Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mapainia Huzoezwa Katika Shule Gani?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 14

      Mapainia Huzoezwa Katika Shule Gani?

      Watumishi wa wakati wote wakihubiri hadharani

      Marekani

      Wanafunzi wakiwa katika Shule ya Gileadi
      Wanafunzi wakijitayarisha kwa ajili ya utumishi

      Shule ya Gileadi, Patterson, New York

      Wenzi wa ndoa wamishonari wakihubiri nchini Panama

      Panama

      Kwa miaka mingi elimu ya kitheokrasi imekaziwa sana na Mashahidi wa Yehova. Shule za pekee huandaliwa kwa ajili ya wale wanaotumikia wakiwa wahubiri wa wakati wote wa Ufalme ili ‘watimize kikamili huduma yao.’—2 Timotheo 4:5.

      Shule ya Utumishi wa Painia. Mwaka mmoja baada ya kuwa painia wa kawaida, mapainia huhudhuria shule ya siku sita ambayo hufanywa kwenye Jumba la Ufalme. Kusudi la shule hiyo ni kumsaidia painia amkaribie zaidi Yehova, aboreshe uwezo wake katika sehemu mbalimbali za huduma, na aendelee kutumikia kwa uaminifu.

      Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme. Shule hii ya miezi miwili imekusudiwa kuwazoeza mapainia wenye uzoefu ambao wako tayari kuhama nyumbani na kwenda kokote wanakohitajiwa. Ni kana kwamba wanasema, “Mimi hapa! Nitume mimi!” kwa kumwiga Mweneza-Injili mkuu zaidi, Yesu Kristo. (Isaya 6:8; Yohana 7:29) Baada ya kuhamia eneo lingine, huenda wakalazimika kuishi maisha rahisi. Huenda utamaduni, hali ya hewa, na vyakula vikawa tofauti na walivyozoea. Huenda pia wakahitaji kujifunza lugha mpya. Shule hii huwazoeza ndugu na dada waseja pamoja na wenzi wa ndoa, wenye umri kati ya miaka 23 na 65, wasitawishe sifa za kiroho watakazohitaji katika migawo yao na ustadi utakaowasaidia kumtumikia Yehova na tengenezo lake kikamili zaidi.

      Shule ya Gileadi. Katika Kiebrania neno “Gileadi” linamaanisha “Rundo la Ushahidi.” Tangu mwaka wa 1943, zaidi ya wamishonari 8,000 waliozoezwa katika Shule ya Gileadi wametumwa ili kutoa ushahidi “mpaka miisho ya dunia” na hiyo imeleta mafanikio makubwa. (Matendo 13:47) Wamishonari wetu walipofika nchini Peru, hakukuwa na kutaniko lolote huko. Sasa kuna zaidi ya makutaniko 1,000. Wamishonari wetu walipoanza kutumikia nchini Japani, kulikuwa na Mashahidi wasiozidi kumi. Sasa kuna zaidi ya Mashahidi 200,000. Mazoezi ya Gileadi yanayofanywa kwa miezi mitano yanatia ndani kujifunza Neno la Mungu kwa undani. Wale wanaotumikia wakiwa mapainia wa pekee au wamishonari, wale wanaotumikia kwenye ofisi za tawi, au wanaofanya kazi ya kuzungukia makutaniko hualikwa kwenye shule hii ili wajifunze kwa kina na hivyo kusaidia kuimarisha kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote.

      • Shule ya Utumishi wa Painia inatimiza kusudi gani?

      • Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme iliandaliwa kwa ajili ya akina nani?

  • Wazee Hulitumikia Kutaniko Jinsi Gani?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 15

      Wazee Hulitumikia Kutaniko Jinsi Gani?

      Mzee akizungumza na washiriki wa kutaniko

      Finland

      Mzee akifundisha kutanikoni

      Kufundisha

      Wazee wakiwatia moyo washiriki wa kutaniko

      Uchungaji

      Mzee akihubiri hadharani

      Kuhubiri

      Hatuna makasisi wanaolipwa. Badala yake, kama ilivyokuwa kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa, waangalizi wanaostahili huwekwa rasmi ili ‘walichunge kutaniko la Mungu.’ (Matendo 20:28) Wazee ni wanaume wakomavu kiroho ambao wanaongoza katika kutaniko na kulichunga, “si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari mbele za Mungu; si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu.” (1 Petro 5:1-3) Wazee hufanya kazi gani kwa faida yetu?

      Wanatuhangaikia na kutulinda. Wazee huongoza na kulinda kutaniko kiroho. Kwa kuwa wanatambua kwamba Mungu amewakabidhi jukumu zito, wazee hawapigi ubwana, badala yake, wanachangia hali nzuri na shangwe kati ya washiriki wa kutaniko. (2 Wakorintho 1:24) Kama vile mchungaji anavyomtunza kila kondoo kwa bidii, wazee hujitahidi kumjua kila mmoja katika kutaniko.—Methali 27:23.

      Wanatufundisha jinsi ya kufanya mapenzi ya Mungu. Kila juma, wazee huongoza mikutano ya kutaniko ili kuimarisha imani yetu. (Matendo 15:32) Wanaume hao ambao wamejitoa kwa moyo wote huongoza katika kazi ya kutangaza habari njema, wakihubiri pamoja nasi na kutuzoeza aina mbalimbali za huduma.

      Wanatutia moyo. Ili kututunza kiroho, wazee hututembelea nyumbani kwetu au kuzungumza nasi kwenye Jumba la Ufalme ili kutusaidia na kutufariji kwa kutumia Maandiko.—Yakobo 5:14, 15.

      Mbali na majukumu yao katika kutaniko, wazee wengi hufanya kazi ili kujiruzuku na wanahitaji kushughulikia familia zao. Ndugu hao wenye bidii wanastahili heshima kutoka kwetu.—1 Wathesalonike 5:12, 13.

      • Wazee wa kutaniko hufanya kazi gani?

      • Wazee huonyesha jinsi gani kwamba wanapendezwa na kila mmoja wetu?

      PATA KUJUA MENGI ZAIDI

      Ni nani wanaostahili kutumikia? Maandiko yanataja sifa ambazo wazee na watumishi wa huduma wanahitaji kutimiza ili wastahili. Unaweza kusoma kuhusu sifa hizo katika 1 Timotheo 3:1-10, 12, na Tito 1:5-9.

  • Watumishi wa Huduma Wana Majukumu Gani?
    Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
    • SOMO LA 16

      Watumishi wa Huduma Wana Majukumu Gani?

      Mtumishi wa huduma akisaidia kugawa machapisho

      Myanmar

      Mtumishi wa huduma akitoa hotuba

      Mkutano

      Mtumishi wa huduma akiongoza mkutano

      Kikundi cha utumishi

      Mtumishi wa huduma akifanya usafi katika Jumba la Ufalme

      Udumishaji wa Jumba la Ufalme

      Biblia hutaja vikundi viwili vya wanaume Wakristo ambao hushughulikia majukumu ya kutaniko, yaani, “waangalizi na watumishi wa huduma.” (Wafilipi 1:1) Kwa kawaida, katika kila kutaniko kuna wazee na watumishi wa huduma kadhaa. Watumishi wa huduma wanafanya kazi gani kwa faida yetu?

      Wanalisaidia baraza la wazee kutanikoni. Watumishi wa huduma ni wanaume wa kiroho, wenye kutegemeka, na wenye bidii. Baadhi yao ni vijana na wengine wana umri mkubwa. Wanafanya kazi za kawaida lakini ambazo ni muhimu kutanikoni. Utumishi wao huwawezesha wazee kupata wakati wa kukazia fikira ufundishaji na uchungaji.

      Wanatimiza huduma muhimu. Baadhi ya watumishi wa huduma hupewa mgawo wa kuwakaribisha wote wanaofika mikutanoni. Wengine hushughulikia mfumo wa sauti, vitabu na magazeti, hesabu za kutaniko, na migawo ya maeneo kutanikoni. Pia, wao husaidia katika kudumisha Jumba la Ufalme. Wazee wanaweza kuwaomba wawasaidie ndugu na dada waliozeeka. Hata iwe wana migawo gani, wanastahili kuheshimiwa na wote kutanikoni kwa sababu ya roho yao ya kutumikia.—1 Timotheo 3:13.

      Wanaweka mfano mzuri. Watumishi wa huduma huwekwa rasmi kwa sababu ya sifa zao nzuri za kiroho. Wanaposhughulikia migawo yao katika mikutano, wanaimarisha imani yetu. Wanapoongoza katika kazi ya kuhubiri, wanatuchochea kuwa wenye bidii. Roho yao ya ushirikiano huchangia shangwe na umoja. (Waefeso 4:16) Baada ya muda, huenda wao pia wakastahili kutumikia wakiwa wazee.

      • Watumishi wa huduma ni watu wa aina gani?

      • Watumishi wa huduma wanalisaidiaje kutaniko?

      PATA KUJUA MENGI ZAIDI

      Kila mara unapokwenda kwenye Jumba la Ufalme, jitahidi kumfahamu angalau mmoja wa wazee au watumishi wa huduma mpaka utakapowajua wote pamoja na familia zao.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki