Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kwa Nini Tunahudhuria Makusanyiko?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 11

      Kwa Nini Tunahudhuria Makusanyiko?

      Kusanyiko la eneo la Mashahidi wa Yehova nchini Mexico

      Mexico

      Chapisho likitolewa kwenye kusanyiko la eneo nchini Ujerumani

      Ujerumani

      Mashahidi wa Yehova wakiwa katika kusanyiko la eneo nchini Botswana

      Botswana

      Kijana akibatizwa nchini Nikaragua

      Nikaragua

      Drama ikiigizwa kwenye kusanyiko la eneo nchini Italia

      Italia

      Kwa nini watu hawa wana furaha? Wamehudhuria mojawapo ya makusanyiko yetu. Kama watumishi wa Mungu wa wakati uliopita ambao waliagizwa wakusanyike mara tatu kwa mwaka, sisi pia hutazamia kwa hamu kukusanyika pamoja katika makusanyiko. (Kumbukumbu la Torati 16:16) Kila mwaka tuna makusanyiko matatu: makusanyiko mawili ya mzunguko, kila kusanyiko kwa siku moja, na kusanyiko la eneo linalofanywa kwa siku tatu. Tunafaidika jinsi gani kwa kuhudhuria makusanyiko hayo?

      Yanaimarisha ushirika wetu wa Kikristo. Kama vile Waisraeli walivyoshangilia kumsifu Yehova katika “makusanyiko,” sisi pia hushangilia kumwabudu Yehova katika makusanyiko. (Zaburi 26:12, maelezo ya chini; 111:1) Makusanyiko hutuwezesha kukutana na kushirikiana na Mashahidi wenzetu wa makutaniko mengine au hata nchi nyingine. Wakati wa mchana, tunafurahia kula pamoja mahali pa kusanyiko, jambo linalochangia mazingira ya kirafiki katika pindi hizo za kiroho. (Matendo 2:42) Katika makusanyiko tunajionea upendo unaotuunganisha tukiwa “ushirika mzima wa akina ndugu” ulimwenguni pote.—1 Petro 2:17.

      Yanatusaidia kufanya maendeleo ya kiroho. Waisraeli walifaidika pia kwa ‘kuelewa maneno’ ya Maandiko yaliyokuwa yakifafanuliwa mbele yao. (Nehemia 8:8, 12) Sisi pia tunathamini mafundisho ya Biblia tunayopokea katika makusanyiko yetu. Kila programu hutegemea habari za Kimaandiko. Kupitia hotuba zenye kusisimua, mifululizo, na maigizo, tunafundishwa jinsi ya kufanya mapenzi ya Mungu katika maisha yetu. Tunatiwa moyo tunaposikia masimulizi ya wale ambao wamefaulu kubaki waaminifu licha ya hali ngumu. Kwenye makusanyiko ya eneo, drama hutusaidia kuona kihalisi masimulizi ya Biblia na kutufundisha masomo muhimu. Katika kila kusanyiko, wale ambao wamejiweka wakfu kwa Mungu na wangependa kubatizwa, hubatizwa.

      • Kwa nini makusanyiko ni pindi zenye furaha?

      • Unaweza kufaidika jinsi gani kwa kuhudhuria kusanyiko?

      PATA KUJUA MENGI ZAIDI

      Ikiwa ungependa kutujua vizuri zaidi, tafadhali hudhuria kusanyiko letu lijalo. Yule anayejifunza Biblia pamoja na wewe anaweza kukuonyesha programu ya kusanyiko ili uone habari zitakazozungumziwa. Tia alama kwenye kalenda yako tarehe na mahali ambapo kusanyiko lijalo litafanywa, na ujitahidi kuhudhuria.

  • Kazi Yetu ya Kuhubiri Ufalme Hufanywaje?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 12

      Kazi Yetu ya Kuhubiri Ufalme Hufanywaje?

      Mashahidi wa Yehova wakihubiri nyumba kwa nyumba

      Hispania

      Shahidi wa Yehova akihubiri katika bustani

      Belarus

      Shahidi wa Yehova akihubiri kupitia simu

      Hong Kong

      Mashahidi wa Yehova wakihubiri hadharani

      Peru

      Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alisema: “Habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Lakini kazi hiyo ya kuhubiri ulimwenguni pote ingetimizwa jinsi gani? Ingetimizwa kwa kufuata kielelezo ambacho Yesu aliweka alipokuwa duniani.—Luka 8:1.

      Tunajitahidi kuhubiri nyumba kwa nyumba. Yesu aliwazoeza wanafunzi wake kuhubiri habari njema nyumba kwa nyumba. (Mathayo 10:11-13; Matendo 5:42; 20:20) Wanafunzi hao walipewa maeneo hususa ya kuhubiri. (Mathayo 10:5, 6; 2 Wakorintho 10:13) Vivyo hivyo leo, kazi yetu ya kuhubiri inafanywa kwa utaratibu, na kila kutaniko huwa na eneo lake la kuhubiri. Utaratibu huo hutuwezesha kutimiza amri ya Yesu ya ‘kuwahubiria watu na kutoa ushahidi kamili.’—Matendo 10:42.

      Tunajitahidi kuwafikia watu mahali popote walipo. Yesu alituwekea mfano kwa kuwahubiria watu katika maeneo mbalimbali yenye watu wengi kama vile kwenye ufuo wa bahari au kisimani. (Marko 4:1; Yohana 4:5-15) Sisi pia huzungumza na watu kuhusu Biblia popote walipo—iwe ni barabarani, katika maeneo ya biashara, kwenye mabustani, au kupitia simu. Pia, tunawahubiria majirani, wafanyakazi, wanafunzi, na watu wetu wa ukoo tunapopata fursa. Jitihada zote hizo zimefanya iwezekane kwa mamilioni ya watu ulimwenguni pote kusikia “habari njema za wokovu.”—Zaburi 96:2.

      Je, kuna mtu yeyote ambaye ungependa kuzungumza naye kuhusu habari njema za Ufalme wa Mungu, na jinsi anavyoweza kufaidika wakati ujao? Zungumza naye mara tu upatapo fursa!

      • Ni “habari njema” zipi zinazohitaji kutangazwa?

      • Mashahidi wa Yehova wanaigaje mbinu ya Yesu ya kuhubiri?

      PATA KUJUA MENGI ZAIDI

      Mwombe yule anayejifunza Biblia pamoja nawe akuonyeshe jinsi unavyoweza kuzungumza kwa busara pamoja na mtu unayemfahamu kuhusu jambo ambalo umejifunza katika Biblia.

  • Painia Ni Nani?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 13

      13 Painia Ni Nani?

      Mhubiri wa wakati wote akihubiri hadharani

      Kanada

      Wahubiri wa wakati wote wakihubiri

      Nyumba kwa nyumba

      Wahubiri mapainia wakiongoza funzo la Biblia

      Funzo la Biblia

      Painia akijifunza Biblia

      Funzo la kibinafsi

      Mara nyingi, “painia” ni mtu anayevumbua maeneo mapya na njia ambayo wengine wanaweza kufuata. Tunaweza kusema kwamba Yesu alikuwa painia kwa sababu alitumwa duniani ili kuhudumu na kuwafungulia watu njia ya kupata wokovu. (Mathayo 20:28) Leo, wafuasi wake wanamwiga kwa kutumia muda mwingi iwezekanavyo katika kazi ya ‘kufanya wanafunzi.’ (Mathayo 28:19, 20) Wengine wamejiunga na utumishi unaoitwa upainia.

      Painia ni mhubiri wa habari njema wa wakati wote. Mashahidi wote wa Yehova ni wahubiri wa habari njema. Hata hivyo, wengine wamepanga mambo yao ili wawe mapainia wa kawaida, wakitumia saa 70 kila mwezi katika kazi ya kuhubiri. Wengi wao wanachagua kufanya kazi ya muda. Huenda wengine wakachaguliwa kuwa mapainia wa pekee katika maeneo ambayo yana uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme, wakitumia saa 130 au zaidi katika huduma kila mwezi. Mapainia wanaridhika na mahitaji ya msingi, nao wana hakika kwamba Yehova atawaandalia mambo ya lazima maishani. (Mathayo 6:31-33; 1 Timotheo 6:6-8) Wale ambao hawawezi kuwa mapainia wa wakati wote wanaweza kuwa mapainia wasaidizi wanapoweza. Wanafanya hivyo kwa kuongeza utendaji wao wakihubiri saa 30 au 50 kwa mwezi.

      Painia anachochewa na upendo wake kwa Mungu na watu. Kama Yesu, tunatambua kwamba watu wengi leo wana uhitaji mkubwa wa kiroho. (Marko 6:34) Lakini tuna ujuzi ambao unaweza kuwasaidia sasa, na kuwapa tumaini hakika la wakati ujao. Kumpenda jirani kunamchochea painia atumie kwa hiari wakati na nguvu zake kuwasaidia wengine kiroho. (Mathayo 22:39; 1 Wathesalonike 2:8) Anapofanya hivyo, imani yake inaimarishwa, anamkaribia zaidi Mungu, naye anakuwa na furaha nyingi.—Matendo 20:35.

      • Painia ni nani?

      • Ni nini kinachowachochea wengine wawe mapainia wa wakati wote?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki