-
Baraza Linaloongoza Hufanyaje Kazi Leo?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 20
Baraza Linaloongoza Hufanyaje Kazi Leo?
Baraza linaloongoza la karne ya kwanza
Kusomwa kwa barua ya baraza linaloongoza
Katika karne ya kwanza, kikundi kidogo, yaani, “mitume na wazee huko Yerusalemu,” kilitumikia kikiwa baraza linaloongoza lililofanya maamuzi muhimu kwa niaba ya kutaniko zima la Wakristo watiwa mafuta. (Matendo 15:2) Kuzungumzia Maandiko na kukubali mwongozo wa roho ya Mungu kuliwawezesha kufanya uamuzi kwa kauli moja. (Matendo 15:25) Ndivyo ilivyo leo pia.
Linatumiwa na Mungu kufanya mapenzi yake. Ndugu waliotiwa mafuta walio katika Baraza Linaloongoza wanapendezwa sana na Neno la Mungu nao wana uzoefu mwingi wa kutoa mwongozo kuhusu jinsi kazi inavyopaswa kufanywa, na pia kujibu maswali yanayohusiana na mambo ya kiroho. Wao hufanya mkutano kila juma ili kufikiria mahitaji ya ushirika wa akina ndugu ulimwenguni pote. Kama ilivyokuwa katika karne ya kwanza, maagizo yanayotegemea Biblia huandaliwa kupitia barua, waangalizi wanaosafiri, au vinginevyo. Jambo hili huwasaidia watu wa Mungu wawe na umoja. (Matendo 16:4, 5) Baraza Linaloongoza husimamia kuandaliwa kwa chakula cha kiroho, huwatia moyo wote washiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme, nalo husimamia kuwekwa kwa akina ndugu katika majukumu ya usimamizi.
Linafuata mwelekezo wa roho ya Mungu. Baraza Linaloongoza humtegemea Mwenye Enzi Kuu, Yehova, na pia Kichwa cha kutaniko, Yesu, ili kupata mwongozo. (1 Wakorintho 11:3; Waefeso 5:23) Ndugu walio katika baraza hilo hawajioni kuwa viongozi wa watu wa Mungu. Wao, pamoja na Wakristo wote watiwa-mafuta, wanaendelea “kumfuata Mwanakondoo [Yesu] popote anapoenda.” (Ufunuo 14:4) Baraza Linaloongoza huthamini sala zetu kwa niaba yao.
Ni nani waliokuwa katika baraza linaloongoza katika karne ya kwanza?
Baraza Linaloongoza hutafuta mwongozo wa Mungu jinsi gani leo?
-
-
Betheli Ni Nini?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 21
Betheli Ni Nini?
Idara ya Uchoraji, Marekani
Ujerumani
Kenya
Kolombia
Betheli ni neno la Kiebrania linalomaanisha “Nyumba ya Mungu.” (Mwanzo 28:17, 19, maelezo ya chini) Ni jina linalofaa ambalo Mashahidi wa Yehova hutumia kurejelea majengo yaliyoko katika nchi mbalimbali ambapo mwongozo na msaada kuhusiana na kazi ya kuhubiri unatolewa. Baraza Linaloongoza linafanya kazi likiwa katika makao makuu katika Jimbo la New York, Marekani, na kutoka huko linasimamia kazi inayofanywa na ofisi za tawi katika nchi mbalimbali. Wakiwa pamoja, wote wanaofanya kazi katika ofisi hizo wanaitwa familia ya Betheli. Kama familia, wanaishi na kufanya kazi pamoja, na wanakula na kujifunza Biblia pamoja kwa umoja.—Zaburi 133:1.
Mahali pa pekee ambapo washiriki wanajitolea kwa hiari. Katika kila ofisi ya Betheli kuna wanaume na wanawake Wakristo ambao wamejitolea kufanya mapenzi ya Mungu na kuendeleza masilahi ya Ufalme kwa wakati wote. (Mathayo 6:33) Hakuna yeyote kati yao anayepokea mshahara. Wote wanapewa mahali pa kulala, chakula, na pesa kidogo kwa ajili ya matumizi ya kibinafsi. Kila Mwanabetheli ana mgawo wake, huenda ikawa ni ofisini, jikoni, au katika chumba cha kulia chakula. Wengine wanafanya kazi ya kuchapisha vitabu, kutunza vyumba, kufua nguo, kudumisha majengo, au kazi nyingine.
Sehemu yenye shughuli nyingi inayosaidia kazi ya kuhubiri Ufalme. Kusudi kuu la Betheli ni kufanya ujumbe wa kweli wa Biblia uwafikie watu wengi iwezekanavyo. Mfano mmoja ni broshua hii. Iliandikwa chini ya usimamizi wa Baraza Linaloongoza, ikatumwa kwa mamia ya vikundi vya watafsiri ulimwenguni pote, ikachapishwa katika mashine zenye uwezo mkubwa zinazopatikana katika Betheli kadhaa, na hatimaye ikatumwa katika makutaniko zaidi ya 110,000. Katika kila hatua ya kazi hii, familia za Betheli zinatekeleza huduma za lazima ili kutegemeza kazi muhimu kuliko zote, kazi ya kuhubiri habari njema.—Marko 13:10.
Ni nani wanaofanya kazi Betheli, na wanatunzwa jinsi gani?
Ni kazi gani muhimu inayotegemezwa na huduma zinazotekelezwa Betheli?
-
-
Ni Kazi Gani Zinazofanywa Katika Ofisi ya Tawi?Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo?
-
-
SOMO LA 22
Ni Kazi Gani Zinazofanywa Katika Ofisi ya Tawi?
Visiwa vya Solomon
Kanada
Afrika Kusini
Wanabetheli wanafanya kazi katika idara mbalimbali zinazosimamia kazi ya kuhubiri katika nchi moja au kadhaa. Huenda baadhi yao wanafanya kazi katika idara ya kutafsiri, kuchapisha magazeti, kutengeneza vitabu, sauti au video, au idara nyingine zinazoshughulikia mambo yanayohusu eneo linalosimamiwa na ofisi ya tawi.
Halmashauri ya Tawi husimamia utendaji. Baraza Linaloongoza limeikabidhi Halmashauri ya Tawi jukumu la kusimamia utendaji wa ofisi ya tawi. Kwa kawaida halmashauri hiyo huwa na wazee watatu au zaidi wanaostahili. Halmashauri ya tawi hulijulisha Baraza Linaloongoza maendeleo ya utendaji mbalimbali katika eneo lililo chini ya usimamizi wake na pia kuhusu matatizo yoyote yanayoweza kutokea. Ripoti hizo hulisaidia Baraza Linaloongoza kuamua habari zinazohitaji kuandikwa katika machapisho na zinazohitaji kuzungumziwa katika mikutano na makusanyiko. Wawakilishi wa Baraza Linaloongoza hutumwa kwa ukawaida kwenye ofisi za tawi ili kuzipatia mwongozo Halmashauri za Tawi kuhusu jinsi ya kufanya kazi zao. (Methali 11:14) Programu ya pekee inayotia ndani hotuba ambayo hutolewa na mwakilishi wa makao makuu huandaliwa ili kuwatia moyo wale wanaoishi katika eneo lililo chini ya usimamizi wa ofisi ya tawi.
Makutaniko yanapata utegemezo. Ndugu waliowekwa katika ofisi ya tawi huidhinisha kuanzishwa kwa makutaniko mapya. Akina ndugu hutoa mwongozo kuhusu utendaji wa mapainia, wamishonari, na waangalizi wa mzunguko ambao wanatumikia katika eneo lililo chini ya ofisi ya tawi. Wanapanga makusanyiko, wanaratibu ujenzi wa Majumba ya Ufalme, na kuhakikisha kwamba machapisho yamefika kwenye makutaniko. Kazi zote zinazofanywa katika ofisi ya tawi huchangia umoja na upatano katika kutimiza kazi ya kuhubiri.—1 Wakorintho 14:33, 40.
Halmashauri za Tawi hulisaidiaje Baraza Linaloongoza?
Ni majukumu gani yanayotimizwa katika ofisi ya tawi?
-