SURA YA KUMI NA TANO
“Siwezi Kunyamaza Kimya”
1. Kwa nini Yeremia na manabii wengine wa Yehova hawakunyamaza kimya?
“LISIKIE neno la Yehova.” Maneno hayo yalisikika katika barabara na viwanja vya Yerusalemu kuanzia mwaka wa 647 K.W.K. Naye nabii wa Mungu hakuchoka kuyasema. Hata jiji hilo lilipoharibiwa miaka 40 baadaye, aliyarudia maneno hayo. (Yer. 2:4; 42:15) Mungu Mweza-Yote aliwatuma manabii kuhakikisha kwamba Wayahudi wamepata nafasi ya kusikia shauri Lake na kutubu. Kama tulivyoona awali katika kitabu hiki, Yeremia alikuwa mmoja wa wasemaji wa pekee kati ya manabii hao wa Mungu. Alipokuwa akimpa mgawo wa kuwa nabii, Mungu alimwambia Yeremia: “Unapaswa . . . kusimama na kuwaambia kila jambo ambalo mimi ninakuamuru. Usiwe na hofu yoyote.” (Yer. 1:17) Hiyo ilikuwa kazi ngumu. Yeremia aliumia kimwili na kihisia, lakini licha ya hali hizo ngumu, alichochewa kuutimiza mgawo wake. Alisema: “Moyo wangu umechafuka ndani yangu. Siwezi kunyamaza kimya.”—Yer. 4:19.
2, 3. (a) Wanafunzi wa Yesu walimwiga Yeremia jinsi gani? (b) Kwa nini ufuate mfano wa Yeremia?
2 Njia ambayo Yeremia aliutimiza mgawo wake wa kutoa unabii iliwawekea mfano mzuri watumishi wa Yehova wa baadaye. (Yak. 5:10) Muda mfupi baada ya Pentekoste ya 33 W.K., Wayahudi wenye mamlaka walimkamata mtume Petro na Yohana, wakawaamuru waache kuhubiri. Bila shaka unajua jinsi walivyojibu. “Hatuwezi kuacha kusema juu ya mambo ambayo tumeyaona na kuyasikia.” (Mdo. 4:19, 20) Baada ya kuwatisha kwamba watawatendea vibaya zaidi wakati ujao, watawala hao wakawaachilia Petro na Yohana waende zao. Ikawaje? Wanaume hao waaminifu hawangeweza kuacha wala hawakuacha kuhubiri.
3 Je, unaona jinsi maneno ya Petro na Yohana yaliyo katika Matendo 4:20 yanavyolingana na azimio la Yeremia? Ukiwa mhudumu wa Yehova Mungu katika hizi siku za mwisho, bila shaka wewe pia umeazimia na kusema, “siwezi kunyamaza kimya!” Acheni tuone jinsi tunavyoweza kuwa na nguvu kama za Yeremia za kuendelea kuhubiri habari njema hata hali zinapozidi kuwa mbaya.
ENDELEA HATA IKIWA WATU HAWAPENDEZWI
4. Watu wengi walikuwa na maoni gani katika Yerusalemu la kale?
4 Je, huamini kwamba ahadi ya Mungu kuhusu wakati ujao ulio bora chini ya utawala wa Mwana wake ndiyo habari njema zaidi ambayo watu wanastahili kusikia? Hata hivyo, wengi leo wana maoni kama ya baadhi ya Wayahudi waliomwambia Yeremia: “Kuhusu lile neno ambalo umetuambia katika jina la Yehova, sisi hatutakusikiliza.” (Yer. 29:19; 44:16) Yeremia alisikia maneno kama hayo mara nyingi. Na ndivyo na watumishi wa Yehova leo, kwa kuwa watu wengi husema, “Sitaki.” Kutopendezwa kwa watu wengi kunaweza kuwavunja moyo wahubiri wa Ufalme. Ikiwa wengine katika kutaniko lenu, au hata wewe mwenyewe, mmekumbana na hali kama hizo katika eneo lenu, ni nini kinachoweza kufanywa?
5. (a) Yeremia alifanya nini watu walipoukataa ujumbe wake? (b) Kwa nini wale wanaokataa habari njema wako hatarini?
5 Fikiria mtazamo ambao Yeremia alisitawisha mbele ya watu wengi wa Yuda ambao hawakutaka kuusikiliza ujumbe wake. Mapema katika mgawo wake, Yehova alikuwa amemwonyesha jinsi hukumu inayokuja itakavyokuwa. (Soma Yeremia 4:23-26.) Hivyo nabii huyo angeweza kuona kwamba maisha ya maelfu ya watu yalitegemea kusikia maneno aliyokuwa akiwaambia na kutenda kulingana nayo. Leo, watu wako katika hali hiyohiyo, kutia ndani watu walio katika eneo lenu. Kuhusu “siku hiyo” ya hukumu ya Mungu dhidi ya watu waovu wa ulimwengu huu, Yesu alisema: “Itakuja juu ya wale wote wanaokaa juu ya uso wa dunia yote. Basi, endeleeni kukesha wakati wote mkiomba dua ili mpate kufanikiwa kuponyoka mambo yote hayo yaliyokusudiwa kutukia, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu.” (Luka 21:34-36) Basi ni wazi kutokana na maneno hayo ya Yesu kwamba wale wanaokataa habari njema wamo hatarini.
6. Kwa nini uendelee kuwahubiria hata wale wasiopendezwa na ujumbe wetu?
6 Hata hivyo, wale wanaosikiliza na kukubali neno la Yehova tunalowahubiria watapata baraka nyingi. Mungu anatufungulia njia ya kuokoka uharibifu na kuingia katika ulimwengu wake mpya. Kwa njia fulani, ndivyo ilivyokuwa wakati wa huduma ya Yeremia. Wakaaji wa Yuda wangeweza kuokoka. (Soma Yeremia 26:2, 3.) Ili kuwasaidia, Yeremia aliwasihi kwa miaka mingi ‘wasikilize na kurudi,’ yaani, walitii neno la Mungu wa kweli. Hatujui ni wangapi waliotubu na kubadili maisha yao baada ya kusikiliza ujumbe wake. Lakini baadhi yao walifanya hivyo na ndivyo ilivyo leo pia. Tunapoendelea kuhubiri habari njema, mara nyingi tunasikia jinsi mioyo ya watu ambao wakati fulani hawakupendezwa inavyobadilika. (Ona sanduku “Mtu Asiyependezwa Anaweza Kubadilika,” katika ukurasa wa 184.) Je, hilo halituchochei kuendelea kuwa na bidii katika huduma yetu yenye kuokoa uhai ya kutangaza habari njema?
Kwa nini umeazimia kuhubiri habari njema hata ikiwa wengi hawapendezwi?
WAPINZANI HAWAWEZI KUTUUMIZA MILELE
7. Adui walijaribu jinsi gani kukomesha kazi ya Yeremia ya kutoa unabii?
7 Mara nyingi Yeremia alipokuwa katika huduma yake, wapinzani walijaribu kumwangamiza na kukomesha kazi yake. Manabii wa uwongo walimpinga hadharani. (Yer. 14:13-16) Yeremia alipokuwa akitembea katika barabara za Yerusalemu, watu walimtusi na kumdhihaki. (Yer. 15:10) Baadhi ya adui zake walitafuta njia nyingine za kumwaibisha. (Yer. 18:18) Wengine walieneza porojo za kumvunjia heshima ili kuwageuza watu wanyoofu kutoka katika kweli za Mungu ambazo Yeremia alikuwa akihubiri. (Omb. 3:61, 62) Je, Yeremia alikufa moyo? Hapana, badala yake aliendelea kuhubiri. Alifanya hivyo jinsi gani?
8. Yeremia alifanya nini wapinzani walipozidisha jitihada zao dhidi yake?
8 Silaha kuu ya Yeremia ya kushindana na upinzani wote huo ilikuwa kumtegemea Yehova. Mwanzoni mwa huduma ya Yeremia, Mungu alimwambia kwamba atamtegemeza na kumlinda. (Soma Yeremia 1:18, 19.) Yeremia aliamini ahadi hiyo, na Yehova hakumwacha kamwe. Kadiri wapinzani walivyozidi kumshinikiza na kuchukua hatua kali zaidi, ndivyo alivyoendelea kuwa na ujasiri, uhodari, na uvumilivu. Sifa hizo zilimfaa sana.
9, 10. Ni matukio gani katika maisha ya Yeremia yanayopaswa kukuchochea kuwa na ujasiri?
9 Pindi moja, makuhani na manabii waasi walimfikisha Yeremia mbele ya wakuu wa Yuda ili auawe. Je, vitisho vyao vilimtia hofu na kumfanya Yeremia ajikunyate? Hapana. Jibu lake lilikanusha kabisa madai ya uwongo ya waasi-imani hao hivi kwamba wakuu hawakumuua.—Soma Yeremia 26:11-16; Luka 21:12-15.
10 Kumbuka kwamba baada ya kuusikiliza ujumbe wenye nguvu wa Yeremia, Pashuri, ofisa wa hekalu, alimtia katika mikatale. Lazima Pashuri alifikiri kwamba kwa kufanya hivyo angemnyamazisha Yeremia na kumfundisha somo. Kwa hiyo, siku iliyofuata, Pashuri akamwachilia. Hata hivyo, Yeremia akiwa na maumivu makali kwa sababu kufungiwa kwenye mkatale, alizungumza moja kwa moja na Pashuri, akitangaza hukumu ya Yehova juu yake. Hata mateso hayakumnyamazisha Yeremia! (Yer. 20:1-6) Kwa nini? Yeremia mwenyewe anatuambia: “Yehova alikuwa pamoja nami kama mwenye nguvu anayetisha. Ndiyo sababu wale wanaonitesa watajikwaa nao hawatashinda.” (Yer. 20:11) Hata alipokabiliana na wapinzani wakali, Yeremia hakuogopa. Alimtegemea Yehova kabisa, nawe pia unaweza kufanya hivyo.
11, 12. (a) Ni kwa njia gani Yeremia alitumia akili Hanania alipompinga? (b) Tunaweza kupata faida gani tukiendelea “kujizuia chini ya uovu”?
11 Ni vizuri kukumbuka kwamba Yeremia hakuwa kama watu waliolewa kasumba ya kidini. Alitumia busara alipowakabili wapinzani. Alijua wakati wa kuondoka. Kwa mfano, fikiria alipokutana na Hanania. Baada ya nabii huyo wa uwongo kupinga hadharani neno la Mungu la kinabii, Yeremia alimrekebisha na kueleza jinsi ya kutambua nabii wa kweli. Yeremia alikuwa amebeba nira ili kuonyesha jinsi wangekuja kuwa chini ya nira ya Babiloni; Hanania aliivunja kijeuri. Hakuna aliyejua Hanania angefanya nini baada ya hapo! Kwa hiyo, Yeremia alifanya nini? Tunasoma: “Nabii akaenda zake.” Ndiyo Yeremia aliondoka mahali hapo. Baadaye, kwa mwelekezo wa Yehova, alirudi na kumwambia Hanania kile ambacho Mungu angefanya. Mfalme wa Babiloni angewateka Wayahudi naye Hanania angekufa.—Yer. 28:1-17.
12 Ni wazi kutokana na masimulizi haya yaliyoongozwa kwa roho kwamba tunapohubiri, mbali na kuwa na ujasiri, tunapaswa pia kutenda kwa busara. Katika nyumba moja tukimpata mtu anayekataa ujumbe wa Kimaandiko na hata kuwaka kwa hasira, huenda hata anatutisha kwa jeuri, tunaweza kumwacha kwa heshima na kwenda nyumba nyingine. Hakuna haja ya kubishana na yeyote kuhusu habari njema ya Ufalme. Tukiendelea “kujizuia chini ya uovu,” tunamwacha mwenye nyumba katika hali ambayo ikiwezekana, tunaweza kumsaidia wakati unaomfaa zaidi.—Soma 2 Timotheo 2:23-25; Met. 17:14.
Kwa nini ni muhimu kumtegemea Yehova tunapohubiri habari njema? kwa nini mbali na ujasiri tunahitaji pia busara?
“USIOGOPE”
13. Kwa nini Yehova alimwambia Yeremia: “Usiogope,” nasi kwa nini tunapaswa kuzingatia hilo?
13 Waabudu wa kweli waliathiriwa na hali mbaya zilizokuwapo kabla ya uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. Kwa hiyo unaweza kuelewa ni kwa nini Mungu alimwambia Yeremia: “Usiogope.” (Yer. 1:8; Omb. 3:57) Na Yehova alimwagiza awaambie watu wake maneno hayo yenye kutia moyo. (Soma Yeremia 46:27.) Tunajifunza nini kutokana na hilo? Huenda mara kwa mara tukahisi woga katika siku hizi za mwisho zenye hatari. Wakati kama huo, je, tutamsikiliza Yehova, anayetuambia: ‘Msiogope’? Awali katika kitabu hiki, tulizungumzia jinsi Mungu alivyomtegemeza Yeremia wakati huo wenye kuogopesha kwelikweli. Acheni tuzungumzie kidogo mambo yaliyotokea, ili tujifunze jambo fulani kutokana nayo.
14, 15. (a) Yeremia alijikuta katika hali gani hatari? (b) Yehova alitimiza jinsi gani ahadi yake ya kumlinda Yeremia?
14 Wababiloni walipozidi kuwakandamiza Wayahudi huko Yerusalemu, njaa ilizidi. Punde si punde wengi wakawa hawana chakula. (Yer. 37:21) Mbali na njaa, Yeremia alikuwa mahali ambapo angeweza kufa. Wakuu wa Yuda walikuwa wamemshinikiza Mfalme Sedekia afanye walivyotaka. Kisha wakamtupa Yeremia ndani ya tangi lenye kina kirefu. Halikuwa na maji ila matope mengi. Yeremia alipoanza kuzama, hangeweza kujiokoa. Kama wewe ungekuwa katika hali hiyo, je, hungeogopa?—Yer. 38:4-6.
15 Ingawa alikuwa mwanadamu kama sisi, Yeremia aliamini kabisa ahadi ya Yehova ya kwamba hatamwacha kamwe. (Soma Yeremia 15:20, 21.) Je, Yehova alimthawabisha kwa sababu ya imani yake? Bila shaka. Mungu alimchochea Ebed-meleki kutenda kinyume cha wakuu hao na kumwokoa Yeremia. Kwa ruhusa ya mfalme, alimvuta Yeremia kutoka ndani ya tangi hilo, akamwokoa asifie humo katika tangi hilo lenye matope.—Yer. 38:7-13.
16. Yehova aliwakomboa washikamanifu wake kutoka katika hatari gani?
16 Hata baada ya kutoka ndani ya tangi hilo, bado Yeremia alikuwa hatarini. Alipokuwa akimsihi mfalme kwa niaba ya Yeremia, Ebed-meleki alikuwa amemwambia mfalme: “Atakufa hapo alipo kwa sababu ya njaa. Kwa maana hakuna mkate tena jijini.” (Yer. 38:9) Kwa sababu ya uhaba wa chakula jijini Yerusalemu, watu walianza kula wanadamu wenzao. Hata hivyo, kwa mara nyingine tena Yehova aliingilia kati ili kumwokoa nabii wake. Naye Yeremia akamhakikishia Ebed-meleki kwamba Yehova atamlinda. (Yer. 39:16-18) Yeremia hakusahau ahadi hii ya Mungu: “Niko pamoja nawe ili kukukomboa.” (Yer. 1:8) Wanaume hao wawili washikamanifu wakiwa chini ya ulinzi wa Mungu Mweza-Yote, hawangeweza kuangamizwa na wanadamu wala njaa. Waliponyoka kifo katika jiji hilo lililokuwa limehukumiwa maangamizi. Tunajifunza nini? Yehova aliahidi kuwalinda naye alitimiza ahadi yake.—Yer. 40:1-4.
17. Kwa nini unapaswa kuwa na imani katika ahadi ya Yehova ya kuwalinda watumishi wake?
17 Kutimizwa kwa unabii wa Yesu kuhusu umalizio wa mfumo wa mambo unasonga kasi kuelekea upeo wake. Hivi karibuni kutakuwa na “ishara katika jua na mwezi na nyota, na juu ya dunia maumivu makali ya mataifa, bila kujua njia ya kutokea . . . huku watu wakizimia kwa woga na tarajio la mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa.” (Luka 21:25, 26) Tunangoja kuona ishara hizo zitakuwa ishara za aina gani na hofu ambayo zitasababisha. Hata hivyo, haidhuru kitakachotokea, hatupaswi kamwe kutilia shaka uwezo na utayari wa Yehova wa kuwaokoa watu wake. Lakini mambo yatakuwa tofauti kabisa kwa wale ambao hawana kibali chake. (Soma Yeremia 8:20; 14:9.) Hata watumishi wake wakionekana kuwa hoi kabisa, kana kwamba wako chini kabisa katika tangi lenye giza, anaweza kuwakomboa! Watu wake wataona utimizo wa maneno ambayo Mungu alimwambia Ebed-meleki: “‘Bila shaka nitakuokoa, nawe hutaanguka kwa upanga; na hakika nafsi yako itakuwa kama nyara kwako, kwa sababu umenitegemea mimi,’ asema Yehova.”—Yer. 39:18.
MANENO YALIYOANDIKIWA KWA AJILI YAKO
18. (a) Ni maneno gani yaliyobadili maisha ya Yeremia? (b) Amri ya Mungu katika andiko la Yeremia 1:7 ina maana gani kwako?
18 “Kwa wale wote nitakaokutuma kwao, unapaswa kwenda; na kila jambo nitakalokuamuru, unapaswa kusema.” (Yer. 1:7) Maisha ya Yeremia yalibadilika kabisa aliposikia amri hiyo kutoka kwa Mungu. Kuanzia wakati huo na kuendelea, hangaiko lake kuu lilikuwa kutangaza “neno la Yehova.” Maneno hayo yanarudiwa tena na tena katika kitabu cha Yeremia. Katika sura ya mwisho, Yeremia anasimulia kuhusu kutekwa kwa Yerusalemu na kupelekwa uhamishoni kwa Sedekia, mfalme wa mwisho. Ndiyo, Yeremia aliendelea kuwafundisha na kuwahimiza watu wa Yuda wamtii Yehova mpaka itakapoonekana wazi kwamba kazi yake imekamilika.
19, 20. (a) Kwa nini utumishi wa Yeremia ni kielelezo kwetu? (b) Kuna uhusiano gani kati ya kuhubiri habari njema kwa bidii na kupata shangwe na uradhi? (c) Kuchunguza kitabu cha Yeremia na cha Maombolezo kumekuwa na matokeo gani kwako?
19 Kuna ulinganifu mwingi kati ya mgawo wa Yeremia na huduma ya Mashahidi wa Yehova leo. Kama Yeremia, tunamtumikia Mungu wa kweli katika wakati wa hukumu. Majukumu mengine yanahitaji wakati na nguvu zako; hata hivyo, kuhubiri habari njema ndiyo kazi muhimu zaidi unayoweza kufanya katika mfumo huu wa mambo. Kupitia habari njema, unalitukuza jina kuu la Mungu na kukubali haki yake ya kutawala na mamlaka yake akiwa Mwenye Enzi Kuu. (Soma Maombolezo 5:19.) Pia, unaonyesha upendo kwa jirani kwa kuwasaidia wengine wamjue Mungu wa kweli na matakwa yake.—Yer. 25:3-6.
20 Yeremia alisema hivi kuhusu kazi ambayo Yehova alimpa afanye: “Neno lako linakuwa kwangu furaha na kushangilia kwa moyo wangu; kwa maana jina lako limeitwa juu yangu, Ee Yehova Mungu wa majeshi.” (Yer. 15:16) Wote ambao mioyo yao inawachochea kuzungumza kwa niaba ya Mungu watapata shangwe na uradhi wakati ujao. Hivyo basi, una sababu nzuri ya kuendelea kutangaza ujumbe wa Yehova, kama Yeremia alivyofanya.
Mfano wa Yeremia na Ebed-meleki unaweza kukusaidia jinsi gani kuwa na ujasiri? Ni sifa gani ya Yeremia ungependa kuiga unapohubiri?