhusiwa kwenda kwenye maeneo mengi. Tulipojua mahali ambapo majumba mapya yanahitajika, Baraza Linaloongoza lilitoa fedha za ujenzi kutoka katika programu ya kusaidia nchi zisizo na uwezo mkubwa wa kifedha.
“Baada ya kuunda timu ya wajitoleaji, wafanyakazi walienda huko Shwepyitha, ambacho ni kitongoji katika jiji la Yangon, kujenga jumba jipya la kwanza. Wageni na ndugu wenyeji walifanya kazi pamoja katika mradi huo, jambo lililowashangaza polisi katika eneo hilo ambao walisimamisha ujenzi huo mara kwa mara ili kuwauliza wakubwa zao ikiwa ni sawa kwa wenyeji kuchangamana na watu kutoka nchi nyingine. Watu wengine walioshuhudia waliwapongeza akina ndugu. ‘Nilimwona mgeni kutoka nchi nyingine akisafisha choo!’ mtu mmoja akasema. ‘Sijawahi kuwaona wageni kutoka nchi nyingine wakifanya kazi kama hizo. Kwa kweli, ninyi watu mko tofauti!’
“Wakati huohuo, timu nyingine ilianza kujenga jumba jipya huko Tachileik, mji ulio katika mpaka wa Myanmar na Thailand. Mashahidi wengi wa Thailand walivuka mpaka kila siku ili wafanye kazi na ndugu wa Myanmar katika mradi huo. Akina ndugu hao walifanya kazi kwa umoja hata ingawa walizungumza lugha tofauti. Kinyume kabisa na hali hiyo, wakati jumba lilipokuwa linakaribia kumalizika, vikosi vya kijeshi vya nchi hizo vilivyokuwa mpakani vilianza kupigana. Risasi na mabomu vilianguka kuzunguka jumba, lakini halikuharibiwa. Mapigano yalipopungua, watu 72 walikusanyika kwenye jumba ili kuliweka wakfu kwa Yehova, Mungu wa amani.”
Tangu mwaka 1999, timu za ujenzi wa Majumba ya Ufalme zimejenga zaidi ya Majumba ya Ufalme mapya 65 kotekote nchini Myanmar. Wahubiri wenyeji walihisije? Mfano mmoja ni maneno ya dada mmoja mwenye shukrani, ambaye alisema hivi huku akitokwa na machozi ya furaha: “Sikuwahi kuwazia kwamba tutakuwa na jumba jipya zuri kama hili! Sasa nitajitahidi hata zaidi kuwakaribisha watu wanaopendezwa waje kwenye mikutano. Ninamshukuru Yehova na tengenezo lake kwa fadhili ambazo wametuonyesha!”
Wamishonari Wawasili
Katika miaka ya 1990, baada ya miaka mingi ya kujitenga na mataifa mengine, hatua kwa hatua nchi ya Myanmar ilianza kuruhusu watu kutoka mataifa mengine waingie katika nchi hiyo. Ofisi ya tawi ilitumia nafasi hiyo vizuri kwa kuomba ruhusa serikalini ili wamishonari waruhusiwe kuingia tena nchini Myanmar. Hatimaye, mnamo Januari 2003, wahitimu wa Gileadi, Hiroshi na Junko Aoki wakawasili kutoka Japani, wamishonari wa kwanza kuingia Myanmar baada ya karibu miaka 37.
Hiroshi na Junko Aoki, wamishonari wa kwanza kuingia Myanmar baada ya karibu miaka 37
“Kukiwa na wageni wachache nchini Myanmar, tulihitaji kuwa waangalifu ili wenye mamlaka wasiielewe vibaya kazi yetu ya kuhubiri,” anasema Hiroshi. “Hivyo tulianza kuandamana na ndugu na dada wenyeji kwenye ziara zao za kurudia na mafunzo ya Biblia. Mara moja tuligundua kwamba watu wa Myanmar wanapenda kuzungumza kuhusu mambo ya kiroho. Tulianzisha mafunzo matano ya Biblia katika asubuhi yetu ya kwanza utumishini!”
“Mara nyingi tuliona Yehova akiongoza mambo,” Junko anaongeza. “Pindi moja, tulipokuwa tunarudi kwa pikipiki kutoka kwenye funzo la Biblia karibu na Mandalay, tulipata pancha. Tukasukuma pikipiki hadi kwenye kiwanda kilichokuwa karibu na kuomba msaada wa kurekebisha gurudumu. Mlinzi akamruhusu Hiroshi aingie ndani na pikipiki, nami nikabaki kwenye kibanda cha mlinzi. Mlinzi alikuwa mdadisi.
“‘Mnafanya nini hapa?’ akauliza.
“‘Tunawatembelea rafiki zetu,’ nikamjibu.
“‘Kwa ajili ya nini?’akauliza. ‘Kwa ajili ya mambo ya kidini?’
“Bila kujua lengo lake, nikalipuuza swali lake.
“‘Sema tu ukweli!’ akasisitiza. ‘Unatoka katika dini gani?’
“Nikatoa gazeti la Mnara wa Mlinzi kutoka katika mkoba wangu na kumwonyesha.
“‘Nilijua tu!’ akapaza sauti kwa msisimko. Akiwageukia wafanyakazi wenzake, akawapazia sauti: ‘Oneni! Malaika amelitia pancha gurudumu ili Mashahidi wa Yehova watutembelee!’
“Mwanaume huyo akaingiza mkono kwenye mkoba wake na kutoa Biblia na moja ya trakti zetu. Alikuwa amejifunza na Mashahidi wa Yehova katika eneo lingine lakini alikuwa amepoteza mawasiliano nao alipokuwa amehamia Mandalay. Tukaanza kujifunza naye Biblia palepale. Baadaye, baadhi ya wafanyakazi wenzake walijifunza pia.”
Mnamo 2005, wamishonari wengine wanne walifika nchini Myanmar, wakati huu kutoka katika Shule ya Mazoezi ya Kihuduma (sasa inaitwa Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja) nchini Ufilipino. Mmoja wa ndugu hao, Nelson Junio, alikabili tatizo linalowapata wamishonari wengi, yaani, tamaa ya kurudi nyumbani. Anasema hivi: “Kabla ya kulala, mara nyingi nililia na kusali. Kisha ndugu mmoja mwenye fadhili alinionyesha andiko la Waebrania 11:15, 16. Andiko hilo linazungumza kuhusu jinsi ambavyo Abrahamu na Sara hawakuendelea kutamani makazi yao ya zamani kule Uru, lakini waliendelea kusonga mbele kama kusudi la Mungu lilivyokuwa. Baada ya kusoma andiko hilo, sikuendelea kulia tena. Nilianza kuona mahali nilipopewa mgawo ndio nyumbani.”
Mifano Mizuri Yawanufaisha Wengi
Katika karne ya kwanza, mtume Paulo alimshauri Timotheo hivi: “Mambo uliyoyasikia kutoka kwangu . . . uwakabidhi watu waaminifu, ambao nao watakuwa na sifa za kustahili vya kutosha kufundisha wengine.” (2 Tim. 2:2) Kwa kuzingatia kanuni hiyo, wamishonari walijitahidi kuwafundisha ndugu na dada katika makutaniko nchini Myanmar wafuate taratibu zinazofuatwa na watu wa Yehova ulimwenguni pote.
Kwa mfano, wamishonari waligundua kwamba wahubiri wengi wenyeji waliwafundisha wanafunzi wao wa Biblia warudie majibu kama yalivyoandikwa katika kitabu—mbinu inayotumiwa katika shule nyingi nchini Myanmar. “Kwa subira tuliwatia moyo wahubiri watumie maswali ya maoni ili wanafunzi waeleze yaliyo mioyoni mwao,” anasema Joemar Ubiña. “Wahubiri walitumia mashauri hayo bila kusita, na matokeo yake wakawa walimu wenye matokeo mazuri.”
Pia, wamishonari hao waligundua kwamba makutaniko mengi yalikuwa na mzee au mtumishi wa huduma mmoja tu. Baadhi ya ndugu hao waliowekwa rasmi, hata ingawa walikuwa waaminifu na wachapa kazi, waliwawekea ndugu na dada sheria nyingi ngumu. Bila shaka, tabia kama hiyo ilikuwepo pia katika karne ya kwanza, mtume Petro alipowahimiza wazee hivi: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya uangalizi wenu, si . . . kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali kuwa vielelezo kwa kundi.” (1 Pet. 5:2, 3) Wamishonari wangewasaidiaje ndugu zao? “Tulijitahidi kuwawekea mfano mzuri kwa kuwa wenye fadhili zaidi, wapole, na wenye kufikika,” anasema Benjamin Reyes. Baada ya muda fulani ndugu wenyeji walianza kuiga mfano wao mzuri. Wazee wengi walibadili njia yao ya kuwafikia akina ndugu na kuanza kutunza kondoo kwa huruma hata zaidi.
Tafsiri Bora Yaleta Manufaa
Kwa miaka mingi akina ndugu nchini Myanmar walitumia Biblia ya karne ya 19 iliyotafsiriwa na wamishonari wa dini zinazodai kuwa za Kikristo wakisaidiwa na watawa wa Kibudha. Tafsiri hiyo ina maneno ya lugha ya Kipali yaliyopitwa na wakati na ni vigumu kuielewa. Kwa hiyo, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ya lugha ya Kimyanmar ilipotolewa mwaka 2008, akina ndugu walijawa na shangwe. Maurice Raj anakumbuka hivi: “Wasikilizaji walipiga makofi kwa muda mrefu, na hata wengine walilia kwa furaha walipopokea nakala zao. Tafsiri hiyo mpya iko wazi, rahisi, na sahihi. Hata Wabudha wanaielewa kwa urahisi!” Mara tu baada ya tafsiri hiyo kutolewa, idadi ya mafunzo ya Biblia nchini Myanmar iliongezeka kwa zaidi ya asilimia 40.
Leo,miaka 50 hivi baadaye, bado Doris Raj anafanya kazi akiwamtafsiri katika Betheli ya Yangon
Kama zilivyo lugha nyingine, kuna aina mbili za lugha ya Kimyanmar—Kimyanmar rasmi kinachotokana na lugha ya Kipali na Kisanskrit, na Kimyanmar kisicho rasmi kile kinachotumiwa katika mawasiliano ya kila siku. Aina hizo zote mbili zinatumiwa kwa mazungumzo na kuandika. Mengi ya machapisho yetu ya zamani yalitumia lugha rasmi, ambayo idadi kubwa ya watu sasa huona vigumu kuyaelewa. Ikiwa na jambo hilo akilini, hivi karibuni ofisi ya tawi ilianza kutafsiri machapisho katika lugha ya kila siku ya Myanmar, ambayo karibu watu wengi wanaielewa.
Timu za tafsiri katika ofisi ya tawi ya Myanmar
Kumekuwa na matokeo mazuri na ya haraka kwa sababu ya machapisho hayo mapya. Than Htwe Oo, msimamizi wa Idara ya Tafsiri, anaeleza hivi: “Watu walizoea kusema, ‘Machapisho yenu ni ya hali ya juu, lakini siwezi kuyaelewa.’ Sasa wanafurahi sana wanapopokea machapisho yetu, na wanaanza kuyasoma mara moja. Wengi husema hivi: ‘Machapisho haya yanaeleweka kwa urahisi!’” Hata maelezo yanayotolewa katika mikutano yamekuwa bora, kwa kuwa sasa wasikilizaji wanaelewa vizuri kile ambacho kimeandikwa katika machapisho yetu.
Kwa sasa, Idara ya Tafsiri ina watafsiri wa kudumu 26 wanaotafsiri lugha tatu—Kimyanmar, Kihakha Chin, na Kisgaw Kayin. Pia, machapisho yetu yamekuwa yakitafsiriwa katika lugha nyingine 11 za kienyeji.
Kimbunga Nargis
Mnamo Mei 2, 2008, Kimbunga kinachoitwa Nargis, upepo mkali uliokuwa ukisafiri kilomita 240 kwa saa, kiliipiga nchi ya Myanmar, kikisababisha vifo vingi na uharibifu mkubwa kuanzia Delta ya Ayeyarwady hadi kwenye mpaka wa Thailand. Kimbunga hicho kiliwaathiri watu zaidi ya milioni mbili na kuwaacha wengine 140,000 ama wakiwa wamekufa au hawajulikani walipo.
Maelfu ya Mashahidi wa Yehova waliathiriwa na kimbunga hicho, hata hivyo kwa kushangaza hakuna yeyote aliyeumia. Wengi waliokoka kwa kukimbilia kwenye Majumba yao mapya ya Ufalme. Huko Bothingone, kijiji kilicho pwani katika Delta ya Ayeyarwady, Mashahidi 20 na wanakijiji wengine 80 walikaa juu kwenye kenchi za Jumba la Ufalme, maji ya mafuriko yalipokuwa yamejaa hadi karibu na dari hadi yalipopungua.
Timu ya kutoa msaada ikiwa imesimamana Ndugu na Dada Htun Khin mbele ya nyumba yao iliyojengwa upya baada ya kuharibiwa na Kimbunga Nargis
Mara moja ofisi ya tawi ilituma timu ya kutoa msaada katika maeneo yaliyoathiriwa zaidi kwenye mlango wa delta. Ikipita katika maeneo yaliyoharibika na kujaa maiti za watu, timu ya kutoa msaada ilifika kijijini ikiwa na chakula, maji, na dawa. Ilikuwa ndiyo timu ya kwanza ya kutoa msaada kufika katika eneo hilo. Baada ya kutoa msaada kwa ndugu na dada wenyeji, timu hiyo iliwatia moyo kwa hotuba za Kimaandiko na kuwapa Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia, kwa kuwa mali zao zote zilikuwa zimefagiliwa mbali na kimbunga.
Ili kusimamia kazi kubwa ya kutoa misaada, ofisi ya tawi iliunda Halmashauri za Kutoa Misaada huko Yan-gon na Pathein. Halmashauri hizo zilipanga mamia ya wajitoleaji ili kugawa maji, mchele, na mahitaji mengine muhimu kwa ajili ya watu walioathiriwa na kimbunga. Walipanga pia timu za ujenzi zilizoenda sehemu mbalimbali ili kujenga upya nyumba za Mashahidi zilizoharibiwa au kubomolewa na kimbunga.
Mmoja wa wajitoleaji hao, Tobias Lund, anasema hivi: “Mimi na mke wangu, Sofia, tulimkuta May Sin Oo, mhubiri pekee katika familia yake, mwenye umri wa miaka 16 akiwa anaanika juani Biblia yake kwenye nyumba yao iliyobomoka. Alitabasamu alipotuona, lakini alikuwa akitiririkwa na machozi. Muda si mrefu, timu yetu moja ya ujenzi ikafika ikiwa na kofia ngumu, vifaa vya umeme pamoja na vifaa vya ujenzi na kuanza kuijengea familia yake nyumba mpya. Majirani walishangaa! Kwa siku kadhaa watu walikaa kuzunguka eneo hilo la ujenzi ili kuitazama nyumba hiyo, nyumba iliyokuwa kivutio pekee katika eneo hilo. Watazamaji walisema hivi: ‘Hatujawahi kuona jambo lolote kama hili! Tengenezo lenu lina umoja na upendo. Sisi pia tungependa kuwa Mashahidi wa Yehova.’ Wazazi na wadogo za May Sin Oo sasa wanahudhuria mikutano, na familia nzima inafanya maendeleo mazuri ya kiroho.”
Kazi ya kutoa misaada iliendelea kwa miezi mingi. Akina ndugu waligawa tani nyingi za misaada na kukarabati au kujenga upya nyumba 160 na Majumba ya Ufalme 8. Kimbunga Nargis kilileta msiba na hali ngumu nchini Myanmar, lakini katika hali hiyo ngumu watu waliweza kuona jinsi upendo unavyowaunganisha watu wa Mungu na kulitukuza jina la Yehova.
Tukio Ambalo Halitasahaulika
Mapema mnamo 2007, ofisi ya tawi ya Myanmar ilipokea barua yenye kusisimua. “Baraza Linaloongoza lilituomba tuandae kusanyiko la kimataifa jijini Yangon,” anasema Jon Sharp, ambaye pamoja na mke wake, Janet, walikuwa wamewasili katika ofisi ya tawi mwaka mmoja kabla. “Kusanyiko la mwaka 2009 lingetia ndani mamia ya wajumbe wa kigeni kutoka nchi mbalimbali kumi—tukio la aina yake katika historia ya tawi letu!”
Jon anaendelea: “Tulijiuliza maswali mengi: ‘Ni ukumbi gani nchini Myanmar unaoweza kubeba watu wengi? Je, wahubiri kutoka maeneo ya mbali watahudhuria? Watakaa wapi? Watasafiri jinsi gani? Je, wataweza kulisha familia zao? Pia, vipi kuhusu wenye mamlaka nchini Myanmar? Je, wanaweza kuruhusu mkusanyiko kama huo?’ Ilionekana kulikuwa na vizuizi vingi. Hata hivyo, tulikumbuka maneno ya Yesu: ‘Mambo yasiyowezekana kwa wanadamu yanawezekana kwa Mungu.’ (Luka 18:27) Hivyo, tukiwa tumeweka tumaini letu kwa Mungu, tukaanza kufanya mipango kwa bidii.
“Mara moja tukapata ukumbi unaofaa—Uwanja wa Taifa wa Ndani wa Myanmar, wenye uwezo wa kubeba watu 11,000, uwanja huo una viyoyozi na uko karibu katikati ya jiji. Mara moja tukawaomba wenye mamlaka ili tuweze kutumia uwanja huo. Hata hivyo, miezi kadhaa baadaye na majuma machache tu kabla ya kusanyiko, ombi letu bado halikuwa limekubaliwa. Kisha tukapata habari zenye kuvunja moyo: Wasimamizi wa uwanja walikuwa wamekubali kuukodisha uwanja huo kwa waandaaji wa shindano la mchezo wa mateke na ngumi katika tarehe zilezile ambazo tungefanya kusanyiko letu! Tukiwa hatuna wakati wa kutosha kutafuta ukumbi mwingine, tulizungumza na mwandaaji wa shindano hilo na maofisa wengine kadhaa ili kutatua jambo hilo. Hatimaye, mwandaaji wa mchezo huo alikubali kwamba angeweza kusogeza mbele shindano hilo ikiwa tu wachezaji 16 wa kimataifa wa mchezo huo wangekubali kubadili mikataba yao. Wachezaji hao waliposikia kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wanataka kutumia uwanja huo kwa ajili ya kusanyiko la kimataifa, kila mmoja wao alikubali kubadilisha.”
Halmashauri ya Tawi, kuanzia kushoto kwenda kulia: Kyaw Win, Hla Aung, Jon Sharp, Donald Dewar, na Maurice Raj
Kyaw Win, mshiriki mwingine wa Halmashauri ya Tawi anasema: “Hata hivyo, bado tulihitaji kibali cha kuutumia uwanja huo kutoka serikalini, na tayari ombi letu lilikuwa limekataliwa mara nne! Baada ya kusali kwa Yehova, tulikutana na jenerali anayesimamia viwanja vyote nchini Myanmar. Majuma mawili tu kabla ya kusanyiko yalikuwa yamebaki na ilikuwa mara yetu ya kwanza kuzungumza na ofisa wa cheo cha juu kadiri hiyo katika serikali. Tulifurahi alipokubali ombi letu!”
Bila kujua kilichokuwa kikiendelea, maelfu ya wajumbe kutoka kotekote nchini Myanmar na nchi za nje walikuwa wakimiminika jijini Yangon kwa ndege, treni, boti, basi, malori, na kwa miguu. Familia nyingi nchini Myanmar zilihifadhi fedha kwa miezi mingi ili ziweze kuhudhuria. Ndugu wengi walilima mazao, wengine walifuga nguruwe, wengine walishona nguo, na wachache walijaribu kuchimba dhahabu. Wengi hawakuwa wamewahi kufika jijini au hata kumwona mgeni kutoka nchi za nje.
Zaidi ya wajumbe 1,300 kutoka kaskazini mwa Myanmar walikusanyika katika Kituo cha Reli cha Mandalay kwa ajili ya kupanda treni ya pekee iliyokodiwa ili kuwafikisha Yangon. Akina ndugu kutoka Naga Hills walisafiri kwa siku sita, wakiwabeba mgongoni wahubiri wawili ambao viti vyao vya magurudumu ambavyo walikuwa wamejitengenezea vilikuwa vimeharibika mapema katika safari yao. Mamia walipiga kambi kwenye jukwaa la kituo cha reli, wakiongea, wakicheka, na kuimba nyimbo za Ufalme. “Kila mmoja alikuwa amefurahi,” anasema Pum Cin Khai, ambaye alisaidia mipango ya usafiri. “Tuliwapa chakula, maji, na mikeka ya kulalia. Hatimaye treni ilipowasili, wazee waliongoza kila kikundi kwenye behewa walilopangiwa. Hatimaye, sauti ikasikika kwenye kikuza sauti ikitangaza: ‘Treni ya Mashahidi wa Yehova inaondoka!’ Nikahakikisha hakuna yeyote ambaye amebaki, kisha, nikadandia kwenye behewa!”
Wakati huohuo, jijini Yangon, karibu wajumbe 700 kutoka nchi za nje walikuwa wakiingia kwenye hoteli walizopangiwa. Hata hivyo, wajumbe wapatao 3,000 wa Myanmar wangeishi wapi? “Yehova alifungua mioyo ya Mashahidi wa Yehova jijini Yangon ili wawakaribishe ndugu na dada zao,” anasema Myint Lwin, ambaye alifanya kazi katika Idara ya Mahali pa Kulala. “Baadhi ya familia zilikaribisha hadi wageni 15. Familia hizo zilipa ada ya kuwaandikisha kwa wenye mamlaka na kuwaandalia wageni wao kiamsha kinywa na usafiri wa kwenda na kurudi kutoka uwanjani kila siku. Wajumbe wengi walikaa katika Majumba ya Ufalme; wengine wengi walilala kwenye kiwanda kikubwa. Hata hivyo, licha ya jitihada hizo kubwa, bado wajumbe wapatao 500 walihitaji mahali pa kulala. Tuliueleza uongozi wa uwanja huo tatizo letu, na wakawaruhusu wajumbe hao walale uwanjani—jambo ambalo hatukutegemea kabisa!”
Kwa kuwa uwanja ulikuwa katika hali mbaya, zaidi ya wajitoleaji 350 walifanya kazi kwa siku kumi ili kuutayarisha kwa ajili ya kusanyiko. “Tulikarabati mabomba, umeme, na mfumo wa viyoyozi. Kisha, tukapaka rangi na kusafisha uwanja mzima,” anasema Htay Win, mwangalizi wa kusanyiko. “Ushahidi mkubwa ulitolewa kwa sababu ya kazi hiyo kubwa iliyofanywa. Ofisa wa jeshi anayesimamia uwanja huo alisema hivi: ‘Asanteni! Asanteni! Ninasali kwa Mungu kwamba ninyi watu muutumie uwanja wangu kila mwaka!’”
Zaidi ya watu 5,000 walihudhuria kusanyiko lililofanywa Desemba 3-6, 2009. Katika siku ya mwisho, wajumbe wengi walivaa mavazi yao ya asili, na kufanya mandhari iwe yenye kuvutia kwelikweli. “Wote walikuwa wakikumbatiana na kulia—kabla hata ya programu kuanza!” anasema dada mmoja. Baada ya Gerrit Lösch wa Baraza Linaloongoza kutoa sala ya mwisho, wahudhuriaji walipiga makofi na kupunga mikono kwa dakika kadhaa. Wengi walihisi kama dada mmoja mwenye umri wa miaka 86 alivyohisi, ambaye alisema hivi,“Nilihisi kama niko katika ulimwengu mpya!”
Maofisa wengi wa serikali walivutiwa sana. Ofisa mmoja alisema hivi: “Kusanyiko hili ni la pekee. Hakuna anayetukana, kuvuta sigara, au kutafuna tambuu. Watu wa jamii mbalimbali wana umoja. Sijawahi kuona kikundi kama hiki!” Maurice Raj anasema hivi, “Hata kamanda wa jeshi mwenye cheo cha juu jijini Yangon alituambia kwamba yeye pamoja na wenzake hawajawahi kuona tukio lenye kuvutia kama hilo.”
Wajumbe wengi walikubali kwamba walikuwa wameshuhudia tukio fulani la pekee. Ndugu mmoja mwenyeji alisema hivi: “Kabla ya kusanyiko tulikuwa tukisikia tu kuhusu undugu wetu wa ulimwenguni pote. Sasa tumejionea wenyewe! Hatutasahau upendo ambao ndugu zetu wametuonyesha.”
“Meupe kwa Ajili ya Kuvunwa”
Karibu miaka 2,000 iliyopita, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Inueni macho yenu myatazame mashamba, kwamba ni meupe kwa ajili ya kuvunwa.” (Yoh. 4:35) Hivyo ndivyo inavyoweza kusemwa kuhusu Myanmar leo. Kwa wakati huu, nchi ina wahubiri 3,790, kadirio la mhubiri 1 kwa watu 15,931—kwa kweli, shamba kubwa kwa ajili ya kuvunwa! Kukiwa na watu 8,005 waliohudhuria Ukumbusho mwaka 2012, kuna matarajio ya kuwa na ongezeko kubwa!
Ili kuthibitisha hilo, fikiria Jimbo la Rakhine, lililo pwani linalopakana na nchi ya Bangladesh ambalo linawakazi karibu milioni nne lakini hakuna Shahidi wa Yehova hata mmoja. “Kila mwezi, tunapokea barua nyingi kutoka kwa watu katika eneo hilo wanaoomba machapisho na msaada wa kiroho,” anasema Maurice Raj. “Pia, idadi inayoongezeka ya Wabudha nchini Myanmar, hasa vijana, wanaonyesha kupendezwa na kweli. Hivyo, tunaendelea kumwomba Bwana atume wafanyakazi zaidi katika mavuno.”—Mt. 9:37, 38.
Karibu miaka 100 iliyopita, mapainia wawili jasiri walileta habari njema katika nchi hii yenye Wabudha wengi. Tangu wakati huo, maelfu ya watu kutoka katika makabila mbalimbali wameikubali kweli. Licha ya mapigano makali, misukosuko ya kisiasa, umaskini uliokithiri, kuteswa na dini, kujitenga na mataifa mengine, na majanga ya asili, Mashahidi wa Yehova nchini Myanmar wameonyesha imani isiyoyumbayumba kwa Yehova na Mwana wake, Yesu Kristo. Wanaendelea kuazimia kuhubiri habari njema ya Ufalme na “kuvumilia kikamili na kuwa wenye ustahimilivu pamoja na shangwe.”—Kol. 1:11.
a Zamani nchi ya Myanmar iliitwa Burma, jina linalotokana na kabila kubwa zaidi la Myanmar linaloitwa Bamar (Waburma). Mnamo 1989 nchi hiyo ilipewa jina jipya, Muungano wa Myanmar, ili kuwakilisha makabila mengine mengi yaliyo nchini humo. Tutatumia jina Burma katika matukio yaliyotokea kabla ya mwaka 1989 na jina Myanmar katika matukio yaliyotokea baada mwaka huo.
b Waingereza-Wahindi ni watu ambao wametokana na mchanganyiko wa mababu Wahindi na Waingereza. Chini ya utawala wa Waingereza, maelfu ya Wahindi walihamia Burma, ambayo wakati huo ilionwa kuwa sehemu ya “Uingereza India.”
c Bertram Marcelline ndiye aliyekuwa mtu wa kwanza kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova nchini Burma. Alikufa nchini Burma mwishoni mwa miaka ya 1960, akiwa mwaminifu hadi mwisho.
d Wakati huo, Kyats hizo zilikuwa sawa na dola 95 hivi za Marekani, kiasi kikubwa cha pesa.
e Ona Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1966 cha Kiingereza ukurasa wa 192.
f Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi.
g MEPS sasa inaweza kuunganisha zaidi ya lugha 600.
Kwa miaka 100 hivi, ndugu zetu nchini Myanmar wamekuwa na imani isiyoyumbayumba na uvumilivu
“Hakuna shaka, isipokuwa tu iwe unataka wengine wapate uzima wa milele kwa niaba yako”
Wenye mamlaka walipofika, machapisho yote yalikuwa yameondolewa
“Leo, miji iliyo kandokando ya reli, Namti, Hopin, Mohnyin,na Katha ina makutaniko makubwa”
‘Walikata mabehewa sita, lakini si mabehewa yetu!’
Sasa wanaume hawa wawili wameunganishwa katika vifungo vya upendo kwa msaada wa Neno la Mungu
“Nilifarijika sana kutokana na upendo nilioonyeshwa na akina ndugu”
“Yehova ni msaidizi wangu; sitaogopa. Mwanadamu anaweza kunitenda nini?”—Ebr. 13:6
Kwa zaidi ya miaka 20 iliyopita, idadi ya nakala za magazeti zilizochapishwa imeongezeka kwa zaidi ya asilimia 900!
Kufika Jumba jipya la Ufalme kwa boti
Tangu mwaka 1999, timu za ujenzi wa Majumba ya Ufalme zimejenga zaidi ya Majumba ya Ufalme 65 kotekote nchini Myanmar
Kusanyiko la Kimataifa la “Endeleeni Kukesha!” la mwaka 2009 liliimarisha imani ya akina ndugu na kutoa ushahidi mkubwa jijini Yangon
“Yehova alifungua mioyo ya Mashahidi wa Yehova jijini Yangon ili wawakaribishe ndugu na dada zao”
“Kabla ya kusanyiko tulikuwa tukisikia tu kuhusu undugu wetu wa ulimwenguni pote. Sasa tumejionea wenyewe!”
“Tunaendelea kumwomba Bwana atume wafanyakazi zaidi katika mavuno”