Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kwa Nini Tunavalia Vizuri Tunapohudhuria Mikutano?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 8

      Kwa Nini Tunavalia Vizuri Tunapohudhuria Mikutano?

      Baba na mvulana wakivaa kwa ajili ya kuhudhuria mkutano

      Iceland

      Mama na binti wakijitayarisha kuhudhuria mkutano

      Mexico

      Mashahidi wa Yehova wamevaa nguo nadhifu nchini Guinea-Bissau

      Guinea-Bissau

      Familia ikienda kwenye mkutano nchini Filipino

      Filipino

      Katika picha za broshua hii, je, umeona jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyovalia vizuri wanapohudhuria mikutano? Kwa nini tunachukua kwa uzito jinsi tunavyovalia na kujipamba?

      Ili kuonyesha kwamba tunamheshimu Mungu wetu. Ni kweli kwamba Mungu hakazii fikira jinsi tulivyo kwa nje. (1 Samweli 16:7) Hata hivyo, tunapokutanika pamoja, tamaa yetu kuu ni kumwonyesha Mungu heshima na pia waabudu wenzetu. Ikiwa ungemtembelea mfalme au rais, bila shaka ungevalia kwa heshima kwa sababu ya cheo chake. Vivyo hivyo, tunapovalia vizuri katika mikutano, tunamheshimu “Mfalme wa mataifa,” Yehova Mungu, na pia mahali tunapomwabudia.—Yeremia 10:7.

      Ili kuonyesha viwango tunavyofuata maishani. Biblia inawatia moyo Wakristo wavalie kwa “kiasi na utimamu wa akili.” (1 Timotheo 2:9, 10) Kuvalia kwa “kiasi” kunamaanisha kuepuka mavazi ambayo yanaweza kuwafanya watu watukazie fikira kama vile mavazi ya kujionyesha, yanayoamsha tamaa mbaya, au yanayoonyesha uchi. Pia, kuwa na “utimamu wa akili” kunatusaidia kuchagua mavazi yenye kupendeza ambayo si ya kizembe au yanayopita kiasi. Kanuni hizi hazitubani, bado tuna uhuru wa kuchagua mavazi yanayotupendeza. Tunapovalia vizuri, ‘tunalipamba fundisho la Mwokozi wetu,’ na ‘kumtukuza Mungu.’ (Tito 2:10; 1 Petro 2:12) Hivyo, wengine wanaiheshimu ibada ya Yehova.

      Si lazima mtu avae mavazi rasmi ili ahudhurie mikutano katika Jumba la Ufalme. Mavazi ya kawaida yanaweza kuwa safi, nadhifu, na yenye kufaa.

      • Kwa nini ni muhimu kuvalia vizuri tunapomwabudu Mungu?

      • Ni kanuni gani zinazotuongoza tunapochagua jinsi tunavyovalia na kujipamba?

  • Ni Njia Gani Bora ya Kujitayarisha kwa Ajili ya Mikutano?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 9

      Ni Njia Gani Bora ya Kujitayarisha kwa Ajili ya Mikutano?

      Shahidi wa Yehova akitayarisha habari atakazojifunza mkutanoni

      Kambodia

      Shahidi wa Yehova akitayarisha habari atakazojifunza mkutanoni
      Shahidi wa Yehova akitayarisha habari atakazojifunza mkutanoni

      Ukrainia

      Ikiwa unajifunza Biblia na Shahidi wa Yehova, huenda wewe husoma mapema habari ambazo mtajifunza. Ili ufaidike na mikutano pia, ni vizuri ufanye vivyo hivyo kabla ya kuhudhuria. Ukiwa na ratiba nzuri, utafanikiwa.

      Amua wakati na mahali pa kujifunzia. Ni wakati gani unapoweza kukaza fikira? Je, ni asubuhi na mapema kabla ya kuanza kazi za kila siku au ni usiku baada ya watoto kulala? Hata ikiwa huwezi kujifunza kwa muda mrefu, amua wakati unaoweza kutenga kwa ajili ya kujifunza, nawe usiruhusu chochote kivuruge ratiba yako. Tafuta mahali patulivu, na uepuke vitu vinavyokengeusha fikira kwa kuzima redio, televisheni, na hata simu ya mkononi. Kusali kabla ya kujifunza kutakusaidia upunguze mahangaiko ili uweze kukazia fikira Neno la Mungu.—Wafilipi 4:6, 7.

      Tia alama mambo makuu, na ujitayarishe kushiriki katika mikutano. Kwanza, jaribu kuelewa wazo kuu la habari unayojifunza. Fikiria kichwa kikuu cha makala au sura hiyo, chunguza jinsi kila kichwa kidogo kinavyohusiana na kichwa kikuu, na uchunguze picha na maswali yanayokazia mambo makuu. Kisha, usome kila fungu, na utafute majibu ya maswali yaliyochapishwa. Fungua na usome maandiko ambayo yametajwa, na ufikirie jinsi yanavyounga mkono kichwa kikuu. (Matendo 17:11) Unapopata majibu ya maswali, tia alama au upige mstari chini ya maneno makuu machache yatakayokusaidia kukumbuka majibu. Kwenye mikutano, unaweza kuinua mkono na kutoa maelezo mafupi ukitumia maneno yako mwenyewe.

      Ukichanganua habari tofauti-tofauti ambazo zinazungumziwa kila juma katika mikutano, utaongeza “hazina” yako ya ujuzi wa Biblia.—Mathayo 13:51, 52.

      • Ni maamuzi gani unayohitaji kufanya ili kuwa na ratiba nzuri ya kujitayarisha kwa ajili ya mikutano?

      • Unaweza kujitayarishaje ili uweze kutoa maelezo katika mikutano?

      PATA KUJUA MENGI ZAIDI

      Kwa kutumia mapendekezo yaliyotajwa hapa, jitayarishe kwa ajili ya Funzo la Mnara wa Mlinzi au Funzo la Biblia la Kutaniko. Ukisaidiwa na yule anayejifunza Biblia pamoja nawe, tayarisha maelezo mafupi unayoweza kutoa katika mkutano unaofuata.

  • Ibada ya Familia Ni Nini?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 10

      Ibada ya Familia Ni Nini?

      Familia ikifurahia ibada ya familia

      Korea Kusini

      Wenzi wa ndoa wakijifunza Biblia

      Brazili

      Shahidi wa Yehova akijifunza Biblia

      Australia

      Familia ikijadili habari fulani katika Biblia

      Guinea

      Tangu nyakati za kale, Yehova alitaka kila familia iwe na wakati wa kuwa pamoja ili kuimarisha hali yao ya kiroho na vilevile kujenga uhusiano wa karibu miongoni mwao. (Kumbukumbu la Torati 6:6, 7) Ndiyo sababu Mashahidi wa Yehova wanatenga wakati kila juma kwa ajili ya ibada ya familia. Katika pindi hizo, wakiwa wamestarehe, wanazungumzia mambo ya kiroho yanayohusu familia zao. Hata ikiwa unaishi peke yako, unaweza kutumia wakati huo pamoja na Mungu kwa kujifunza jambo fulani katika Biblia.

      Ni wakati wa kumkaribia Yehova. “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:8) Tunaweza kumjua Yehova vizuri hata zaidi tunapojifunza mambo hususa kuhusu utu wake na matendo yake kupitia Neno lake. Ikiwa hamna ibada ya familia, njia rahisi ya kuianzisha ni kusoma Biblia kwa sauti mkiwa pamoja. Labda mnaweza kutumia ratiba ya kila juma ya Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo. Mnaweza kusoma kwa zamu, kisha mzungumzie mambo mliyojifunza katika Maandiko.

      Ni wakati wa kuimarisha uhusiano katika familia. Waume na wake, na vilevile wazazi na watoto, wanaweza kuimarisha uhusiano wao wanapojifunza Biblia pamoja wakiwa familia. Huo unapaswa kuwa wakati wa furaha na utulivu ambao kila mtu anatazamia kwa hamu kila juma. Ikitegemea umri wa watoto, wazazi wanaweza kuchagua habari zinazoifaa familia, labda makala ya Mnara wa Mlinzi au Amkeni! Mnaweza kuzungumzia matatizo ambayo watoto wenu walikabili shuleni na jinsi ya kuyashughulikia. Kwa nini msitazame Programu kwenye JW Broadcasting (tv.jw.org) na kisha muizungumzie pamoja? Mnaweza kufanya mazoezi ya nyimbo zitakazoimbwa katika mikutano na hata kuwa na viburudisho baada ya ibada ya familia.

      Wakati huo wa pekee mnaotumia pamoja kila juma katika kumwabudu Yehova utamsaidia kila mmoja katika familia afurahie kujifunza Neno la Mungu, naye atabariki jitihada zenu.—Zaburi 1:1-3.

      • Kwa nini tunatenga wakati kwa ajili ya ibada ya familia?

      • Wazazi wanawezaje kufanya pindi hiyo iwe yenye kufurahisha?

      PATA KUJUA MENGI ZAIDI

      Waulize wengine kutanikoni mambo wanayofanya katika ibada ya familia. Pia, tafuta machapisho yanayopatikana katika Jumba la Ufalme ambayo unaweza kutumia kuwafundisha watoto wako kumhusu Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki