Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kweli za Biblia Zilifunuliwaje Tena?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 3

      Kweli za Biblia Zilifunuliwaje Tena?

      Wanaume wakijifunza Biblia katika miaka ya 1870

      Wanafunzi wa Biblia wa miaka ya 1870

      Mwanamume akisoma nakala ya kwanza ya gazeti Mnara wa Mlinzi

      Toleo la kwanza la Mnara wa Mlinzi, 1879

      Mwanamke ameshika magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!

      Mnara wa Mlinzi la wakati huu

      Biblia ilitabiri kwamba baada ya kifo cha Kristo, walimu wa uwongo wangetokea miongoni mwa Wakristo wa mapema na kupotosha kweli za Biblia. (Matendo 20:29, 30) Baada ya muda, jambo hilo lilitukia. Walimu hao walichanganya mafundisho ya Yesu na mafundisho ya dini za kipagani, na hivyo Ukristo bandia ukatokea. (2 Timotheo 4:3, 4) Tunawezaje kuwa na uhakika kwamba leo tunaelewa kwa usahihi yale ambayo Biblia inafundisha hasa?

      Wakati ulifika wa Yehova kufunua ukweli. Alitabiri kwamba ‘wakati wa mwisho ujuzi wa kweli ungekuwa mwingi.’ (Danieli 12:4) Mnamo 1870, kikundi kidogo cha watu waliokuwa wakitafuta ukweli kilitambua kwamba mafundisho mengi ya kidini hayakupatana na Maandiko. Kwa hiyo, walianza kufanya utafiti ili kuelewa mafundisho ya kweli ya Biblia, na Yehova akawasaidia kuelewa Maandiko.

      Watu wanyoofu waliichunguza Biblia kwa makini. Wanafunzi hao wa Biblia waliotutangulia, walitumia njia ya kujifunza ambayo bado tunaitumia leo. Walizungumzia Biblia kwa kuchunguza jambo moja baada ya lingine. Waliposoma sehemu ya Biblia ambayo haikueleweka kwa urahisi, walichunguza maandiko mengine ili kuielewa. Walipofikia uamuzi uliopatana na Maandiko yote, waliandika jambo hilo. Kwa kuacha Biblia ijieleze yenyewe walifanikiwa kufunua tena ukweli kuhusu jina la Mungu na Ufalme wake, kusudi lake kuelekea wanadamu na dunia, hali ya wafu, na tumaini la ufufuo. Uchunguzi wao uliwaweka huru kutokana na mafundisho na desturi nyingi za uwongo.—Yohana 8:31, 32.

      Kufikia mwaka wa 1879 Wanafunzi wa Biblia walitambua kwamba wakati ulikuwa umefika wa kutangaza kweli za Biblia kotekote. Basi, mwaka huo wakaanza kuchapisha gazeti la Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova, ambalo bado tunaendelea kulichapisha. Leo, tunawatangazia watu ujumbe wa kweli za Biblia katika nchi 240, tukitumia lugha 750 hivi. Leo, ujuzi wa kweli ni mwingi kuliko wakati mwingine wowote!

      • Ni nini kilichotokea kuhusiana na kweli za Biblia baada ya kifo cha Kristo?

      • Ni nini ambacho kimetusaidia kufunua tena ukweli ulio katika Neno la Mungu?

  • Kwa Nini Tumechapisha Tafsiri ya Ulimwengu Mpya?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 4

      Kwa Nini Tumechapisha Tafsiri ya Ulimwengu Mpya?

      Mashine ya zamani ya uchapishaji
      Toleo la kwanza la Biblia Takatifu Tafsiri ya Ulimwengu Mpya likitolewa
      Watu nchini Kongo (Kinshasa) wakiangalia Biblia Takatifu Tafsiri ya Ulimwengu Mpya

      Kongo (Kinshasa)

      Biblia Takatifu Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ikitolewa nchini Rwanda

      Rwanda

      Kisehemu cha nakala ya tafsiri ya Symmachus kilicho na jina la Mungu

      Kisehemu cha tafsiri ya Kigiriki ya Symmachus cha karne ya tatu au ya nne kilicho na jina la Mungu kwenye Zaburi 69:31

      Kwa miaka mingi, Mashahidi wa Yehova walitumia, wakachapisha, na kusambaza tafsiri mbalimbali za Biblia. Lakini tukaona uhitaji wa kuchapisha tafsiri mpya ya Biblia ambayo ingewasaidia zaidi watu wajifunze “ujuzi sahihi wa kweli,” na hayo ndiyo mapenzi ya Mungu kwa kila mtu. (1 Timotheo 2:3, 4) Hivyo, mwaka wa 1950 tukaanza hatua kwa hatua kuchapisha Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inayotumia lugha ya kisasa. Biblia hii imetafsiriwa kwa uaminifu na kwa usahihi katika lugha zaidi ya 130.

      Biblia inayoeleweka kwa urahisi ilihitajiwa. Lugha hubadilika baada ya muda, na tafsiri nyingi za Biblia zina maneno ambayo hayatumiki tena au hayaeleweki kwa urahisi. Pia, maandishi ya kale ambayo ni sahihi zaidi na ambayo yaliandikwa muda mfupi baada ya nakala za kwanza kuandikwa yamepatikana na hivyo kufanya iwezekane kuelewa vizuri zaidi Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki kilichotumiwa kuandika Biblia.

      Tafsiri ambayo haipotoshi neno la Mungu ilihitajiwa. Badala ya kubadili maandishi yaliyoongozwa na roho ya Mungu, watafsiri wa Biblia wanapaswa kutafsiri maandishi ya awali kwa uaminifu. Hata hivyo, katika tafsiri nyingi, jina la Mungu, Yehova, halipatikani katika Maandiko Matakatifu.

      Biblia ambayo inamheshimu Mtungaji wake ilihitajiwa. (2 Samweli 23:2) Katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, jina la Yehova limerudishwa kila mahali ambapo jina hilo linapatikana mara 7,000 hivi katika maandishi ya zamani zaidi ya Biblia, kama inavyoonyeshwa katika picha iliyo hapa chini. (Zaburi 83:18) Kwa sababu ya utafiti uliofanywa kwa makini kwa miaka mingi, utafurahia kuisoma Biblia hii, kwa kuwa inaeleza mawazo ya Mungu waziwazi. Iwe una Tafsiri ya Ulimwengu Mpya katika lugha yako au la, tunakutia moyo uwe na mazoea ya kusoma Neno la Yehova kila siku.—Yoshua 1:8; Zaburi 1:2, 3.

      • Kwa nini tuliamua kwamba tafsiri mpya ya Biblia inahitajiwa?

      • Kila mtu anayetaka kujifunza mapenzi ya Mungu anapaswa kuwa na mazoea ya kufanya nini kila siku?

      PATA KUJUA MENGI ZAIDI

      Soma utangulizi wa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, na ujibu swali hili: “Wachapishaji wa Biblia hii walikuwa na wajibu gani?” Kisha linganisha walivyotafsiri mistari ifuatayo na jinsi mistari hiyo ilivyotafsiriwa katika Biblia nyingine ambazo huenda ukawa nazo: Mwanzo 25:29; Isaya 14:23; Mathayo 5:3; 11:12; 1 Wakorintho 10:24, 25; Wafilipi 1:8.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki